Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita
Katika kuendelea
kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha utoaji wa haki nchini,
watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Manyara, wamefanya ziara
ya mafunzo na kubadilishana uzoefu katika Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Geita.
Ziara hiyo iliyofanyika
Septemba 7 na 8, 2026, imelenga kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika uratibu na
uendeshaji wa mashauri, pamoja na shughuli za kiutawala.
Ujumbe wa Mahakama Manyara
uliongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Adam Mambi na ulihusisha Naibu Wasajili,
Mtendaji, Hakimu, Maafisa Rasilimali Watu na Utawala, Mkaguzi wa Ndani,
Madereva pamoja na watumishi wengine kutoka vituo mbalimbali vya Masjala hiyo.
Akizungumza wakati wa
kuupokea ujumbe huo katika Ukumbi wa Mafunzo wa Mahakama Kuu Geita, Jaji
Mfawidhi, Mhe. Projestus Kahyoza, aliwakaribisha na kuwapongeza viongozi na
watumishi wa Manyara kwa kuichagua Geita kuwa kituo cha kujifunza na
kubadilishana uzoefu.
“Tunawakaribisha sana
ndugu zetu kutoka Manyara. Hapa ni mahali sahihi kwenu kujifunza. Tumekuwa
tukiwezesha Mahakama kutoka maeneo mbalimbali kupata mafunzo na kubadilishana
uzoefu katika masuala ya TEHAMA kwa lengo la kuboresha utoaji wa haki. Nanyi
mtajifunza kutoka kwetu na sisi pia tutajifunza kutoka kwenu,” alisema Mhe.
Kahyoza.
Kwa upande wake, Mhe.
Dkt. Mambi aliipongeza Mahakama Kuu Geita kwa mapokezi mazuri na kueleza kuwa
mafanikio yaliyopatikana katika matumizi ya TEHAMA ndiyo yaliyowavutia kufanya
ziara hiyo.
“Tumesikia mambo mazuri
ambayo Wanageita mnayafanya katika mapinduzi ya matumizi ya TEHAMA. Hivyo,
tukaona ni vema tufike tujifunze kutoka kwenu na pia tushirikiane uzoefu wa
Masjala zetu ili tuboreshe utendaji wetu wa kila siku,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.
Katika ziara hiyo,
watumishi wa Mahakama Kuu Geita, waliwasilisha mada mbalimbali kuhusu matumizi
ya TEHAMA katika shughuli za kimahakama na kiutawala.
Miongoni mwa mada
zilizowasilishwa ni matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa mashauri, unaowezesha
uendeshaji wa mashauri kwa njia ya kielektroniki bila kutegemea matumizi ya
karatasi. Mada hiyo iliwasilishwa na Naibu Msajili wa Masjala Ndogo Geita, Mhe.
Fredrick Lukuna.
Washiriki pia walijifunza
namna Mahakama za Wilaya zinavyotumia mifumo ya TEHAMA katika kutekeleza
shughuli za kimahakama na kiutawala, pamoja na hatua zinazochukuliwa na
Mahakama za Mwanzo katika kupunguza matumizi ya karatasi, kupitia mfumo
wa Mahakama za Mwanzo Electronic Register.
Aidha, washiriki walipata
fursa ya kujifunza namna huduma ya Kiosk inavyofanya kazi kwa
kuwasaidia wananchi ambao hawana uelewa wa kutosha kuhusu matumizi ya TEHAMA
ili waweze kupata huduma za kimahakama kwa urahisi. Mada hiyo iliwasilishwa na
Afisa Kumbukumbu, Bi. Winfrida Warsha.
Kwa upande wa shughuli za
kiutawala, Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, aliwasilisha mada
kuhusu namna Mahakama hiyo ilivyopunguza na kuachana na matumizi ya karatasi
katika shughuli mbalimbali za kiutawala kupitia matumizi ya mifumo ya
kielektroniki.
Naye Afisa TEHAMA, Bw.
Dotto Nkaja, aliwasilisha mifumo mbalimbali iliyobuniwa na Mahakama Geita kwa
lengo la kurahisisha upatikanaji, uhifadhi na matumizi ya taarifa za
kimahakama. Mifumo hiyo ni pamoja na Geita Repository Database, Geita
Electronic Visitors na Geita Legal Decisions.
Katika kuendeleza mafunzo
hayo, Septemba 8, 2026, Mhe. Dkt. Mambi, aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya
teknolojia za kisasa, ikiwemo Akili Bandia (Artificial Intelligence – AI),
katika kufanya tafiti za kimahakama pamoja na maadili yanayopaswa kuzingatiwa
katika matumizi ya AI wakati wa tafiti na uratibu wa mashauri mahakamani.
Mada hiyo iliwapa
washiriki fursa ya kutafakari namna teknolojia mpya zinavyoweza kutumika
kuongeza ufanisi katika shughuli za Mahakama, huku wakizingatia misingi ya
maadili na utoaji wa haki.
Akitoa neno la shukrani
kwa niaba ya ujumbe huo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Manyara,
Mhe. Charles Mnzava, aliwapongeza watumishi wa Geita kwa bidii na weledi wao,
akieleza kuwa juhudi hizo zimechangia kuboresha utendaji kazi na kupunguza
mlundikano wa mashauri.
“Kwa kweli tumeona
jitihada zenu katika usikilizwaji wa mashauri ya kila siku, lakini pia katika
usimamizi wa rasilimali. Tunaahidi kutumia elimu tuliyoipata katika kuboresha
utendaji wetu tutakaporejea Manyara,” alisema Mhe. Mnzava.
Ziara hiyo imehitimishwa
kwa viongozi wa Masjala hizo mbili kuweka mikakati ya kuimarisha uhusiano na
ushirikiano kati yao, ikiwemo kuanzisha utaratibu wa kuwa “Kanda
Rafiki” katika masuala ya kikazi, kijamii na kiutawala.
Aidha, Uongozi wa
Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Geita, umeahidi kufanya ziara ya kimafunzo
katika Mkoa wa Manyara hivi karibuni. Hatua hiyo inatarajiwa kuendeleza na
kuimarisha utamaduni wa kujifunza, kushirikishana uzoefu na kubadilishana mbinu
bora za utendaji kazi ndani ya Mahakama.
Ziara hiyo ni sehemu ya
jitihada za kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika Mahakama na kuhakikisha
teknolojia inatumika ipasavyo katika kuongeza ufanisi, kurahisisha upatikanaji
wa huduma za haki na kuboresha utoaji wa haki kwa wananchi.
Naibu Msajili wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna,
akieleza namna Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri unavyorahisisha
usikilizaji na uendeshaji wa mashauri, pamoja na kupunguza matumizi ya karatasi
mahakamani.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Geita, Bi. Masalu Kisasila, akielezea namna matumizi ya TEHAMA yanavyorahisisha na kuboresha utekelezaji wa shughuli za kiutawala Mahakamani.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Manyara, Mhe. Charles Mnzava, akitoa shukrani baada ya kukamilika kwa mafunzo.
Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (kulia) na Mhe. Griffin Mwakapeje (kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi.








Hakuna maoni:
Chapisha Maoni