Alhamisi, 18 Juni 2026

TUTEKELEZE MAJUKUMU YETU VEMA; JAJI NGUNYALE

Na MICHAEL RITTE, Mahakama-Bukoba

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Nyanguye amewasihi watumishi wa Masjala hiyo kuhakikisha kazi za usikilizwaji wa mashauri zinaendeshwa vema pasipo kukwama na jukumu hilo liambatane na juhudi katika utendaji wa majukumu ya kila siku kwa kuzingatia Maadili na kanuni za nafasi husika wanazozitumikia.

Mhe. Ngunyale aliyasema hayo jana tarehe 17 Juni, 2026 katika Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba wakati wa makabidhiano ya Ofisi kati yake na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ambaye ameteuliwa hivi karibuni kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani.

Kabla ya makabidhiano ya ofisi, kulikuwa na  mapokezi ya awali katika viwanja vya Mahakama hiyo.

Jaji Ngunyale alisema kuwa, kila mtumishi ana wajibu wa kuhakikisha huduma za utoaji haki zinafanyika kwa uadilifu na weledi. Huku akisisitiza kuwa, “tujivunie nafasi tulizopewa na kuzisimamia ipasavyo.”

“Tukifanikiwa kusimamia majukumu yetu na kuwekeza nguvu na muda katika kazi, itatuletea nafasi thabiti ya kujengeana uwezo katika kazi na katika majukumu mbalimbali,” amesisitiza Mhe. Ngunyale.

Ameongeza kuwa, katika utekelezaji wa majukumu ni muhimu kujali afya, familia zetu na jamii sambamba na kuwa na ukaribu na kutenga muda na  nafasi kushiriki shughuli za kijamii ambazo kwa namna moja hudumisha afya ya kiakili na kiutendaji kwa mtumishi.

Alisisistiza kwa kunukuu, “To be trusted is a greater Compliment than to be loved,” Usemi kutoka kwa Mwandishi George MacDonald ambao unamaanisha kuwa, ‘Kuaminiwa ni sifa kubwa kuliko kupendwa.’

Kwa upande wake, aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, aliwasihi watumishi hao kuendelea kuishi kwa upendo kama walivyoishi naye kipindi akiwa katika nafasi hiyo.

Kadhalika, Mhe. Banzi amewasihi watumishi hao kuendeleza ushirikiano. Na kuhitimisha kwa kumtakia Mhe. Ngunyale kila la kheri katika utekelezaji wa majukumu mapya katika Kituo hicho.

Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Ngunyale akisalimiana na Watumishi wa Mahakama hiyo alipowasili katika Kituo chake kipya cha kazi jana tarehe 17 Juni, 2026. 

Jaji wa Mahakama ya Rufani na aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Bukoba, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi (kulia) akimkabidhi taarifa ya makabidhiano ya ofisi Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Ngunyale.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi (wa pili kulia) akiwa katika picha na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. David Ngunyale (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Lillian Itemba (wa kwanza kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Ferdinand Kiwonde. 

 Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi (wa pili kushoto) akizungumza jambo wakati wa hafla ya makabidhiano ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba kwa Mhe. David Ngunyale. Wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Lillian Itemba na wa kwanza kulia ni Mhe. Ferdinand Kiwonde, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, wakiwa kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Bukoba.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Bukoba, Mhe. Said Mkasiwa akitoa neno la kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama hiyo, Mhe. David Ngunyale (wa kwanza kushoto).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni