Na MWANAIDI MSEKWA-Mahakama, Kazi
Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam hivi karibuni ilifanya
kikao cha Baraza la Wafanyakazi kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji.
Baraza hilo ambalo lilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri
ya Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani, liliongozwa na
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. David
Ngunyale.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, Mhe. Ngunyale, ambaye pia
ni Mwenyekiti
wa Baraza hilo aliwashukuru Viongozi
wote waliowezesha kufanyika kwa Baraza hilo.
‘Baraza
la Wafanyakazi ni chombo muhimu kinachowakutanisha
meza moja Wafanyakazi pamoja na Uongozi ambao ni Mwajiri kwa
ajili ya kujadili, kutathimini na kuangalia ustawi wa Wafanyakazi
na thamani ya Mfanyakazi na ya yule anaye hudumiwa,’ alisema.
Alieleza pia kuwa Baraza hilo ni muhimu ambalo
kila mmoja anahitaji ushiriki wa pekee kwa kutoa maoni na kuhoji
ili kuweza kujenga malengo mahususi yanayohusu Wafanyakazi,
mazingira ya kazi, nidhamu na kujengeana uwezo.
Mwenyekiti huyo aliwapongeza Watumishi katika
ngazi zote za Mahakama, Kanda ya Dar es Salaam kwa kazi nzuri wanazofanya kwani kazi
kubwa imefanyika na mafanikio yanaonekana.
‘Changamoto
za watu wasio wajibika ni chache sana katika maeneo ya kazi na ambazo
zinashughulikiwa kwa ukaribu na kuhakikisha
hazileti athari zinazoweza kuleta madhara kwa Wananchi
wanaotegemea huduma katika Mahakama,’ Jaji Ngunyale
alisema.
Aliwataka
kusimamia maelekezo yote yanayotolewa na Viongozi, akiwemo Jaji
Mkuu, Jaji Kiongozi na wengine kupitia waraka mbalimbali katika
kuhakikisha kazi zinaenda kwa jinsi ilivyopangiliwa.
Jaji Ngunyale alitumia fursa hiyo kuwakumbusha msisitizo
wa Jaji Mkuu kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano-TEHAMA-
ili kurahisisha kazi na kuwafikia Wananchi kwa
kupitia mifumo iliyopo.
‘Kufanya
hivi inasaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri, lengo ni
kuhakikisha kuwa Mwananchi hatumii gharama kubwa katika kuendesha kesi
yake,’ alisema.
Katika mkutano huo,
Mtendaji wa Mahakama, Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Moses Mashaka aliwasilisha taarifa ya utendaji,
matumizi ya teknolojia na hali ya miundombinu ya
majengo ya Mahakama inayoendelea
kuboreshwa.
Naye Naibu Msajili Mwandamizi
wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe.
Mary Moyo alielezea hali ya uendeshaji na takwimu za mashauri na kuwahimiza Mahakimu kuongeza
kasi ya uondoshaji mashauri na kuongeza jitihada za makusudi katika kila ngazi
ya Mahakama ili kufikia malengo ya kitaifa kwa kupunguza au kuondoa kabisa mlundikano.
Kwa kutambua na
kuthamini jitihada na mchango wa Watumishi katika
utendaji kazi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda
ya Dar es Salaam, Mhe. Salma
Maghimbi alimchagua Bi. Riziki Sakoro, ambaye ni Msaidizi wa
Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Bungu, Wilaya ya Kibiti katika
Mkoa wa Pwani, kuwa Mfanyakazi Bora wa Kanda kwa mwaka 2025.
Meza Kuu ikiongoza kuimba Wimbo wa Mshikamano, katikati ni Mwenyekiti wa
Baraza, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. David
Ngunyale, aliyeshika kipaza sauti ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi na upande
wa kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa Pwani Mhe.
Joyce Mkhoi.
Wajumbe wakiwa katika kikao.
Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Bw. Moses Mashaka
akiwasilisha taarifa ya utendaji wa shughuli za kimahakama.
Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es
Salaam, Mhe. Mary Moyo akielezea hali ya uendeshaji na takwimu za mashauri.
Mfanyakazi Bora Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Riziki Sakoro, ambaye ni
Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Mwanzo Bungu, Wilaya ya Kibiti katika Mkoa
wa Pwani.
Meza Kuu pamoja na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Dar es
Salaam -picha mbili juu na picha mbili chini-wakiwa katika picha ya pamoja.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Morogoro.