Jumatatu, 30 Juni 2025

KAMPUNI YA URUSI, MWAJIRIWA KUTOKA UKRAINE WAKAA MEZA MOJA

  • Wakubali kusuluhishwa kwenye mgogoro wa kikazi kuhusu mapunjo ya mshahara

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, imefanikisha kusuluhisha mgogoro wa kazi kati ya Mwajiri, Kampuni la Maendeleo Technologies inayoongozwa na Raia wa Urusi na Mwajiriwa, Bw. Sergiy Lyeshchynskyy, ambaye ni Raia wa Ukraine, uliokuwa unahusu mapunjo ya mishahara.

Usuluhishi huo uliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, kwenye shauri la kazi lililowakutanisha Kampuni hiyo na Kamishna wa Kazi Tanzania, aliyemwakilisha Mwajiriwa huyo.

Kufuatia usuluhishi huo, kampuni hiyo imekubali kulipa kwa awamu mbili Dola za Kimarekani 40,000, ambayo ni zaidi ya Shilingi za Kitanzania milioni 100 kwa Mwajiriwa huyo, ambaye alikuwa Fundi Mitambo katika kampuni hiyo inayojihusisha na kukodi mitambo ya uchimbaji madini.

‘Mwajiri atamlipa Mwajiriwa Dola za Kimarekani 20,000 siku au kabla ya tarehe 30 Juni, 2025 na kiwango kitakachobaki cha Dola za Kimarekani 20,000 zitalipwa siku au kabla ya tarehe 31 Julai 31, 2025 na kufanya jumla ya Dola za Kimarekani 40,000 ya madai yote,’ inaeleza sehemu ya amri iliyotolewa hivi karibuni.

Katika makubaliano hayo, Mwajiri pia amekubali kulipa gharama za shauri ambazo ni sawa na asilimia tano ya Dola za Kimarekani 40,000 (Dola za Kimarekani 2,000) moja kwa moja kwa Wakili wa Mwajiriwa.

Kadhalika, Mwajiri amekubali kutoa tiketi ya ndege kwa mwajiriwa ya kurudi nchini kwake siku au kabla ya tarehe 31 Julai, 2025.

‘Kama Mwajiri atashindwa kutekeleza malipo hayo kama walivyokubaliana, Mwajiriwa atakuwa na haki ya kuomba amri ya utekelezaji wa makubaliano hayo dhidi yake,’ inaeleza sehemu ya amri hiyo.

Kukamilika kwa mgogoro huu kunatoa somo kuwa usuluhishi una faida nyingi, ikiwemo kama ukisimamiwa vizuri unawapatia nafasi  waajiri na waajiriwa kujielekeza zaidi katika shughuli za uzalishaji na kukuza uchumi endelevu kwa maslahi yao na kwa Taifa, kuliko kupoteza muda mwingi pamoja na rasilimali fedha katika kufuatilia migogoro kwenye hatua ya uamuzi na marejeo.

Usuluhishi pia ni njia inayoweza kumaliza shauri kwa wakati na kwa urafiki na unaepusha upatikanaji wa tuzo isiyotekelezeka, mfano: Wakati kesi inaisha mdaiwa wa hukumu ana kuwa hana kitu cha kumlipa, mmiliki wa tuzo, kwa sababu ya muda mrefu ulitumika kusikiliza shauri lake na pengine anakuwa amefirisika.

Aidha, usuluhishi unaondoa uadui baina ya pande mbili zenye mgogoro na ukifanywa vizuri unaponya.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina.


Jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi.

JAJI MWAKAPEJE AFANYA ZIARA YA MAHAKAMA GEITA

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita

Hivi karibuni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje alifanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama kwenye Kanda hiyo ili kujionea maendeleo ya kiutenda, kuwaongezea maarifa katika utoaji haki Mahakimu na Watumishi wengine pamoja na kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili.

Mhe. Mwakapeje alifanya ziara hiyo kwa niaba ya Jaji Mfawidhi, Mhe. Kevin Mhina kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mahakama ya Wilaya Geita na Mahakama za Mwanzo Nyankumbu, Katoro, Bugando na Butundwe.

Akiwa katika ziara hiyo, Jaji Mwakapeje alijionea jinsi Mahakama hizo zinavyokwenda na kasi aliyoelekeza na Jaji Mfawidhi, ikiwemo kusikiliza mashauri kwa wakati na kwa kufuata misingi iliyowekwa.

Akizungumuza na Watumishi katika Mahakama hizo, Mhe. Mwakapeje aliwaasa kujiepukane na vitendo vya rushwa na kufanya kazi kwa upendo na ushirikiano.

Katika ziara hiyo, Jaji Mwakapeje aliambatana na Naibu Msajili, Mhe. Fredrick Lukuna, Mtendaji wa Mahakama Geita, Bi. Masalu Kisasila, Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, Mhe. Clefas Waane, Kaimu Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Bruno Bongole na Viongozi wengine.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje akisaini kitabu cha wageni katika Mahakama ya Mwanzo Butundwe wilayani Geita.

Kaimu Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Geita, Mhe. Bruno Bongole akiwakaribisha timu ya ukaguzi iliyoongozwa na Jaji Mwakapeje katika Mahakama ya Mwanzo Katoro.

Jaji Mwakapeje akikagua majalada kwa njia ya mfumo katika Mahakama ya Mwanzo Katoro.

Watumishi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Geita pamoja na Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu wakiwa kwenye kikao na Jaji Mwakapeje.


 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje- katikati kwenye mstari wa kwanza pamoja na Viongozi wengine wakiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Katoro wilayani Geita.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

 

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJIKITA KIMKAKATI VIWANJA VYA 'SABASABA'

  •         Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Mahakama awaita wananchi kupata huduma na elimu
  • Huduma ya usikilizaji mashauri kwenye Mahakama Inayotembea nayo yatolewa moja kwa moja viwanjani hapo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam 

Mahakama ya Tanzania imeweka kambi katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba), 2025 yanayoendelea kufanyika katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam kwa lengo la kutoa huduma na elimu kwenye masuala mbalimbali ya Mahakama na sheria kwa ujumla.

Kwa mwaka huu, Viongozi na watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau mbalimbali ambao ni watalaam na wabobezi katika masuala ya kisheria wanaendelea kutoa huduma na elimu ya sheria kwa muda wote wa Maonesho ambayo yameanza tarehe 28 Juni, 2025.

Katika kipindi chote cha Maonesho, Mahakama inatoa huduma mbalimbali zikiwemo za kusikiliza Mashauri kwenye Mahakama Inayotembea ‘Mobile Court Services’, kutoa Msaada wa Kisheria ‘TLS’, elimu kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Mahakamani na safari ya Mahakama kuelekea Mahakama Mtandao ‘e-Judiciary’. 

Akizungumza katika mahojiano maalum leo 30 Juni, 2025 katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya ushiriki wa Mahakama katika Maonesho ya hayo, Mhe. Hussein Mushi ametoa rai kwa wananchi kutumia nafasi adhimu inayotolewa na Mahakama kwa kuwaleta pamoja watumishi wake na wadau katika kutoa elimu ya sheria bure na kuelimisha taratibu mbalimbali za kupata haki Mahakamani.

“Nawaomba wananchi kutumia fursa hii ya maonesho kuja kutoa maoni, malalamiko pamoja na kupata msaada wa kisheria kutoka kwa Mawakili kutoka Chama cha Mawakili wa Kujitegemea Tanganyika (TLS), Kituo cha Haki za Binadamu na Msaada wa Kisheria pia kujua taratibu mbalimbali za Kimahakama,” amesema Mhe. Mushi.

Aidha, ametoa wito kwa wananchi wote wa Dar es Salaam na Mikoa ya karibu kufika katika banda la Mahakama. 

Huduma nyingine zinazotolewa katika banda la Mahakama ni elimu kuhusu huduma na taratibu mbalimbali za ufunguaji wa mashauri, yakiwemo mashauri ya mirathi, elimu kuhusu Mahakama ya Watoto, kuelezea manufaa au faida za Mfumo ulioboreshwa wa Kusajili, Kuratibu na Kusimamia Uendeshaji wa Mashauri (Advanced Case Management System).

Nyingine ni kutoa elimu kwa wananchi kutambua umuhimu wa kutumia Kituo cha Huduma kwa Mteja ‘Call Centre’ ya Mahakama ya Tanzania kutoa malalamiko na maoni yao.

Kueleza huduma zinazotolewa na ngazi mbalimbali za Mahakama ikiwemo Divisheni za Mahakama Kuu na Kituo cha Usuluhishi.

Katika kipindi chote cha Maonesho hayo, Mahakama ya Tanzania ipo pamoja na baadhi ya Wadau wake ambao ni Tume ya Utumishi wa Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Chama Cha Majaji Wanawake Tanzania (TAWJA),  Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Chama Cha Wanasheria Tanganyika (TLS) ambao wote wanatoa elimu kuhusu maeneo yao.

Banda la Mahakama ya Tanzania linapatikana ndani ya Viwanja vya Mwalimu Nyerere almaarufu Viwanja vya Sabasaba na linapatikana mkabala na banda la JKT.


Muonekano wa Banda la Mahakama ya Tanzania lililopo ndani ya Viwanja vya Mwalimu Nyerere mkabala na banda la Jeshi la Kujenga Taifa (JKT). Huduma mbalimbali ikiwemo elimu kuhusu Mahakama na Sheria kwa ujumla zinatolewa.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Ushiriki wa Mahakama ya Tanzania kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba), 2025, Mhe. Hussein Mushi akizungumza kuhusu ushiriki wa Mhimili huo kwenye Maonesho ya (Sabasaba). 

Mmoja kati ya wananchi waliofika katika banda la Mahakama akisubiri kupata huduma kwenye Mahakama Inayotembea iliyopo ndani ya Viwanja vya Mwalimu Nyerere (Sabasaba) vilivyopo barabara ya Kilwa-Temeke jijini Dar es Salaam.



Idara, Divisheni na wadau mbalimbali waliopo kwenye Banda la Mahakama ya Tanzania kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba), 2025.


Wananchi wakipata msaada wa kisheria kutoka kwa Mawakili wa Kujitegemea kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS).

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

 

Ijumaa, 27 Juni 2025

VIONGOZI KANDA YA MOSHI WAKAGUA MRADI WA UJENZI MAHAKAMA YA WILAYA SIHA

  • Jaji Mfawidhi amtaka Mkandarasi kuzingatia muda wa ukamilishwaji wa mradi huo  
  • Wazungumza pia na Watumishi wa Mahakama za Wilaya Siha, Hai
  • Wawakumbusha watumishi kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma

Na PAUL PASCAL, Mahakama-Moshi

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi imehitimisha ziara ya ukaguzi katika Mahakama za Wilaya za Hai na Siha sambamba na kufanya ukaguzi wa Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Siha. 

Ukaguzi huo ulifanyika tarehe 24 Juni, 2025 na kuongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella aliambatana na Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje pamoja na Mtendaji wa Mahakama-Kanda ya Moshi, Bi. Maria Itala. 

Baada ya ukaguzi wa Mahakama za Wilaya ya Siha na Hai, Jaji Mfawidhi pamoja na wajumbe alioambatana nao katika ukaguzi huo walipokea taarifa na maelezo ya kina kutoka kwa mkandarasi anaetekeleza mradi huo sambamba na kutoa maelekezo ya aliyoyaona wakati akikagua mradi huo.

“Nimepita nimejionea yote yanayoendelea kazi ni nzuri ila changamoto iko kwenye kasi ya kukamilisha kazi hii. Mkandarasi ongeza kasi ya utendaji kwa taarifa mradi huu unapaswa kukabidhiwa ifikapo tarehe 30 Juni mwaka huu ila kwa kazi ambazo hazijafanyika sidhani kama siku hizi sita zilizosalia mtaweza kukamilisha,” alisema Mhe. Dkt. Mongella.

Kwa upande wake, Mkandarasi anayetekeleza mradi huo, ‘Pioneer Construction’ kupitia Mhandisi anayesimamia mradi huo, Mhandisi Mike Laswai alibainisha kazi zilizosalia kukamilisha mradi huo.

“Mhe. ‘Jaji Mfawidhi’ nikushukuru sana kwa maelekezo yako naahidi kuongeza kasi katika kukamilisha kazi hii kwa sasa nguvu kubwa tunaweka katika kazi za nje yaani kutengeneza bustani, kuweka usawa wa ardhi pamoja na kukamilisha uzio tutajitahidi ipasavyo kuendana na muda ili kampuni yetu isikwamishe matakwa ya mteja wetu,” alisema Mhandisi Laswai.

Katika hatua nyingine wakati wa ukaguzi huo, viongozi hao walizungumza  na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Siha na Hai pamoja na Mahakama za Mwanzo Ngarenairobi na Bomang’ombe kwa nyakati tofauti ambapo Mhe. Dkt. Mongella aliwakumbusha watumishi kufanya kazi kwa weledi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao pamoja na kutunza rasilimali za Mahakama kufuatia uboreshaji unaofanywa na Mahakama ya Tanzania.

“Kwanza kabisa niwapongeze watumishi wote wa Mahakama hizi kwa kutimiza majukumu yenu ya msingi hali inayowezesha kuondokana na mashauri ya mlundikano katika vituo vyenu, vilevile niwasihi kuendelea kuchapa kazi kwa weledi, kutunza rasilimali zetu zinazotuwezesha kutekeleza majukumu yetu, hivi karibuni tunakwenda kuwa na majengo ya kisasa niwaombe tuyatunze,” alisema Jaji Mongella.

Naye, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje alisema, “nawasihi watumishi wa Mahakama za Wilaya za Hai na Siha kutambua na kuiishi Dira ya Mahakama ya Tanzania na kuongeza ufanisi katika matumizi ya TEHAMA ili kuongeza kasi ya utoaji haki kwa wakati.”

Mhe. Mwaiseje aliwapongeza watumishi wa kada zote na kusema kuwa anaamini utendaji mzuri waliouona katika vituo hivyo ni kufuatia ushirikiano uliopo.

Aidha, Naibu Msajili huyo, aliwahishi watumishi wote kushiriki kikamilifu katika mabadiliko ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuendana na kasi ya mabadiliko kuboresha utoaji haki.

“Sote ni mashahidi kwa sasa suala la matumizi ya teknolojia halina mbadala hivyo hatuna budi kila mmoja kwa nafasi yake kuhusika katika mabadiliko haya ili tuweze kuwahudumia wananchi ipasavyo kwa Mahakama za Mwanzo ni lazima tusajili na kutoa mashauri yote katika mfumo wetu wa ‘primary courts App’ kama ilivyo kwa Mahakama za Wilaya kwenye mfumo Wa e- CMS  na Mahakama Mtandao,” alisema Naibu Msajili huyo.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Bi. Maria Itala aliwahimiza watumishi wa Mahakama za wilaya Hai  na Siha kutambua umuhimu wa kutunza rasilimali zote za Mahakama pamoja na kuwa na maadili ya utumishi wa umma.

“Kama ambavyo wamekwisha sema mengi mazuri watangulizi wangu niwaombe kila mmoja wetu kuona thamani ya uboreshaji uliofanywa na Mahakama ya Tanzania katika Wilaya hizi.ni jukumu letu kulinda rasilimali zote za Mahakama, tujitahidi kuishi maisha ya kizalendo ikiwa ni sambamba na kuheshimu maadili ya mtumishi wa umma sitegemei kusikia malalamiko juu ya vitendo visivyo vya kimaadili katika vituo vyetu,” alisema Bi. Itala.

Ukaguzi huo ni wa robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2024/2025 ambao unakwenda kukamilisha ukaguzi wa jumla ya Mahakama za wilaya sita zinazounda Kanda ya Moshi. Ukaguzi huu ni wa kawaida na hufanyika kwa mujibu wa miongozo ya ukaguzi kwa Mahakama ya Tanzania.

Ukaguzi huo ulilenga kukagua shughuli zote za utoaji haki na uendeshwaji wa Mahakama hizo katika kipindi hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt Lillian Mongella akikagua maeneo mbalimbali katika eneo la Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Siha ili kujionea shughuli zinazoendelea katika mradi huo.

Msimamizi wa Mradi wa Ujenzi Mahakama ya Wilaya Siha, Mhandisi Mike Laswai (kushoto) akitoa maelezo kuhusu mradi huo kwa Jaji  Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella wakati wa ukaguzi uliofanyika kwenye mradi huo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Lillian Mongella (katikati) akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika katika eneo la Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Siha kwa ajili ya ukaguzi wa Mradi huo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Lillian Mongella (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa mahakama ya Mwanzo Ngarenairobi Wilayani Siha wakati wa ukaguzi huo uliofanyika tarehe 24 Juni, 2025.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Lillian Mongella (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Bomang'ombe wilayani Hai wakati wa ukaguzi huo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)









 

 

 

 

Alhamisi, 26 Juni 2025

RC KATAVI ATEMBELEA UJENZI WA JENGO LA KITUO JUMUISHI CHA UTOAJI HAKI

·      Aziagiza Tanesco, Mamlaka ya Maji kutatua changamoto za Maji na Umeme

Na ALLY RAMADHANI – Mahakama Katavi

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko, ameitaka Mamlaka ya Maji na Shirika la umeme Tanzania (TANESCO) mkoani humo kutatua changamoto za maji na umeme kwenye eneo la mradi wa ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Katavi ili mradi huo ukamilike kwa wakati.

Akizungumza wakati alipotembelea mradi wa ujenzi wa jengo hilo la Mahakama, Mkuu huyo wa Mkoa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama mkoa wa Katavi alisema jengo hilo linalojengwa na Kampuni ya M/s AZHAR Construction Co. Ltd. linatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu mpaka minne ijayo.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa alisema ujenzi wa Kituo hicho hauna budi  kukamilishwa kwa kwa wakati na kwa viwango na ubora uliokusudiwa kwa mujibu wa mkataba wa ujenzi wa jengo hilo.

“Kukamilika kwa Kituo Jumuishi cha Utoaji haki Katavi, kutasogeza huduma za Mahakama karibu zaidi na wananchi na kupunguza kwa kiasi kikubwa adha wanayopata ya kutoka Mkoa wa Katavi Kwenda Sumbawanga mkoani Rukwa kufuata Huduma za Mahakama Kuu, ”alisema Mkuu wa Mkoa.

Akitoa taarifa ya  maendeleo ya mradi wa ujenzi wa jengo hilo kwa Mkuu wa mkoa, Msimamizi wa Mradi huo Mhandisi Victor Vedasto Ntungamo, alisema mradi huo umefikia asilimia 57 na kwa upande wa jengo umefikia  asilimia 60. Aliongeza kuwa mradi huo unahusisha sehemu tatu ambazo ni jengo Kuu, eneo la nje (uzio, mgahawa, chumba cha ulinzi) pamoja na Manzari ( Landscaping).

Aidha, Mhandisi huyo alimweleza Mkuu wa Mkoa wa Katavi kuwa mradi huo unakabiliwa na changamoto ya kukosekana kwa umeme na maji ambazo kwa kiasi kikubwa zinachangia kupunguza kasi ya ujenzi wa jengo hilo.

Nguzo ya pili ya Mpango Mkakakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania inasisitiza Utoaji Haki kwa wakati. Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huu kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki kwa wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hii.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko (mwenye miwani) akiwa kwenye eneo la ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki mkoa wa Katavi alipotembelea hivi karibuni.

Mhandisi Victor Ntungamo, akitoa maelezo kuhusu maendeleo ya mradi wa ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mkoa wa Katavi kwa Mkuu wa mkoa huo Mhe. Mwanamvua Mrindoko.

(Habari hii Imehaririwa na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama)

 

 

 

Jumatano, 25 Juni 2025

MAHAKAMA SONGEA YAENDESHA MAFUNZO KUHUSU UKATILI KIJINSIA, KINGONO

Na NOEL SYLIVESTER-Mahakama, Songea

Mahakama Kanda ya Songea inaendesha mafunzo maalum kuwajengea uelewa Mahakimi na Wadau mbalimbali kuhusu kuepuka kutonesha majeraha kwa waathirika na mashahidi wa ukatili wa kijinsia na kingono.

Mafunzo hayo ya siku tatu yalifunguliwa jana tarehe 24 Juni, 2025 na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha, yakikutanisha Mahakimu Wakazi, Waendesha Mashtaka na Maafisa Ustawi wa Jamii.

Mafunzo hayo ni endelevu, yakiwa yameandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Irish Rule of Law International (IRLI), kwa ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo washiriki katika kushughulikia mashauri ya ukatili wa kijinsia kwa kuzingatia athari za kiakili na kihisia kwa waathirika, sambamba na kuheshimu haki za watuhumiwa.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mhe. Karayemaha alisisitiza Wanasheria, Polisi na Mahakama kuwatendea ubinadamu na heshima waathirika wanapofikishwa mbele yao na kuheshimu waathirika wa ngono na unyanyasaji kijinsia pale kesi au mashauri yanapofikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Wawezeshaji wa mafunzo hayo ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe Victoria Nongwa pamoja na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga.  Wapo pia waratibu wa mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mahakama Kuu, Kanda ya Songea, Mhe. Goodluck Ndimbo pamoja na Patric Lipiki kutoka IJA ambao ndio watakaoongoza washiriki kupitia mijadala na mafunzo ya vitendo yenye kuhusisha uzoefu wa kiutendaji.

Mafunzo haya yatagusa maeneo mbalimbali muhimu ikiwemo: uelewa wa athari za kiakili na kihisia kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, mbinu rafiki na salama za kuwauliza maswali mashahidi wa aina hiyo, ushirikiano baina ya Taasisi katika kusaidia mashahidi waliopo katika mazingira magumu na mizania ya kulinda haki za waathirika sambamba na zile za watuhumiwa.

Washiriki watapata fursa ya kujadili matukio halisi, kushiriki mazoezi ya vitendo, na kuibua maeneo yanayohitaji uboreshaji wa kitaasisi, kujifunza kwa pamoja na kuandaa mikakati ya utekelezaji wa maarifa watakayoyapata kazini.

Mafunzo hayo yamekuwa sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania kuboresha mifumo ya utoaji haki ili iwe jumuishi, yenye huruma na inayowajali wahitaji wa huduma za haki, hasa kutoka makundi yaliyo hatarini.

Chuo cha IJA na IRLI wanatarajia kufanya tathimini ya utekelezaji wa mafunzo hayo ili kupima mafanikio yake na kuchangia uboreshaji wa muda mrefu katika upatikanaji wa haki kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na kingono.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha akitoa hotuba wakati wa ufunguzi wa mafunzo.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe Victoria Nongwa akiwa katika uwezeshaji wa mafunzo.


Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Momba, Mhe. Raymond Kaswaga akiwa katika uwezeshaji wa mafunzo.


Sehemu ya wawakilishi wakifuatilia mafunzo hayo.


Picha ya pamoja ya washiriki wa mafunzo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

Jumanne, 24 Juni 2025

JAJI NKWABI AFUNGUA MAFUNZO MAALUM YA 'SGBV'

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi amefungua rasmi mafunzo maalum kuhusu Kuepuka Kutonesha Majeraha kwa Waathirika na Mashahidi wa Ukatili wa Kijinsia na Kingono (SGBV).

Mafunzo hayo ya siku tatu, yanayoanza kufanyika kuanzia tarehe 24 hadi 26 Juni, 2025 katika Mahakama Kuu Kigoma, yamewakutanisha jumla ya washiriki 18 wakiwemo Mahakimu Wakazi, Waendesha Mashtaka, na Maafisa Ustawi wa Jamii.

Akifungua mafunzo hayo, Mhe. Nkwabi alisisitiza kuwa, ni muhimu  kutumia lugha yenye huruma, staha na weledi mkubwa, pamoja na kujenga mazingira ya kimahakama yenye usalama kwa waathirika wa ukatili huo.

Kadhalika, Jaji Nkwabi aliwahimiza washiriki kuwa makini na mbinu wanazotumia katika kushughulikia mashahidi walio katika mazingira magumu ili wasiwajengee hali ya woga au kukumbuka majeraha yao ya awali.

“Mafunzo haya yatagusa maeneo mbalimbali muhimu ikiwemo: Uelewa wa athari za kiakili na kihisia kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, Mbinu rafiki na salama za kuwauliza maswali mashahidi wa aina hiyo, Ushirikiano baina ya taasisi katika kusaidia mashahidi walioko katika mazingira magumu na Mizania ya kulinda haki za waathirika sambamba na zile za watuhumiwa,” alisema Mhe. Nkwabi.

Washiriki wa mafunzo hayo watapata fursa ya kujadili matukio halisi, kushiriki mazoezi ya vitendo na kuibua maeneo yanayohitaji maboresho ya kitaasisi. Msistizo na mkazo  vimewekwa katika kujifunza kwa pamoja na kuandaa mikakati ya utekelezaji wa maarifa watakayoyapata kazini.

Mafunzo haya ni sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania za kuboresha mifumo ya utoaji haki ili iwe jumuishi, yenye huruma, na inayowajali wahitaji wa huduma za haki hasa kutoka makundi yaliyo hatarini.

Mafunzo hayo ni ya awamu ya nne ya mwendelezo wa mafunzo kama hayo ambayo yamefanyika katika mikoa ya Tanga, hususani Wilaya ya Lushoto, Dodoma na Dar es Salaam. Sambamba na mkoani Kigoma napo Songea mkoani Ruvuma yameandaliwa mafunzo hayo na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na ‘Irish Rule’ of Law International (IRLI) na kwa ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania.

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na IRLI wanatarajia kufanya tathmini ya utekelezaji wa mafunzo hayo ili kupima mafanikio yake na kuchangia maboresho ya muda mrefu katika upatikanaji wa haki kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na kingono.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi akifungua rasmi mafunzo maalum kuhusu Kuepuka Kutonesha Majeraha kwa Waathirika na Mashahidi wa Ukatili wa Kijinsia na Kingono (SGBV) katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma.

Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Bi. Gloria Shuma akitoa neno la utangulizi kwa Mgeni rasmi na washiriki wa mafunzo hayo yanayofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo maalum kuhusu Kuepuka Kutonesha Majeraha kwa Waathirika na Mashahidi wa Ukatili wa Kijinsia na Kingono (SGBV) wakifuatilia mada iliyokuwa ikitolewa katika ukumbi wa mikutano uliopo katika jengo la Mahakama Kuu Kigoma.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya  Kigoma,  Mhe. Fadhili Mbelwa, (katikati) akimtambulisha Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo (kulia) kwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi.

Meza kuu ikiongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo (waliosimama) kuhusu Kuepuka Kutonesha Majeraha kwa Waathirika na Mashahidi wa Ukatili wa Kijinsia na Kingono (SGBV). Wa pili kushoto ni  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo, wa pili kulia ni Naibu Msajili wa Mhakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, na wa kwanza kulia ni  Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA),  Bi. Gloria Shuma na wa kwanza kushoto ni Afisa Ustawi wa Jamii, Bi Roseana Philemon.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)






MAHAKIMU KIGOMA WAPONGEZWA KUONDOSHA MASHAURI KWA WAKATI

  • Waazimia kumaliza mashauri kwa muda mfupi kabla ya kuwa mlundikano mahakamani

 Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mwendesha Mashataka Mfawidhi Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Mbwana Mgumbo amewapongeza Mahakimu wa Wilaya Kigoma kwa kazi kubwa ya kusikiliza na kuamua mashauri kwa wakati.

Bw. Mbwana alisema hayo katika kikao cha kusukuma mashauri ya jinai kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma tarehe 20 Juni, 2025 na kuoongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo.

Mwendesha Mashtaka huyo Mfawidhi alisema kuwa, Ofisi ya Taifa ya Mashataka imejipanga vema kuhakikisha inaisaidia Mahakama kuondosha mashauri yake kwa muda uliopangwa na kuhakikisha mashauri yote yanayosimamiwa na ofisi hiyo yanamalizika kwa muda uliopangwa na Mahakama.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kikao hicho ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo alisema kuwa, Mahakama inategemea uwajibikaji wa wadau wake ili kuharakisha utoaji haki kwa wakati.

Aidha, Mhe. Tarimo alilitaka jukwaa la Mawakili wa Kujitegemea Tanganyika (TLS) kuongeza Mawakili katika umoja wao mkoani Kigoma ili kuongeza kasi ya usikilizwaji wa mashauri  kwa Mahakama za Wilaya za mkoani Kigoma.

Alisisitiza kuwa, “Mahakama inatambua  juhudi kubwa za Mahakimu na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Kigoma pamoja na wadau wote wa Mahakama kwa kufanikisha umalizwaji wa mashauri 45 kabla ya kuwa mlundikano katika robo mwaka iliyopita.” 

Aidha, aliwataka Mahakimu wa Wilaya kuzingatia umri wa mashauri yaliyopo katika Mahakama zao ikiwa ni moja ya mikakati ya kuzuia mlundikano wa mashauri mahakamani.

Alisisitiza kuwa, wadau wote wasipende ahirisho la mashauri mahakamani kwa sababu zisizo za msingi katika kuisaidia Mahakama kutunza muda wake wakuondosha shauri mahakamani ili kuepuka mashauri mlundikano.

Katika kikao hicho Mahakimu wameazimia kumaliza mashauri kwa muda mfupi kabla ya kuwa mlundikano mahakamani.

Wadau walioshiriki kwenye kikao hicho ni pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa, Mahakimu wa Mahakama za Wilaya Kigoma, Kibondo, Kasulu, Uvinza, Buhigwe na Kakonko.

Wengine ni kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Ofisi ya Huduma kwa Jamii, Ofisi ya Upelelezi Mkoa, Ofisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa (TAKUKURU), Ofisi ya Uhamiaji Mkoa na Magereza Mkoa wa Kigoma.

Wajumbe wa kikao cha kusukuma mashauri ya jinai ngazi ya Mkoa wa Kigoma wakifuatilia kwa makini maelekezo ya Mwenyekiti wa kikao hicho, ambaye ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo (aliyeketi mbele kulia).

Sehemu ya wajumbe wa kikao cha wadau wa kusukuma mashauri ya jinai ngazi ya Mkoa, wakifuatilia kwa makini mjadala uliokuwa ukiendelea katika kikao wadau wa haki jinai kilicofanyika tarehe 20 Juni, 2025.

Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Kigoma, Bw. Waziri Mbwana akifafanua jambo wakati wa kikao cha wadau wa kusukumu mashauri ya jinai ngazi ya Mkoa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu Kigoma.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo
  akisisitiza jambo wakati wa kikao cha wadau wa kusukuma mashauri cha mkoa huo kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe, Mhe. Venance Mwakitalu akifuatilia kwa makini mjadala uliokuwa ukiendelea katika kikao cha wadau wa haki jinai ngazi ya Mkoa kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)

 

 



Ijumaa, 20 Juni 2025

WADAU HAKI JINAI MOROGORO WAPATIWA MAFUNZO YA UTEKELEZAJI ADHABU MBADALA

Na ASHA JUMA- Mahakama Morogoro

Wizara ya Mambo ya Ndani, kwa kushirikiana na Kamati ya Taifa ya Huduma kwa Jamii na Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro imeendesha mafunzo maalum juu ya utekelezaji wa adhabu mbadala kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Mafunzo hayo yamefanyika jana tarehe 19 Juni, 2025 katika Ukumbi wa Magadu Hotel Morogoro na yalifunguliwa na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Mjini, Mhe. Musa Kilakala.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango wa kitaifa unolenga kuwajengea uwezo wadau wa haki jinai katika maeneo mbalimbali nchini ili kukuza matumizi ya adhabu mbadala kama njia ya kupunguza msongamano magerezani na kuimarisha urejeshaji wa wahalifu katika jamii.

Aidha, mafunzo hayo yametolewa kwa lengo la kujenga uelewa mpana juu ya sheria na kanuni zinazo simamia adhabu mbadala Tanzania, kufahamu faida za utoaji wa adhabu za huduma kwa jamii kwa maendeleo ya taifa, kujadili changamoto za utekelezaji wa sheria na mapendekezo ya utatuzi wake na kuongezeka kasi ya utoaji wa adhabu mbadala.

Washiriki wa mafunzo hayo walijumuisha Majaji na Mahakimu kutoka Mahakama Kanda ya Morogoro, wakiongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Rose Ebrahim. Walikuwepo pia Maofisa wa Magereza, uangalizi wa jamii, wawakilishi wa Chama cha Mawakili Tanganyika, Jeshi la Polisi (NPS) na Wadau wengine muhimu wa haki jinai.

Mafunzo hayo yamewezeshwa na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Huduma kwa Jamii, pamoja na Bw. Ahmed Mwen-dadi na wengine.

Miongoni mwa mada zilizotolewa ni pamoja na Sheria na kanuni zinazosimamia utoaji na utekelezaji wa adhabu mbadala Tanzania, Sheria ya kifungo cha nje, Utaratibu wa uandaaji wa taarifa ya uchunguzi, Faida za utekelezaji wa adhabu mbadala na Wajibu wa Ofisa Uangalizi katika utekelezaji wa huduma kwa jamii.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Mhe. Ebrahim aliwaasa Majaji pamoja na Mahakimu juu ya matumizi ya adhabu mbadala ili kupumguza idadi kubwa ya watu gerezani pamoja na kujenga familia bora, kwani mfungwa atakua karibu na familia yake na kulea Watoto na mwenza wake.

“Tujitahidini sana kuitekeleza sheria hii ya adhabu mbadala kwani inafaida kwa jamii haswa kwenye malezi ya Watoto na husaidia mfungwa anakua karibu zaidi na familia yake , ” alisisitiza. 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe.MStephen Magoiga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Huduma kwa Jamii akitoa elimu kwa Wadau wa haki jinai.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim akitoa hotuba ya kufunga mafunzo kwa Wadau wa haki jinai.

 

Wadau mbalimbali wa haki jinai wakifatilia mafunzo-juu na chini.

 

Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe.  Musa Kilakala (katikati) akiwa katika Picha ya pamoja ya Wadau wa haki jinai na watoaji wa mafunzo ya Sheria na kanuni za adhabu mbadala Tanzania.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.