Ijumaa, 29 Mei 2026

MAHAKAMA NJOMBE YAACHANA NA MATUMIZI YA KARATASI

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Mahakama ya Njombe imeacha rasmi kutumia karatasi katika huduma za Mahakama zinazotolewazo kwa wananchi na Mahakama hiyo kuanzia ngazi za Mahakama za Mwanzo mpaka ngazi ya Mahakama Kuu Njombe.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya kikao kilichofanyika tarehe 25 Mei, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe.

Katika kikao hicho cha Mrejesho wa Mafunzo ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama Njombe ambao hivi karibuni walienda Mahakama Kuu ya Geita kufanya ziara ya kujifunza mambo mbalimbali yenye lengo la kubadilishana uzoefu wa Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji haki kwa wananchi.

Kikao hicho kilifunguliwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Bw. Richard Mbambe ambaye alimkaribisha Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Njombe, Mhe.Victoria Nongwa pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mahakama Njombe, Mhe. Joseph Luambano kwa ajili ya kutoa mada mbalimbali za Mafunzo waliyoyapata wakiwa Mahakama Kuu Geita. 

Mhe. Luambano aliwasilisha mada mbalimbali kwa watumishi waliohudhuria katika kikao hicho pamoja na watumishi waliopo Wilaya za Wanging’ombe, Makete na Ludewa ambao waliweza kuudhuria kwa njia ya Teknolojia ya video mtandao.

 Mhe.Luambano alitoa mada kuhusu  kutimiza majukumu ya kila siku ya kazi kwa kutumia  Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)  kwa kuanza na Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) pamoja na mifumo inayosimamia masuala ya kiutawala hasa mfumo wa Ofisi Mtandao (e-Office) pamoja na malipo ya uhasibu na manunuzi ya vifaa vya ofisi pamoja na mafuta ya Magari ya Serikali.

Akiendelea kutoa mada mbalimbali, kwa upande wa Wahudumu pamoja na Madereva aliwaeleza kuwa, “kwa sasa suala la kuomba vifaa au mafuta ya magari pamoja na matengenezo ya magari watumie njia mbadala na siyo kuomba mafuta kwa kuandika kwenye makaratasi au matengenezo magari hivyo, watumie nakala laini kwa mifumo itakayowezeshwa katika utekelezaji wa majukumu yenu ya kila.”

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Njombe, Bw.Mbambe alipata fursa wa kuzungumza na watumishi na kuahidi kwamba, katika uchakataji wa Mifumo hiyo vifaa vinaitajika na mwaka fedha wa 2026/2027  watumishi wote watanunuliwa vifaa vya kisasa ili waweze kuendana na kasi ya teknolojia ya sasa na kuwasisitiza watumishi waweze kubadilika waendane na mabadiliko ya sasa katika ufanyaji kazi.

Aidha, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Victoria Nongwa alifunga kikao hicho ambacho Maofisa Mbalimbali wa Mahakama walipata fursa ya kuchangia mada mbalimbali pamoja na kuuliza maswali na majibu yalitoka papo kwa hapo.

Mhe. Nongwa aliwasisitiza Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kuchapa wenyewe mashauri wanayoyasikiliza na kuyaweka katika nakala laini ambapo yatakuwa yanahifadhiwa katika mfumo maalum.

Kadhalika, Jaji Nongwa pia  aliwasisitiza pia watumishi ambao sio Mahakimu  kuyapokea mafunzo hayo na kuwaeleza kuwa, wawe na utayari wa kubadilika kutoka kwenye majukumu ambayo yalikuwa yanafanywa kwa njia ya kawaida yaani matumizi ya karatasi kwa sasa yaweze kuwa yanafanyika kwa njia ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa kuwa mifumo hiyo inaleta ufanisi na uwazi katika kazi za Mahakama.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Njombe,Mhe. Victoria Nongwa (kulia) pamoja Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge wakimsikiliza Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe ,Mhe.Joseph Luambano (hayupo katika picha) wakati akitoa mada mbalimbali juu ya Mafunzo waliyoyapata kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Njombe, Mhe.Joseph Luambano (kulia) akitoa mada mbalimbali kwa Watumishi wa Mahakama Njombe (hawapo katika picha) juu ya Mafunzo waliyoyapata kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita kwa kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Bw.Richard Mbambe (aliyesimama) akizungumza na watumishi kuhusu umuhimu wa kuwa na vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA). Walioketi meza kuu katikati ni Jaji  Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Njombe, Mhe. Victoria Nongwa, kushoto ni  Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe.Obadia Bwegoge na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano.

Ofisa TEHAMA wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Bw.Fadhili Lwena akisisitiza juu ya matumizi ya baruapepe za ofisi kwa watumishi wa Mahakama hiyo. Walioketi mbele kulia ni Jaji  Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya  Njombe, Mhe. Victoria Nongwa, anayefuata ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Mhe. Obadia Bwegoge.


Ofisa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Njombe, Bi.Tumaini Jembe (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao hicho. Walioketi ni sehemu ya  Maofisa wa  Mahakama na watumishi ambao siyo Maofisa wa Mahakama kwa pamoja wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa.


Picha ya juu na chini ni watumishi waliohudhuria katika kikao hicho wakifuatilia kilichokuwa kikijiri katika kikao hicho.

(Habari imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni