Na. DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus
Kahyoza, amewataka watumishi wa Mahakama kuongeza ubunifu na uwajibikaji ili
kuleta tija katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku na kuhakikisha wananchi
wanapata huduma bora za utoaji haki kwa wakati.
Wito
huo ametolewa wakati akifungua kikao cha Menejimenti cha Mahakama Kuu, Masjala
Ndogo ya Geita, kilichofanyika hivi karibuni, katika ukumbi wa mafunzo uliopo
Kituo Jumuishi cha utoaji haki mjini Geita.
Akizungumza
katika kikao hicho, Mhe. Kahyoza alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha
viongozi na watumishi kukutana kwa lengo la kutathmini utendaji wa kazi wa Mahakama
na kujadili mbinu bora za kuendelea kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.
Mhe.
Kahyoza alisema kuwa, kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kinatoa fursa ya
kutathmini utekelezaji wa majukumu, kubaini mafanikio yaliyopatikana,
changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuongeza ufanisi katika maeneo
yanayohitaji maboresho.
Alieleza
kuwa, pamoja na kikao hicho kuwa sehemu ya utaratibu wa kisheria wa Mahakama,
umuhimu wake unakwenda mbali zaidi ya kutekeleza matakwa ya kisheria, kwani
kinatoa nafasi ya kutafakari namna ya kuifanya Mahakama iendelee kupiga hatua
katika utoaji wa huduma kwa wananchi.
Jaji
Kahyoza alisisitiza kuwa, utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama unapaswa
kuzingatia maslahi mapana ya wananchi wa Mkoa wa Geita na Tanzania kwa ujumla.
Alibainisha kuwa kila mtumishi anapaswa kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi na
viwango vya juu vya weledi.
“Ni muhimu kila mmoja wetu kutathmini tumefanikiwa
kwa kiwango gani, ni maeneo yapi tunasuasua na ni hatua zipi tunapaswa kuchukua
ili kuhakikisha shughuli zetu zinaendelea kufanyika kwa ufanisi zaidi,”
alisema Jaji Kahyoza.
Nao,
Wakuu wa vitengo pamoja na Viongozi wa Utawala kutoka Mahakama za Wilaya na Mahakama
Kuu waliwasilisha taarifa za maeneo yao ya kiutendaji.
Wajumbe
walipata nafasi ya kujadili taarifa mbalimbali zilizowasilishwa, huku mijadala
ikijikita katika namna ya kuongeza ubunifu na tija katika uendeshaji wa
shughuli za Mahakama, hususan kuimarisha usikilizaji na utoaji wa maamuzi ya
mashauri kwa wakati.
Miongoni
mwa changamoto zilizojadiliwa ni uchakavu wa baadhi ya majengo ya Mahakama
pamoja na kuwepo kwa fedha za mirathi ambazo hazijachukuliwa na wanufaika wake.
Taarifa
ya Mashauri ilionesha Mahakama zote kufanya vizuri kwa kipindi cha Machi mpaka
Juni 30, 2026. Mashauri ya Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, na Wilaya
zote hazikuwa na shauri la mlundikano kwa mashauri yaliyofunguliwa mwaka 2025.
Pongezi
pia zilienda Mahakama za Mwanzo kwa kuendelea kuondosha Mashauri kwa wakati
kwani Mahakama zote zina wastani wa siku 9 wa umri wa shauri kukaa mahakamani.
Hata
hivyo, kikao kilibaini kuwa bado kuna changamoto kuhusu fedha za mirathi,
ambapo baadhi ya fedha hizo zimeendelea kubaki bila kuchukuliwa kutokana na
kutopatikana kwa wanufaika au baadhi yao kukataa kuzichukua kwa madai kuwa
kiasi kilichopo ni kidogo.
Wajumbe
kutoka Mahakama za Wilaya za Chato, Geita, Bukombe, Mbogwe na Nyang'hwale
walieleza kuwa changamoto hiyo imeendelea kujitokeza katika maeneo yao. Kutokana
na hali hiyo, Mwenyekiti alisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za haraka ili
kupata suluhisho la kudumu.
Katika
kikao hicho, wajumbe walichangia umuhimu wa kuendelea kutafuta viwanja na
kuvipatia hati angalau viwanja viwili kwa kila Halmashauri. Mtendaji wa Mahakama
Kuu Masjala Ndogo ya Geita Bi. Masalu Kisasila asisitiza kuwa, hatua hiyo ni
muhimu katika kuwezesha upatikanaji wa miradi ya maendeleo na kulinda mali za Mahakama.
Kutokana
na umuhimu wa suala hilo, Mwenyekiti wa kikao hicho alielekeza kuwa, ifikapo
Septemba 30, 2026, viwanja na majengo yote ya Mahakama ambayo bado hayana hati
miliki viwe vimekamilisha taratibu za umiliki.
Aidha,
viongozi wa Mahakama waliagizwa kushirikiana kwa karibu na Wakurugenzi wa
Halmashauri katika maeneo yao ili kutatua kwa wakati changamoto zinazohusu
miundombinu pamoja na masuala mengine ya kiutendaji.
Mhe.
Kahyoza alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama na taasisi nyingine
za Serikali, akieleza kuwa ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika kuhakikisha
mipango ya maendeleo ya Mahakama inatekelezwa kwa ufanisi na huduma kwa
wananchi zinaendelea kuimarika.
Mhe.
Kahyoza alisisitiza kuwa, ubunifu, uwajibikaji, matumizi bora ya rasilimali na
tathmini ya mara kwa mara ya utekelezaji wa mipango ni nguzo muhimu za kuongeza
ufanisi katika utoaji wa huduma za Mahakama. Alieleza kuwa hatua hizo
zitawezesha Mahakama kuendelea kuboresha mazingira ya utendaji, kuharakisha
usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa
ufanisi.
Mhasibu
wa Mahakama Kuu Geita, Bw. Goodluck Machange akiwasilisha Taarifa ya
utekelezaji wa Fedha.
Afisa
Ugavi wa Mahakama Kuu Geita, Bw. Abel Bunzali akiwasilisha Taarifa ya
utekelezaji wa robo ya nne ya mwaka 2025/2026.
Meza
Kuu katika kikao cha menejimenti, aliyesimama ni Katibu wa kikao, Bi. Masalu
kisasila, katikati ni Mwenyekiti wa Kikao, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu
ya Tanzania, Masjala Ndogo Mhe. Fredrick Lukuna.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni