Jumatano, 15 Oktoba 2025

MAHAKAMA KUU KAZI YAKABIDHI JUZUU ZA MAAMUZI CHUO CHA USTAWI WA JAMII

Na Mwandishi Wetu

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, tarehe 10 Oktoba 2025, amekabidhi Juzuu za Maamuzi ya Migogoro ya Kazi kwa Chuo cha Ustawi wa Jamii.

Mhe. Dkt. Mlyambina alikabidhi nakala mbili (2) za Juzuu za Maamuzi ya Migogoro ya Kazi Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na nakala sabini (70) za Labour Court Case Digest, akiwa ameambatana na mahakimu wa Mahakama Kuu.

Akizungumza katika makabidhiano hayo, Jaji Dkt. Mlyambina amesema kuwa kuleta Juzuu hizo Chuo cha Ustawi wa Jamii ni heshima ya kutambua mchango na kazi inayofanywa na Chuo cha Ustawi wa Jamii, ambacho ni Chuo pekee nchini kinachotoa taaluma za kazi na kuzalisha maafisa wanaokwenda kufanya kazi katika Mahakama za kazi kama wasuluhishi na watatuzi wa migogoro ya ajira.

Aidha, Juzuu hizo zimepokelewa na Naibu Mkuu wa Chuo - Fedha na Utawala, Dkt. Eventus Mugyabuso, kwa niaba ya Mkuu wa Chuo hicho.

Kadhalika Juzuu za Maamuzi ya Migogoro ya Kazi zinahusu kesi zilizotolewa maamuzi kuanzia mwaka 2010 hadi 2024, na zinatarajiwa kusaidia wanafunzi, wanazuoni wa sheria na watafiti kupata rejea sahihi na kuelewa mwenendo wa tafsiri za kisheria katika migogoro ya ajira nchini.

Kwa Upande wake Naibu Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Dkt. Eventus Mugyabuso amemshukuru Jaji Mlyambina kwa kuona umuhimu wa kuleta Juzuu hizo chuoni hapo ambazo zitaongeza ujuzi kwa wanafunzi wa Taaluma za kazi na wanazuoni kwa ujumla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina (wa tatu kushoto) akikabidhi Juzuu za Maamuzi ya Migogoro ya Kazi kwa Chuo cha Ustawi wa Jamii.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina (kulia) akiteta jambo na Naibu Mkuu wa Chuo - Fedha na Utawala, Dkt. Eventus Mugyabuso
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina (wa tatu kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Divisheni ya Kazi mara baada ya kukabidhi Juzuu za Maamuzi ya migogoro ya kazi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina (kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na Naibu Mkuu wa Chuo - Fedha na Utawala, Dkt. Eventus Mugyabuso.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi Mhe. Cassian Matembei akiwa na sehemu ya watumishi wa Mahakama hiyo.





MWILI WA MAREHEMU FREDRICK BINAMUNGU KAKURWA WAAGWA KWA IBADA MAALUM

Na. Rehema Awet – Mahakama, Mwanza

Mwili wa marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa aliyekuwa Hakimu Mkazi II Mahakama ya Mwanzo Nyanchenche umeagwa tarehe 13 Oktoba, 2025 nyumbani kwake maeneo ya Kabwalo Buswelu Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza.

Ibada ya kuaga mwili wa marehemu ilihudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiongozwa na Mhe. Winifrida Beatrice Korosso, Majaji wa Mahakama Kuu, Mahakimu wa Mkoa wa Mwanza pamoja na viongozi mbalimbali wa Mahakama Kanda ya Mwanza.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Mwanza, Bw. Tutubi Deo Mangazeni alitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Mahakama na kuwapa pole wafiwa wote wakiwemo familia, ndugu jamaa marafiki na wafanyakazi wenzake waliohudhuria ibada ya kuaga mwili wa marehemu.

Aidha, kwa masikitiko makubwa alieleza namna ambavyo Mahakama imepata pengo kwa kuondokewa na mfanyakazi wake ambaye alikuwa kijana hodari na mchapakazi.

Vilevile, alieleza kuwa Mahakama kama mwajiri ilivyoshiriki katika taratibu zote za kuhifadhi na hatimaye kuusafirisha mwili wa marehemu kwa ajili ya kuupumzisha kwenye nyumba yake ya milele huko kijijini kwao ambapo mazishi yamepangwa kufanyika mnamo tarehe 14 Octoba, 2025

Baada ya ibada ya kuaga mwili wa marehemu, ulisafirishwa kuelekea kijijini kwao Bundaza Kata ya Nyakibimbili mkoani Kagera.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Bw.Tutubi Deo Mangazeni akiaga mwili wa marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa.

Sehemu ya Majaji, Wasajili na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania wakishiriki Ibada ya kuuaga mwili wa marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa, kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Winifrida Beatrice Korosso akiwaongoza Majaji wenzake Mhe. Penterine Kente na Mhe. Amour Khamis, wengine ni Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, Mhe. Kassim Robert, Mhe. Emmanuel Ngigwana na Mhe. Kamana Kamana, Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Mhe. Janeth Musaroche na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Mwanza Mhe. Erick Marley 

Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. Winifrida Beatrice Korosso akiaga mwili wa marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Mhe. Kamana S Kamana akiaga mwili wa marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa.

Sehemu ya waombolezaji na watumishi wa Mahakama Kanda ya Mwanza wakishiriki kuaga mwili wa marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa.




 

 


Jumanne, 14 Oktoba 2025

TANZIA; NAIBU MSAJILI MAHAKAMA KUU KANDA YA SHINYANGA, MHE. ASHA MWETINDWA AFARIKI DUNIA


 Aliyekuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Marehemu Mhe. Asha Khamis Mwetindwa enzi za uhai wake.

                                                 TANZIA

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake, aliyekuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga, Mhe. Asha Khamis Mwetindwa kilichotokea leo tarehe 14 Oktoba, 2025 Saa 1 asubuhi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga, Bw. Bakari Mketo, Marehemu Asha Mwetindwa alianza kujisikia vibaya wiki moja iliyopita ambapo alianza kupata matibabu katika Hospitali za Kolandoto Shinyanga na baadaye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga.

Bw. Mketo amesema kuwa, baadaye Marehemu Mhe. Asha Mwetindwa alikuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma mpaka alipofikwa na umauti.

Mtendaji huyo amebainisha kwamba, kwa sasa taratibu za mazishi zinaendelea kuratibiwa na taarifa kamili itatolewa mara baada ya kukamilisha taratibu.

Marehemu Asha Mwetindwa aliajiriwa na Mahakama ya Tanzania tarehe 6 Juni, 2007 kama Hakimu Mkazi Daraja la II na amewahi kufanya kazi katika Wilaya za Lindi na Singida.

Aidha, marehemu Mwetindwa aliteuliwa kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama za Wilaya za Masasi na Muleba na mwaka 2022 aliteuliwa kuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Shinyanga.

Mwaka 2023 Marehemu Asha Mwetindwa aliteuliwa kuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania na kupangiwa Kituo cha Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga nafasi aliyoitumikia hadi umauti ulipomkuta.

Mahakama ya Tanzania inaungana na ndugu, jamaa na marafiki katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza msiba huo mzito wa kuondokewa na Mpendwa wetu.

HAKIKA SISI SOTE NI WA MWENYEZI MUNGU NA KWAKE YEYE TUTAREJEA (INNA LILLAH WA INNA ILLAH RAJIUN). 

 

 


1.    

 

 

 

 

Jumatatu, 13 Oktoba 2025

WANAFUNZI KIDATO CHA NNE BUTEKO WAFANYA KAZI MRADI MAHAKAMA KUU KIGOMA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma 

Jumla ya Wanafunzi nane wa Kidato cha nne kutoka Shule ya Sekondari Buteko iliyopo mkoani Kigoma wamefanya Kazi Mradi (Project) yenye mada isemayo ‘Nini changamoto zinazoikabili Mahakama ya Tanzania katika kutoa haki kwa wananchi’ ikiwa ni mchakato wa kuhitimisha masomo yao katika ngazi hiyo ya masomo.

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Hassan Galiatano akishirikiana na Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Kanda hiyo, Mhe. Valerian Msola walitoa elimu kwa wanafunzi hao waliofika mahakamani hapo tarehe 10 Oktoba, 2025 ili kufahamu kuhusu  shughuli  mbalimbali na nafasi ya Mahakama katika kutoa haki kwa wananchi.

Mhe. Galiatano aliwaeleza wanafunzi hao kuwa, Mahakama inatoa haki kwa mujibu wa Katiba na Sheria na kwamba hujikita katika usahihi wa shauri lililopo mbele ya Mahakama husika ili kuhakikisha kila anayefikishwa au kufika mahakamani anapata haki yake mapema ipasavyo na bila upendeleo wa aina yoyote.

Alisema kwamba, zipo changamoto kadhaa ambazo Mahakama inakutana nazo inapotekeleza wajibu wake wa kutoa haki ambapo alisema, “Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ni changamoto kwa sasa, kwakuwa Mahakama mtandao inahitaji vifaa na mtandao imara katika kuendesha mashauri Mahakamani, hivyo wadau wanaoshirikiana na Mahakama wanapokuwa hawana mtandao imara husababisha kukwama kwa usikilizwaji wa mashauri Mahakamani.”

Hata hivyo aliwaeleza wanafunzi hao kuwa, uelewa mdogo wa matumizi ya Mahakama Mtandao  kwa wananchi umechangia pakubwa changamoto ya kitehama, kwani kwa sasa Mahakama inafanya shughuli zake zote kwa mtandao.

Kwa upande wake, Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Kanda hiyo, Mhe. Valerian Msola alisema kuwa, Mahakama ni kati ya Mihimili mitatu ya Dola kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatimiza wajibu wake kisheria na ni Chombo pekee chenye mamla ya utoaji haki nchini, hivyo ina wajibu wa  kutoa haki bila kuacha shaka.

Aidha, Mhe. Msola aliwataka wanafunzi wasome kwa bidii ili wafikapo katika ngazi ya elimu ya juu waweze kusoma Sheria na baadaye waweze kuwa Wanasheria wazuri na wenye maadili katika kuhudumia jamii ya Watanzania.

Aliongeza kwa kuwaomba wanafunzi hao kuendelea kuipenda Mahakama na kwamba elimu waliyopata waipeleke katika jamii wanayoishi ili jamii ifahamu kuwa Mahakama ndio chombo pekee kinachotoa haki bila upendeleo wowote.

Kwa upande wake Kiongozi wa Wanafunzi hao, Bi. Amina Husein aliushukuru Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma kwa kuridhia wao kuja kujifunza mambo mengi ya Mahakama na umuhimu wa Mahakama katika jamii ya Watanzania. 

Msaidizi wa sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Kigoma Mhe. Valerian Msola (katikati) na Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Hassan Galiatano, (kulia) pamoja na Msaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma , Bi. Happiness Elia wakiwa katika picha ya pamoja na Wanafunzi wa Kidato cha Nne wa Shule ya Sekondari Buteko mkoani Kigoma waliotembelea Mahakama Kuu Kigoma tarehe 10 Oktoba, 2025 kwa ajili ya kufanya Kazi Mradi (Project) yenye mada isemayo ‘Nini changamoto zinazoikabili Mahakama ya Tanzania katika kutoa haki kwa wananchi.’ 

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Hassan Galiatano akisisitiza jambo wakati alipokuwa akitoa elimu kwa Wanafunzi wa Kidato cha Nne wa Shule ya Sekondari Buteko iliyopo mkoani Kigoma.

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola akiwafundisha kwa vitendo wanafunzi wa kidato cha nne shule ya Sekondari Buteko jinsi Mahakama huketi wakati wa kusikiliza mashauri.


 Kiongozi wa Wanafunzi hao, Bi. Amina Husein akiuliza swali la kutaka kufahamu changamoto ambazo Mahakama inakabiliana nayo kwa sasa katika usikilizaji mashauri na utoaji hukumu.

Mwanafunzi Bi. Sania Yenga Msabaha, aliyevutiwa  kukalia kiti cha mamlaka ya Mahakama mara baada ya kusema kuwa yeye anayo nia ya kuwa Hakimu na hatimaye Jaji.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

MBEYA YAFANYA KIKAO CHA MENEJIMENTI YA KANDA

Na. Muksini Nakuvamba-Mahakama, Mbeya

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Said Kalunde ameongoza kikao cha Menejimenti ya Kanda ya Mbeya inayojumuisha mikoa ya Mbeya na Songwe shughuli hiyo ilichofanyika tarehe 09 Oktoba, 2025 Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya.

Akiwasilisha taarifa ya utawala na ushughulikiaji wa mashauri kwa robo ya kwanza ya mwaka 2025/2026 kwa Mahakama za Mkoa wa Mbeya Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Wilaya Rungwe Bw. Alintula Ngalile alifafanua kuwa taarifa hiyo inaainisha uwajibikaji, usimamizi wa rasilimali, utoaji na upatikanaji wa haki kwa wakati.

Taarifa hiyo pia, ilieleza maendeleo ya matumizi ya mifumo ya TEHAMA, hali ya majengo, viwanja na miradi ya maendeleo inayoendelea katika mkoa wa Mbeya pamoja na ushirikishwaji wa wadau katika utoaji wa elimu kwa umma na ushirikishwaji wa sekta binafsi katika mnyororo wa utoaji haki.

Vilevile, taarifa hiyo ilieleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi hicho cha robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026, changamoto pamoja na mikakati waliyojiwekea katika kupambana na chanagamoto hizo.

Afisa Utumishi huyo akatoa shukurani “Mhe. Mwenyekiti tunashukuru kwa uongozi wako ambao unasisitiza katika uwajibikaji na utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia uweledi, kanuni na taratibu katika utumishi wa Umma, ili kufanikisha haya yote msisitizo mkubwa unawekwa kwa watumishi na viongozi kuwa waadilifu wakati wa kutekeleza wajibu wao kiuweledi na kufanya kazi kwa umoja.”alisema Bw. Ngalile.

Aidha, iliwasilishwa taarifa ya kiutendaji na usimamizi wa mashauri katika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026 kwa Mahakama za Mkoa wa Songwe.

Akiwasilisha taarifa hiyo Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Bw. Sostenes mayoka, alifafanua hali ya rasilimali watu, usimamizi wa rasilimali fedha, hali ya majengo, viwanja na miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Songwe, vyombo vya usafiri hali ya mashauri na ziara za kutembelea Magereza Wilaya ya Mbozi na Ileje.  

Aidha, taarifa hiyo pia ilieleza mafanikio, changamoto, mikakati waliyojiwekea katika kupambana na chanagamoto hizo na mipango ya baadae

“Tuna mipango kazi ya baadae ikiwemo kuanza zoezi la kupima maeneo yote ya viwanja vinavyomilikiwa na Mahakama za Mkoa wa Songwe ili kupata hati. Pia tunalenga kupunguza mlundikano wa mahabusu katika magereza yetu kwa kupunguza masharti ya dhamana ili wale wanaodhaminika waweze kuwekewa dhamana.” alisema Bw. Mayoka.

Aidha, taarifa za mirathi na malipo ya mirathi ilikuwa sehemu ya utekelezaji ikimtaka kila Hakimu wa Mahakama za Wilaya na Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Songwe aliwasilisha taarifa za Mirathi kwenye wilaya yake.

Kwa upande wa Mahakama za Mkoa wa Mbeya taarifa ya jumla kuhusu malipo ya mirathi kwa Mahakama zote za Mkoa wa Mbeya iliyowasilishwa na Msaidizi wa Hesabu Mahakama Kuu Mbeya Bw. Nassir Upete.

Mhe. Kalunde akatoa shukurani kwa wajumbe wote kwa kushiriki na kusisitiza kuwa, viongozi wawe na desturi ya kushirikisha watumishi wa chini katika kujadili mambo mbalimbali ya kiofisi ili kuboresha utendaji kazi.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Said Kalunde (Kulia) akiongoza kikao cha Menejimenti Kanda ya Mbeya, Kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi. Mavis Miti.

Sehemu ya wajumbe wa menejimenti kanda ya Mbeya

Afisa Utumishi Mwandamizi (wa kwanza kushoto) akiwasilisha taarifa ya kiutendaji na ushughulikiaji wa mashauri kwa robo ya kwanza ya mwaka 2025/2026 kwa Mahakama za Mkoa wa Mbeya.

Msaidizi wa Hesabu Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bw. Nassir Upete akiwasilisha taarifa ya mirathi katika kikao hicho

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe  Bw. Sostenes Mayoka (kulia) akiwasilisha taarifa ya utawala na uendeshaji wa mashauri kwa robo ya kwanza ya mwaka 2025/2026 kwa Mahakama za Mkoa wa songwe.

Hakimu Mkazi Mfawidhi mahakama ya wilaya Mbozi Mhe. Nemes Chami akiwasilisha taarifa za Mirathi Mahakama ya Wilaya ya Mbozi -Songwe.




TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA AFARIKI DUNIA

 TANZIA


Marehemu Fredrick Binamungu Kakurwa enzi za uhai wake.

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha mtumishi wake wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza Mhe. Fredrick Binamungu Kakurwa aliyekuwa ameajiriwa kwa nafasi ya Hakimu Mkazi II akihudumu Mahakama ya Mwanzo Nyancheche iliyopo wilaya ya Sengerema.

Kifo hicho kilitokea mnamo tarehe 10 Oktoba, 2025 majira ya saa nne usiku eneo la Kiseke wilaya ya Ilemela akielekea nyumbani, akitokea kazini kwake Mahakama ya Mwanzo Nyancheche iliyopo wilaya ya Sengerema

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Bw. Tutubi Mangazeni, marehemu Bw Fredrick Binamungu Kakurwa alifikwa na umauti kutokana na ajali ya pikipiki iliyotokea eneo la kiseke.

Marehemu Fredrick aliajiriwa mnamo tarehe 28 Novemba, 2024 kama Hakimu Mkazi II na kupangiwa kituo cha kazi Mahakama ya mwanzo Nyancheche ambako amehudumu mpaka umauti ulipomfika.

Wakati wa ajira yake marehemu alikuwa na elimu ya shahada ya sheria na Astashahada ya mafunzo ya sheria kwa vitendo kutoka Chuo cha Sheria Tanzania (Law school of Tanzania).

Marehemu Fredrick anatarajiwa kuzikwa mnamo tarehe 14 Octoba, 2025 nyumbani kwao, kijiji cha Bundaza, kata ya Nyakibimbili mkoani Kagera.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA JINA LA BWANA LIHIMIDIWE.

 

UJENZI WA JENGO LA MAHAKAMA YA MWANZO NG’ANZO WAKAMILIKA

Na DOTTO NKAJA-Mahakama, Geita.

Kampuni ya Parik Limited Moshi Tanzania imekamilisha mradi wa ujenzi wa jengo la Mahakama ya Mwanzo Ng’anzo iliyopo Wilaya ya Bukombe mkoani Geita ulioanza tarehe 27 Julai 2024.

Jengo la Mahakama hiyo lilikabidhiwa tarehe 10 Octoba, 2025 kwa Mahakama Kuu Kanda ya Geita ili lianze kutumika.  

Mhandisi Mshauri, Venjislous Mgeni kutoka Kampuni ya Norman and Dawbarn alikabidhi jengo pamoja na rasilimali zilizopo kwa Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Geita, Bi. Happiness Mushi.

Zoezi hilo lilishuhudiwa na Mhandisi Aika Kileo kutoka Makao Makuu ya Mahakama, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Bukombe, Mhe. Zawald Nyekelela.

Wengine ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Ng’anzo, Vitus Mfumya Ofisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Bukombe, Bw. Hafidhi Mtunzi na watumishi wengine kutoka Mahakama ya Wilaya Bukombe.

Kampini ya Parik Limited ikiwakilishwa na Mhandisi Joseph Baleke ambaye alikabidhi funguo na ramani ya jengo hilo kwa Bi. Mushi.

Naye Mhe. Lukuna baada ya kushuhudia makabidhiano hayo alisema, “Kazi iliyobaki ni kungoja kibali cha ufunguzi wa jengo hili. Zoezi hilo linaratibiwa na Ofisi ya Jaji Mfawidhi.”

Mhandisi Joseph Baleke akikabidhi funguo na ramani ya jengo la Mahakama ya Mwanzo Ng’anzo kwa Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Geita, Bi. Happiness Mushi.


Timu nzima ya makabidhiano ikikagua miundombinu iliyowekwa kwenye jengo la Mahakama ya Mwanzo Ng’anzo.

Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna [wa kwanza kulia] akiwa na Kaimu Mtendaji wa Mahakama Geita , Bi. Happiness Mushi [katikati] na Mhandisi kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Bi. Aika Kileo ndani ya jengo hilo.



Timu ya makabidhiano ikifanya tathmini sehemu ya kupanda miti siku ya uzindizi wa Mahakama hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA AFARIKI DUNIA

 TANZIA


Marehemu Patrick Michael Masenge enzi za Uhai wake.

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha mtumishi wake wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma Mhe. Patrick Michael Masenge mwenye cheki namba 113357034 aliyekuwa ameajiriwa kwa nafasi ya Hakimu Mkazi II Mahakama ya Mwanzo Bunda Mjini.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma Bw. Leonard John Maufi, marehemu Patrick amefikwa na umauti tarehe 10. Oktoba, 2025 katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu. Marehemu Patrick aliajiliwa na Mahakama mnamo tarehe 28 Mwezi wa 10 Mwaka, 2024

Taratibu za mazishi zinaendelea kuratibiwa na Mahakama kwa kushirikiana na familia.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA JINA LA BWANA LIHIMIDIWE.

Ijumaa, 10 Oktoba 2025

JAJI DINGO’HI AFANYA ZIARA YA UKAGUZI MKOANI LINDI


  • ·Apongeza kasi ya uondashaji wa Mashauri Mahakamani
  • ·Awaasa watendaji kukaza buti kwenye matumizi ya TEHAMA
  • ·Asisitiza kufanya kazi kwa uadilifu

Na. Hilary Lorry – Mahakama, Lindi

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Saidi Dingo’hi amefanya ziara ya ukaguzi katika Mkoa wa Lindi na kukagua Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi, Mahakama za Wilaya tano (5) za Mkoa wa Lindi, Mahakama ya Wilaya ya Lindi, Kilwa, Liwale, Ruangwa, Nachingwea na Mahakama za mwanzo zilizopo katika Mkoa huo.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama kwa nyakati tofauti wakati wa ziara hiyo Mhe. Dingo’hi alisema nimeshuhudia kazi nzuri mnayofanya alipokuwa akikagua Mahakama za Wilaya hizo na kuwakumbusha watumishi kufanya kazi kwa bidii na kwa uadilifu wa hali ya juu.

Aidha, Mhe. Dingo’hi aliwapongeza watumishi katika mkoa huo kwa kuchukua jitihada za makusudi  katika ufanyaji wa  kazi kwa bidii hasa Mahakimu kwa  kusikiliza mashauri kwa wakati  bila kuzalisha mashauri ya muda mrefu (mashauri ya Mlundikano)  na kutokuwa na mashauri mengi yanayoendelea mahakamani (pending cases) hiyo ni kutokana na kasi ya usikilizaji na umalizaji wa mashauri kwa wakati.

“Nawapongeza Mahakimu wote  kwa kutekeleza jukumu lenu la  msingi la usikilizaji na uondoshaji wa Mashauri kwa wakati lakini pia niwatake mtekeleze jukumu hilo kwa uadilifu ili haki isionekene tu bali ionekane ikitendeka hii itarejesha imani ya jamii kwa Mahakama” alisisitiza Jaji Dingo’hi.

Aidha, Mhe. Dingo’hi aliwaasa watumishi katika mkoa huu kuachana kabisa na matumizi ya karatasi na kujikita zaidi  katika matumizi  ya Mifumo ya TEHAMA, pamoja na mifumo ya uratibu wa Mashauri na Mifumo Mingene yote iliyoanzishwa au kutumiwa na Mahakama ya Tanzania  kwani lengo ni  kurahisishia utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Vilevile, Mhe. Dingo’hi aliwataka watumishi kuwachukulia wateja wote kwa usawa  bila kujali vyeo vyao, hadhi  zao hili kuwachukulia kwa usawa Mawakili wa Serikali na Mawakili wakujitegemea vyivyo hivyo.

Aidha, Jaji Dingo’hi aliwataka watumishi kuendelea kuleana kielimu (Mentorship) ikiwa ni mwendelezo wa utekelezaji wa agizo la Jaji Mfawidhi Kanda ya Mtwara Mhe.Edwin Kakolaki.

Mhe.Dingo’hi pia alitembelea na kukagua Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi (IJC) Lindi pamoja na gereza la Wilaya ya Lindi.

Kwa upande wao viongozi wengine walioambatana na Jaji Dingo’hi katika ziara hiyo ya ukaguzi ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Seraphina Nsana, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Lindi Mhe. Consolata Peter Singano, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Bw. Yusuph Msawanga na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela  kwa nyakati tofauti wakati wa ziara hiyo waliwataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kwa nidhamu.

Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe.Saidi Dingo’hi (katikati) akiteta Jambo na watumishi (hawapo kwenye picha) wakati wa ziara ya ukaguzi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano akisoma taarifa ya Mahakama ya Mkoa wa Lindi Mbele ya Mhe.Jaji Dingo’hi.

Mtendaji wa Mahakama Kuu kanda ya Mtwara Bw. Yusuph Msawanga akiteteta jambo na watumishi katika ziara hiyo ya ukaguzi.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Godfrey Mbeyela akieleza jambo wakati wa ukaguzi.





Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Saidi Dingo’hi akipanda Mti wa Kumbukizi alipotembelea Mahakama ya Mwanzo Mandawa iliyopo Wilaya ya Ruangwa.

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi wakiwa katika Picha ya pamoja na Jaji wa mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Saidi Dingo’hi (aliyesimama katikati).

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe Saidi Dingo’hi na Jopo lake wakionyeshwa mwenendo wa Ujenzi wa Mradi wa chumba cha Mahakama Mtandao kinajojengwa Gereza kuu Lindi.


Picha ikionyesha zoezi la ukaguzi wa mradi wa Ujenzi wa kituo Jumuishi (IJC) Lindi.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Ruangwa wakiwa katika Picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Saidi Dingo’hi wakati wa ziara yake ya ukaguzu wilaya ya Ruangwa.

Picha ikionyesha zoezi la ukaguzi wa mradi wa Ujenzi wa kituo Jumuishi (IJC) Lindi.

Picha ikionyesha zoezi la ukaguzi wa mradi wa Ujenzi wa kituo Jumuishi (IJC) Lindi.







KIKAO CHA MENEJIMENTI MKOA WA MBEYA CHAKETI

Na. Muksini Nakuvamba – Mhakama, Mbeya

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Said Kalunde amengoza kikao cha menejimenti mkoa wa Mbeya kilichofanyika jana tarehe 09 Oktoba 2025 katika ukumbi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya.

 Akiwasilishwa taarifa ya utendaji kazi kwa kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2025/2026 Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya ambaye pia alikuwa Katibu katika kikao hicho Bi. Mervis Miti alitoa taarifa ya rasilimali watu ambapo ilieleza kuhusu hali ya watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, upimaji wa watumishi na motisha za watumishi.

Aidha, taarifa hiyo ilieleza kuhusu taarifa ya usimamizi wa rasilimali fedha, vyombo vya usafiri, taarifa ya mashauri, taarifa ya matumizi ya TEHAMA na ushughulikiaji wa malalamiko na mapendekezo, utoaji wa elimu kwa umma na hali ya majengo mbalimbali ya Mahakama mkoa wa Mbeya.

Vilevile, taarifa hiyo ilifafanua juu ya mafanikio kadhaa ikiwemo kupokea watumishi 18 wa ajira mpya, ukarabati na uboreshaji wa baadhi ya majengo ya Mahakama, kusimamia nidhamu ya watumishi, matengenezo ya magari ya ofisi na kupokea na kuanza kutumika kwa Majengo mapya matatu yaliyojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia.

Kwa upande mwingine, taarifa hiyo ilieleza changamoto kadhaa ikiwemo uchakavu wa magari na majengo ya ofisi kama majengo ya Mahakama za mwanzo na nyumba ya kuishi Jaji Mfawidhi hali inayopelekea kupanga nyumba mtaani kwa gharama kubwa.

Changamoto zingine ni usajili wa mashauri kwa jina moja la wadaawa au washitakiwa kwa mashauri ambayo yana washitakiwa zaidi ya mmoja, sambamba na hilo pia kumekuwa na changamoto ya uwepo wa vielelezo vya muda mrefu katika mahakani, alisema Mtendaji huyo.

Taarifa hiyo pia ilifafanua juu ya mikakati kadhaa ya kuimarisha mifumo ya TEHAMA kwa kuhakikisha upatikanaji wa nishati na mtandao, kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa majengo na kuendelea kulipa mirathi kwa wakati.

Aidha, iliwasilishwa taarifa ya mashauri kwa Mahakama zote za mkoa wa Mbeya na Mahakama Kuu, Kanda ya mbeya, taarifa hiyo iliwasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba.

“Baki ya mashauri hadi mwezi juni ni 639 na yaliyofunguliwa kuanzia julai hadi septemba ni 2481, yaliyomalizika kati ya julai hadi septemba ni 2501 na mashauri yaliyobaki hadi kufikia Septemba ni mashauri 619,” alisema Mhe. Mlimba.

Aidha, kikao kilijadili taarifa za Mirathi kwa Mahakama zote za Wilaya Mkoa wa Mbeya ambapo Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama zote waliwasilisha taarifa zao.

Mtendaji hiyo wa Mahakama aliwasilisha taarifa ya mirathi inayowataka kushirikiana katika kufanya tathimini ya fedha zote zilizopo kwenye akaunti ya mirathi kwa Mahakama zote na kuzilipa kwa haraka na kutuma taarifa ya utekelezaji wa jambo hilo kabla ya tarehe 05 novemba, 2025.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya ambaye ni mwenyekiti katika kikao hicho akifuatilia mawasilisho.


Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya ambaye pia alikuwa Katibu katika kikao hicho Bi. Mervis Miti akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kanda hiyo.

Sehemu ya wajumbe wa kikao

Hakimu mkazi mfawidhi mahakama ya wilaya Rungwe Mhe. Jackson Banobi (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya mirathi mahakama ya wilaya Rungwe

Afisa Hesabu Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Bi. Nancy Rwebembela (aliyesimama) Akichangia Hoja katika kikao hicho

Sehemu ya wajumbe wa kikao

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (kulia) akiwasilisha taarifa ya mashauri na mirathi kwa Mahakama za Mkoa wa Mbeya.