Jumanne, 14 Aprili 2026

WASHIRIKI WA MAFUNZO KIGOMA WAPITISHWA KWENYE SHERIA, KANUNI NA MIONGOZO YA USULUHISHI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile amewapitisha washiriki wa mafunzo ya Usuluhishi kuhusu sheria, kanuni na miongozo ya usuluhishi inayotoa mwelekeo wa utatuzi na  utambuzi wa kiini cha mgogoro inayofikishwa Mahakamani.

Mhe. Rwizile ametoa mada hiyo leo tarehe 14 Aprili, 2026 mkoani Kigoma kwa washiriki 16 wa mafunzo ya  usuluhishi wa migogoro yanayoendelea Mahakama Kuu Kigoma. 

“Tunazo sheria, kanuni na miongozo ya usuluhishi inayotoa welekeo wa utatuzi na utambuzi wa kiini cha mgogoro inayofikishwa Mahakamani, hata hivyo zipo hatua nne muhimu za usuluhishi zikifuatwa na kuzingatiwa na msuluhishi yeyote basi mgogoro uliopo mbele ya msuluhishi utaleta matokeo mazuri,” amesema Jaji Rwizile.

Ameongeza kuwa, ni muhimu kwa Msuluhishi kuwa na ufahamu mkubwa wa kanuni za usuluhishi ili kufikia makubaliano ya usuluhisi wa mgogoro, na kwamba wasifungwe na uelewa mbalimbali unaotokana na kanuni, sheria na miongozo mingine inayotumika katika usuluhishi wa migogoro kutoka nchi mbalimbali duniani bali wajielekeze kwenye utatuzi wa mgogoro husika.

Kwa upande wake Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa amewasilisha mada juu ya utambuzi wa kiini cha mgogoro, ikiwa ni kuwasikiliza walengwa wa mgogoro, nini wanahitaji kila mmoja katika mgogoro huo, kisha kuwapa nafasi kila mdau kuweza kutoa mawazo ya kile anachohitaji katika kusuluhisha mgogoro huo, kuwapatia kila mmoja kile ambacho ataridhika nacho ili kumaliza migogoro iliyopo mahakamani.

Aidha, alifafanua mbinu mbalimbali wanazopaswa kutumia wasuluhishi hao ili kuendelea kuwa bora katika usuluhishi, hasa kutengeneza mazingira rafiki kwa walengwa wa mgogoro, mpangilio wa kuketi katika chumba cha usuluhishi, utoaji wa taarifa juu ya kila kitu kitakachofanyika katika usuluhishi, kuwaeleza malengo ya usuluhishi huo na jukumu lao la msingi katika usuluhishi, kuwatambua wadau wenye mgogoro husika bila upendeleo wala ubaguzi ikiwa ni sambamba na matarajio yao kupitia usuluhishi huo, kuwapa muda sawa wa kuzungumza, kujieleza na uwazi usio na mashaka.

Leo ni siku ya pili ya mafunzo kwa washiriki hao, wakiendelea kunolewa kwa ufasaha ili waje kuwa Wasuluhishi maridadi wa kutatua migogoro iliyopo hapa nchini.

Washiriki wa mafunzo hayo ni Mahakimu wa Kanda za Kigoma, Bukoba, Musoma na Mwanza.



Sehemu ya washiriki wa mafunzo  ya Usuluhishi wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikiwasilishwa na moja ya Mkufunzi wa mafunzo ya usuluhishi leo tarehe 14, Aprili 2026 Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile akiwasilisha mada leo tarehe 14 Aprili, 2026 katika Mafunzo ya Usuluhishi yanayoendelea kufanyika Mahakama Kuu Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akisisitiza jambo wakati akiwasilisha mada kwa washiriki wa Mafunzo ya Usuluhishi leo tarehe 14 Aprili, 2026.

Washiriki wa mafunzo wakitoa mfano halisi wa jinsi Msuluhishi na Mdau wanaweza kukaa na kuzungumza juu ya jambo fulani linalohitaji usuluhishi.


Moja ya picha inayotumika na wakufunzi katika chumba cha kutolea mafunzo ya usuluhishi Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni