Na ARAPHA RUSHEKE & JAMES BUSANYA - Mahakama
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher
Mohamed Siyani, amefanya ziara katika Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua
miundombinu ya Mahakama hiyo, huku akitoa maelekezo mbalimbali yanayolenga
kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.
Ziara
hiyo imefanyika leo tarehe 10 Agosti 2026 wakati alipotembelea Mahakama ya
Wilaya Chamwino iliyoanza kutoa huduma rasmi kuanzia tarehe 24 Julai 2026, ikiwa ni sehemu ya
jitihada za Mahakama ya Tanzania za kusogeza huduma za haki karibu zaidi na
wananchi. Kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama hiyo, huduma za kimahakama kwa
wananchi wa Wilaya ya Chamwino zilikuwa zikitolewa na Mahakama ya Wilaya Dodoma
mjini.
Katika
ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani alikagua jengo na miundombinu ya Mahakama hiyo
pamoja na kuzungumza na watumishi, ambapo alieleza kufurahishwa na jengo hilo
na kuwapongeza waliokuwa wakisimamia ujenzi wake.
“Nimefurahi
leo tuna jengo zuri lenye viwango. Nawapongeza waliokuwa wanasimamia ujenzi
huu. Tumesogeza huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Chamwino. Mahakama hii
itawaletea nafuu, kuwaokolea muda na gharama,” alisema Jaji Kiongozi.
Alisema
kuanzishwa kwa Mahakama hiyo ni hatua muhimu katika kuhakikisha wananchi
wanapata huduma za haki karibu na maeneo yao, akiwataka viongozi wa Mahakama
kuendelea kufikiria namna ya kusogeza huduma kwa wananchi bila kuathiriwa na
mipaka ya kijiografia.
Jaji
Kiongozi aliutaka Uongozi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kushirikiana na
viongozi wa Kata katika maeneo yanayohudumiwa na Mahakama hiyo, ili kuhakikisha
wananchi wanapata taarifa kuhusu huduma zinazotolewa na Mahakama, ikiwemo
kupitia njia za mtandao nakufanya vipindi kwa njia ya Radio.
Aidha,
alisisitiza matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma za Mahakama, akieleza
kuwa teknolojia inaweza kusaidia kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wananchi
na kupunguza utegemezi wa matumizi ya makaratasi.
Katika
kusisitiza matumizi ya TEHAMA, Mhe. Dkt. Siyani aliagiza timu ya wataalum
kuhakikisha huduma za mtandao ziunganishwe
haraka katika Mahakama hiyo ili ziweze kusadifu ubora wa jengo na huduma za
kimahakama kwa wananchi, akieleza kuwa uwepo wa Mkongo wa Taifa wa
Mawasiliano ni fursa inayopaswa kutumika kikamilifu katika kuboresha huduma za
Mahakama.
Alibainisha
pia kuwa, ushahidi unaweza kutolewa katika Mahakama kwa njia ya Mahakama
Mtandao, pale ambapo utaratibu huo unaruhusiwa kisheria, hatua ambayo inaweza
kusaidia kurahisisha mwenendo wa mashauri na kupunguza usumbufu kwa wananchi.
Katika
hatua nyingine, Jaji Kiongozi alisisitiza umuhimu wa Mahakama kuweka mazingira
rafiki na wezeshi kwa wananchi wanaofika kupata huduma, akionya watumishi dhidi
ya kuweka vikwazo visivyo vya lazima, hivyo mwananchi anapofika mahakamani
anapaswa kuhudumiwa kwa wakati.
Mhe.
Dkt. Siyani pia alitoa maelekezo kuhusu utunzaji wa vielelezo na kuvirejesha
kwa wahusika mara baada ya mashauri kukamilika mahakamani, akitaka kuwepo kwa
utaratibu maalum wa kuhakikisha vielelezo hivyo vinatunzwa kwa usalama na
kwamba wenye mali wanarejeshewa kwa kufuata sheria na taratibu zinazokubalika.
Akizungumzia
utunzaji wa mazingira, Jaji Kiongozi alisisitiza kuwa, majengo ya Mahakama
yanapaswa kwenda sambamba na mazingira safi na yanayovutia, akiwataka watumishi
kupanda miti na maua pamoja na kuhakikisha uchafu unaondolewa katika maeneo ya
Mahakama.
“Tusikubali
jengo letu na miundombinu yetu ichakae kwa wepesi. Watumishi tushirikiane
kulitunza jengo letu na kulifanyia usafi. Mazingira yetu ya ndani na nje ya
Mahakama yawe vizuri,”
alisema Dkt Siyani.
Aliagiza
uongozi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kusimamia utekelezaji wa mpango wa
utunzaji mazingira na upandaji miti katika maeneo ya Mahakama, akieleza kuwa
taasisi jirani zinapaswa kuvutiwa na mazingira bora yatakayowekwa na Mahakama
hiyo.
Katika
kuimarisha utendaji kazi, Jaji Kiongozi aliwataka watumishi wa Mahakama ya
Wilaya Chamwino kuwa na utamaduni wa kujifunza, kukumbushana na kufundishana,
akisema kuwa mafanikio yanahitaji watumishi wenye utayari wa kujifunza mambo
mapya kila wakati.
“Kama
mnataka mafanikio muwe na utaratibu wa kukumbushana kwa kufundishana. Watu bora
ni wale wanaojifunza. Msibweteke na mnachokijua, vipo vingine hamvijui. Mnaweza
kufundishana wenyewe mambo mengi na muhimu,” alisema Jaji Kiongozi
Akihitimisha
ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani aliwataka watumishi kujitathmini mara kwa mara
kuhusu namna wanavyowahudumia wananchi na kuhakikisha kila anayefika mahakamani
anapata huduma kwa heshima, weledi, uadilifu na kwa wakati.
Mahakama
ya Wilaya Chamwino inahudumia wananchi wapatao 486,176, Wilaya hiyo inayoundwa na
tarafa tano (5), Kata 36, Vijiji 107 na Vitongoji 814. Kuanzishwa kwa Mahakama
hiyo ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi,
kuwaokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha imani ya wananchi katika mfumo
wa utoaji haki nchini.
Muonekano wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.
(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)













Hakuna maoni:
Chapisha Maoni