Jumatano, 26 Machi 2025

KUWENI WABUNIFU KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAFUNGWA; JAJI KIONGOZI

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewaasa viongozi wa Magereza na wadau wote katika sekta ya sheria kutumia mbinu za ubunifu kutatua changamoto zinazoikumba Magereza nchini. 

Mhe. Dkt. Siyani aliyasema hayo jana tarehe 25 Machi, 2025 alipofanya ziara ya kikazi katika Magereza mawili yaliyopo katika Manispaa ya Tabora ambayo ni Gereza Kuu Uyui na Gereza la Mahabusu maarufu kama Gereza la Zuberi. 

"Nimeona kwenye taarifa yenu kuwa kwa sasa hakuna msongamamo katika magereza haya,  ninatambua pia kuna changamoto ya uhaba wa rasilimali, binafsi ninawaasa viongozi wa Magereza na wadau wote katika sekta ya haki kutafuta na kutumia mbinu za ubunifu kutatua changamoto zinazoikumba magereza. Ni muhimu kushirikiana na wadau mbalimbali, ikiwa ni pamoja na mashirika ya kijamii, asasi zisizo za kiserikali na taasisi za Serikali ili kutatua changamoto zinazohusiana na haki za wafungwa na ustawi wa magereza," alisema Mhe. Dkt. Siyani.

Jaji Kiongozi alikagua maeneo mbalimbali ya magereza ikiwa ni pamoja na malazi ya wafungwa, sehemu za kuandalia chakula na vifaa vya kisasa vilivyotolewa na Mahakama kwa ajili ya kuboresha huduma za kisheria kwa wafungwa kupitia mfumo wa Mahakama ya Mtandao (Virtual Court) ambao unawezesha kusikiliza mashauri ya wafungwa kwa njia ya mtandao hivyo kupunguza idadi ya wafungwa wanaohitaji kusafirishwa kwenda mahakamani na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa Mahakama.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani alikubaliana na juhudi za magereza katika kutumia nishati mbadala kwa ajili ya kuandaa chakula cha wafungwa kwa njia ya kupunguza utegemezi wa vyanzo vya nishati vya kiasili na pia kutunza mazingira ambapo alikiri kuwa hatua hiyo muhimu inayosaidia kupunguza athari za mazingira.

Ziara hiyo ililenga katika kuangalia hali ya mazingira, miundombinu na huduma zinazotolewa kwa wafungwa katika magereza hayo. Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Mahakama ya Tanzania katika kuhakikisha haki za wafungwa zinaheshimiwa na mazingira ya magereza yanaboreshwa ili kuendana na viwango vya kimataifa.

Jaji Kiongozi aliongozana na viongozi wa Mahakama ya Tanzania na Wakuu wa Taasisi mbalimbali ambao ni wadau muhimu katika utendaji wa haki na usalama wa jamii. Viongozi hao ni Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Jeshi la Magereza na vyombo vingine Pamoja na taasisi za haki jinai na madai.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akikagua kasha la Mahakama jana tarehe 25 Machi, 2025 liliopo katika Gereza Kuu Uyui lililotolewa kwa ajili ya kufanyia shughuli za Mahakama ya Mtandao (Virtual Court) na kuboresha utoaji wa haki kwa wafungwa.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akipokelewa na watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora alipofika katika Mahakama hiyo kabla ya kwenda Magereza kwa ukaguzi jana tarehe 25 Machi, 2025.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akisaini kitabu cha wageni kwenye Ofisi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa kwanza kulia). Wengine katika picha  ni viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Kuu na wa Kanda hiyo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa mbalimbali alioambatana nao katika gereza Kuu Uyui mkoani Tabora.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


JAJI BWEGOGE AFANYA UKAGUZI GEREZA LA MKUZA, MAHAKAMA YA MKOA NA WILAYA KIBAHA

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Pwani

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Obadia Bwegoge jana tarehe 25 Machi, 2025 alifanya ukaguzi wa kikazi katika Gereza la Mahabusu Mkuza na Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha.

Akipokea taarifa ya Gereza la Mahabusu Mkuza iliyosomwa na Mkuu wa Gereza hilo, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza (SSP) Ibrahim Nyamka alisema kutawanyika kwa Mahakama kunasababisha kushindwa kuwafikisha Mahabusu mahakamani kwa wakati.

Licha ya kwamba kwa sasa kuna basi kwa ajili ya kusafirishia mahabusu bado mtawanyiko wa Mahakama umekuwa changamoto, Mkuu huyo wa Gereza alisema kuwa, kutokana na changamoto hiyo Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha vijijini umeahidi kutoa eneo la hekari 60 kwa ajili ya ujenzi wa Gereza ambapo baada ya kukamilika kwa ujenzi huo kutaondoa changamoto ya umbali wa Mahakama mfano Mahakama ya Mwanzo Magindu na Soga ambazo ziko pembezoni kijiografia  ambapo umbali wake umekadiriwa kuwa kilometa zaidi ya 50.

SSP Nyamka alisema katika kutekeleza maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhusiana na kuachana na matumizi ya kuni (nishati chafu) na kutumia nishati safi, Gereza hilo limeanza matumizi ya nishati safi kwa kutumia makaa ya mawe huku wakiendelea na mchakato wa matumizi ya gesi.

Katika ukaguzi huo, Jaji Bwegoge alikutana na wafungwa na mahabusu wa Gereza hilo na kupokea changamoto mbalimbali na kuzitatua, changamoto hizo ni pamoja na kutoleta mashahidi kwa wakati, washtakiwa kufutiwa mashauri na kukamatwa tena na pia kuchelewa kusikilizwa kunasababisha mahabusu kukaa kwa muda mrefu.

Akijibu changamoto hizo, kuhusu suala la kufutiwa shauri na kukamatwa tena, Mhe. Bwegoge alisema shauri likifutwa likarudishwa inabidi upelelezi uwe umekamilika na lianze kusikilizwa mara moja na kama litakuwa kwa Hakimu mwingine ni jukumu la mshtakiwa kumwambia Hakimu kwamba shauri hilo lilifutwa na sasa limeletwa tena ili Hakimu husika aweze kuchukua hatua.

“Kama itafutwa kesi kwa sababu shahidi hajaja mahakamani kwa hiyo siku anarudishwa  mahakamani  lazima awe na  shahidi mlangoni kama ikienda ndivyo sivyo na wewe unaweza kukumbusha utaratibu huo,” alisema Jaji Bwegoge.

Pamoja na kuzungumza na wafungwa na mahabusu, Mhe. Bwegoge alifanya ukaguzi maeneo mbalimbali ya gereza hilo ikiwemo jikoni na kwenye mabweni ya wafungwa na mahabusu.

Kadhalika, Mhe. Bwegoge alifanya ukaguzi pia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Kibaha na kuona namna ambavyo kazi ya usikilizwaji wa mashauri inavyofanyika.

Baada ya ukaguzi huo, Jaji Bwegoge alifanya mazungumzo na watumishi wa kada mbalimbali katika Mahakama hizo na kuwapongeza watumishi kwa  utendaji kazi na mazingira   kutokana na kwamba hakuna changamoto nyingi ambazo zinaashiria  vinginevyo, na pia amewakumbusha kuendelea kuwajibika kama ilivyo ada.

Mhe. Bwegoge aliwakumbusha watumishi kuwa, taswira ya Mahakama inatokana na namna wanavyowahudumia wananchi. Amewakumbusha kwamba vile wanavyowahudumia wateja ni ndivyo wanavyochukulia sura ya Mahakama ilivyo. 

Aliwataka watumishi pia kuepuka kuzunguka na kupiga hadithi na wateja hata kama wanafahamiana ili kuondoa wasiwasi kwa upande wa pili, ili wajue kwamba wateja wote kwa usawa bila kuegamia upande wowote. Amewataka watumishi hao kuweka imani kwa wateja ili wasiwashuku kwa lolote.

Aidha, Jaji Bwegoge alisema kwamba Mahakama ya miaka 12 iliyopita sio Mahakama ya sasa siku zinakwenda na mazingira ya Mahakama yamebadilika, kwakuwa huko nyuma mazingira hayakuwa rafiki kama sasa hivyo amewataka watumishi hao kuendelea kuishi kwa matumaini. 

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe.Aziza Mbadjo aliwapongeza watumishi wa Mahakama hizo kwa kufanya kazi kwa utaratibu na kutokuwa na kashfa yoyote na kwamba siku zote wamekuwa wafuata maelekezo ya viongozi na usikivu wa watumishi hao.

Aidha, Mhe. Mbadjo amemueleza Jaji Bwegoge kuwa, amefanya ukaguzi na kukuta vitu vimepangwa vizuri huku akitoa mfano wa stoo ya vielelezo ambapo alisema stoo hiyo ina vielelezo vya Mahakama zote mbili vilivyopangwa vizuri. Amekagua pia mifumo yote na kudai iko vizuri licha ya changamoto ndogondogo za kibinadamu.

Naye, Afisa Tawala wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Lucy Tirukaizile alifanya ukaguzi kwenye mifumo ya PEPMIS na Ofisi Mtandao ‘e-Office’ na kubainisha kuwa iko vizuri na kuwasihi Watumishi wa Mahakama hizo kufanya kazi kwa bidii na kujiendeleza kielimu kwani elimu haina mwisho. 

Katika ukaguzi huo Jaji Bwegoge aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo, Msaidizi wa Sheria wa Jaji, Mhe. Suda Mbilinyi na Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Lucy Tirukaizile.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Obadia Bwegoge akisaini kitabu cha wageni jana tarehe 25 Machi, 2025 baada ya kuwasili katika Gereza la Mahabusu Mkuza Kibaha.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Obadia Bwegoge 
akisaliamia na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha-Pwani alipowasili katika Mahakama hiyo jana tarehe 25 Machi, 2025. 


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Aziza Mbadjo (kushoto) akikagua na kutoa maelekezo katika mfumo wa Usimamizi wa Mashauri 'e-CMS' kwa Wakuu wa Masjala wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha.

Afisa Tawala wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, BI. Lucy 
Tirukaizile (katikati) akikagua Mfumo wa Manunuzi. Kulia ni Afisa Tawala wa Mahakama ya Hakimu Mkazi, Bi. Stumai Hozza na kushoto ni Afisa Ugavi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha, Bi. Deborah Muyenjwa.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


JAJI MFAWIDHI SHINYANGA AMTAKA MKANDARASI KUMALIZA MIRADI YA UJENZI KWA WAKATI

Na EMMANUEL OGUDA, Mahakama-Simiyu

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe.Frank Mahimbali amemtaka Mkandarasi ‘Skywards Ltd’ anayetekeleza miradi ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Nyalikungu Maswa, Lagangabilili Itilima na Mhango Bariadi kuhakikisha wanakamilisha miradi ya ujenzi wa Mahakama hizo kwa muda uliopangwa bila nyongeza ya muda wa ziada.

Mhe. Mahimbali aliyasema hayo jana tarehe 25 Machi, 2025 wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Mahakama hizo na kumuhimiza Mkandarasi kukimbizana na muda uliobaki ili wananchi katika maeneo hayo waanze kupata huduma katika majengo hayo.

“Ni muhimu sana kukamilisha miradi hii na kuutumia vizuri muda uliobaki kukamilisha shughuli zote kwenye miradi hii, kwani wananchi wanahitaji kuanza kupata huduma katika majengo haya,’’ alisema Jaji Mahimbali.

Kwa mwaka huu wa fedha Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga imepata jumla ya miradi mitano ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo inayotekelezwa katika Wilaya za Shinyanga, Kahama, Maswa, Bariadi na Itilima na miradi yote ilianza kutekelezwa mwezi Agosti, 2024 na inatarajiwa kukamilika mwezi Machi, 2025.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mahimbali aliwataka Watumishi wa Mahakama Kanda ya Shinyanga wanaopata fursa ya kuhudhuria mafunzo, wanaporejea katika vituo vyao wahakikishe wanawapatia elimu waliyoipata watumishi waliobaki vituoni ili kuwa na uelewa wa pamoja. Aliwahimiza pia watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo, kuhakikisha wanapata fursa ya kujiendeleza kielimu kila wanapopata fursa. 

Jaji Mahimbali anaendelea na ziara ya ukaguzi wa kawaida wa Mahakama unaofanyika kila robo mwaka ambapo hadi kufikia jana alikuwa ameshatembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Mahakama za Wilaya Maswa, Bariadi, Itilima na Busega. Aidha, ziara ya ukaguzi inaendelea kwa Mahakama zilizobaki ambazo ni Mahakama ya Hakimu Mkazi Shinyanga, Mahakama za Wilaya Shinyanga, Kahama, Kishapu na Busega.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe Frank Mahimbali (kulia) akipokea maelezo ya mradi kutoka kwa Mhandisi Alex Silas (wa pili kulia) wakati akikagua ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Nyalikungu-Maswa jana tarehe 25 Machi, 2025.

Mkadiriaji Ujenzi QS Edson Minata akitoa maelezo ya Mradi wa Mahakama ya Mwanzo Lagangabilili-Itilima kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga (hayupo katika picha) wakati alipotembelea jana tarehe 25 Machi, 2025 kufahamu maendeleo ya mradi huo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. Frank Mahimbali (kushoto) akisisitiza jambo wakati alipofanya ukaguzi wa Mradi wa Mahakama ya Mwanzo Lagangabilili- Itilima jana tarehe 25 Machi, 2025.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Bw. Gasto Kanyairita akifafanua jambo wakati Jaji Mahimbali alipotembelea Mradi wa Mahakama ya Mwanzo Lagangabilili-Itilima.

Muonekano wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo Lagangabilili- Itilima ambalo lipo katika hatua ya upauaji kwa sasa.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. Frank Mahimbali (wa tano kulia) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Meatu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


MTENDAJI MAGACHA : AHIMIZA KUKAMILIKA KWA MRADI WA UJENZI WA IJC KATAVI KWA MUDA ULIOPANGWA

-     .

Na. ALLY. RAMADHANI -Mahakama, Katavi

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha, ameitaka Mkandarasi wa Kampuni ya M/s AZHAR Construction Co. Ltd kukamilisha ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC), Katavi kinachoendelea kujengwa katika Mkoani Katavi kwa wakati na kuzingatia viwango na ubora uliokusudiwa kwa mujibu wa mkataba. 

Bw. Magacha ametoa  maelekezo hayo mahsusi  tarehe 25 Machi, 2025  kwa ajili ya kukagua shughuli zinazoendelea katika mradi wa ujenzi wa Kituo   hicho.

Akitoa maelekezo kwa mkandarasi wa mradi huo, Mtendaji wa huyo alisisitiza kuwa ni muhimu   kwa mkandarasi huyo kuongeza vifaa (vilivyopungua ili kusaidia kukamilika kwa mradi huo ndani ya muda.

Aidha, Magacha amesema hayo baada ya kugundua changamoto zinazosababisha kusuasua kwa mradi huo, katika kikao kinachohusu ujenzi huo.

 “Tupo tayari kutumia aina yeyote ya rasilimali iwe fedha, nguvu kazi, na muda yani usiku na mchana ili kabla ya kuvuka kwa nusu ya mwezi Juni  mwaka huu mradi wa ujenzi huu uwe tayari umekamilika,” anasema Magacha.

Naye Meneja Mradi wa ujenzi huo, Msanifu Linda Kasilima alitoa ushauri kwa mkandarasi kuongeza nguvu kazi watu ili kuharakisha mradi huo, ambapo wazo hilo liliridhiwa na Mkurugenzi wa kampuni hiyo,Mhandisi Shabani Kapinga ambaye ndiye Mkandarasi.  

“…tayari kuna idadi ya nguvu kazi watu tunategemea iongezeke kuanzia kesho kutoka sehemu tofauti tofauti ndani ya Mkoa wa Katavi na nje ya mkoa,” amesema Kapinga.

Pia timu ya Wahandisi kutoka upande wa Mahakama ya Tanzania, baada ya kikao hicho kilichofanyika kwa zaidi ya masaa matano walipata wasaa wa kutembelea jengo na kuangalia shughuli zinazoendelea.

Aidha akiwa katika eneo la mradi wa ujenzi wa Kituo hicho,Mtendaji wa huyo alipata wasaa wa kusalimiana na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi.

Akihitimisha kikao chake na wakandarasi hao, amewataka kuzingatia kalenda ya shughuli zilizopangwa kufanyika kwa kipindi cha utekelezaji wa mkataba pamoja na ubora wa vifaa vinayonunuliwa, na kusisitiza kwamba vifaa vyote viwepo tayari na hiyo idadi ya nguvu kazi watu iwe tayari.

Moja ya nguzo katika Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ni Utoaji Haki kwa wakati. Mahakama inatekeleza mpango huu kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki kwa wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hii.

 

Mtendaji  wa Mahakama Kuu  ya  Tanzania, Bw. Leornad Magacha akisalimiana na baadhi ya watumishi wa Mahakama Mkoa wa Katavi. 

Mtendaji  wa Mahakama Kuu ya  Tanzania Bw. Leornad Magacha (aliyevaa kofia) akiwa kwenye kikao cha usimamizi wa miradi, alipokuwa akikagua shughuli zinazoendelea katika mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachoendelea kujengwa mkoani Katavi.


 W
ataalamu kutoka upande wa Mahakama,  wakikagua shughuli zinazoendelea katika mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachoendelea kujengwa.

Masanifu wa ujenzi huo, Bi. Linda Kasilima, ambaye pia ni Meneja  wa Mradi huo akizungumza  kwenye kikao cha usimamizi wa miradi, wakati wa ukaguzi wa shughuli zinazoendelea katika mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachoendelea kujengwa mkoani Katavi.

 

(Habari hii imehaririwa na MAGRETH KINABO- Mahakama, Dodoma)

 

 

 

JAJI MFAWIDHI MTWARA AONGOZA WATUMISHI KUTEMBELEA KITUO CHA KULELEA WATOTO

Na HUBERT MAANGA-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, hivi karibuni aliungana na Watumishi kutoka Kanda hiyo kutembelea Kituo cha Elimu ya Watoto wenye mahitaji maalumu na changamoto mbalimbali, ikiwemo usonji, kilichopo Mtwara mjini.

Watoto wa Kituo hicho kinachoitwa ‘Upendo Rehabilitation Day Center,’ wakiongozwa na Walezi wao, waliwapokea wageni wao kwa furaha na kuwakaribisha.

Baada ya hapo, Jaji Mfawidhi alizungumza machache na Msimamizi wa Kituo hicho kuhusu watoto na uendeshaji wake kwa ujumla. Mhe Kakolaki aliwashukuru Walezi wa watoto hao kwa kazi ya kipekee ya kuwalea na kuwafunza.

"Hawa ni watoto wetu na wanahitaji msaada na uangalifu maalumu, ninawaomba wasiwe na wasiwasi, bali waendelee kuwaongoza na kuwatunza. Endeleeni juhudi hii ya upendo kwani mnajaza moyo wa matumaini,’ alisema.

Jaji Mfawidhi aliwaeleza Walezi hao kuwa kila wanachokifanya kwa watoto hao ni kikubwa na dhamana kubwa ya kibinadamu ambayo Mungu atawabariki. Pia aliwasihi Watumishi wenzake kutokuishia hapo, bali waendelee kuwasaidia na kuwatia nguvu wenzao katika kuwalea watoto hao.

Vile vile, Mhe. Kakolaki alishirikiana na Watumishi wa Mahakama kuwawezesha watoto hao baadhi ya mahitaji kama vyakula na vifaa vya kuwasaidia, akitambua changamoto zinazowakabili.

Alihimiza jamii yote kushiriki katika kulinda na kuendeleza haki kwani ni Kituo kinachoendelea kukuza matumaini kwa watoto wenye mahitaji maalum na changamoto mbalimbali.

Baada ya shughuli hiyo matendo ya hisani, Watumishi wa Mahakama na Wadau mbalimbali walikutana katika Iftar ya pamoja iliyofanyika kwenye Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara. Iftar hiyo ilikuwa sehemu ya kukuza ukaribu na upendo, hasa katika kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramdhan na Kwaresma.

Wakati wa hafla hiyo, Jaji Mfawidhi aliwasihi Watumishi wote kuendelea kujisogeza kwa Mwenyezi Mungu na kufanya matendo mema.

Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Sheikh Jamaldin Chamwi, ambaye alikuwa miongoni mwa Viongozi wa Dini waliohudhuria, alisisitiza ibada na kukazia juu ya yale aliyoyataja Jaji Mfawidhi kabla ya kafunga kwa dua.  


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akiungana na Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mtwara kukabidhi kwa Msimamizi wa Kituo vyakula na vifaa mbalimbali kwa ajili ya watoto hao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto) baada ya kupokelewa kituoni pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Saidi Ding’hoi (katikati) na Naibu Msajilli wa Mahakama Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana (kulia).

Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mtwara wakishuhudia uchangamfu na ukarimu kutoka kwa watoto.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akizungumza na watoto, wakionyesha tabasamu na kumfurahia.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akitoa neno katika Iftar iliofanyika kwenye Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara.

Majaji wakiwa kwenye meza moja na Viongozi wa Dini wakati wa Iftar.

Watumishi na Wadau mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo ya Iftar (juu na chini).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma


 

 

MAHAKAMA KUU KANDA YA GEITA YAFANYA UKAGUZI MAHAKAMA ZA WILAYA YA CHATO

 

Na DOTTO  NKAJA-Mahakama, Geita

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Venance Mwakapeje amefanya ukaguzi wa kwanza kwa mwaka 2025 tarehe 25 Machi, 2025 katika Mahakama ya Wilaya Chato na Mahakama za Mwanzo wilayani hapo kwa lengo la kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama, kukutana na watumishi kusikiliza na kutatua changamoto wanazokutana nazo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mhe. Jaji Mwakapeje amefanya ziara hiyo kwa niaba ya Jaji Mfawidhi Mhe. Kevin David Mhina wa Mahakama hiyo, ambapo aliongozana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Rutashobya Lukuna na Mtendaji wa Mahakama hiyo Bi. Masalu Cosmas Kisasila. 

Pia Mhe. Jaji Mwakapeje alikagua Mahakama ya Mwanzo Muganza, Bwanga, Buseresere, Chato Mjini na Mahakama ya Wilaya ya Chato. 

Vile vile ziara hiyo ilihusisha kutembelea mradi wa ujenzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Muganza ili kujionea maendeleo yake. 

Aidha, Mhe. Jaji Mwakapeje akiwa na viongozi wengine walisikitishwa na kusuasua kwa maendeleo ya ujenzi huo kwani ulikuwa umesimama na hakuna kilichokuwa kinaendelea  likiwa limefikia kwenye hatua ya linta.

Wakati wa kikao pamoja na watumishi wa Mahakama za Wilaya hiyo, Mhe. Jaji Mwakapeje aliwapongeza kwa kazi nzuri walioionesha katika mwaka 2024 kwa kumaliza mashauri ndani ya wakati, ikiwemo kasi ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika uendeshaji wa mashauri. 

Aidha, Mhe. Jaji Mwakapeje amewaasa watumishi kuzingatia sana suala la maadili kwani ndiyo wa mgongo wa Mahakama. Vilevile Mhe. Jaji Mwakapeje amewakumbusha kila Mahakama kuendelea na utaratibu wa kutoa elimu kwa Wadau mbalimbali ili kupunguza changamoto za watu kutofuatilia kesi zao na kuchelewa kuisha kwa kesi.

Mhe. Jaji Mwakapeje pamoja na timu yake baada ya kumaliza ukaguzi katika Mahakama ya Mwanzo Muganza walienda Mahakama ya Wilaya Chato. Kwa kuzingatia taratibu walikagua Mahakama hiyo na kusisitiza kuwa uendeshaji wa mashauri ufanyike hatua kwa hatua.

Jaji huyo alimaliza ukaguzi katika Mahakama za Mwanzo Chato Mjini, Bwanga na Buseresere akiwa na timu yake na kuwaomba watumishi wote wafanye kazi kwa kuzingatia taratibu na sheria. Pia amewataka wajitahidi kuwahudumia wateja kwa uadilifu, uaminifu na weledi.

Kwa upande wake Naibu Msajili wa Mahakama hiyo, Mhe.Lukuna amewapongeza watumishi wa Mahakama ya Chato kwa kufanya kazi kwa shirikiano, huku akiwataka waendelee kufuata taratibu na sheria za Mahakama katika kutoa haki kwa wananchi.

Naye Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bi.  Kisasila alipongeza jinsi wanavyojituma katika utoaji wa huduma kwa wananchi na aliwakumbusha kuhusu kuwa wepesi na mabadiliko ili kuendana na kasi katika utendajikazi. Vilevile alikazia kuhusu suala la nidhamu katika utumishi wao pamoja na utoaji huduma yenye tija.

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Venance Mwakapeje akisaini kitabu cha wageni katika Mahakama ya Mwanzo Buseresere.

 Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Jaji Griffin Venance Mwakapeje(katikati) akiwa pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Rutashobya Lukuna(kushoto) na Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Chato, Mhe. Amalia Ludovic Mushi (kula)wakizungumuza na watumishi wote Wilaya ya Chato.

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Jaji Griffin Venance Mwakapeje Mtendaji wa Mahakama hiyo Bi. Masalu Cosmas Kisasila, Naibu Msajili Mhe. Fredrick Rutashobya Lukuna, Hakimu Mfawidhi wa Wilaya ya Chato Mhe. Amalia Ludovic Mushi na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Muganza wakitembelea ujenzi wa jengo ya Mahakama hiyo.

 Picha ya pamoja  viongozi hao na watumishi baada ya kumaliza ukaguzi Mahakama ya Wilaya ya Chato.

 

(Habari hii imehaririwa na MAGRTETH KINABO,Mahakama, Dodoma)

Jumanne, 25 Machi 2025

JAJI KIONGOZI AANZA ZIARA MAHAKAMA KUU KANDA YA TABORA

Awasisitiza watumishi wa Mahakama kujipanga thabiti kurejesha Imani ya wananchi kwa Mahakama

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ameanza ziara ya kikazi katika Mahakama Kuu Kanda ya Tabora lengo likiwa ni kukagua shughuli za Mahakama na kukutana na watumishi kuwasikiliza, kutatua changamoto zao, kuwapa motisha sambamba na kuhimiza utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia maadili ya kazi. 

Katika siku ya kwanza ya ziara yake jana tarehe 24 Machi 2025, Mhe. Dkt. Siyani alitembelea katika Wilaya za Igunga, Nzega na Uyui na kufanya mazungumzo na watumishi wa Mahakama hizo.

Akiwa katika ziara hiyo, Jaji Kiongozi aliwataka watumishi kufanya kazi kwa moyo na kujenga utamaduni wa kujituma katika utendaji wao huku akisisitiza juu ya umuhimu wa kuweka malengo ya kazi na kuyafikia, kuzingatia viwango vya juu vya maadili katika utendaji kazi. 

“Ni muhimu kwa watumishi wa Mahakama kufanya kazi kwa moyo na kujenga utamaduni wa kujituma katika utendaji wao, kila mtumishi anapaswa kuweka malengo ya kazi ya wazi na kuyafikia kwa ufanisi, huku akizingatia viwango vya juu vya maadili katika utendaji wake. Vilevile viongozi wa Mahakama na Kamati za Maadili wanapaswa kusimamia nidhamu kwa ukamilifu na kuchukua hatua stahiki dhidi ya maofisa watakaobainika kukiuka maadili ya kazi. Lengo letu ni kuhakikisha kwamba Mahakama inabaki kuwa chombo cha kuaminika kinachotoa haki kwa usawa na kwa kuzingatia maadili,” alisema Mhe.Dkt. Siyani.

Kadhalika, Jaji Kiongozi aliwahimiza Viongozi wa Mahakama na Kamati za Maadili kusimamia nidhamu na kuchukua hatua stahiki dhidi ya maofisa watakaobainika kukiuka maadili ya kazi.

Aidha, Jaji Kiongozi pia alikumbusha juu ya umuhimu wa kujenga imani ya wananchi kwa Mahakama, huku akisisitiza kuwa hatua madhubuti zinapaswa kuchukuliwa ili kurejesha imani kwa wananchi ili kuhakikisha utoaji haki unaenda sambamba na wananchi kuiamini Mahakama na mfumo wa mzima wa utoaji haki.

“Ni muhimu sana, tunapaswa kujenga imani ya wananchi kwa Mahakama. Sisi watumishi wa Mahakama lazima tuchukue hatua thabiti ili kurejesha imani hiyo kwa kuhakikisha kwamba utoaji haki unakwenda sambamba na wananchi kuiamini Mahakama pamoja na mfumo mzima wa utoaji haki, Mahakama inapaswa kuwa ni chombo cha haki kinachozingatia uwazi, usawa na maadili ili wananchi wawe na imani katika mfumo wetu wa haki," alisisitiza Mhe. Dkt. Siyani.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kulia) akizungumza na Mhe. William Nchana Hakimu Mkazi baada ya kumaliza kikao na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Uyui katika ziara yake Kanda ya Tabora.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Siyani akisaini kitabu cha wageni alipowasili katika  Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Uyui alipotembelea wakati wa ziara yake jana tarehe 24 Machi, 2025.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiteta jambo na mwenyeji wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi.

 Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa kwanza kushoto) akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Igunga akiwa ziarani katika Mahakama hiyo jana tarehe 24 Machi, 2025.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa sita kulia) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi kutoka Mahakama Kuu Masjala Kuu na wa Mahakama Kanda ya Tabora. 

Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Mhe. Sauda Mtondoo aliyesimama akitoa neno wakati wa ziara ya Jaji Kiongozi katika Mahakama ya Wilaya Igunga.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi akizungumza na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Zainabu Mango (kulia) wakati wa ziara ya Jaji Kiongozi katika Kanda hiyo aliyoanza jana tarehe 24 Machi, 2025. Aliyesimama nyuma kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Frank Mirindo na aliyesimama nyuma kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Rhoda Ngimilanga.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


MENEJIMENTI MAHAKAMA KANDA YA DAR ES SALAAM YAFANYA KIKAO

Na EUNICE LUGIANA-Mahakama, Pwani

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi amewataka Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama zote kwenye Kanda hiyo kuwa wabunifu katika kusikiliza mashauri ili kuondokana na mlundikano.

Mhe. Maghimbi alitoa wito huo hivi karibuni alipokua akifungua kikao cha menejimenti cha Mahakama Kanda ya Dar es Salaam kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Pwani.

Aliwahimiza kuendesha kesi kwa njia ya mtandao, hata kama hawaonani bali Hakimu ajiridhishe kwamba anayeongea naye ndio mhusika.

Jaji Mfawidhi alisema kuwa Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi Kisutu na Kinondoni kuondoa dhana ya kwamba Mahakama hizo haziwezi kuondoa kesi zote za mlundikano.

“Kumekuwa na dhana kwamba kesi ni nyingi na haziwezekaniki, hiyo ni dhana tu ambayo pia ilikuwepo Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam. Sasa mashauri hayo yamepungua kama siyo kuisha kabisa,” alisema Mhe. Maghimbi.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi waliwataka Viongozi hao kusimamia rasilimali za Mahakama, hasa majengo mapya ili yabaki katika ubora wake.

Katika kikao hicho, Mhe. Maghimbi pia aliwakumbusha wajumbe kuwa   ukaguzi wa Magereza ufanyike mara kwa mara na sio kusubiri mpaka kutembelea, kwani Mahabusu wengine hawawezi kuongea pindi wakitembelewa.

Alitumia fursa hiyo kuwapongeza Wafawidhi hao kwa kuafanya vizuri kwenye mashauri kutoka katika mlundikano wa mashauri uliokuwepo awali kwani jitihada kubwa imefanyika.

Katika kikao hicho, wajumbe waliadhimia kwamba kila Mahakama ya Mwanzo iwe na rejista ya kuandika matukio yote yanayotokea kwa siku kama kuna mtu kaja kutaka huduma yoyote.

Pia waliadhimia kila Hakimu Mfawidhi akague akaunti yake ya mirathi ili kujua kama kuna fedha ambazo hazijalipwa ili zilipwe kwa wahusikana na kama wahusika hawajulikani watafute kwa namna yoyote ili waweze kulipwa.

Azimio lingine ni kwamba kwa mahakama ambazo zimekuwa na mlundikano  wa mashauri kuondoa dhana hiyo na hatua za makusudi zichukuliwe.

Kikao hicho kilihudhuliwa na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya, Watendaji, Maofisa Utumishi na Maafisa Tawala, Wahasibu na Wakaguzi wa Ndani,  Maofisa TEHAMA, Mafundi Sanifu, Ofisa Kumbukumbu na Wasaidizi wa Kumbukumbu wa  Kanda ya Dar es Salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi na Mwenyekiti akifungua kikao hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Moses Mashaka, ambaye ni Katibu wa kikao hicho akisoma agenda.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (katikati), kushoto ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe Mary Moyo na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Moses Mashaka.

Wajumbe wa menejimenti wakiendelea na kikao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akibadilishana mawazo na  Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe Abubakar Kunenge.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.