Jumanne, 11 Agosti 2026

WATUMISHI IJC DODOMA WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO HIFADHI YA NGORONGORO

Na ARAPHA RUSHEKE – Mahakama, Dodoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Doodoma, Mhe. Joachim Tiganga, hivi karibuni aliwaongoza watumishi kufanya ziara ya mafunzo katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Lengo la ziara hiyo lilikuwa kujifunza kuhusu uhifadhi wa mazingira na wanyamapori, historia, utamaduni pamoja na vivutio mbalimbali vya utalii vinavyopatikana katika eneo hilo.

Ziara hiyo ilijumuisha pia Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Suleimani Hassan, Naibu Wasajili na Watumishi wa Mahakama kutoka Mkoa wa Dodoma na Wilaya zake za Kongwa, Chamwino, Mpwapwa, Chemba na Kondoa.

Wakiwa kwenye ziara hiyo, watumishi hao walipatiwa elimu kuhusu historia ya Hifadhi ya Ngorongoro, wanyamapori wanaopatikana katika eneo hilo, shughuli za uhifadhi pamoja na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika kulinda mazingira na wanyamapori.

Elimu hiyo imewasaidia watumishi kupata uelewa mpana kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na wanyamapori, pamoja na nafasi ya Hifadhi ya Ngorongoro katika kulinda urithi wa Taifa na kukuza utalii nchini.

Watumishi hao walitembelea eneo lenye mchanga unaohama, ambapo walipata maelezo kutoka kwa Bw. Ndengere Ngisaruni kuhusu hali hiyo ya kipekee ya kimaumbile ambayo imekuwa miongoni mwa vivutio vinavyowavutia watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani.

Aidha, watumishi hao walitembelea Olduvai Gorge, eneo maarufu kwa historia ya mwanadamu wa kale, ambapo walipata fursa ya kujifunza kuhusu ugunduzi wa mabaki ya viumbe wa kale na historia ya mwanadamu.

Katika eneo hilo, watumishi walielezwa pia kuhusu historia ya Faru Fausta, aliyefariki akiwa na takribani miaka 57, pamoja na taarifa mbalimbali zinazohusiana na historia ya wanyamapori na urithi wa eneo hilo.

Ziara hiyo pia iliwapa watumishi hao fursa ya kutembelea Boma la Kimasai, ambapo walijifunza kuhusu maisha, mila, desturi na utamaduni wa jamii ya kimasai, pamoja na namna utamaduni huo unavyohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Akitoa shukrani kwa niaba ya watumishi hao, Mhe. Tiganga aliushukuru uongozi wa Hifadhi ya Ngorongoro kwa mapokezi mazuri, ushirikiano na elimu waliyopewa wakati wa ziara hiyo.

Mhe. Tiganga alisema ziara hiyo imekuwa fursa muhimu kwa watumishi kujifunza mambo mapya nje ya mazingira yao ya kawaida ya kazi, huku ikiwapa nafasi ya kujenga mshikamano, kubadilishana uzoefu na kuongeza uelewa kuhusu historia, mazingira na utamaduni wa Tanzania.

Kwa ujumla, ziara hiyo imekuwa sehemu ya kujenga maarifa na mshikamano miongoni mwa watumishi wa Mahakama, sambamba na kuwapa fursa ya kutambua kwa undani zaidi utajiri wa historia, mazingira, wanyamapori na tamaduni zinazopatikana nchini.

Ziara hiyo imehitimisha kwa mafanikio, ikiwaacha watumishi hao na maarifa mapya kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira, wanyamapori, historia na utamaduni wa Tanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Bdogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiwa katika picha ya pamoja na watumishi baadaya ya kuwasili katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akifafanua kitu mara baada ya kuwasili katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akifafanua kitu mara baada ya kufika katika mabaki na masalia ya vitu vya kale.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakipatiwa elimu wakati walipofika katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiendelea na utalii katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiwa na watumishi wakiangalia mabaki ya Faru Fausta aliishi miaka 57.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wakiwa katika picha ya pamoja katika sehemu ya mchanga unaohama uliopo Hifadhi ya Ngorongoro. 

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni