- Yaahidi kuendeleza ushirikiano na Jaji Mfawidhi mpya
Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama, Divisheni ya Kazi
Viongozi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) Ofisi ya Dar
es Salaam, jana tarehe 1 Julai, 2026 walikutana na Viongozi wa Mahakama Kuu
Divisheni ya Kazi kwa ajili ya kumuaga aliyekuwa Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, ambaye kwa sasa ni Jaji
wa Mahakama ya Rufani.
Katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa
mikutano ILO Kazi House, Viongozi hao walimkaribisha pia Jaji Mfawidhi mpya,
Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na wawakilishi wa Mahakama Kuu
Divisheni ya Kazi, ILO na Wadau wengine wa haki kazi na ajira.
Mhe. Dkt. Mlyambina aliwasilisha shukrani zake kwa ILO kwa
kuwa bega kwa bega na Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi katika kufanikisha
shughuli mbalimbali kwa kipindi chote alichohudumu katika ofisi hiyo.
Alieleza kuwa ILO imekuwa ikishirikiana na Mahakama hiyo
katika kuimarisha haki kazi nchini. Ushirikiano huo ni pamoja na kuwezesha
machapisho ya (Labour Case Reports) ambazo zimekuwa msaada mkubwa katika
kuimarisha utoaji wa haki kazi.
Aidha, alieleza kuwa ILO imekuwa ikiwezesha mafunzo
mbalimbali ndani na nje ya nchi ambapo watumishi na Wadau wengine wamekuwa
wakinufaika kwa kuongeza ufanisi katika utendaji kazi.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Ofisi ya
ILO, anayehudumia Tanzania, Kenya, Rwanda na Uganda, Bi. Caroline Mugalla,
alisema kuwa mfumo madhubuti wa haki za kazi ni msingi muhimu wa kuendeleza
ajira zenye staha na haki za kijamii.
Vilevile, alisisitiza kuwa ushirikiano wa muda mrefu
kati ya ILO na Mahakama ya Tanzania umechangia kuimarisha upatikanaji wa haki
kwa wafanyakazi na waajiri kupitia mfumo wenye ufanisi wa utoaji haki.
Bi. Caroline, kwa niaba ya ILO, alitumia nafasi hiyo kumshukuru
Jaji Mlyambina kwa utendaji kazi wake katika kipindi chote alichohudumu, huku
akimpongeza kwa kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama
ya Rufani.
Katika kumkaribisha Jaji Mfawidhi mpya, Bi. Caroline alieleza
kuwa ILO itaendelea kushirikiana na Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha
mfumo wa haki kazi nchini kwa manufaa ya Taifa kwa ujumla.


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni