Jumanne, 8 Aprili 2025

BARAZA LA WAFANYAKAZI MAHAKAMA KUU MASJALA KUU LAFANYIKA

Na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama Kuu Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani   leo tarehe 8 Aprili, 2025 amefungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu, Masjala Kuu kujadili mambo mbalimbali ambayo wanakutana nayo kazini.

Baraza hilo limefanyika kikao katika Ukumbi wa Mikutano uliopo katika Hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhe. Dkt Siyani ambaye ni Mwenyekiti aliwaambia wajumbe kuwa mabaraza hayo ni muhimu kwani yanawapa fursa ya kutoa maoni na ushauri kuhusu nini kinatakiwa kifanyike katika kuboresha mazingira mazuri mahala pakazi.

Kadhalika, Jaji Kiongozi aliwaeleza wajumbe wa Baraza hilo kuwa ili madhumuni ya uwepo wake yatimie, mazingira ya ushiriki na ushirikishwaji wa Wafanyakazi lazima yawe mazuri.

“Kwa Taasisi kama Mahakama, uwepo wa mazingira rafiki yanayowezesha Watumishi kuelewa umuhimu wa Mabaraza ya Wafanyakazi na kudiriki ni muhimu sana,” alisema Dkt.Siyani.

Alisema pia kuwa Viongozi ni lazima waelewe juu ya umuhimu wa kuweka mazingira mazuri yasiyowajengea Watumishi hofu ya kutoa malalamiko, maoni na kushauri.

Jaji Kiongozi alisema kuwa uwezo wa kushiriki na kushirikisha wengine ni sifa muhimu kwa Kiongozi, kwani ukuaji wa Taasisi hautokani na mawazo ya mtu mmoja.

Aliwataka kusimamia maelekezo yote yanayotolewa na Viongozi katika kuhakikisha na kurahisisha kazi kama ambavyo sheria na taratibu zinavyowakataka.

Alimaliza kwa kuwapongeza kwa mafanikio ambayo Mahakama imeendelea kuyapata katika utekelezaji wa jukumu lake la msingi la utoaji haki.

“Ninatarajia kupitia majadiliano katika Baraza hili mtapata fursa ya kuweka mikakati ya kuimarisha zaidi utoaji haki. Baraza hili liwe kioo cha kujitazama na hivyo kurekebisha pale ambapo hatukufanikiwa kama mnavyojua, kwa kufanya hivyo malengo ya uwepo wa Baraza hili yatakuwa yamefikiwa,” alisema Dkt. Siyani.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt.Mustapher Siyani akizungumza wakati wa ufunguzi wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu Masjala Kuu lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Rafiki Hoteli uliopo Jijini Dodoma.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Siyani (aliesimama) akizungumza wakati wa ufunguzi wa Baraza hilo.
Sehemu ya wajumbe wa kikao hicho wakisikiliza kwa umakini wakati wa kikao hicho.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

BARAZA LA WAFANYAKAZI WA MAHAKAMA KANDA YA DAR ES SALAAM LAFANYIKA

Na MWANAIDI MSEKWA-Mahakama, Kazi

Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam hivi karibuni ilifanya kikao cha Baraza la Wafanyakazi kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji.

Baraza hilo ambalo lilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani, liliongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, Mhe. Ngunyale, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo aliwashukuru Viongozi wote waliowezesha kufanyika kwa Baraza hilo.

Baraza la Wafanyakazi ni chombo muhimu kinachowakutanisha meza moja Wafanyakazi pamoja na Uongozi ambao ni Mwajiri kwa ajili ya kujadili, kutathimini na kuangalia ustawi wa Wafanyakazi na thamani ya Mfanyakazi na ya yule anaye hudumiwa,’ alisema.

Alieleza pia kuwa Baraza hilo ni muhimu ambalo kila mmoja anahitaji ushiriki wa pekee kwa kutoa maoni na kuhoji ili kuweza kujenga malengo mahususi yanayohusu Wafanyakazi, mazingira ya kazi, nidhamu na kujengeana uwezo.

Mwenyekiti huyo aliwapongeza Watumishi katika ngazi zote za Mahakama, Kanda ya Dar es Salaam kwa kazi nzuri wanazofanya kwani kazi kubwa imefanyika na mafanikio yanaonekana.

‘Changamoto za watu wasio wajibika ni chache sana katika maeneo ya kazi na ambazo zinashughulikiwa kwa ukaribu na kuhakikisha hazileti athari zinazoweza kuleta madhara kwa Wananchi wanaotegemea huduma katika Mahakama,’ Jaji Ngunyale alisema.

Aliwataka kusimamia maelekezo yote yanayotolewa na Viongozi, akiwemo Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi na wengine kupitia waraka mbalimbali katika kuhakikisha kazi zinaenda kwa jinsi ilivyopangiliwa.

Jaji Ngunyale alitumia fursa hiyo kuwakumbusha msisitizo wa Jaji Mkuu kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA- ili kurahisisha kazi na kuwafikia Wananchi kwa kupitia mifumo iliyopo.

Kufanya hivi inasaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri, lengo ni kuhakikisha kuwa Mwananchi hatumii gharama kubwa katika kuendesha kesi yake,’ alisema.

Katika mkutano huo, Mtendaji wa Mahakama, Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Moses Mashaka aliwasilisha taarifa ya utendaji, matumizi ya teknolojia na hali ya miundombinu ya majengo ya Mahakama inayoendelea kuboreshwa.

Naye Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Mary Moyo alielezea hali ya uendeshaji na takwimu za mashauri na kuwahimiza Mahakimu kuongeza kasi ya uondoshaji mashauri na kuongeza jitihada za makusudi katika kila ngazi ya Mahakama ili kufikia malengo ya kitaifa kwa kupunguza au kuondoa kabisa mlundikano.

Kwa kutambua na kuthamini jitihada na mchango wa Watumishi katika utendaji kazi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi alimchagua Bi. Riziki Sakoro, ambaye ni Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Bungu, Wilaya ya Kibiti katika Mkoa wa Pwani, kuwa Mfanyakazi Bora wa Kanda kwa mwaka 2025.

 

Meza Kuu ikiongoza kuimba Wimbo wa Mshikamano, katikati ni Mwenyekiti wa Baraza, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. David Ngunyale, aliyeshika kipaza sauti ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi na upande wa kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa Pwani Mhe. Joyce Mkhoi.

Wajumbe wakiwa katika kikao.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Moses Mashaka akiwasilisha taarifa ya utendaji wa shughuli za kimahakama.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Mary Moyo akielezea hali ya uendeshaji na takwimu za mashauri.

Mfanyakazi Bora Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Riziki Sakoro, ambaye ni Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Bungu, Wilaya ya Kibiti katika Mkoa wa Pwani.



Meza Kuu pamoja na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dar es Salaam -picha mbili juu na picha mbili chini-wakiwa katika picha ya pamoja.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

 

 

 

 

 

 

  

JAJI MFAWIDHI DIVISHENI YA ARDHI AONGOZA KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na DHILLON UISSO-Mahakama, Ardhi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda, hivi karibuni aliwaongoza Watumishi kufanya kikao cha Baraza la Wafanyakazi cha mwaka 2025.

Akifungua kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Wazi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Luvanda aliwaambia Watumishi hao kuwa Mabaraza hayo ni muhimu kwani yanawapa fursa ya kutoa maoni na ushauri kuhusu nini kinatakiwa kifanyike katika kuboresha mazingira ya mahala pakazi.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi aliwaelezea kuwa vikao vya mabaraza hayo vinafanyika mara chahe kwa mwaka, hivyo ni muhimu kwa Watumishi kuchangia Mawazo chanya ili kuboresha maslahi yao.

Akizungumza na wajumbe katika kuchangia hoja ya utawala na mashauri, Mhe. Luvanda alisisitiza kuwa Chama cha Wafanyakazi ni chombo muhimu kwa ajili ya kusimamia maslahi mapana ya Wafanyakazi.

Pamoja na hilo, Jaji Mfawidhi alisisitiza Viongozi wa TUGHE Tawi kushiriki mafunzo mbalimbali ili kuwa mabalozi wazuri kwa Watumishi wengine kujiunga na Chama hicho kwa maslahi mapana ya kusimamia hoja za Watumishi.

Kiongozi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Bw. Shaibu Kanyochole alisema kuwa miongoni mwa hoja zilizotolewa na Watumishi wa Mahakama ni pamoja na kupatiwa mafunzo ya mara kwa mara kwa ajili ya kuongeza motisha ili waweze kwenda na mabadiliko ya matumizi ya TEHAMA ambayo yanajitokeza kwa sasa na kuongezewa vitendea kazi.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu wa TUGHE Mkoa wa Dar es Salaam, Bi. Grace Magereli aliwashauri wajumbe kujenga hoja zao vizuri ili zitakapopelekwa katika Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi Taifa ziweze kujibiwa vizuri na Viongozi.

 Aliendelea kufafanua na kushauri Watumishi kujiunga kwenye chama kwa lengo la kuwa na nguvu ya pampoja ili chombo hicho kiweze kuongea kwa nguvu zaidi na kubeba hoja zitakazopelekwa TUGHE Taifa.

Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi wameweza kushiriki katika kikao hicho cha kujadili masuala mbalimbali ya kiutumishi, bajeti na ikiwa ni maandalizi ya Kikao kitakachofanyika Dodoma tarehe 10 na 11 Aprili, 2025.

Kwa upande wake, Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Bw. Peter Mbaguli alizitolea ufafanuzi baadhi ya hoja ambazo zinaweza kutatulika ndani ya Divisheni na kuahidi kuwasilisha kwenye Baraza Kuu hoja ambazo zitahitaji majibu ya mwajiri.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi.

Mjumbe wa TUGHE Mkowa wa Dar es Salaam, Bi. Grace Magereli.

Kaimu Mtendaji wa Divisheni ya Ardhi, Bw. Peter  Mbanguli.

Kaimu katibu wa Baraza, Bi. Tumaini Mwalyoga.

Mjumbe wa TUGHE Mahakama ya Tanzania Bw. Kilenza.

Picha za wajumbe wa Baraza la Wafanya Kazi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro

 

JAJI MFAWIDHI TANGA AONGOZA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na MUSSA MWINJUMA-Mahakama Kuu Tanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Katarina Revocati Mteule hivi karibuni aliongoza Baraza la Wafanyakazi kwenye Kanda hiyo kujadili mambo mbalimnbali ya kiutendaji.

Akifungua mkutano wa Baraza hilo uliofanyika kwenye Ukumbi wa Wazi wa Mahakama Kuu Tanga, Mhe. Mteule aliwashukuru wajumbe wote kufika kwa wakati pamoja na kwamba wengine wanatoka mbali.

Mhe. Jaji Katarina ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo aliwakumbusha wajumbe umuhimu wa uwepo wa Baraza hilo kwani ni jukwaa la kujadili mambo mbalimbali muhimu yanayowahusu wafanyakazi.

 “Baraza la Wafanyakazi ni chombo ambacho wajumbe hutoa maoni, ushauri, mapendekezo na hata kukosoa kwa niaba ya Watumishi wengine ambao hawako hapa ili michango hiyo iingie kwenye utekelezaji wa shughuli za Mahakama, usiwe hapa kwa ajili ya kuongea matatizo yako binafsi ya kiutumishi,” alisema

Naye Afisa Kazi, Bw. Juma Mkali aliwapitisha wajumbe kwenye umuhimu,d humuni la mabaraza ya wafanyakazi. Pia aliwapitisha katika sheria mbalimbali za uundwaji wa mabaraza na kazi zake, ikiwemo ushauri juu ya maslahi ya wafanyakazi, utaratibu wa vyeo na nidhamu, kupokea na kujadili mapato na matumizi ya Taasisi.

Katika mkutano huo kulifanyika uchaguzi wa Katibu na Naibu Katibu kwa mujibu wa sheria za uundwaji wa baraza zinavyotaka ambapo Bw. Alinani Mwaiswelo alichaguliwa kuwa Katibu na Mhe. Bahati Manongi akiwa Naibu Katibu. Naye Bw. Farid Mnyamike ambaye ni Afisa Utumishi wa Kanda hiyo alichaguliwa kuwa mwakilishi wa Wafanyakazi katika Baraza la Wafanyakazi Taifa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Mhe. Katarina Revocati Mteule (katikati) akiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi, kushoto kwake ni Jaji Messe Chaba na kulia kwake ni Katibu wa Baraza, Bw. Alinani Mwaiswelo na mwisho ni Naibu Katibu, Mhe. Bahati Manongi.

Sekretarieti ya Baraza la Wafanyakazi Mhe. Hudi Majid Hudi (mwenye suti) Naibu Msajili Mahakama Kuu Tanga na Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Tanga, Bi Subira Mwishashi.

Baadhi ya wajumbe wa Mkutano wa Baraza wakimsikilzia Jaji Mfawidhi Katarina Revocati Mteule (hayupo pichani).

Wajumbe wa Baraza wakiendelea na kikao.

Bw. Farid Mnyamike ambaye amechaguliwa kuwa mwakilishi wa Wafanyakazi katika Baraza la Wafanyakazi Taifa akitoa shukrani zake kwa wajumbe baada ya kuchaguliwa.

Bi. Alice Haule ambaye ni Mwenyekiti TUGHE Taifa-Mahakama, akichangia mada katika mkutano huo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.

Jumatatu, 7 Aprili 2025

JAJI KAINDA AFUNGUA MAFUNZO YA USIMAMIZI WA NYARAKA NA KUMBUKUMBU KIELEKTRONIKI

  • Lengo  ni kuwajengea uwezo Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama- Arusha

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha na mgeni rasmi, Mhe. Sylvester Kainda amefungua mafunzo ya Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu kwa njia ya Kielektroniki ambayo yameanza kutolewa leo tarehe 07 Aprili, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Akizungumza na Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama ya Rufani, Masjala ndogo za Mahakama ya Rufani zilizopo katika Kanda mbalimbali na Zanzibar kwa niaba ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Kainda ameeleza kuwa, lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo walengwa hao katika kutekeleza majukumu yao kwa kutumia mifumo ya kidigiti na hatimaye kutoa huduma bora za kimahakama kwa njia ya mtandao.

“Miongoni mwa maboresho ambayo Mahakama imeyafanya ni matumizi ya TEHAMA katika mifumo yake mbalimbali ya utoaji huduma kwa wananchi, hivyo matumizi ya Teknolojia yanalenga kuboresha utendaji kazi na ufanisi wa huduma tunazotoa,” alisisitiza Mhe. Kainda.

Katika maelezo ya awali, Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu amesema kuwa, kwa sasa Mahakama inatumia mifumo mbalimbali ya kielektroniki kama vile mifumo ya uendeshaji mashauri, mifumo ya manunuzi na ya malipo na kadhalika.

Bi. Patricia ameongeza kwamba, ili mifumo hii na mingine itakayojengwa iweze kutumika vizuri, inahitaji Mahakama iwatayarishe watumishi wake kwa kuwapatia maarifa na ujuzi wa kuitumia, hivyo mafunzo hayo ni sehemu ya kuwatayarisha na kuwawezesha watumishi kutumia mifumo hiyo ipasavyo.

Wasaidizi wa Kumbukumbu hao wamesisitizwa juu ya umuhimu wa kuwa na uelewa mkubwa wa matumizi ya mifumo ya kidigiti ili kuwezesha Mahakama ya Rufani kuwa na watumishi wenye ujuzi zaidi wa namna ya kutekeleza majukumu yao kwa kutumia mifumo ya kielektroniki.

Wawezeshaji katika Mafunzo hayo ni kutoka Chuo cha Upskill Training Institute cha Nairobi Kenya na mada mbalimbali zinazohusiana na Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu kwa njia ya Mtandao  zitafundishwa kwa njia ya vitendo zaidi ili walengwa waweze kupata maarifa yaliyokusudiwa.

Mafunzo hayo yatatolewa kwa kipindi cha wiki mbili kwa makundi mawili tofauti ya Wasaidizi wa Kumbukumbu kwa awamu ambapo jumla ya Wasaidizi wa Kumbukumbu 62 watanufaika na mafunzo hayo.

Ufunguzi wa mafunzo hayo, umehudhuriwa na watu mbalimbali wakiwemo Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati na Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Arusha, Bi. Asha Abdallah.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sylvester Kainda akizungumza leo tarehe 07 Aprili, 2025 wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC).



Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama ya Rufani, Masjala ndogo za Mahakama ya Rufani zilizopo katika Kanda mbalimbali na Zanzibar wakipatiwa mafunzo ya Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu kwa njia ya kielectroniki yaliyoanza kufanyika leo tarehe 07 Aprili, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Mgeni rasmi katika Mafunzo ya Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu, Mhe. Sylvester Kainda (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha leo tarehe 07 Aprili, 2025.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sylivester Kainda (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wawezeshaji wa Mafunzo Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu yaliyofanyika leo tarehe 07 Aprili, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha. Walioketi kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati na kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo Mahakama ya Tanznia, Bi. Patricia Ngungulu (kulia). Waliosimama ni wakufunzi wa mafunzo kutoka chuo cha Upskill Nairobi Kenya. (kushoto Kwenda kulia) Bw. Amos Kamau, Bi. Evelyn Mwihaki na Bw. Shadrack. Odondi. 

Mgeni rasmi katika Mafunzo ya Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu ambaye ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Sylvester Kainda (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wawezeshaji wa Mafunzo hayo yaliyoanza kufanyika leo tarehe 07 Aprili, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa IJC Arusha. Walioketi ni kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Sophia Massati (kushoto) na kuia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo Mahakama ya Tanznia, Bi. Patricia Ngungulu. Waliosimama ni Sekretarieti katika mafunzo hayo kutoka Makao Makuu ya Mahakama Dodoma. Kutoka kushoto ni Bw. Nazar Moshi, Bi. Doris Kaniki na Bw. Rajab Singana.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


MFUMO WA USAJILI WA TAARIFA ZA WATEJA NA MAWAKILI WABORESHA HUDUMA DIVISHENI YA BIASHARA

Na AMINA SAID, Mahakama Kuu-Divisheni ya Biashara

Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara imeendelea kuvuna mafanikio makubwa kupitia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ambapo Mfumo wa Usajili wa Taarifa za Wateja na Mawakili umeleta mapinduzi katika utoaji wa huduma kwa wateja wa Mahakama hiyo.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bw. Edward Mbara, alieleza jinsi mfumo huo unavyosaidia katika ufuatiliaji na uboreshaji wa huduma.

"Kwakuwa mfumo huu unarekodi taarifa za wateja zikiwemo namba za simu, siku moja nilipitia takwimu na kupata mteja mmoja aliyekaa mahakamani zaidi ya masaa Matano, nilimpigia simu kutaka kufahamu kwanini alitumia muda mrefu, akanijibu kwamba alikuwa maktaba anajisomea nyaraka mbalimbali," alisema Bw. Mbara.

Aidha, aliongeza kuwa mfumo huo umesaidia kuongeza ufanisi kwa kuwawezesha viongozi wa Mahakama kufahamu kwa undani aina ya wateja wanaohudumiwa, jambo linalorahisisha utoaji wa huduma bora na kwa wakati.

Katika kikao hicho, Mtendaji huyo aliweka bayana vipaumbele vya Mahakama hiyo kwa robo mwaka unaofuata, ambavyo ni pamoja na Kumaliza mashauri ya mlundikano, kuboresha na kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) sambamba na kuwajengea uwezo watumishi juu ya matumizi ya mifumo Teknolojia.

Vipaumbele vingine ni kulipa stahiki za watumishi na watoa huduma pamoja na kufanya vikao vya kusukuma mashauri na vikao vya utawala

Baraza hilo pia lilihusisha uchaguzi wa Naibu Katibu wa Baraza la Wafanyakazi ambapo, Bi. Fullness Katekela na Bi. Tausi Mwambujule walichuana kuwania nafasi hiyo. Katika uchaguzi huo ulioshirikisha jumla ya wajumbe 21, Bi. Fullness alipata kura 11 na Bi. Tausi alipata kura 10. Hivyo, Bi. Fullness Katekela alitangazwa mshindi na kuchukua nafasi ya Naibu Katibu wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama hiyo.

Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mhe. Jaji Cyprian Mkeha aliwapongeza Majaji kwa kazi kubwa ya kusikiliza na kuamua mashauri kwa kasi na ufanisi mkubwa, hali iliyosaidia Mahakama hiyo kuendelea kuonesha mafanikio makubwa.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Baishara ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Cyprian Mkeha  (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza jambo wakati wa kikao cha Baraza la Mahakama hiyo kilichofanyika hivi karibuni.


Katibu wa Baraza (katikati), Bw. Justine Kilenza akichangia jambo wakati wa kikao hicho kilichofanyika hivi karibuni.

Afisa Utumishi Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara mmoja wa Wajumbe wa Baraza hilo, Bi. Adventina Kambuga akisisitiza jambo juu ya umuhimu wa kujiunga katika mfumo wa “PSSSF Kiganjani”.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara   Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Cyprian Mkeha  (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama hiyo. Kulia ni Katibu wa Baraza hilo, Bw. Justine Kilenza na kushoto ni Naibu Katibu wa Baraza, Bi. Fullness Katekela. 

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wakiimba wimbo wa mshikamano.


Picha ya juu na chini ni Viongozi wa meza kuu wakiwa katika picha za pamoja na wajumbe wa Baraza hilo.

(Picha na ASHURA YUSUPH, Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara)

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Jumapili, 6 Aprili 2025

MAHAKIMU MBEYA WAHIMIZWA UMALIZAJI WA MASHAURI KWA WAKATI

Na Mwinga Mpoli – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga amewahimizwa Mahakimu kuhusu suala la usikilizaji na umalizaji wa mashauri kwa wakati na matumizi sahihi ya mifumo ya Mahakama lakini pia kuhakikisha wanaepuka kujaza mahabusu magereza ambao wana haki kudhaniniwa kwa mujibu wa sheria.

Mhe. Tiganga aliyasema hayo hivi karibuni katika kikao cha menejementi ya Kanda ya Mbeya kilichojumuisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa Songwe na kusisistiza kufuata miongozo, kanuni, sera na sheria zilizopo ili kufanikisha utendaji kazi kwa ueledi na ufanisi wakati wa utoaji haki kwa wananchi.

“Tukumbuke kuwa tunalojukumu la kuhakikisha tunasikiliza mashauri na kuyamaliza kwa wakati. Aidha tuepuke kupeleka watuhumiwa mahabusu na magereza ambao wanaweza kupata dhamana au adhabu mbadala. Pia niwakumbushe tunapaswa kuhakikisha tuna matumizi sahihi ya mifumo yetu na kuwa tunaipitia mara kwa mara ili tuweze kutathmini utendaji kazi wetu,” alisema Jaji Tiganga.

Aidha, Mhe. Tiganga aliwasisitiza juu ya kusimamia utekelezaji wa mashauri na kama kutakuwa na changamoto wahakikishe wanatumia ubunifu ili kuhakikisha hawakwami katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Kikao kazi hicho kilihudhuriwa na wajumbe kutoka mkoa wa songwe na Mbeya ambao kwa pamoja wanaunda Kanda ya Mbeya.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga akieleza jambo katika kikao hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Charles Tiganga (katikati) kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Emily Temu na kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Mbeya Bi Mavis Miti katika kikao hicho.