Jumatatu, 14 Septemba 2026

MAHAKAMA KIGOMA YAKUTANA NA WADAU KUWEKA MIKAKATI YA KUMALIZA MASHAURI YA MAUAJI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma imefanya kikao maalum cha maandalizi (pre-session) kilichoongozwa na Jaji wa Kanda hiyo, Mhe. John Francis Nkwabi kwa lengo la kuweka mikakati madhubuti ya kumaliza mashauri nane ya mauaji yaliyopangwa kusikilizwa Wilayani Kasulu mkoani humo tarehe 21 Septemba, 2026.

Katika kikao hicho kilichofanyika tarehe 11 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma kiliwaunganisha wajumbe wa haki jinai kwa njia Mahakama Mtandao (Virtual Court) ambapo Mhe. Nkwabi aliwakumbusha wadau wote kutimiza wajibu wao kwa uadilifu mkubwa ili wananchi waweze kuona na kupata haki kwa mapema ipasavyo.

Jaji Nkwabi alisema, hatua hiyo itasaidia kuimarisha amani na usalama katika jamii, na kueleza kuwa, ratiba maalum ya usikilizwaji wa mashauri hayo nane imepangwa kwa umakini ili kuzuia kuahirishwa kwa mashauri bila sababu za msingi.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa aliwashukuru Wadau kwa ushiriki wao na ushirikiano mkubwa waliotoa kwa Mahakama ili kuendelea kutimiza majukumu yake ya kusikiliza mashauri.

Kwa upande wake Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusufu Kasuka ameahidi juu ya uwepo wa vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya kurahisisha usikilizwaji wa mashauri hayo ikiwa ni sambamba na kutoa uwezesho kwa watumishi na Mawakili upande wa utetezi katika mashauri hayo.

Aidha, Wadau walikubaliana kuimarisha mawasiliano na ushirikiano wa karibu na Mahakama, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na upande wa utetezi ili kuhakikisha ushahidi na vielelezo vinawasilishwa kwa wakati.

Kikao kilisisitiza kuhusu umuhimu wa kutumia kikamilifu vikao vya maandalizi ili kupunguza muda unaotumika mahakamani na kuharakisha usikilizwaji wa mashauri ya jinai, hasa ya mauaji.

Kikao hicho kilichowahusisha Waendesha Mashtaka wa Serikali, Mawakili wa utetezi na Maofisa Magereza na Polisi kililenga kuondoa vikwazo vyote vya kiutawala na kiufundi vinavyoweza kuchelewesha mwenendo wa mashauri hayo, na hivyo kuhakikisha haki inatendeka mapema ipasavyo.

 


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. John Nkwabi (katikati) akiongoza kikao cha pamoja na Wadau wa Mahakama Kigoma. Aliyeketi kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusufu Kasuka, wakifuatilia kwa makini hoja za wadau walizokuwa wakitoa kupitia Mahakama Mtandao wakati wa kikao kilichofanyika tarehe 11 Septemba, 2026.


Wajumbe wa Kikao  cha Tathmini ya maandalizi ya kikao cha mashauri ya mauaji waliojiunga kwenye kikao kwa njia ya Mahakama Mtandao wakiwa katika Taasisi zao. Kikao hicho kilifanyika tarehe 11 Septemba, 2026.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. John Francis Nkwabi akisikiliza kwa makini Mdau wa Haki Jinai alipokuwa akiwasilisha mchango wake kwenye kikao cha tathmini ya maandalizi ya kikao cha mashauri ya mauaji kilichofanyika tarehe 11 Septemba, 2026.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akifafanua jambo wakati wa kikao cha tathmini ya maandalizi ya kikao cha mashauri ya mauaji mkoani humo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma, Bw. Yusufu Kasuka akifuatilia kwa makini mjadala uliokuwa ukiendelea kwenye kikao cha tathmini ya maandalizi ya kikao cha mashauri ya mauaji.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni