Jumamosi, 5 Aprili 2025

KWA TAKRIBANI MIAKA 100 MAHAKAMA YA TANZANIA YAANDIKA HISTORIA YA KIPEKEE

·       Wananchi na wadau wafurahishwa na miundombinu ya kisasa ya Mahakama

Na Salum Tawani na Arapha Rusheke- Mahakama, Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Damas Ndumbaro amesema kuwa, kwa mara ya kwanza Mahakama ya Tanzania kuwa na Ofisi yake ya Makao Makuu ya Mahakama italeta tija katika kutekeleza Majukumu yake kwa ufasaha.

Amezungumza hayo katika uzinduzi wa Makao Makuu ya Mahakama uliofanyika katika eneo la Tambuka reli lililopo Jijini Dodoma leo tarehe 05 Aprili, 2025.

“Kwa uzinduzi wa majengo haya na mambo mengine ambayo yameonekana kwa watanzania siyo tu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametenda haki bali sisi watanzania wote tumeona haki ambayo ameutendea Mhimili wa Mahakama, sekta ya Sheria na sekta ya haki,” alisema Mhe. Dkt. Ndumbaro.

Aidha, Waziri huyo amesema kuwa, amefurahishwa na ujenzi huo ambao umewashirikisha wazawa na mchango wa maudhui ya asili (Local Content) wa wazawa kwenye kazi hiyo ni asilimia kubwa, na asilimia 95 ya wataalam kwa maana  wahandisi ni watanzania na Mshauri elekezi ni kampuni ya kitanzania, hiyo ni hatua muhimu ya kuwajengea uwezo wataalam wa ndani pamoja na makampuni ya wazawa, niwaombe Wizara na Taasisi zingine za Kiserikali zizingatie umuhimu wa kuwashirikisha wazawa katika miradi mikubwa kama ilivyofanya Mahakama.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema imekuwa ni historia kubwa kwa  Dodoma ilikuwa na  Mhimili miwili na leo Mhimili wa tatu umekamilika na  kuwa Makao Makuu  ya nchi, hiyo ni historia ya pekee ambayo itakuandika Mhe. Rais katika vitabu vyote vya historia ya nchi ya Tanzania.

“Mhe Rais dhamira yako ya kutaka haki tunaiona jinsi wakati wote umetamani watanzania watendewe haki lakini jinsi ambavyo umetamani ardhi ya Tanzania iandike haki kwa kila mtanzania anayekanyaga katika nchi hii,” alisema Mhe. Rosemary...

Mambo haya Mhe. Rais  tumeyaona ukiyasema kwa maneno yako na tumeyasikia  lakini zaidi  tumeona kwa vitendo ambavyo umekuwa ukifanya  vya kutenda haki, mfano mdogo tu  ulipoanzisha Mama Samia Msaada wa Kisheria (Mama Samia Legal Aid) kupitia Wizara ya Katiba na Sheria ulitaka hata watu wa chini wapate haki yao katika nchi yetu ya Tanzania,” alisema Mhe. Rosemary

Mhe. Senyamule amesema, jambo linaloonekana la kutoa fedha nyingi kwa ajili ya utayari wa kujenga majengo kubwa ya kisasa ya Mahakama inaonyesha dhamira yako ya dhati ya kutaka haki kwa kila Mtanzani.

Aidha, Mkuu wa Mkoa huyo amempongeza Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwa kutengeneza historia ya Mapinduzi makubwa katika Mhimili wa Mahakama ambao Dunia inashuhudia majengo lakini amefanya na mambo mengine mengi ameyafanya katika kipindi chake.

Ni wazi kuwa, majengo yanayozinduliwa yatafanya watumiaji wafanye kazi kwa furaha, amani na utulivu na kupelekea kuwatendea haki watanzania wote ambao watapata huduma katika eneo hilo.

Vilevile, viongozi wa dini kwa nyakati tofauti wametoa pongezi kwa uongozi wa Mahakama kwa hatua hiyo ya kuwa na majengo yao katika Mkoa wa Dodoma kwani imekuwa ni faraja na jambo la kihistoria katika Nchi kushuhudia Majengo mazuri nay a kisasa yakizinduliwa.

Wananchi nao hawakuwa nyuma wameipongeza sana Mahakama ya Tanzania kwa kuboresha miundombinu ya Mahakama na kushukuru kwa kupata majengo ya kihistoria katika Mkoa wa Dodoma.

HISTORIA YAANDIKWA, JENGO LA KWANZA LA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA YA TANZANIA LAZINDULIWA

·        Rais Samia akiri kuwa jengo hilo lina hadhi na sifa ya kuwa Makao Makuu ya Mahakama

·        Aipa kongole Mahakama kwakuwa na Mifumo ya TEHAMA inayosomana na kuzitaka Taasisi nyingine za Serikali kuiga

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo tarehe 05 Aprili, 2025 ameweka historia kwa Mhimili wa Mahakama kwa kuzindua rasmi Jengo la kwanza la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na kukiri kuwa jengo hilo la kisasa na la Kimataifa lina kila sifa na hadhi ya kuwa Makao Makuu ya Mhimili huo.

Uzinduzi wa jengo hilo ni hatua kubwa kwa historia ya Mahakama nchini kufuatia ukweli kwamba, Mhimili huo haukuwahi kuwa na jengo la makao makuu kwa kipindi cha miaka 104 tangu kuanzishwa kwake.

Akizungumza wakati akitoa hotuba yake kwenye hafla ya uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji, Mhe. Dkt. Samia amesema kuwa, hatua ya upatikanaji wa jengo hilo ni moja ya maboresho makubwa yaliyofanyika ndani ya Mhimili wa Mahakama lengo likiwa ni kuboresha huduma ya upatikanaji haki.

“Leo tumeandika historia nyingine kubwa zaidi kwa upande wa Mahakama na Nchi, ni zaidi ya ile ya awali ya uzinduzi wa majengo ya Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJCs) sita. Nimelikagua jengo hili kwenye baadhi ya Ofisi zikiwemo Vyumba vya Magereza, Chumba maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa mbalimbali za Mahakama, Ofisi za Mawakili Watoto na nikiri kuwa lina kila sifa la kuwa Makao Makuu ya Mahakama,” amesema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia hakusita kuipongeza Mahakama ya Tanzania chini ya Uongozi wa Jaji Mkuu wa Tanzania kwa kuendelea kuwa mfano mzuri wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), ambapo ameonesha kufurahishwa na Chumba maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa mbalimbali za Mahakama (Judiciary Visual Situation Room).

“Nimeona Chumba maalum cha Mifumo ya utoaji taarifa mbalimbali (Judiciary Situation Room) ambayo nimeambiwa ni ya pili kwa ukubwa duniani, kwakweli nimeshangazwa na yaliyomo ndani, tunayoyashuhudia leo ni matokeo ya tuliyashuhudia kwenye nchi za wenzetu,” amesema Mhe. Samia.

Ameongeza kuwa, Serikali inachukua suala la utoaji wa haki kwa uzito wa pekee na kwamba mpaka sasa jumla ya miradi 144 ya ujenzi na ukarabati wa majengo ya ngazi mbalimbali za Mahakama unaendelea na kuahidi kuwa, miradi itakamilika kwa wakati.

Rais Samia, amebainisha kuwa kazi iliyofanywa na Mahakama ni zaidi ya kile kilichoahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na Dira ya Taifa ya Maendeleo.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Samia amesema kuwa, “Serikali itaendelea kuboresha maslahi ya watumishi wake kadri uwezo wa kibajeti utakavyoruhusu.”

Kwa upande mwingine, amewakumbusha watumishi wa Mahakama kuimarisha utoaji wa huduma ya haki kwa wananchi na kugusia juu ya umuhimu wa Mahakama za Mwanzo kutofungwa na masharti ya kiufundi yanayozuia haki kutendeka kwa wakati.

Katika hotuba yake, Rais Samia amewasisitiza pia watumishi wa Mahakama kuhusu utunzaji wa miundombinu ya majengo ya Mahakama ambapo amekazia kwa kusema kwamba, “Jengo hili la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na mengine niliyoyazindua nikipita hata baada ya miaka mitatu yawe hivihivi kwakuwa gharama za ukarabati ni kubwa.”

Ameikumbusha pia Mahakama kufanya maboresho ambayo pia yanazingatia Mahakama maalum mfano Mahakama ya Ardhi, Mahakama ya Masuala ya Familia na kadhalika.

Miradi mitatu iliyozinduliwa leo imegharimu kiasi ya fedha za kitanzania bilioni 185.4. Kupatikana kwa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama kunafanya Mihimili yote mitatu ya Dola ikiwemo Serikali na Bunge kuwepo Makao Makuu ya Nchi jijini Dodoma.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania sambamba na Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji, hafla hiyo imefanyika leo tarehe 05 Aprili, 2025 katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama Mtaa wa Tambukareli jijini Dodoma. Wa nne kushoto ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wa tatu kushoto ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa pili kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa nne kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro, wa tatu kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, wa kwanza kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitoa hotuba yake leo tarehe 05 Aprili, 2025 wakati wa uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji.


Muonekano wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililozinduliwa leo tarehe 05 Aprili, 2025.

Muonekano wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania na Tume ya Utumishi wa Mahakama yaliyozinduliwa leo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Nyumba 48 za Makazi ya Majaji ambazo zimezinduliwa leo pia na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto) akimkabidhi Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma mfano wa ufunguo wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililozinduliwa leo tarehe 05 Aprili, 2025.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kulia) pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani na sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo tarehe 05 Aprili, 2025 wakati wa hafla ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji.

Meza Kuu ikiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Kamati ya Maandalizi ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba 48 za Makazi ya Majaji.





Kwaya ya Mahakama ikitumbuiza katika hafla hiyo.

Mtendaji Mkuu wa kwanza wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga (kushoto) pamoja na Mtendaji Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru pamoja na wageni wengine wakiwa katika uzinduzi wa majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Nyumba za Makazi ya Majaji iliyofanyika leo tarehe 05 Aprili, 2025.

Sehemu ya Viongozi mbalimbali wa Serikali, Watumishi wa Mahakama ya Tanzania pamoja na wageni waalikwa wakiwa katika hafla ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tume ya Utumishi wa Mahakama pamoja na Nyumba za Makazi ya Majaji.














 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

PROF: OLE GABRIEL MAHAKAMA HAIFANYI BIASHARA

Na MAGRETH    KINABO- Mahakama, Dodoma

 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema kwamba Mahakama ya Tanzania haifanyi biashara bali inatoa huduma ya utaoaji ya haki kwa Wananchi, hivyo ndio maana Serikali imewekeza rasilimali fedha ya kiasi cha Sh. bilioni 416.16 kwa ajili kuboresha miundombinu ya Mahakama nchini katika kipindi cha miaka minne.

 

Aidha amesema kuwa fedha hizo, zimetolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ikiwa ni ahadi yake aliyoitoa wakati akihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha jukumu la utoaji haki linatekelezeka.

 

Ahadi hiyo, ilitolewa na Rais Dkt. Samia mara  baada ya kushika wadhifa huo wa juu zaidi hapa nchini, tarehe 19 Machi, 2021 jijini Dodoma.

 

Prof. Ole Gabriel amesema  hayo, leo tarehe 5 Aprili, 2025 wakati akitoa taarifa ya miradi yote iliyotekelezwa kwa kipindi hicho, kwa Rais Dkt. Samia.

 

“Fedha hizi ni jumla ya miradi yote iliyotekelezwa na keendelea kutekelezwa ikiwemo mradi wa ujenzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililopo  jijini Dodoma, ambapo ndio Makao Makuu ya  Nchi.Mradi mwingine ni Ujenzi wa Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama  yote imejengwa eneo la Tambuka Reli na mradi wa Makazi ya Majaji, ambayo yamejengwa kwa mtindo wa block mbili zenye nyumba 48, yapo eneo la Iyumbu, jijini Dodoma,”amesema Prof.Ole Gabriel.

 

Majengo hayo ya Mahakama ambayo  matatu yamezinduliwa leo na Rais Dkt. Samia  ambaye alikuwa mgeni rasmi  yaliyogharimu Sh.bilioni 185.4.

 

Akizungumzia kuhusu  Jengo la  Makao Makuu ya Mahakama,  amesema  ni la kisasa na kimataifa , pia utekelezaji wa Dira  ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2025 na lina ngazi 31 ambazo zinahakisi kuwa ni eneo la  Mamlaka na limegharimu Sh. bilioni 129.7. pia lina hekari 12 kwa shamba la kawaida na linachukua  watumishi 780 wa makao hayo.

 

“Jengo hili lina Chumba Maalumu cha  kisasa  chenye Mifumo 17 ya  Teknolojia  Habari na Mawasiliano(TEHAMA) ya Kutolea Taarifa  mbalimbali za Kimahakama nchi  nzima(JSR) iliyojengwa na wataalamu wa ndani ya nchi ,Kituo cha Huduma kwa Mteja, Mahakama za Wazi 10, kumbi ndogo 22 zenye uwezo wa kuchukua watu kuanzia 15,30,50,85, na Faragha, Ukumbi Mkubwa wa Mikutano  wenye uwezo kuchukua watu  346,  mita za mraba 63, 244  lina sehemu ya utawala... mabwawa ya kuogelea,

 

 “Afrika na dunia ifahamu kuwa  jengo hili linashika nafasi ya sita kwa majengo ya Makao Makuu ya Mahakama Duniani kwa ukubwa na lina  sakafu tisa, ni la kwanza Barani Afrika”amesisitiza.

 

Kuhusu  Makazi ya Majaji  amesema kuwa hivi sasa Majaji wameshahamia kwenye nyumba hizo, ambazo zina  mifumo ya usalama, maegesho ya magari, huduma za mtandao ili kuboresha mazingira ya kazi.

 

Ameongeza kuwa fedha zingine zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJC) sita vya awamu ya kwanza na vingine tisa vya awamu ya pili vinavyoendelea kujengwa, ambapo kimoja kiko Pemba.

 

Nyingine  ni   baadhi ya Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya  na Mahakama za Mwanzo na kukarabati  majengo ya Mahakama Kuu mbili ili ziwe Mahakama za Familia ambazo ni iliyokuwa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora na Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma. 


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akati akitoa taarifa ya miradi yote iliyotekelezwa  na Serikali ya Awamu ya Sita  kwa upande wa Mhimili wa Mahakama katika kipindi cha miaka minne kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakiwemo wageni wengine waalikwa kwenye hafla ya uzinduzi wa Majengo Matatu ya Mahakama yaliyopo jijini Dodoma. Hafla hiyo imefanyika leo tarihe 5 Aprili, 2025 katika Viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania vilivyopo eneo la Tambuka Reli jijini hapa, ambapo ndipo Makao Makuu ya Nchi na kuandika historia, kwamba Mihimili Mitatu ya Dola sasa imehamia Dodoma.

 

 

               CAPTION 

 


Mtendaji Mkuu wa Mah

HISTORIA MPYA YAANDIKWA TANZANIA

  • Mhimili wa Mahakama wapata Makao Makuu mapya
  • Rais Samia azindua jengo kubwa la kisasa Dodoma
  • Jengo hilo la sita duniani, la kwanza Afrika

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 5 Aprili, 2025 ameandika historia mpya Tanzania baada ya kuzindua jengo jipya la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini hapa.

Hatua hiyo inaufanya Mhimili huo wa Dola kuwa na Makao Makuu mapya ambayo, hapo awali yalikuwa katika jiji la kibiashara, Dar es Salaam. Jengo hilo lenye ukubwa wa mita za mraba 63,244, kwa majengo ya Makao Makuu ya Mahakama, ni la sita duniani na la kwanza Afrika.

Jengo la Makao Makuu ya Mahakama lililogharimu kiasi cha bilioni 129.7 za Kitanzania lina jumla ya vyumba vya ofisi 510 vyenye samani za kisasa, vyumba vya Mahakama za wazi 10, ukumbi mkubwa wa mikutano wenye uwezo wa kuchukua watu 346 na kumbi ndogo 22 za mikutano.

Sherehe za uzinduzi wa jengo hilo lililopo katika eneo la Tambuka Reli, zilianza saa 2.30 asubuhi na kuhudhuriwa na Viongozi wa Serikali, Bunge, Mahakama, Watumishi, Wastaafu na Wananchi kutoka maeneo mbalimbali katika jiji la Dodoma, ambalo ni Makao Makuu ya Tanzania.

Katika sherehe hiyo, Rais Samia pia alizindua Nyumba za Makazi ya Majaji zilizopo katika eneo la Iyumbu, pembezoni mwa barabara inayoelekea Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), ambazo zimegharimu kiasi cha bilioni 42.3 za Kitanzania.

Kadhalika, Mkuu wa Nchi alizindua Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama, lililopo pembezoni mwa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, ambalo limegharimu kiasi cha bilioni 14.3 za Kitanzania.

Rais Samia aliwasili katika eneo la sherehe hiyo majira ya saa 5.00 hivi asubuhi na kupokelewa na wenyeji wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Wakati wa mapokezi hayo, walikuwepo pia Viongozi wengine wa Mahakama, wakiwemo Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Viongozi wengine ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule na wengine wengi.

Baada ya kuwasili katika viunga vya Makao Makuu mapya ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Samia alielekea kwenye eneo maalum lililokuwa limeandaliwa kwa ajili ya kupanda mti wa kumbukumbu.

Viongozi wengine waliopanda miti wakati huo ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Baada ya tukio hilo, Mhe. Prof. Juma alimwongoza Rais Samia kwenye eneo la uzinduzi ambapo alipata maelezo mafupi kuhusu miradi mitatu ya majengo ambayo yamezinduliwa, yaani Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Nyumba za Makazi ya Majaji na Jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Rais Samia, baada ya kupata maelezo hayo, alifunua kitambaa maalum kwenye jiwe la uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu kama ishara ya uzinduzi rasmi wa majengo hayo matatu na baadaye kukata utepe.

Zoezi hilo lilimwezesha Rais Samia kuingia ndani na kuanza kulitembelea rasmi jengo hilo la Makao Makuu ya Mahakama lenye sakafu tisa na mbawa tatu, yaani Mahakama ya Juu/Upeo (Supreme Court), Mahakama ya Rufani (Court of Appeal) na Mahakama Kuu, ambazo katikati zinaunda eneo la Ofisi za Utawala.

Rais Samia alianza kutembelea Chumba kikubwa cha kisasa cha wazi cha kuendeshea mashauri ambacho kimefungwa vifaa bora vya teknolojia na mifumo ya kisasa, ikiwemo ule wa kusikiliza mashauri kupitia Mkutano Mtandao na ule wa Tafsiri na Unukuzi unaowawezesha Majaji na Mahakimu kuendesha mashauri bila kuandika mwenendo kwa mkono.

Baadaye, Rais Samia aliongozwa kwenye Chumba Maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa za Kimahakama (Judiciary Situation Room) kinachowawezesha Viongozi wa Mahakama kujua kila kitu kwa wakati mmoja kinachofanyika katika Mahakama zote nchini.

Mhe. Dkt. Samia pia alitembelea Chumba cha Huduma kwa Mteja (Customer Service Center), ambacho kina Watumishi wanaofanya kazi kwa masaa 24 kupokea mrejesho, yaani malalamiko, pongezi na changamoto mbalimbali zinazohusu huduma za utoaji haki kwa ujumla kutoka kwa Wananchi.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Samia aliongozwa kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu na kujionea kumbukumbu kadhaa ikiwemo picha za Majaji Wakuu ambao wamehudumu kabla na baada ya uhuru hadi sasa. Akiwa ndani ya ofisi hiyo, Rais Samia alifanya mazungumzo mafupi na Jaji Mkuu.

Baada ya kutembelea maeneo hayo, Rais Samia alielekea kwenye eneo maalum lililokuwa limeandaliwa kwa ajili ya kukabidhi funguo baada ya kuzindua na kutembelea jengo hilo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Rais Samia alikabidhi funguo tatu kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, moja wa Makao Makuu ya Mahakama, mwingine wa Makazi ya Majaji na tatu wa Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama, tukio lililopokelewa kwa shangwe, nderemo na vifijo na Wananchi waliokuwa wamefurika kuzidi uwezo wa eneo lililokuwa limeandaliwa kwa ajili ya sherehe hiyo.

Baada ya zoezi hili lililoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Samia, akiwa ameongozana na Wenyeji wake, alielekea Jukwaa Kuu kabla ya Bendi ya Jeshi la Polisi kuwaongoza Watanzani kuimba na Wimbo wa Taifa na ule wa Afrika Mashariki kwenye sherehe iliyokuwa inarushwa mubashara na vyombo mbalimbali vya Habari ya Kimataifa na Kitaifa, ikiwemo mtandao wa Mahakama ya Tanzania.

Muda mchache baada ya Rais Samia kukaa kwenye nafasi yake, Muongozaji wa Sherehe hiyo, Bw.  Shaban Kisu, ambaye alishirikiana kwa karibu na Mzee Peter Mavunde pamoja na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mashauri wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha, aliendelea na ratiba nyingine, ikiwemo kutoa nafasi kwa Viongozi mbalimbali kuzungumza na Taifa.

Sherehe hizo zimepambwa na burudani kutoka vikundi mbalimbali, ikiwemo Kwaya ya Mahakama ya Tanzania, maarufu kama Ng’aring’ari, Kwaya ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Kwaya ya Utumishi wa Umma. Kulikuwa pia na vikundi vya ngoma vya Kibati kutoka jijini Dodoma na Nyota kutoka Zanzibar.  


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto-akimkabidhi ufunguo wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwenye sherehe ya uzinduzi wa Majengo Matatu ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Nyumba za Makazi za Majaji na Jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto-akikabidhi ufunguo wa Nyumba za Makazi ya Majaji.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto-akikabidhi ufunguo wa Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-katikati-akijiandaa kukata utepe kama ishara ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Makazi ya Majaji na Tume ya Utumishi wa Mahakama, huku Viongozi wengine wakishuhudia. Picha chini akikata utepe huo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-wa pili kulia- akifungua kitambaa maalum kuashiria uzinduzi wa majengo hayo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-juu na chini- akipata maelezo mafupi kuhusu miradi ya ujenzi wa majengo hayo kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.


Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Kalege Enock akitoa maelezo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan namna Chumba Maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa mbalimbali za Mahakama kinavyofanya kazi. Picha chini akipata maelezo kwenye Chumba cha Huduma kwa Mteja.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongozwa na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania kuelekea kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu wa Tanzania. Picha chini akiingia kwenye eneo la Ofisi hiyo.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini kitabu cha wageni akiwa kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa ndani ya Ofisi ya Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimwonyesha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan moja ya picha ya majengo ya Mahakama ya zamani yaliyotumiwa na Majaji.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto- akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimwagilia mti wa kumbukumbu kufuatia uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimwagilia mti wa kumbukumbu kufuatia uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Kikundi cha Ngoma cha Kibati kutoka Zanzibar kikitumbuiza kwenye uzinduzi huo huku Viongozi na wageni mbalimbali wakimiminika kuwatunza.

Kwaya ya Mahakama ya Tanzania, maarufu Ng'aring'ari kikikonga mioyo ya Viongozi na wageni mbalimbali waliohudhuria uzinduzi huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwaaga Wananchi baada ya kuhitimishwa kwa sherehe ya uzinduzi huo.


JAJI MKUU AMWAGIA SIFA KEMKEM RAIS DKT. SAMIA

 Na INNOCENT KANSHA- Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake mkubwa wa kufanikisha maboresho yaliyotekelezwa na yanayoendelea kutekelezwa na Mahakama ya Tanzania kwa kuongeza idadi ya Majaji, Mahakimu na ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma ya haki kwa wananchi.

Ameyasema hayo, leo tarehe 05 Aprili, 2025 jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa kihistoria wa majengo matatu ya Mahakama likiwemo jengo la Makao Makuu ya Mahakama, jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama na Majengo ya makazi ya Majaji.

Mhe. Prof. Juma amenukuu hotuba ya Mhe. Dkt. Samia ya kwanza alipolihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mara ya kwanza mara baada ya kuapishwa kwake kuwa Rais, alisema "tutaenzi na kuendeleza mambo yote mazuri lakini pia tutafanya mabadiliko pale inapobidi kwa lengo la kukuza ufanisi na tija katika kazi,".

Aidha, Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa, Mahakama ya Tanzania ni wanufaika wakubwa sana wa hiyo sehemu ya hotuba ya Mhe. Dkt. Samia kwa sababu Mahakama imeshuhudia mapinduzi makubwa ya kuuwezesha Muhimili kutimiza ndoto ya miaka takribani 100 ya uwepo wa Mahakama nchini Tanzania.

Vilevile, Mhe. Prof. Juma amesema kuwa, Mhe. Dkt. Samia aliahidi kwamba, "tutashirikiana na Mhimili wa Mahakama katika kuimarisha mifumo ya utoaji haki ikiwemo kuendeleza kujenga miundombinu ya Mahakama na tumeshudia katika kipindi cha miaka minne Mahakama imejenga sana nchi nzima majengo ya kisasa ya kutolea huduma za haki kwa wakati kwa wananchi,".

“Kuongeza idadi ya Majaji na Mahakimu tumeona Rais akifanya hivyo, kukuza matumizi ya TEHAMA ambayo Mhe. Dkt. Samia umejionea mwenyewe wakati wa ukaguzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama, namna ambavyo Mahakama inatumia TEHAMA, na pia wakati ukiwa kwenye chumba maalum cha taarifa za kimahakama (Situation Room) na ulielezwa na wataalum wetu kwamba, katika chumba hicho teknolojia hiyo Mahakama ilikwenda kujifunza nchini Kazakhstan na ambao wao pia watakuja kujifunza kwetu kwa sababu katika zama hizi za teknolojia kila mmoja anajaribu kumshinda mwenzake,” amesisitiza Mhe. Prof. Juma.

Mhe. Prof. Juma amechukua wasaha huo kumshukuru sana Mhe. Dkt. Samia kwa hotuba yako "uliyoitoa Bungeni ilinisaidia sana, ilinipa nguvu na kuweza kwenda kuweka jiwe la msingi la jengo hili ambalo umelizindua leo. Hii simulizi imethibitisha kwamba Mhe. Dkt. Samia amejitoa kwa kiasi kikubwa kuhakikisha Mahakama inatimiza Dira yake ya Utoaji Haki sawa kwa wote na kwa wakati,".  

    


Ijumaa, 4 Aprili 2025

JAJI MFAWIDHI BUKOBA AONGOZA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na AHMED MBILINYI – Mahakama, Bukoba

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, Mhe. Immakulata Banzi hivi karibuni aliongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Kanda   ili kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji na utumishi.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Bukoba, kilihudhuriwa pia na Viongozi Waandamizi wa Mahakama hiyo, akiwemo, Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba, Mhe. Saidi Mkasiwa, Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Bukoba Bw. Lothan Simkoko, na wajumbe kutoka wilaya zote za Mkoa wa Kagera.

Baada ya kufungua Kikao hicho, Mhe. Banzi aliwakaribisha wajumbe kuimba wimbo maarufu wa wafanyakazi wa ‘solidarity forever’ na baadaye kufanya utambulisho wa wajumbe na kumruhusu Katibu wa Baraza hilo, Bi. Febronia Serapion kusoma agenda.

Akiwakaribisha wajumbe katika Kikao hicho, Mhe. Banzi aliwaomba kuwa huru kuchangia na kutoa maoni mazuri yatakayosaidia Baraza hilo kufikia maazimio yatakayowasaidia siyo tu watumishi wa mahakama kanda ya Bukoba, bali pia wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.

“Niwashukuru wajumbe kwa kuhudhuria kwenye Kikao cha Baraza hili. Ushiriki wenu ni muhimu  kwani michango ya mawazo mtakayotoa itasaidia kufikia maazimio yenye tija yatakayopelekwa kwenye Baraza Kuu siyo kwa manufaa yetu sisi bali pia watumishi wa Mahakama kwa ujumla,” alisema.

Katika Baraza hilo, wajumbe walijadili masuala mbalimbali yakiwemo mapitio ya Bajeti, ukomo wa bajeti, utekelezaji wa bajeti, changamoto za utekelezaji wa bajeti, kupokea na kujadili hoja za watumishi na pia majibu na ufafanuzi ulitolewa na viongozi mbalimbali.

Kadhalika Mhe. Banzi alisisitiza kwa watumishi wote kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu, ushirikiano kwa watumishi na wadau wa mahakama, na   kuwakumbusha kujiendeleza kielimu katika taaluma zao pamoja na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Katika Kikao hicho kilichohudhuriwa piya na Katibu wa TUGHE wa Mkoa wa Kagera, Bw.  Edward Mwashitanda aliyeelezea faida za kutumia mabaraza ya wafanyakazi katika kutatua changamoto za watumishi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, Mhe. Immaculata Banzi (katikati) akiongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo. (Kulia) ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Lucas Mwilu na (kushoto) ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Bukoba, Bi. Febronia Serapion.

Mtendaji wa Mahakama  Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, Bw. Lothan Simkoko akiwasilisha Taarifa ya Utendaji kazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba  ya 2024 /2025.

Kaimu Afisa Bajeti wa Mahakama  Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, Bw. Rojas Rwanyumba akiwasilisha Taarifa ya Bajeti ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, 2024 /2025.

Katibu wa Tughe Mkoa wa Kagera, Bw. Edward Mwashitanda mwenye suti nyeusi akiwa  katika Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Bukoba (kulia) ni Afisa Tawala Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Bukoba, Bi. Luciana Lucas.

Picha ya juu na chini ni wajumbe waliokuwepo kwenye mkutano wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Bukoba wakifuatilia kwa makini kinachoendelea kwenye mkutano huo.

(Habari hii imehaririwa na MAGRETH  KINABO, Mahakama, Dodoma)