Ijumaa, 11 Septemba 2026

JAJI KAKOLAKI ASISITIZA UMUHIMU WA MAZOEZI KWA WATUMISHI

Na FRANCISCA SWAI – Mahakama, Musoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki, amezindua rasmi utaratibu wa mazoezi kwa watumishi wa Mahakama Musoma kwa kuwasisitiza kuzingatia utaratibu wa mazoezi ya mara kwa mara, kwani mazoezi ni afya, ajira, furaha na ushirikiano.

Katika uzinduzi huo, Mhe. Kakolak, amewashukuru viongozi wa Mahakama Sports Club Musoma kwa kuonesha umahiri wao katika kusisitiza na kufuatilia suala hili.

Aidha, ametoa rai kwa viongozi na watumishi kuhakikisha utaratibu huu wa mazoezi haupotei, bali uwe endelevu kwa ajili ya  kuimarisha afya za watumishi ili waweze kufanya kazi zao kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji.

Aidha, viongozi wa Mahakama Sports Cub Musoma waliwasilisha taarifa yao iliyowashukuru viongozi chini ya mlezi wao, ambaye ni Mtendaji wa Mahakama Musoma Bw. Leonard Maufi, kwa kuwaunga mkono kutafuta Mwalimu wa Mazoezi na kusisitiza utaratibu huu wa mazoezi kwa watumishi kuwa endelevu.

Pamoja na shukrani hizo, walieleza mikakati mbalimbali ya michezo waliyojiwekea ikiwa ni pamoja na kuandaa bonanza la michezo litakalohusisha Mahakama za jirani pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama.

Uzinduzi wa program hii ya mazoezi umefanyika baada ya kuona faida za mazoezi kwa watumishi wa Mahakama Kuu Musoma ambao wamekuwa wakifanya mazoezi ya pamoja kila siku ya Jumanne na Alhamisi jioni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (mwenye kofia), na mbele yake ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Musoma, Bw. Leonard Maufi, wakiwa katika mazoezi yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mahakama Kuu Musoma.

Watumishi wa Mahakama wakiendelea na mazoezi yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mahakama Kuu Musoma.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Tarime wakiwa katika mazoezi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Musoma, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), akiwa pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Musoma, Mhe. Marlin Komba (kulia) na Mhe. Kamazima Idd (kushoto) wakati akiongea na watumishi (hawapo pichani) waliohudhuria uzinduzi rasmi wa mazoezi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni