.Asisitiza Ushirikiano katika kuimarisha utendaji kazi
Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya amefanya
ziara ya kikazi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Jumanne Abdallah
Sagini, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuimarisha ushirikiano na uhusiano baina
ya Mahakama na Ofisi hiyo ili kuwezesha utendaji bora wa shughuli za kimahakama.
Ziara
hiyo imelenga pia kujitambulisha kwa Mkuu wa Mkoa pamoja na kujadili changamoto
mbalimbali za kiutawala zinazohusiana na utendaji wa Mahakama katika Masjala
hiyo, hususan masuala yanayohitaji ushirikiano na mamlaka za Serikali ya Mkoa,
Halmashauri, Kata na Vijiji.
Akizungumza
katika ziara hiyo, Mhe. Mtulya, alieleza kuwa baadhi ya maeneo na miundombinu
ya Mahakama katika Mkoa wa Mbeya yamekuwa yakiingiliwa na mamlaka nyingine bila
ushirikishwaji wa Mahakama, hali ambayo inaweza kuathiri matumizi na ulinzi wa
mali na maeneo ya Mahakama.
Katika
ziara hiyo, Jaji Mfawidhi pia alitoa pongezi kwa Diwani wa Kata ya Makongolosi
kwa jitihada za kuwashirikisha wananchi na wadau mbalimbali katika ujenzi wa
jengo jipya la Mahakama ya Mwanzo Makongolosi, baada ya jengo la awali
kuharibiwa wakati wa ghasia zilizotokea kipindi cha uchaguzi Mkuu mwishoni mwa
mwezi Oktoba 2025.
Akizungumzia
utekelezaji wa Nguzo ya Tatu ya Mpango Mkakati wa Mahakama, inayolenga
kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama na ushirikishwaji wa wadau, Jaji
Mfawidhi alibainisha kuwa Mahakama Kuu Mbeya imeendelea kuwa na ushirikiano
mzuri na wadau mbalimbali wa haki, wakiwemo Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza,
TAKUKURU na taasisi nyingine zinazohusika katika mfumo wa utoaji haki.
Kwa
upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Jumanne Abdallah Sagini, amemshukuru
Jaji Mfawidhi kwa ziara hiyo na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha
ushirikiano baina ya Ofisi yake na Mahakama.
Mhe.
Sagini amesema ziara hiyo imempa fursa ya kupata taarifa na uelewa zaidi kuhusu
baadhi ya changamoto zinazoikabili Mahakama katika Mkoa wa Mbeya na kwamba
Ofisi yake iko tayari kushirikiana na Mahakama katika kuzitafutia ufumbuzi.
“Nashukuru
kwa ujio wenu na kunifungua macho katika baadhi ya mambo ambayo sikuyafahamu
katika mkoa wangu na kunipa mwanga wa namna ya kuyafanyia kazi. Naahidi
ushirikiano mkubwa kwa Mahakama na pale uonapo masuala yangu ya kiutawala
yanakwamisha utendaji wa shughuli za kimahakama, milango iko wazi,
nakukaribisha wakati wowote kuweza kurekebisha hilo,” alisema Mhe. Sagini.
Mkuu wa
Mkoa pia ameeleza kuwa Serikali ya Mkoa itafuatilia migogoro na changamoto
zilizobainishwa, huku akimuagiza Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya, Bw. Festo Chonya, kuwasilisha taarifa rasmi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
inayoainisha maeneo yenye changamoto za kiutawala katika Mkoa wa Mbeya, ili
kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa katika kuzitatua.
Hatua
hiyo imetia msisitizo wa kuendelea kujenga ushirikiano wa karibu, mawasiliano
na mahusiano ya kikazi kati ya Mahakama na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, hatua
inayotarajiwa kuchangia katika kuondoa vikwazo vya kiutawala na kuweka
mazingira bora kwa Mahakama kutekeleza jukumu lake la msingi la utoaji wa haki
kwa wananchi.
Viongozi
wengine walioambatana na Mhe. Mtulya, katika ziara hiyo ni Naibu Msajili
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Naibu
Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer, Mtendaji wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, Afisa Utumishi
Mwandamizi wa Mahakama Kuu Mbeya, Bw. Alintula Ngalile na Msaidizi wa Sheria wa
Jaji Mfawidhi Mhe. Jane Mwaitumile.
Mkuu wa
Mkoa wa Mbeya, Mhe. Jumanne Abdallah Sagini (wanne kulia) akiwa kwenye picha ya
pamoja na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
walipotembelea ofisini kwake wakiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wanne kushoto).
Mtendaji
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, (aliyesimama) akijitambulisha
kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Jumanne Abdallah Sagini, Kulia ni Naibu Msajili
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.
Mkuu
wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Jumanne Abdallah Sagini akiwa ofisini kwake akiwasikiliza
Viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya (hawapo pichani) walipotembelea
ofisini kwake.
Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, akiwasili
katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mbeya.
Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya akitia sahihi
kitabu cha wageni wakati alipowasili ofisini ya Mkuu wa Mkoa Mbeya.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni