Na ARAPHA RUSHEKE – Mahakama, Dodoma
Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma
(IJC), tarehe 9 Agosti, 2026 walitembelea Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara kwa
lengo la kujifunza, kujenga uelewa kuhusu uhifadhi wa mazingira na kutambua
fursa mbalimbali za utalii zinazopatikana nchini Tanzania.
Ziara hiyo iliongozwa na Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga. Wakiwa kwenye ziara
hiyo, watumishi hao walipata fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu historia,
mazingira, wanyamapori pamoja na shughuli mbalimbali za utalii zinazopatikana
katika hifadhi hiyo.
Akitoa elimu kwa watumishi hao, Afisa Utalii,
Afande Clara Temu, alisema Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara ina ukubwa wa
takribani kilomita za mraba 648.7, ambapo kilomita za mraba 386 ni eneo kavu
huku sehemu nyingine ikiwa ni eneo la Ziwa.
Temu amesema hifadhi hiyo ina vivutio mbalimbali
vinavyowavutia watalii kutoka ndani na nje ya Tanzania, ikiwemo Simba
wanaopanda miti, chemchem za maji ya moto, Ziwa Manyara pamoja na utalii wa
ndege, ambapo hifadhi hiyo ina zaidi ya aina 400 za ndege.
Ameongeza kuwa Ziwa Manyara pia ni muhimu kwa
uhifadhi wa ndege wa majini na ni makazi ya wanyama mbalimbali wakiwemo viboko.
Katika ziara hiyo, watumishi hao walipata fursa
ya kutembelea Tree Canopy Walkway, kivutio kinachowawezesha watalii kutembea
juu ya njia zilizojengwa katikati ya miti na kupata mwonekano wa kipekee wa
mazingira ya hifadhi.
Akitoa maelezo kuhusu kivutio hicho, Muongoza
Watalii Regina Dunduli alisema Tree Canopy Walkway ilijengwa mwaka 2016 na
kuanza kutumika mwaka 2017, ikiwa na madaraja tisa (9) pamoja na majukwaa 10.
Bi. Dunduli alisema kuwa njia hiyo imejengwa
katikati ya miti ikiwemo miti ya mahogany na inawapa watalii fursa ya kuona kwa
karibu aina mbalimbali za ndege, wanyama na mimea.
Alieleza kuwa watu wasiozidi wanne wanaruhusiwa
kutumia sehemu hiyo kwa wakati mmoja, huku watalii wakitakiwa kuzingatia
maelekezo ya waongoza watalii na taratibu za usalama.
Kwa mujibu wa Bi. Dunduli, shughuli hiyo
huchukua kati ya dakika 45 hadi saa moja, huku watalii wakitakiwa kuwa watulivu
na kuzungumza kwa sauti ya chini ili kutowasumbua wanyama.
Watumishi hao pia walielezwa kuwa Hifadhi ya
Taifa ya Lake Manyara inatoa fursa za shughuli mbalimbali za utalii, zikiwemo
walking safari, kuangalia machweo ya jua (sunset viewing), kupiga makasia,
utalii wa ndege pamoja na utalii wa usiku.
Aidha, watalii wanaweza kufanya matembezi marefu
kwa miguu yanayoweza kuchukua kati ya saa moja hadi saa nne, kulingana na aina
ya shughuli wanayochagua. Kwa watalii
wenye mahitaji maalum ya usafiri, pia kuna uwezekano wa kutumia helikopta
kutembelea maeneo mbalimbali ya hifadhi.
Ziara hiyo imewapa watumishi hao fursa ya
kujifunza kwa vitendo umuhimu wa utalii wa ndani, uhifadhi wa mazingira na
matumizi endelevu ya rasilimali za asili, huku ikiwahamasisha kutambua na
kuthamini utajiri wa vivutio vilivyopo nchini.
Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha
watumishi kujifunza nje ya mazingira ya kazi, kujenga uelewa mpana na kuendelea
kuutangaza utalii wa ndani kwa kutembelea na kufahamu vivutio mbalimbali
vinavyopatikana nchini.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni