Alhamisi, 2 Julai 2026

MASJALA NDOGO MBEYA YAWAKARIBISHA VIONGOZI WAPYA

Na. MUKSINI NAKUVAMBA –Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya wamekutana katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu kwa ajili ya hafla ya kuwakaribisha na kuwatambulisha viongozi wapya waliohamia kuhudumu katika kanda hiyo.

Viongozi waliokaribishwa katika hafla hiyo ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya.

Hafla hiyo, iliongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Said Kalunde na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu, Mahakimu wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo zilizopo Jijini Mbeya.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo alisisitiza umuhimu wa kujenga ushirikiano mzuri kati ya viongozi na watumishi ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi. .

Aidha, aliwahimiza watumishi kuendelea kuendana na maboresho yanayoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania, hususan katika matumizi ya mifumo ya TEHAMA, ambayo imekuwa nyenzo muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma za haki.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, aliwahimiza watumishi kuendelea kudumisha upendo, kuheshimiana na kushirikiana katika kutekeleza majukumu yao.

Pia alisisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, kuhakikisha usafi na usalama wa miundombinu ya Mahakama, kutumia mifumo ya TEHAMA kwa usahihi na kuwajibika kikamilifu katika maeneo yao ya kazi.

Hafla hiyo pia, ilitoa fursa kwa wawakilishi wa watumishi kutoka katika kila Mahakama kutoa salamu za ukaribisho kwa viongozi hao wapya na kuahidi ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya Mahakama.

Aidha, hafla hiyo ya utambulisho na ukaribisho wa viongozi wapya ni hatua muhimu katika kuimarisha mshikamano, kujenga uhusiano mzuri wa kikazi na kuweka msingi wa ushirikiano kati ya viongozi na watumishi.

Vilevile, hutoa fursa ya kuelekeza matarajio ya utendaji, kuimarisha uwajibikaji na kuongeza ari ya pamoja katika kuboresha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi kwa kuzingatia maadili, ueledi na matumizi bora ya mifumo ya kisasa ya Mahakama.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho cha kuwakaribisha Viongozi, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya, na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo akizungumza na watumishi katika kikao hicho. (hawapo pichani) kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Bw. Festo Chonya, akizungumza na watumishi wa kanda ya Mbeya katika kikao hicho. (hawapo pichani)

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika hafla fupi ya kuwakaribisha Viongozi wapya wa Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia kwa makini shughuli zilizokuwa zikiendelea katika kikao hicho.

 

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika hafla fupi ya kuwakaribisha Viongozi wapya wa Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia kwa makini shughuli zilizokuwa zikiendelea katika kikao hicho.

Sehemu ya watumishi walioshiriki katika hafla fupi ya kuwakaribisha Viongozi wapya wa Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia kwa makini shughuli zilizokuwa zikiendelea katika kikao hicho

Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Happines Chuwa (aliyesimama) akitoa neno la shukurani katika kikao hicho kwa niaba ya watumishi.


Afisa Utumishi Mahakama Kuu na Mahakama ya Watoto Mbeya Bw. Ibrahim Mgallah (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho katika kikao hicho.






 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni