- Mhimili wa Mahakama
wapata Makao Makuu mapya
- Rais Samia azindua
jengo kubwa la kisasa Dodoma
- Jengo hilo la sita
duniani, la kwanza Afrika
Na FAUSTINE
KAPAMA-Mahakama, Dodoma
Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 5 Aprili, 2025
ameandika historia mpya Tanzania baada ya kuzindua jengo jipya la Makao Makuu
ya Mahakama ya Tanzania jijini hapa.
Hatua hiyo inaufanya
Mhimili huo wa Dola kuwa na Makao Makuu mapya ambayo, hapo awali yalikuwa
katika jiji la kibiashara, Dar es Salaam. Jengo hilo lenye ukubwa wa mita za
mraba 63,244, kwa majengo ya Makao Makuu ya Mahakama, ni la sita duniani na la
kwanza Afrika.
Jengo la Makao Makuu
ya Mahakama lililogharimu kiasi cha bilioni 129.7 za Kitanzania lina jumla ya
vyumba vya ofisi 510 vyenye samani za kisasa, vyumba vya Mahakama za wazi 10,
ukumbi mkubwa wa mikutano wenye uwezo wa kuchukua watu 346 na kumbi ndogo 22 za
mikutano.
Sherehe za uzinduzi
wa jengo hilo lililopo katika eneo la Tambuka Reli, zilianza saa 2.30 asubuhi
na kuhudhuriwa na Viongozi wa Serikali, Bunge, Mahakama, Watumishi, Wastaafu na
Wananchi kutoka maeneo mbalimbali katika jiji la Dodoma, ambalo ni Makao Makuu
ya Tanzania.
Katika sherehe hiyo,
Rais Samia pia alizindua Nyumba za Makazi ya Majaji zilizopo katika eneo la Iyumbu,
pembezoni mwa barabara inayoelekea Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), ambazo
zimegharimu kiasi cha bilioni 42.3 za Kitanzania.
Kadhalika, Mkuu wa
Nchi alizindua Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama, lililopo
pembezoni mwa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, ambalo limegharimu
kiasi cha bilioni 14.3 za Kitanzania.
Rais Samia aliwasili
katika eneo la sherehe hiyo majira ya saa 5.00 hivi asubuhi na kupokelewa na
wenyeji wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.
Wakati wa mapokezi
hayo, walikuwepo pia Viongozi wengine wa Mahakama, wakiwemo Jaji Mkuu wa
Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania,
Mhe. Eva Nkya.
Viongozi wengine ni
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,
Mhe. Rosemary Senyamule na wengine wengi.
Baada ya kuwasili
katika viunga vya Makao Makuu mapya ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Samia
alielekea kwenye eneo maalum lililokuwa limeandaliwa kwa ajili ya kupanda mti
wa kumbukumbu.
Viongozi wengine
waliopanda miti wakati huo ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan
Abdalla na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher
Mohamed Siyani.
Baada ya tukio hilo,
Mhe. Prof. Juma alimwongoza Rais Samia kwenye eneo la uzinduzi ambapo alipata
maelezo mafupi kuhusu miradi mitatu ya majengo ambayo yamezinduliwa, yaani
Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Nyumba za Makazi ya Majaji na
Jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Rais Samia, baada ya
kupata maelezo hayo, alifunua kitambaa maalum kwenye jiwe la uzinduzi wa Jengo la
Makao Makuu kama ishara ya uzinduzi rasmi wa majengo hayo matatu na baadaye kukata
utepe.
Zoezi hilo
lilimwezesha Rais Samia kuingia ndani na kuanza kulitembelea rasmi jengo hilo la
Makao Makuu ya Mahakama lenye sakafu tisa na mbawa tatu, yaani Mahakama ya
Juu/Upeo (Supreme Court), Mahakama ya Rufani (Court of Appeal) na Mahakama Kuu,
ambazo katikati zinaunda eneo la Ofisi za Utawala.
Rais Samia alianza
kutembelea Chumba kikubwa cha kisasa cha wazi cha kuendeshea mashauri ambacho
kimefungwa vifaa bora vya teknolojia na mifumo ya kisasa, ikiwemo ule wa
kusikiliza mashauri kupitia Mkutano Mtandao na ule wa Tafsiri na Unukuzi
unaowawezesha Majaji na Mahakimu kuendesha mashauri bila kuandika mwenendo kwa
mkono.
Baadaye, Rais Samia
aliongozwa kwenye Chumba Maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa za Kimahakama
(Judiciary Situation Room) kinachowawezesha Viongozi wa Mahakama kujua kila
kitu kwa wakati mmoja kinachofanyika katika Mahakama zote nchini.
Mhe. Dkt. Samia pia
alitembelea Chumba cha Huduma kwa Mteja (Customer Service Center), ambacho kina
Watumishi wanaofanya kazi kwa masaa 24 kupokea mrejesho, yaani malalamiko,
pongezi na changamoto mbalimbali zinazohusu huduma za utoaji haki kwa ujumla
kutoka kwa Wananchi.
Kadhalika, Mhe. Dkt.
Samia aliongozwa kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu na kujionea kumbukumbu kadhaa ikiwemo
picha za Majaji Wakuu ambao wamehudumu kabla na baada ya uhuru hadi sasa. Akiwa
ndani ya ofisi hiyo, Rais Samia alifanya mazungumzo mafupi na Jaji Mkuu.
Baada ya kutembelea
maeneo hayo, Rais Samia alielekea kwenye eneo maalum lililokuwa limeandaliwa
kwa ajili ya kukabidhi funguo baada ya kuzindua na kutembelea jengo hilo la Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania.
Rais Samia alikabidhi
funguo tatu kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, moja wa Makao Makuu ya Mahakama, mwingine
wa Makazi ya Majaji na tatu wa Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa
Mahakama, tukio lililopokelewa kwa shangwe, nderemo na vifijo na Wananchi waliokuwa
wamefurika kuzidi uwezo wa eneo lililokuwa limeandaliwa kwa ajili ya sherehe hiyo.
Baada ya zoezi hili
lililoongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Samia, akiwa
ameongozana na Wenyeji wake, alielekea Jukwaa Kuu kabla ya Bendi ya Jeshi la
Polisi kuwaongoza Watanzani kuimba na Wimbo wa Taifa na ule wa Afrika Mashariki
kwenye sherehe iliyokuwa inarushwa mubashara na vyombo mbalimbali vya Habari ya
Kimataifa na Kitaifa, ikiwemo mtandao wa Mahakama ya Tanzania.
Muda mchache baada
ya Rais Samia kukaa kwenye nafasi yake, Muongozaji wa Sherehe hiyo, Bw. Shaban Kisu, ambaye alishirikiana kwa karibu
na Mzee Peter Mavunde pamoja na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mashauri wa Mahakama
ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha, aliendelea na ratiba nyingine, ikiwemo
kutoa nafasi kwa Viongozi mbalimbali kuzungumza na Taifa.
Sherehe hizo
zimepambwa na burudani kutoka vikundi mbalimbali, ikiwemo Kwaya ya Mahakama ya
Tanzania, maarufu kama Ng’aring’ari, Kwaya ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Kwaya ya Utumishi wa Umma. Kulikuwa pia na vikundi vya ngoma vya
Kibati kutoka jijini Dodoma na Nyota kutoka Zanzibar.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto-akimkabidhi ufunguo wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwenye sherehe ya uzinduzi wa Majengo Matatu ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Nyumba za Makazi za Majaji na Jengo la Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto-akikabidhi ufunguo wa Nyumba za Makazi ya Majaji.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto-akikabidhi ufunguo wa Jengo la Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-katikati-akijiandaa kukata utepe kama ishara ya uzinduzi wa Majengo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Makazi ya Majaji na Tume ya Utumishi wa Mahakama, huku Viongozi wengine wakishuhudia. Picha chini akikata utepe huo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-wa pili kulia- akifungua kitambaa maalum kuashiria uzinduzi wa majengo hayo.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-juu na chini- akipata maelezo mafupi kuhusu miradi ya ujenzi wa majengo hayo kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.
Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Kalege Enock akitoa maelezo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan namna Chumba Maalum cha Mifumo ya Kutolea Taarifa mbalimbali za Mahakama kinavyofanya kazi. Picha chini akipata maelezo kwenye Chumba cha Huduma kwa Mteja.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongozwa na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania kuelekea kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu wa Tanzania. Picha chini akiingia kwenye eneo la Ofisi hiyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini kitabu cha wageni akiwa kwenye Ofisi ya Jaji Mkuu.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa ndani ya Ofisi ya Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimwonyesha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan moja ya picha ya majengo ya Mahakama ya zamani yaliyotumiwa na Majaji.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan-kushoto- akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimwagilia mti wa kumbukumbu kufuatia uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimwagilia mti wa kumbukumbu kufuatia uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Kikundi cha Ngoma cha Kibati kutoka Zanzibar kikitumbuiza kwenye uzinduzi huo huku Viongozi na wageni mbalimbali wakimiminika kuwatunza.
Kwaya ya Mahakama ya Tanzania, maarufu Ng'aring'ari kikikonga mioyo ya Viongozi na wageni mbalimbali waliohudhuria uzinduzi huo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwaaga Wananchi baada ya kuhitimishwa kwa sherehe ya uzinduzi huo.