Ijumaa, 11 Septemba 2026

GEREZA KONGWE LA NGWALA SONGWE LAPOKEA VIFAA VYA TEHAMA

Na IMAN MZUMBWE - Mahakama, Songwe

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Songwe Mhe. Abubakar Amin Mrisha amefanya ziara ya ukaguzi katika Gereza la Ngwala lililopo katika Wilaya ya Songwe mkoani Songwe.

Ziara hiyo iliambatana na tukio la kukabidhi vifaa vya TEHAMA kama vile Televisheni na Kamera kwa ajili ya kuwezesha upatikanaji wa huduma za Mahakama Mtandao ili kurahishisha upatikanaji wa haki kwa wakati mapema ipasavyo kwa Wafungwa na Mahabusu wanaohifadhiwa mahala hapo.

Aidha, Ukaguzi huo unatokana na utekelezaji wa ahadi iliyotolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata alipofanya ziara katika Gereza hilo miezi miwili iliyopita na kubaini changamoto ya usafiri kwa wafungwa na mahabusu kutoka gerezani kwenda mahakamani kwa ajili ya usikilizwaji wa mashauri yao.

“Tumekuja kukabidhi vifaa vitavyosaidia kuweza kutatua changamoto ya usafiri kwa wafungwa na mahabusu kutoka gerezani kwenda mahakamani kupitia matumizi ya vifaa vya TEHAMA maarufu kama Mahakama mtandao,” alisema Mhe. Mrisha.

Mhe. Mrisha alisema kuwa, matumizi ya Mahakama mtandao ni hatua muhimu katika kuboresha utoaji huduma kwa wakati kwani teknolojia hiyo itawezesha baadhi ya taratibu za kimahakama kufanyika kwa njia ya mtandao bila ulazima wa wafungwa na mahabusu kusafirishwa kila mara kutoka gerezani kwenda mahakamani.

Kwa upande, Afisa wa Magereza SP Kassim Akalama alisema kwamba, vifaa hivyo vitasaidia kwa kiasi kikubwa usikilizwaji wa mashauri ya wafungwa na mahabusu pamoja na gharama zingine zinazotumika katika kuwasafirisha kutoka gerezani kwenda mahakamani. 

SP Akalama alisema kwamba, Jeshi la Magereza limepokea vifaa hivyo TEHAMA na vitatumika kama ilivyokusudiwa, hatua hii ni muhimu kwani itasaidia kuboresha huduma za utoaji haki kwa wafungwa na mahabusu na kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati mapema ipasavyo alisema afisa huyo wa magereza.

Ziara hiyo ya kutembele na kukagua gereza hilo ni mwendelezo wa juhudi za Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utendaji kazi wa Jeshi la Magereza, huku matumizi ya TEHAMA yakitarajiwa kuwa nyenzo muhimu katika kupunguza changamoto za utoaji haki kwa wafungwa na mahabusu.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni