Ijumaa, 10 Julai 2026

JAJI TIGANGA ASISITIZA UTEKELEZAJI MIKAKATI YA JAJI MKUU USIKILIZAJI MASHAURI YA MADAI

Na ARAPHA- RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, hivi karibuni ilifanya Kikao cha Kusukuma Mashauri ya Madai (Bench Bar) kilichowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya sheria na haki, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa mashauri ya madai, kupunguza mlundikano na kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa wakati.

Kikao hicho kiliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, na kuhudhuriwa na wawakilishi kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Ofisi ya Msajili wa Hati pamoja na Baraza la Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Akifungua kikao hicho, Jaji Mfawidhi alisisitiza umuhimu wa wadau wote wa sekta ya sheria na haki kuendelea kutekeleza na kufuatilia kwa vitendo mikakati iliyoelekezwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, yenye lengo la kuhakikisha mashauri yanasikilizwa na kuamuliwa mapema ipasavyo, kupunguza mlundikano na kuimarisha utoaji wa haki nchini.

Akiwasilisha taarifa ya hali ya mashauri ya madai, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, alisema Mahakama inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuhakikisha mashauri yanasikilizwa na kuamuliwa kwa wakati, sambamba na kudhibiti mashauri ya mlundikano.

Alieleza kuwa Mahakama imeendelea kufanya vikao maalum vya kusafisha mashauri (clean-up sessions), kutoa kipaumbele kwa mashauri ya kimkakati na   matumizi ya hati ya maelezo ya shahidi (Witness statement)  kwa dhumuni la kumaliza mashauri haraka na kupata kumbukumbu nzuri ya kile alichokikusudia mteja.

Mikakati mingine ni kusikiliza mashauri kadri inavyokuwa yamekamilika au yameiva bila kujali yamepokelewa lini, kuhimiza matumizi ya usuluhishi pale inapowezekana, kukamilisha hatua za awali  ya mashauri ya awali ndani ya siku 30, kutoa ahirisho lisilozidi wiki mbili na kuimarisha ushirikiano na wadau wa mnyororo wa haki ili kuondoa vikwazo vinavyochelewesha usikilizaji wa mashauri.

Kikao hicho pia kilibaini mashauri yanayokaribia kuwa ya mlundikano na kuweka mikakati ya kuyashughulikia mapema. Aidha, wadau walisisitiza umuhimu wa kushughulikia migogoro katika ngazi zinazotakiwa kisheria kabla ya kufikishwa mahakamani, hususan mashauri ya ardhi, pamoja na kuhakikisha mashauri yanaamuliwa kwa kuzingatia ushahidi na hoja za msingi badala ya kasoro za kiufundi.

Miongoni mwa mikakatii iliyofikiwa ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na Taasisi za mnyororo wa haki, kuongeza matumizi ya usuluhishi katika kutatua migogoro, kuharakisha utekelezaji wa hukumu na kuhakikisha mashauri yanayosikilizwa yanakamilika kwa wakati kwa kuzingatia sheria na kanuni.

Mikakati mingine iliyofikiwa ni kutosajili mashauri ya ardhi ambayo yalipaswa kuanzia  kwa Msajili wa Hati kwa mjibu wa sheria pamoja na kufuatilia utekelezaji wa mikakati ya kikao cha Jaji Mkuun na Wadau wa Haki Madai inayolenga kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wote wa sekta ya sheria na haki ili kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama, kupunguza mlundikano wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki mapema ipasavyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiongoza kikao cha kusukuma mashauri ya madai.

 Wadau wa kikao hicho (juu na chin) wakisikiliza hoja mbalimbali ambazo zilikuwa zinatolewa.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, (aliyepo katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe na wadau wa kikao hicho. Kulia kwake waliokaa ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kushoto kwake ni Naibu Msajili, Mhe.Zabibu Mpangule.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni