Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Kanda hiyo, Bw. Emmanuel Munda pamoja na viongozi wa Mahakama ya Wilaya ya Uyui kwa pamoja wameambatana katika ziara ya kikazi iliyolenga kukagua miundombinu ya Mahakama za Mwanzo Upuge na Imalakaseko zilizopo katika Wilaya ya Uyui mkoani Tabora.
Ziara hiyo iliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita ililenga kufanya tathmini ya hali ya miundombinu ya majengo ya Mahakama hizo ili kuangalia mazingira ya utoaji huduma za kimahakama katika maeneo hayo.
Viongozi hao waliangazia masuala muhimu yanayohusu maandalizi ya kuanzisha huduma za kimahakama katika maeneo hayo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Mahakama ya Tanzania za kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi.
Wakiwa katika Kijiji cha Upuge, viongozi hao walikutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Kata na Serikali ya Kijiji, wakiongozwa na Diwani wa Kata hiyo, Mhe. Juma Luwanga ambaye alitoa shukrani zake kwa uongozi wa Mahakama kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kusogeza huduma za haki karibu na wananchi wa Kata hiyo.
“Tunaishukuru Mahakama kwa kutambua umuhimu wa wananchi kupata huduma karibu hivyo kuamua kuanza mipango ya kuanzisha Mahakama ya Mwanzo Upuge, hatua hii ni ya kupongezwa, sisi kama viongozi wa Serikali ya Mtaa na kwa niaba ya wananchi wa eneo hili tupo tayari kushirikiana katika utekelezaji wa jambo hili,” alisema Mhe. Luwanga.
Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo alieleza kuwa, Mahakama ya Tanzania inatekeleza Mpango Mkakati wake kwa kuhakikisha kuwa huduma za utoaji haki zinapatikana kwa urahisi, ufanisi na kwa wakati na kusisitiza juu ya umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama na wadau wa maendeleo katika jamii ili kufanikisha azma ya utoaji wa haki kwa wote na kwa wakati.
Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi katika eneo lililopendekezwa kwa ajili ya uanzishwaji wa Mahakama ya Mwanzo Upuge, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Bw. Emmanuel Munda, alieleza kwamba, taratibu za awali zinaendelea vizuri na mara tu maandalizi hayo yatakapokamilika, utekelezaji utaanza mara moja lengo likiwa ni kusogeza huduma za kimahakama kwa wananchi wa eneo hilo.
"Mara baada ya mipango hii kukamilika, Mahakama ya Mwanzo Upuge itaanza kazi mara moja ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kimahakama karibu na maeneo yao," alisema Bw. Munda.
Mahakama za Mwanzo Upuge na Imalakaseko zilianzishwa miaka mingi iliyopita kama sehemu ya kuimarisha utawala wa sheria katika maeneo hayo. Mahakama ya Mwanzo Upuge ilianzishwa mwaka 1953 kwa lengo la kutoa huduma za kisheria kwa wananchi wa kijiji hicho na maeneo jirani. Hata hivyo, kwa sasa mahakama hiyo haifanyi kazi katika eneo hilo kwa zaidi ya miaka 30 kwa mujibu wa uongozi wa Kijiji cha Upuge.
Shughuli za Mahakama ya Upuge kwa sasa zinafanyikia majengo ya Wilaya ya Uyui ambayo iko takriban kilometa 30 kutoka kijiji cha Upuge. Hali hiyo inawaathiri wananchi wa eneo hilo kwa kuwa wanakutana na changamoto za usafiri na upatikanaji wa huduma za kisheria kwa wakati muafaka.
Ziara hiyo imeonesha dhamira ya dhati ya Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utoaji huduma kwa wananchi kama ilivyoainishwa kwenye Mpango Mkakati wake.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo akizungumza jambo hivi karibuni wakati wa kikao na wajumbe wa Kata na Serikali ya Upuge.
Diwani wa Kata ya Upuge, Mhe. Juma Luwanga akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kwa niaba ya wananchi wa Kata hiyo.
Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Tabora (walioketi) wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Kata na Kijiji cha Upuge wakati wa kikao baina yao.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Bw. Emmanuel Munda akielekeza jambo wakati wa ukaguzi katika jengo linalotarajiwa kukarabatiwa kwa ajili ya kuanza kutoa huduma za Mahakama ya Mwanzo Kigwa.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)