Ijumaa, 17 Oktoba 2025

MAFUNZO ELEKEZI KWA MAHAKIMU WAPYA YAHITIMISHWA

  • Msajili Mahakama ya Rufani awataka kuzingatia maadili, viapo vyao
  • Awakumbusha kazi ya uhakimu ni nyeti, haiwezi kufanywa na mtu yoyote

Na FAUSTINE KAPAMA na HALIMA MNETE-MAHAKAMA, Dodoma

Mafunzo elekezi ya siku tisa yaliyoandaliwa na Mahakama ya Tanzania, kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], kwa Mahakimu Wakazi wapya 89 yamehitimishwa leo tarehe 17 Octoba, 2025.

Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert amehitimisha mafunzo hayo yaliyokuwa yanafanyika kwenye moja ya Kumbi za Mikutano zilizopo katika jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mhe. Herbert amewaeleza Mahakimu hao walioapishwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, hivi karibuni kuwa anaamini mafunzo hayo yaliyoanza kutolewa tarehe 7 Octoba, 2025 yamekuwa ya mafanikio makubwa kwao.

‘Nimatumaini yangu kwamba katika siku tisa za mafunzo mmeweza kupata uelewa mkubwa wa viwango vya kitaaluma na kimaadili kwa nafasi mnayoenda kufanyia kazi. Napenda kuwakumbusha na kuwasisitiza kuzingatia yale yote mliyofundishwa, iwe kwa upande wa weledi wa kitaaluma au kwa upande wa unyoofu wa kimaadili,’ amesema.

Msajili wa Mahakama ya Rufani amewaeleza washiriki hao kuwa pande hizo mbili zina umuhimu kwa Hakimu kwani zinategemeana. Amesema kuwa Mahakama bora inajengwa na Maofisa wa Mahakama wenye weledi wa kutosha na maadili ya kiwango cha juu.

Mhe. Herbert amesema kuwa matendo ya kila mmoja wao yanaweza kuinua au kuharibu taswira ya Mahakama nzima kwa jamii ambao ndiyo wanailenga katika kuihudumia. Amewasihi kuzingatia mafunzo waliyopatiwa na kuishi kwa viapo vyao.

Amewakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuwa kazi ya uhakimu ni nyeti, muhimu na ya kipekee na kwamba haipo sawa na kazi nyingine yoyote. Huku akinukuu kutoka kwenye maandiko matakatifu, Msajili wa Mahakama ya Rufani amewaeleza Mahakimu hao kuwa kazi ya uhakimu inatoka kwa Mwenyezi Mungu.

‘Hivyo nyinyi Mahakimu mmekasimiwa mamlaka haya na Mwenyezi Mungu ili mtende kazi yake ya kutoa uamuzi mkiwa hapa duniani, huku mkijua uamuzi wenu utapimwa na Mwenyezi Mungu. Kazi hii ya uhakimu muichukulie kwa uzito mkubwa, umakini na uadilifu wa hali ya juu,’ amesema.

Mhe. Herbert alimnukuu pia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ambaye aliwahi kusema kwamba kazi ya uhakimu au ujaji siyo kazi ambayo inaweza kufanywa na mtu yoyote, ni kazi ambayo inahitaji umakini, uadilifu na kuwa na fikra tofauti na watu wengine.

Ametumia fursa hiyo kutoa shukrani kwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwa kutoa kibali cha kufanyika na kwa yeye mwenyewe kufungua mafunzo hayo.

Kadhalika, Mhe. Herbert ametoa shukrani kwa IJA, chini ya Uongozi wa Mkuu wa Chuo Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, kwa kuandaa na kuratibu mafunzo hayo kuanzia yalipoanza hadi kufikia tamati.

Awali akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Mafunzo wa IJA, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda amewashukuru Mahakimu hao kwa kushiriki kikamilifu kwenye mafunzo hayo ya wiki mbili.

‘Sisi kama IJA kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania tunajisikia fahari kuwa mafunzo haya yameleta ufahamu na maarifa ya kutosha kwa washiriki na imekuwa wakati mzuri kwao kukaa Dodoma na kufurahia mazingira yake,’ alisema.

Mhe. Dkt. Kisinda aliwapongeza wawezeshaji wa mafunzo hayo ambapo jumla ya mada 27 ziliwasilishwa. Amewaeleza washiriki kuwa watakubaliana na yeye kwamba maarifa waliyopata ni matokeo ya ujuzi na uzoefu wa kina ambao wawezeshaji wameupata wakati wa utumishi wao mahakamani.


Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert akizungumza wakati wa kuhitimisha mafunzo elekezi yaliyokuwa yanatolewa kwa Mahakimu Wakazi wapya 89 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda akizunguza kwenye hafla hiyo.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo [juu na chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri. 


Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo hayo [juu na chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri. 


Sehemu nyingine ya tatu ya washiriki wa mafunzo hayo [juu na picha mbili chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri. 




 

TANZIA; NAIBU MSAJILI MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA BIASHARA, MHE DKT. ANGELA TEYE AFARIKI DUNIA

Mhe. Dkt. Angela Benedict Teye enzi za uhai wake.

                                               TANZIA

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake, aliyekuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara. 

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama, Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara, Bw. Anatory Kagaruki Marehemu Dkt. Angela Teye alifikwa na umauti tarehe 16 Oktoba, 2025 katika Hospitali ya John Muir 'Medical Center' iliyopo Walnut Creek mjini California nchini Marekani alipokuwa akipatiwa matibabu.

Bw. Kagaruki amesema taratibu na mipango ya mazishi inaendelea kuratibiwa na familia.

Marehemu Dkt. Teye aliajiriwa na Mahakama ya Tanzania kwa Cheo cha  Hakimu Mkazi tarehe 29 Juni, 2007 na kupangiwa Kituo cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Tanga.

Mwaka 2012, marehemu Dkt. Teye aliteuliwa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania na alipangiwa kituo katika Divisheni ya Biashara Masjala ndogo Arusha.

Baada ya hapo alitumikia wadhifa huo katika Vituo vya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Kurugenzi ya Usimamizi wa Mashauri (DCM) na mnamo Mei 2025, alihamishiwa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara alipotumikia hadi umauti ulipomkuta.

Mahakama ya Tanzania inaungana na ndugu, jamaa na marafiki katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza msiba huo mzito wa kuondokewa na Mpendwa wetu.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA JINA LA BWANA LIHIMIDIWE.

 

 

 

 

JAJI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA TUME YA USULUHISHI NA UAMUZI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 17 Oktoba, 2025 amekutana na kufanya mazungumzo na Viongozi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. 

Viongozi hao kutoka CMA wamepatiwa ushauri na maoni mbalimbali kutoka kwa Viongozi wa Mahakama yote yakilenga kuboresha huduma za utatuzi wa migogoro ya kazi zinazotolewa na Tume hiyo pamoja na kuboresha ushirikiano kati ya Tume na Mahakama.

Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika mazungumzo hayo ni pamoja na Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba, Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Herbert, Makatibu Binafsi wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi na Mhe. Clarence Mhoja

Matukio katika picha mazungumzo kati ya Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akiwa kwenye kikao na Viongozi kutoka Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza jambo wakati wa kikao na Viongozi kutoka Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya  Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Bw. Usekelege Mpulla (kushoto) akichangia jambo wakaati wa mazungumzo na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha). Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi  Utawala wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Bi. Gift Kilimwomeshi.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba (kulia) akichangia jambo wakati wa mazungumzo kati ya Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Herbert (kushoto) 
akichangia jambo wakati wa mazungumzo kati ya Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kulia ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba.


Katibu Binasfi wa Jaji Mkuu ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Venance Mlingi akichangia jambo wakati wa mazungumzo kati ya Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Katibu Binasfi wa Jaji Mkuu, Mhe. Clarence Mhoja akiwa katika kikao kati ya Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Viongozi kutoka CMA wakifuatilia mazungumzo wakati wa kikao na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Jaji Mkuu, Mhe. George Masaju.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Bw. Usekelege Mpulla (kushoto) akimkabidhi zawadi Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 17 Oktoba, 2025 baada ya mazungumzo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba (kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Bw. Usekelege Mpulla leo tarehe 17 Oktoba, 2025.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi wa Mahakama na wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).








KUTENDA HAKI NDIO MSINGI WA TAIFA

  • Kaimu Jaji Kiongozi, Mtendaji Mkuu wamtaka Hakimu mpya kumtegemea Mungu
  • Wasisitiza haki huinua Taifa

 Na HABIBA MBARUKU – Mahakama Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, kwa nyakati tofauti wamesisitiza watumishi wa Mahakama kumtegemea Mungu katika utendaji haki, uwajibikaji na kujituma bila kujali mazingira ili kuendelea kusimamia haki katika maeneo ya kazi.

Viongozi hao wametoa wito huo leo tarehe 17 Octoba, 2025 katika hafla ya uapisho wa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza mara baada ya uapisho huo, Mhe. Kagomba amemtaka Hakimu huyo kumtegemea Mungu katika kutekeleza majukumu yake, huku akizingatia uadilifu, uaminifu na kujituma. Amemuhimiza kujitoa kufanya kazi mahali popote nchini bila kujali changamoto za kimazingira, jambo ambalo litaendelea kumpa uzoefu, ujasiri na kujituma katika kazi.

“Kubwa katika yote ambayo nadhani niseme, kama kurejea katika msisitizo ni kuendelea kumtegemea Mungu katika kazi tunayofanya. Tunatambua kwamba kazi ya kuhukumu ni kazi yake na sisi ambao tumekasimiwa hapa duniani tunaofanya kwa niaba yake tunapaswa kufanya kwa matarajio yake yeye aliyetuleta hapa,” amesema Kaimu Jaji Kiongozi.

Aidha, Mhe. Kagomba amemshauri Hakimu huyo kuchangamkia fursa halali atakazozikuta katika maeneo atakayopangiwa kazi ikiwa ni pamoja na fursa za kilimo, biashara, uvuvi na ufugaji  ili kujiendeleza kiuchumi, hasa kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Wako Watumishi ambao watakwenda Kigoma na utawakuta wamenuna na kukasirika, lakini wakiondolewa huko watanuna na kukasirika pia baada ya kugundua kuwa kuna fursa, kuna kilimo na biashara. Nakushauri kuwa ukijiingiza kwenye biashara utaona changamoto nyingi, lakini kilimo au uvuvi  ni shughuli ambazo hazina migogoro,” amesema.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Ole Gabriel amemtaka Hakimu Mkazi huyo kuzingatia haki katika utendaji kazi, huku akisisitiza kuwa, haki huinua Taifa na kwamba nchi isiyosimamia haki huporomoka.

“Mara zote haki huinua Taifa na haki isipotendeka nchi huanguka na nchi ambayo haisimamii haki kwa kweli ni changamoto,” amesisitiza Prof. Ole Gabriel.


Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba akizungumza jambo mara baada ya hafla ya Uapisho wa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza (hayupo katika picha) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza akisikiliza kwa makini mawaidha/wosia kutoka kwa Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba (hayupo katika).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa neno kwa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza aliyeapishwa leo na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha)


Picha ya Uapisho: Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimuapisha Hakimu Mkazi mpya, 
Mhe. Hillary Massala Kuzenza leo tarehe 17 Oktoba, 2025  kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)






JAJI MKUU AMUAPISHA HAKIMU MKAZI MPYA

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 17 Oktoba, 2025 amemuapisha Mhe. Hillary Massala Kuzenza kuwa Hakimu Mkazi kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mhe. Masaju amemtaka Hakimu huyo kurejea hotuba yake aliyoitoa tarehe 07 Oktoba, 2025 alipowaapisha Mahakimu wenzake wapya.

Uapisho huo umehudhuriwa na Viongozi kadhaa wa Mahakama wakiwemo Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Kaimu Msajili Mkuu ambaye ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Herbert George, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa.

Wengine ni Naibu Msajili Mwandamizi Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Emmanuel Mrangu, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu-Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Kuu, Mhe. Mwajabu Mvungi, Watendaji wa Mahakama Kuu Masjala Kuu, Bw. Humphrey Paya na Bw. Ginaweda Nashon, Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda, Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu na wengine.

Matukio katika picha ya Uapisho wa Hakimu Mkazi, Mhe. Hillary Massala Kuzenza.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimuapisha Mhe. Hillary Massala Kuzenza kuwa Hakimu Mkazi leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba (kulia) pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante wakiwa katika hafla ya uapisho wa Hakimu Mkazi  mpya iliyofanyika leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Viongozi na watumishi wa Mahakama waliohudhuria katika Hafla ya Uapisho wa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akisaini hati ya kiapo cha Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza mara baada ya kumuapisha leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Hakimu Mkazi, Mhe. Hillary Massala Kuzenza  (kushoto) akisaini hati ya kiapo mara baada ya kula kiapo cha kushika wadhifa huo mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia). Aliyesimama katikati ni Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Herbert.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza jambo mara baada ya kumuapisha Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza (hayupo katika picha) leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Hakimu Mkazi aliyeapishwa leo tarehe 17 Oktoba, 2025, Mhe. Hillary Massala Kuzenza akisikiliza kwa makini mawaidha yaliyokuwa yakitolewa na Viongozi mbalimbali mara baada ya kuapishwa kwake.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akizungumza na Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza (aliyesimama kulia) mara baada ya kumuapisha kushika wadhifa huo leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba akizungumza jambo wakati wa hafla ya uapisho wa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala (hayupo katika picha).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa neno wakati wa hafla ya Uapisho wa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza (hayupo katika picha).


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimpongeza Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza mara baada ya kumuapisha kushika wadhifa huo leo tarehe 17 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba (kushoto) na Hakimu Mkazi mpya aliyemuapisha leo, Mhe. Hillary Massala Kuzenza (kulia).



Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) pamoja na baadhi ya Viongozi wengine wa Mahakama wakiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Hillary Massala Kuzenza (wa tatu kulia). Wa tatu kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Abdi Kagomba (wa tatu kushoto), wa pili kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, wa pili kushoto ni Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Herbert, wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu-Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick na wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo-Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)









WIKI YA USULUHISHI KUFANYIKA NOVEMBA 2025

  • Vikao vya maandalizi vikihusisha wadau vyaanza

Na EUNICE LUGIANA-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, jana tarehe 16 Octoba, 2025 imefanya kikao na Watendaji Wakuu wa Taasisi mbalimbali kujadili namna bora ya kushiriki kwenye Wiki ya Usuluhishi itakayofunguliwa tarehe 20 Novemba, 2025 jijini Dodoma.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Banki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kilifunguliwa na Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud, ambaye alimwakilisha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Akizungumza kwenye ufunguzi huo, Mhe. Aboud alisema kuwa japokuwa jukumu kubwa la Mahakama ni kutenda haki mapema ipasavyo, lazima kuzingatia njia mbadala au utatuzi mbadala wa migogoro ambao umesisitizwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977, Ibara ya 107 (d).

Alisema kuwa kwakuwa Mahakama imedhamiria kwa dhati kuona masuala ya utoaji wa haki yanapaswa kufanywa mapema ipaswavyo, hatua hiyo ni mwendelezo katika kukamilisha jukumu kubwa iliyopewa kikatiba la kutoa haki.

Mhe. Aboud alieleza kuwa kikao hicho kina lengo la kujadili utatuzi mbadala wa migogoro, njia ambayo itasaidia kwa upande wa Mahakama kupunguza mashauri ambayo yasingekuwa na ulazima wa kufika mahakamani iwapo wadau husika kwenye Taasisi au Ofisi zao wangeitumia.

Alisisistiza kwamba njia mbadala ya utatuzi wa migogoro ni rahisi, haina gharama na huwafanya pande zote mbili kuwa na mahusiano mazuri. “Hii ni njia ambayo inatakiwa tuienzi na kuhakikisha tunaitafutia mikakati bora ya kuitumia,” alisema Jaji Abood.

Kadhalika, alibainisha kuwa njia hiyo itawavutia wawekezaji kuja kuwekeza Tanzania maana watajua migogoro ya kibishara haichukui muda mrefu kuisha na baadaye kuendelea na biashara kwa amani kwakuwa wafanyabishara wengi hawapendi migogoro.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma alisema kuwa mkutano huo unaweka historia ya safari ya kuhamasisha matumizi ya njia ya usuluhishi katika utatuzi wa migogoro nchini Tanzania.

Alisema kuwa lengo kuu la Mahakama na wadau wake ni kupata uelewa wa pamoja juu ya kuhamasisha usuluhishi wenye kuleta ufanisi na tija, siyo tu kama inavyotajwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bali hata kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025- 2050.

Alibainisha kuwa nchi nyingi duniani hivi sasa zimekuwa zikitumia njia za usuluhishi na kuondokana na dhana ya kuendesha mashauri mahakamani kwa muda mrefu na hii ni kutokana na faida nyingi zinazotokana na njia hiyo.

Akitoa takwimu za migogoro katika Kituo hicho, Mhe. Maruma alisema wameshudia ongezeko kubwa katika kutatua migogoro. ‘Takwimu zinaashiria nia njema kwamba tukiendelea kwa juhudi za pamoja tunaweza kufanikisha sana migogoro mingi ikaishia kwenye hatua za usuluhishi,’ alisema.

Alisema kuwa mwaka 2023 migogoro 82 ilifanikiwa kupitia njia ya usuluhishi, kwa mwaka 2024 migogoro 109 na mpaka Oktoba 2025, migogoro 70 imemalizika kwa njia hiyo.

Naye Prof. Zakayo Lukumai, akitoa taarifa ya hali ya usuluhishi Tanzania, alisema kuwa usuluhishi uliingizwa mahakamani kama kiambata (court annex mediation) na kuanzia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na baadaye Mahakama Kuu na sasa imeenea Mahakama zote.

Alieleza kuwa kwa sasa somo la usuluhishi limeingizwa kwenye mitaala ya Shule ya Sheria kwa Vitendo na linafundishwa kwa vitendo. Mhe. Lukumau alisema kuwa kuanzishwa kwa Kituo cha Usuluhishi kumeongeza kasi kwa njia mbadala kuweza kukubalika katika utatuzi wa migogoro.

Prof Lukumai alitoa wito kwa Vyuo Vikuu nchi kulifanya somo hilo kuwa la lazima ili kuanza kujenga misingi tangu mwanzo.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Viongozi wa Mabenki, Taasisi za Usuluhishi na vitengo vyote vinavyoshughulika na usuluhishi.

Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud [juu na chini] akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akizungumza kwenye hafla hiyo.

Mhadhiri kutoka Shule ya Sheria kwa Vitendo, Mhe. Prof. Zakayo Lukumai akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao hicho.




Sehemu ya washiriki wa kikao hicho [picha mbili juu na moja chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.


Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Iman Aboud [kulia] akiwasili kwenye ukumbi wa kikao akiwa ameongozana na wenyeji wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma [katikati], Naibu Msajili, Mhe. Augustina Mmbando [wa pili kutoka kushoto] na Mtendaji, Bi. Hellen Mkumbwa [wa kwanza kushoto].
[Picha na Bakari Mtaullah-Dar es Salaam]
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma