Jumatano, 26 Agosti 2026

WATUMISHI WANAOFANYA MAJUKUMU YA ZIADA SINGIDA WAJENGEWA UWEZO

Na EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama- Singida

Watumishi wanaofanya majukumu ya ziada Mkoani Singida wamepatiwa mafunzo yaliyosheheni mada mbalimbali kwa ajili ya kuwajengea uwezo ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi.

Watumishi hao 14 wanaonufanika na mafunzo hayo ni Wasaidizi wa Ofisi na Walinzi kutoka Wilaya ya Singida, Manyoni na Iramba ambao mbali na kufanya majukumu ya Kada walizoajiriwa nazo ambazo ni ulinzi na Usaidizi wa Ofisi lakini wamekuwa wakifanya kazi za usaidizi wa kumbukumbu na kuingia Mahakamani.

Akifungua mafunzo hayo tarehe 21 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Singida, Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi aliwapongeza watumishi hao kwa kuwa tayari kufanya majukumu hayo katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa watumishi.

“Watumishi wenzangu kipekee kabisa niwashukuru kwa utayari mliouonesha na kuwa wabunifu kuhakikisha shughuli za kila siku za Mahakama hazikwami, hivyo basi kwa umuhimu tumeona kuandaa mafunzo haya ya kuwajengea uwezo ili kuhakikisha mnatoa huduma bora zaidi kwa wateja na kuhakikisha tunafikia malengo ya taasisi,” alisema Mhe. Kyaruzi.

Aidha, Naibu Msajili huyo aliwasisitiza washiriki kuwa huru wakati wa kuchangia mada na kubainisha maeneo ambayo yanahitaji kuboreshwa kwani Menejimenti inaamini baada ya mafunzo hayo kutakuwa na mabadiliko makubwa katika utendaji kazi.

Mada zilizotolewa ni pamoja na Majukumu ya kila siku katika Masjala za Mahakama za Mwanzo, Masuala ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na matumizi sahihi ya Mashine za kufanyia (POS) na Masuala ya uhasibu hususani kwenye kuandaa taarifa za maduhuli na ujazwaji wa vitabu.

Watoaji wa mada hizo walikuwa ni Bw. Paul Ndonde, Msaidizi wa Kumbukumbu, Bi. Elizabeth Bwaila, Ofisa Hesabu Msaidizi na Bi.Valentina Nkullanga, Ofisa TEHAMA.

Nao washiriki wa mafunzo hayo walishukuru kwa fursa hiyo adhimu ya kupewa nafasi ya kuhuduria mafunzo hayo kwani wamepata uelewa wa mambo mengi na kuhaidi kuacha kufanya kazi kwa mazoea  na kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na weledi.


Watumishi waliohudhuria Mafunzo kutoka Mahakama za Mwanzo zilizopo Wilaya ya Singida, Iramba, na Manyoni. Mafunzo hayo yalifanyika tarehe 21 Agosti, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Singida.

 Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Singida, Mhe. Evodia Kyaruzi (aliyesimama) akifungua  Mafunzo ya kujengeana uwezo kwa Watumishi wa Mahakama (hawapo katika picha) wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo tarehe 21 Agosti, 2026. Kulia ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Singida na Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu Mahakama Singida, Mhe. Aloyce Masua, kushoto ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Singida, Bi.Eva Leshange.
 

Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Utemini, Bw. Paul Ndonde akielekeza jambo kwa watumishi waliohudhuria mafunzo hayo (hawapo katika picha).


Ofisa TEHAMA-Mahakama Kuu SingidaBi. Valentina Nkullanga akielezea  jambo kwa watumishi waliohudhuria mafunzo (hawapo katika picha).


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni