Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Majaji
na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, wametakiwa kuendelea
kudumisha weledi, maadili, mshikamano na mahusiano mema katika utendaji wa
kazi, huku wakihimizwa kuongeza maarifa na kufanya tafiti za kitaalamu kwa
ajili ya kuimarisha weledi katika utoaji haki.
Wito
huo umetolewa katika kikao cha Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA)
Masjala Ndogo ya Mbeya, kilichofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 7 hadi 9
Agosti 2026, katika fukwe za Ziwa Nyasa, Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.
Akizungumza
katika kikao hicho, Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, amewakumbusha
wanachama kuzingatia malengo ya chama hicho, hususan kudumisha hadhi na heshima
baina ya Majaji na Mahakimu, pamoja na kuimarisha maarifa, uelewa na uwezo wao
katika kufanya tafiti za kitaalamu.
“Miongoni
mwa malengo ya TMJA Mbeya ni pamoja na kudumisha hadhi na heshima baina ya
Majaji na Mahakimu na kuimarisha zaidi maarifa, uelewa na uwezo wetu katika
kufanya tafiti za kitaaluma. Hivyo, tupo hapa ikiwa ni sehemu ya kutekeleza
malengo hayo. Tuwe tayari kuzingatia na kujifunza ili tukitoka hapa tuwe
Mahakimu wenye weledi zaidi,” alisema Mhe. Mtulya.
Mhe. Mtulya
pia alisisitiza umuhimu wa kuthaminiana, kujaliana, kuheshimu viongozi,
kuzingatia nidhamu na kuepuka ubaguzi, huku akiwataka wanachama kuendelea
kushikamana kupitia vikundi vilivyoanzishwa kwa ajili ya kusaidiana wakati wa
shida na raha.
Kwa
upande wake, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya,
Mhe. Benard Mpepo, alisisitiza umuhimu wa maadili, mawasiliano na mahusiano
mazuri katika mazingira ya kazi.
“Ili
uwe na utendaji kazi mzuri, ni lazima muwe na mahusiano na mawasiliano mazuri
na viongozi wenu,” amesema Mhe. Mpepo, akiongeza kuwa ni muhimu kujenga
mahusiano mazuri kati ya Majaji, Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama ili
kuboresha utendaji kazi.
Naye,
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, amewataka
watumishi kuepuka ubinafsi, kuzingatia taratibu na itifaki, pamoja na kujenga
utamaduni wa upendo, kujali na kusaidiana, kadhalika amewataka watumishi
kuendelea kumuunga mkono Jaji Mfawidhi katika utekelezaji wa majukumu yake ya
kiuongozi.
Aidha,
Mwenyekiti wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Asha Njovu, amewashukuru
wanachama wanaotekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji,
akiwahimiza kuendelea kudumisha viwango hivyo katika utumishi wao.
Kikao
hicho pia kiliambatana na mafunzo kuhusu mbinu za kukabiliana na msongo wa
mawazo pamoja na umuhimu wa malezi ya kitaaluma kwa Mahakimu (Mentorship Programme) yaliyolenga
kuimarisha uwezo na ustawi wa kitaaluma wa washiriki.
Mbali
na kikao na mafunzo hayo, wanachama walipata fursa ya kuburudika na kushiriki
shughuli za utalii katika fukwe za Ziwa Nyasa, hatua iliyosaidia kuimarisha
zaidi mahusiano na mshikamano miongoni mwa wanachama.
Kikao
hicho ni sehemu ya jitihada za TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya katika kuimarisha weledi,
maadili, mshikamano na uwezo wa kitaaluma wa Majaji na Mahakimu, kwa lengo la
kuendelea kuboresha utoaji wa haki na huduma kwa wananchi.
Mlezi
wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa kwenye kwenye picha ya Pamoja na
viongozi na wanachama wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya wakati wa mafunzo na kikao
hicho.
Mlezi
wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wa pili kushoto) akiwa na viongozi wengine wa Mahakama wakiwa kwenye picha ya pamoja na
wanachama wapya wa TMJA Mbeya
Mlezi
wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wapili kushoto) akiwa na viongozi wengine wakikata
keki kwa pamoja kuwakaribisha wanachama wapya wa TMJA Masjala hiyo.
Mtendaji
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (aliyesimama)
akizungumza katika kikao hicho (katikati) ni Naibu Msajili Mahakama Kuu
Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho, kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Roster Mofuga na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer.
Mwenyekiti
wa TMJA Mbeya Mhe. Asha Njovu (aliyesimama wapili kushoto) akifungua kikao
hicho, (wa kwanza kushoto) ni katibu wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angela
Byera na Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu
Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (Katikati)
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni