Ijumaa, 19 Juni 2026

MASHAURI 48 YA RUFAA ZA MADAI KUSIKILIZWA MBEYA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya.

Mahakama ya Rufani ya Tanzania inatarajia kuendesha Kikao cha usikilizaji wa mashauri 48 ya rufaa za madai katika Masjala Ndogo ya Mbeya kuanzia tarehe 18 Juni 2026 hadi tarehe 17 Julai, 2026.

Kikao hicho kitakua na jopo moja la Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiongozwa na Jaji wa Rufaa ya Tanzania Mhe. Winifrida Beatrice Korosso, Majaji wengine katika jopo hilo ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Mary Calorine Levira na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Agnes Zephania Mgeyekwa.

Akiwasilisha taarifa katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya, ambacho ni kikao cha maandalizi (Pre- Session Meeting), Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. Agatha Chugulu alieleza kuwa Jumla ya mashauri 48 ya Rufaa za madai yamepangwa kusikilizwa katika Masjala Ndogo ya Mbeya.

Aidha Mhe. Chugulu aliongeza kuwa, katika kuhakikisha ufanisi wa kikao hicho na kufikiwa kwa malengo yaliyokusudiwa ratiba ya kikao ilitolewa kwa wakati na Hati za kuitwa shaurini za wadaawa kwa ajili ya usikilizwaji wa mashauri zimesambazwa na juhudi za kuwapata wadaawa amabao hawajapatikana zinaendelea.

Naye, Mwenyekiti wa kikao hicho, Jaji wa Rufaa Mhe. Winifrida Korosso, alihitimisha kwa kuomba ushirikiano baina ya wadau na kusisitiza kuchunga muda wa kufika mahakamani.

“Lengo letu sote ni kupatikana kwa haki kama kuna changamoto yoyote wasilisha mapema ili tufikie lengo la kutafuta haki kwa pamoja ni matarajio yetu kuwa kutokana na mpango wa kusikiliza mashauri kuandaliwa mapema pamoja na ufuatiliaji wa karibu wa kila jalada, kikao hiki kitafikia malengo yaliyokusudiwa,” alisema Mhe. Korosso.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya akiwemo Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba, Mawakili na Wadau wengine wa Haki Madai.

 

Mwenyekiti jopo Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Winifrida Beatrice Korosso (kulia), akiongoza kikao hicho, kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Agnes Zephania Mgeyekwa.

Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliohudhuria kikao hicho, ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (katikati) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Mavis Miti (kushoto).

Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Agatha Chugulu (kushoto) akiwasilisha taarifa katika kikao hicho na (kulia) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba. Ambaye katika kikao hicho alikaimu nafasi ya Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

Sehemu ya Wadau walioshiriki katika kikao hicho hoja mbalimbali kwa makini. 

Sehemu ya Wadau walioshiriki katika kikao hicho wakifuatilia kwa makini.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni