Jumanne, 28 Julai 2026

MAHAKIMU MBEYA WAKUMBUSHWA KUZINGATIA MAADILI, WELEDI KATIKA UTOAJI HAKI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Wilaya ya Mbeya imefanya kikao kazi kilichowakutanisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo zilizopo jijini Mbeya kwa lengo la kusisitiza uimarishaji wa maadili, uwajibikaji na kuzingatia ubora wa utoaji wa huduma za Mahakama sambamba na kujadili changamoto zinazojitokeza katika ushughulikiaji wa malalamiko na uandaaji wa kumbukumbu za mashauri ya rufaa.

Kikao hicho kiliitishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba na kuwashirikisha viongozi kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, walitoa maelekezo na miongozo kadhaa ya utendaji kazi kwa Maafisa Mahakama wakiwa katika vituo vyao.

Viongozi walioshiriki kikao kazi hicho ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo aliwataka Mahakimu kuendelea kudumisha nidhamu, uadilifu na uzingatiaji wa sheria katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yao. Alisisitiza kuwa utoaji wa haki unapaswa kuongozwa na misingi ya haki, uwazi na weledi ili kulinda hadhi ya Mahakama.

“Mahakama ina jukumu la kumfuta machozi mtu aliyedhurumiwa haki zake na nasisitiza kuwa kila shauri linapaswa kushughulikiwa kwa umakini, usawa na kwa kuzingatia sheria ili kuhakikisha haki inatendeka na kuonekana kutendeka,” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, aliwahimiza Mahakimu kuendelea kuzingatia maadili ya kazi, kuwahudumia wananchi kwa weledi na kwa lugha yenye staha, pamoja na kutekeleza kwa vitendo maelekezo yanayotolewa na viongozi kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano, kuheshimiana na kujenga mahusiano mazuri mahali pa kazi. Pia aliwakumbusha Maofisa hao kutunza afya zao, akieleza kuwa afya njema ni msingi wa utendaji bora na huchangia katika kulinda na kutunza rasilimali za Mahakama na kuongeza ufanisi wa taasisi kwa ujumla.

Maofisa Mahakama katika kikao hicho, walikumbushwa umuhimu wa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, missing ya taaluma inayoongoza kazi zao na kuhakikisha kuwa majukumu yao yanatekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Pamoja na hayo, washiriki walijadili mbinu za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi ili kuongeza ufanisi na kuimarisha imani ya jamii kwa Mhimili wa Mahakama.

Aidha, Viongozi hao walisisitiza na kuhimiza Maofisa hao kuhakikisha wananchi wanapatiwa nakala za hukumu na mwenendo wa mashauri kwa wakati, matumizi sahihi ya mifumo ya TEHAMA katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama, kuzingatia mipaka ya mamlaka hayo wakati wa kusikiliza mashauri na kufuata sheria na kanuni katika utekelezaji wa tuzo na amri za Mahakama.

Mahakama ya Tanzania inaendelea kuimarisha uwezo wa watumishi wake kupitia mafunzo ya ndani na vikao vya kitaalamu vinavyolenga kuboresha utendaji kazi, kuimarisha maadili na kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki zenye ubora, kwa wakati na kwa kuzingatia misingi ya sheria na haki.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (wa pili kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo jijini Mbeya.

Meza Kuu ikiongozwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (wa pili kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo jijini Mbeya.

Viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa kikao hicho, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, (wa pili kulia) ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, (wa pili kushoto) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya na kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni