Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu, Dodoma.
Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma, hivi
karibuni walipatiwa elimu muhimu kuhusu afya ya akili na ustawi wa maisha, iliyogusa
moja kwa moja maisha yao ya kazini na nyumbani.
Elimu
hiyo ilitolewa katika Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki
(IJC) Dodoma na Jaji wa Mahakama Kuu kutoka Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David
Ngunyale.
Mbali
na majukumu yake ya kusikiliza mashauri mkoani Dodoma, Mhe. Ngunyale aliona vyema
kutumia nafasi hiyo kuwajengea uelewa Watumishi hao kwenye eneo hilo.
Kabla
ya kuanza zoezi hilo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt.
Juliana Masabo, alimpongeza Jaji Ngunyale kwa moyo wa kujitoa na upendo wa
dhati aliouonesha kwa Watumishi hao, akisisitiza kuwa afya ya akili ni msingi
muhimu wa utendaji bora na maisha yenye mafanikio.
Kupitia
elimu hiyo, Watumishi walipata fursa ya kujifunza kwa kina viashiria vya afya
ya akili, mbinu za kukabiliana na changamoto za kisaikolojia pamoja na namna ya
kujijenga kiakili na kitaaluma.
Si
hivyo tu, mada ya uongozi bora (leading skills) iliyotolewa wakati wa zoezi
hilo la utoaji elimu iliongeza chachu mpya kwa washiriki wengi, ikiwapa mwanga
wa kuwa Viongozi bora katika nafasi zao na katika jamii.
Kilichovutia
zaidi ni namna atumishi walivyoshiriki kwa hamasa kubwa, wakionesha wazi
kufurahishwa na elimu hiyo ambayo waliieleza kuwa imewafungua macho na kuwapa
mwelekeo mpya wa maisha.
Walimshukuru
Jaji Ngunyale kwa kuwapatia maarifa yenye tija na yenye kugusa uhalisia wa
maisha yao ya kila siku.
Zoezi hilo lilihudhuriwa na Watumishi mbalimbali ana kwa ana wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt Fatma Khalfan, pamoja na wengine waliounganishwa kwa njia ya mtandao kutoka wilayani, jambo lililoongeza ushirikishwaji na kuifanya elimu hiyo kuwafikia wengi zaidi kwa wakati mmoja.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo (aliyesimama)
akimkaribisha Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David
Ngunyale, aliyepo kulia kwake, ili kuwapa elimu Watumishi wa Mahakama Kuu
Dodoma. Kushoto kwake ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Bw. Bedson Mariba.
Watumishi
wa Mahakama Kuu Dodoma wakiskiliza kwa makini elimu ya Afya ya Akili kutoka kwa
Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale (hayupo pichani).
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Simiyu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni