Alhamisi, 27 Agosti 2026

MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA ATEMBELEA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA KAZI

Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama ya Kazi, Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, amefanya ziara katika Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, ikiwa ni ziara yake ya kwanza katika Mahakama hiyo tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huo.

Dkt. Jingu aliambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, pamoja na Katibu wa Mtendaji Mkuu, Bw. Thomas Mdenya na Katibu wa Msajili Mkuu, Mhe. Jovin Bishanga.

Ziara hiyo ililenga kujitambulisha rasmi kwa watumishi, kufahamu mwenendo wa utekelezaji wa majukumu na kusikiliza changamoto zinazowakabili katika mazingira yao ya kazi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Dkt. Jingu alisema ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za uongozi wa Mahakama kuendelea kuwa karibu na watumishi na kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu changamoto wanazokutana nazo katika kutekeleza majukumu yao.

Alisisitiza umuhimu wa watumishi kushirikiana na uongozi katika kutafuta suluhisho la changamoto hizo, huku wakizingatia wajibu wao wa kutoa huduma bora, kwa wakati na kwa weledi kwa wananchi.

Katika kikao hicho, watumishi walipata fursa ya kuwasilisha changamoto, hoja na mapendekezo mbalimbali yanayohusu mazingira ya kazi na utekelezaji wa majukumu yao. Dkt. Jingu aliahidi kuzifanyia kazi kwa kuzingatia taratibu na mamlaka zilizopo.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu aliwasihi watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma katika kutekeleza majukumu yao. Alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, mshikamano na misingi ya kazi, akieleza kuwa ushirikiano miongoni mwa watumishi ni muhimu katika kufanikisha malengo ya Mahakama.

Ziara hiyo imeendelea kuonesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuwa karibu na watumishi, kusikiliza changamoto zao na kuweka mazingira bora ya utendaji kazi.

Dhamira hiyo inaenda sambamba na jukumu la Mahakama la kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya haki mapema ipasavyo, kwa ufanisi na kwa kuzingatia misingi ya haki na utawala wa sheria.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt.  John Jingu, akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi (juu na chini).

Mtumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi akitoa hoja kwenye kikao hicho.

Meza Kuu inayoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (katikati).

Picha ya Meza Kuu inayoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (katikati waliokaa) na Viongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi.

Picha ya Meza Kuu inayoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu (katikati waliokaa) na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni