Alhamisi, 17 Oktoba 2024

JAJI MKUU WA TANZANIA AJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 17 Oktoba, 2024 amejiandikisha kwenye Daftari la Wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika nchini tarehe 27 Novemba, 2024.

 

Mhe. Prof. Juma aliwasili kwenye kituo cha kujiandikishia kilichopo katika Shule ya Msingi Oystebay Wilaya ya Kinondoni mkoani Dar es Salaam majira ya saa 9.00 alasiri kwa ajili ya kushiriki zoezi hilo ambalo linatarajia kutamatika tarehe 20 Oktoba, 2024 kabla ya uchanguzi kufanyika mwezi Novemba.

 

Serikali ilitangaza ratiba ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa mwaka 2024 huku Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Mohamed Mchengerwa akieleza kuwa uteuzi wa wagombea utafanyika siku 19 kabla ya uchaguzi.

 

Mhe. Mchengerwa alieleza pia kuwa endapo kutakuwa na mgombea mmoja pekee kwa nafasi husika, atateuliwa moja kwa moja.

 

"Upigaji wa kura utaanza saa 12:00 asubuhi na kumalizika saa 10:00 jioni," alisema na kueleza kuwa nafasi zitakazogombewa ni Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Wenyeviti wa Vitongoji katika mamlaka za wilaya.

 

"Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika mamlaka za Wilaya za mwaka 2024," alisema.

 

Waziri Mchewngerwa alieleza pia kuwa uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kitongoji katika mamlaka za miji midogo utaendeshwa kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kitongoji katika mamlaka za miji midogo za mwaka 2024.

 

Alisema uteuzi wa waandikishaji na waandaaji orodha ya wapigakura kwa mujibu wa kanuni hizo, utafanywa na msimamizi wa uchaguzi atakayeteua watumishi wa umma watakaoandikisha na kuandaa orodha ya wapigakura siku 52 kabla ya siku ya uchaguzi.

 

"Uandikishaji wapigakura kwa mujibu wa kanuni na uandaaji wa orodha ya wapigakura utaanza siku ya 47 kabla ya siku ya uchaguzi na utafanyika kwa muda wa siku 10," alisema.

 

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Ibara 145 na 146 inaelezea uwepo wa Serikali za Mitaa pamoja na madhumuni yake. Mojawapo ya madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi.

 

 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto juu na picha mbili chini) akijiandikisha kwenye Daftari la Wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika nchini tarehe 27 Novemba, 2024.






Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akiwa katika chumba cha kujiandikisha katika Shule ya Msingi Oysterbay Wilaya ya Kinondoni, Mkoa wa Dar es Salaam leo tarehe 17 Oktoba, 2024.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa mwandikishaji wa kati wa zoezi hilo, Bw. Hussein Omary Mohamed.

Jumatano, 16 Oktoba 2024

JAJI NDIKA AFUNGUA WARSHA KUHUSU MAKOSA YA UJANGILI NA ULINZI WA MALIASILI

Na: INNOCENT KANSHA NA SALUM TAWANI-Mahakama

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt.  Gerald Ndika leo tarehe 16 Oktoba, 2024 amefungua warsha ya kikanda ya wadau wa haki jinai kutoka Malawi, Tanzania na Zimbabwe kuhusu biashara haramu ya wanyamapori katika Hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.

Warsha hiyo imehudhuriwa na Maafisa wa Mahakama, Tume ya Utumishi wa Mahakama, Waendesha Mashtaka, Wapepelezi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali kutoka Tanzania, Malawi na Zimbabwe, ikiwa ni baada ya hitimisho la mafunzo ya mfululizo ya kina kuhusu uendeshaji wa mashauri ya wanyapori na misitu yaliyoendeshwa katika nchi hizo tatu.

“Mafunzo hayo yaliyofanyika yameweka msingi wa warsha hii ya kikanda na kwa kuzingatia mafanikio ya mafunzo, washiriki wa warsha hii watajadiliana mambo mengi yanayolenga kuimarisha uwezo wao wa kuvunja mitandao ya biashara haramu ya wanyamapori na kuboresha mifumo ya sheria ya ulinzi wa wanyamapori. Washiriki watapata pia fursa ya kuanzisha ushirikiano mpya na kuimarisha mitandao iliyopo ili kuratibu juhudi za kulinda urithi wa wanyamapori wa Afrika…

 “Ni hatua muhimu katika juhudi zetu za pamoja za kupambana na biashara haramu ya wanyamapori, kwa kufanya kazi pamoja tukivuka mipaka, tunaweza kulinda wanyamapori wetu, jamii zetu, na rasilimali zetu za asili kwa ufanisi zaidi. amesema Mhe.  Ndika.

Jaji Ndika ameendelea kusema kuwa kupitia warsha hiyo kutaimarisha ushirikiano baina ya nchi hizo tatu katika kukomesha biashara haramu ya wanyamapori, kubadilishana uzoefu katika namna bora ya kukabiliana na makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili na kujadiliana jinsi ya kutatua changamoto ya biashara hiyo.

 Aidha amefafanua kuwa biashara hiyo ina athari kubwa kwenye jamii zetu inaharibu mfumo mzima wa uzalishaji viumbe hai pamoja na mazingira yao, kwahiyo warsha hiyo itasaidia kujadili kwa pamoja namna bora ya kudhibiti  mtandao unaohusika na suala hilo. 

“Makosa haya ya uhalifu yanadhoofisha utunzaji wa maliasili zetu, usalama wa Taifa pamoja na uimara wa uchumi katika jamii zetu, kwa nchi kama Tanzania, Zimbabwe pamoja na Malawi utalii ni chombo muhimu cha kuingiza mapato ya Taifa kupotea kwao inamaanisha kutaiingiza nchi hasara katika kujiingizia pato la Taifa na kusababisha kudhoofisha maendeleo ya jamii,” amesisitiza.

Ameongeza kwamba kupambana na biashara haramu ya wanyamapori sio tu suala la kimazingira, bali pia ni la kiuchumi, hivyo basi ukomeshaji wa biashara hiyo haramu ni jambo linalopaswa kutiliwa mkazo katika jamii zetu.,

Jaji Ndika amesema kuwa ukomeshwaji wa biashara hiyo haramu unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya mataifa na taasisi, hakuna Taifa linaloweza kushinda vita hiyo, ikiwa linapambana lenyewe, wawindaji haramu ni ngumu kuwakamata ila kwa ushirikiana katika nyanja zote iwe kitaifa ama kitaasisi na kuimarisha ulinzi katika mipaka husika. 

Amesema zoezi hilo litakuwa na urahisi na hatimaye kuwakamata wawindaji hawa haramu ambao wanaharibu maliasili hizo, sheria za nchi hizo zihusishe namna bora ambayo zitawabana wawindaji haramu wa maliasili zetu na hivyo ziwe kikwazo kwao katika kutekeleza azma yao ya biashara hiyo.

‘’Warsha hii itatumika kama jukwaa muhimu kwa wadau kubadilishana maarifa, uzoefu hasa katika maeneo yenye teknolojia ya hali ya juu katika kuwalinda wanyamapori,” amesema.

Jaji Ndika amebainisha kuwa kumekuwa na ongezeko la umuhimu wa teknolojia  katika kurahisisha ukomeshaji wa  makosa hayo  ya kihalifu ya wanyamapori. Hivyo wawindaji haramu wanatumia teknolojia ya kisasa na mbinu za kufanya  makosa hayo.

 ‘’Teknolojia imekuwa ni chombo muhimu kwa Mahakama, waendesha mashtaka , na wadau wanaojihusisha uwindaji haramu,wadau wanapaswa kuimarisha matumizi ya teknolojia ili kuwa mbele ya wawindaji hao haramu,” amesema.

Jaji Ndika amekipongeza Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto kwa kuandaa semina na warsha za kujenga uwezo kwa watendaji wa makosa ya jinai inayofadhiliwa na Serikali ya Uingereza katika kitengo cha Mazingira, chakula na mambo ya vijijini (DEFRA) kwa kupitia Mfuko wa PAMS.

Naye Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto   Mhe. Paul Kihwelo, amesema warsha hiyo itasaidia kuleta ushirikiano miongoni wa nchi hizo tatu ili kuimarisha zoezi zima la kukomesha biashara hiyo na mtandao wa wale wote wanaojihusisha.

Ameupongeza Mfuko wa PAMS kwa kuwasaidia katika kuendesha warsha hizo kwa takribani miaka mitatu. Huku akisema sasa wapo katika nia nzuri ya kushirikiana na mataifa mengine ili kukomesha biashara hiyo.

Jaji Kihwelo amesema ni wakati mzuri kwa Mahakama, waendesha mashtaka , na wadau wanaojihusisha uwindaji haramu kukaa pamoja ili kujadiliana na kuona namna bora ya kuboresha sheria na kanuni ambazo zitakazosaidia kuwabana wale wote wanaojihusisha na uwindaji haramu wa wanyamapori

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.  Dkt. Gerald Ndika  akifungua wa warsha ya siku mbili ya kikanda  kuhusu makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili inayofanyika katika hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi (IJA) Lushoto  akizungumza jambo katika ufunguzi wa warsha ya siku mbili ya kikanda  kuhusu makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili inayofanyika katika hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.

Hakimu Mkazi Mkuu na Mkurugenzi wa Mafunzo ya Kimahakama(IJA)Mhe. Dkt. Patricia Kisinda akizungumza jambo katika ufunguzi wa warsha ya siku mbili ya kikanda  kuhusu makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili inayofanyika katika hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.
 Mkurugenzi wa Mfuko wa PAMS, Samson Kasala akizungumza jambo katika ufunguzi wa warsha ya siku mbili ya kikanda  kuhusu makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili inayofanyika katika hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya washiriki wa warsha hiyo wakisikiliza kwa makini majadiliano kuhusu makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili inayofanyika katika hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.
 Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.  Dkt. Gerald Ndika (wa kwanza kulia )na (katikati )ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, ambaye ni  Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto wakiwa katika  ufunguzi wa  warsha hiyo inayohusu makosa ya ujangili na ulinzi wa maliasili inayofanyika katika hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya washiriki wa warsha hiyo wakisikiliza kwa makini hoja zilizokuwa zikijadiliwa.
Washiriki wa warsha hiyo wakiwa katika picha ya pamoja kwenye hoteli ya Crowne Plaza jijini Dar es Salaam.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.  Dkt. Gerald Ndika (aliyekaa katikati )na (kushoto wa kwanza aliyekaa) ni Jaji wa Mahakama ya Rufani  Tanzania, ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto Mhe. Dkt.Paul Kihwelo wakiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi kutoka Malawi kwenye ufunguzi wa warsha hiyo.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania,Mhe.  Dkt. Gerald Ndika (aliyekaa katikati) na (kushoto wa kwanza aliyekaa) ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto Mhe. Dkt.Paul Kihwelo wakiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi kutoka Tanzania kwenye ufunguzi wa warsha hiyo.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.  Dkt. Gerald Ndika (aliyekaa katikati) na (kushoto wa kwanza aliyekaa) ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto Mhe. Dkt. Paul Kihwelo wakiwa katika picha ya pamoja na Sekretarieti kwenye ufunguzi wa warsha hiyo.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.  Dkt. Gerald Ndika (aliyekaa katikati )na (kushoto wa kwanza aliyekaa) ni Jaji wa Mahakama ya Rufani  Tanzania, ambaye  ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto Mhe. Dkt.Paul Kihwelo wakiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi kutoka  Zimbabwe kwenye  ufunguzi wa warsha hiyo.

(Picha na Innocent   Kansha- Mahakama)  

MSAJILI MKUU MAHAKAMA TANZANIA, MAAFISA WAANDAMIZI WIPO WAFANYA MAZUNGUMZO USWISI

Na UPENDO NGITIRI- Mahakama ya Tanzania, Uswisi

 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, tarehe 08 October, 2024 alitembelea Divisheni za Shirika la Miliki Bunifu (WIPO) kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya Shirika hilo na Mahakama ya Tanzania.

 

Mhe. Nkya alipata fursa ya kufahamiana na Viongozi  na  Maafisa Waandamizi wa  Divisheni hizo, ikiwemo WIPO Judicial Institute, Kituo cha Usuluhishi na Upatanishi WIPO (WIPO Arbitration and Mediation Centre na “WIPO Academy.”

 

Akiwa “WIPO Judicial Institute” Msajili Mkuu alikutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Bi. Min Eu Joo na Mwanasheria, Bi. Ines Fernandez. Mhe.  Nkya aliwashukuru kwa shughuli mbalimbali ambazo zimefanywa na WIPO Judicial Institute kwa kushirikina na Mahakama ya Tanzania tangu WIPO iliposaini hati ya makubaliano na Mahakama ya Tanzania.  

 

Aliwashukuru pia kwa kuimarisha uwezo wa kimahakama katika eneo la miliki bunifu na juhudi endelevu za ushirikiano ambazo zimekuwa na manufaa makubwa katika kuongeza ufanisi  kwenye ushughulikiaji wa  migogoro ya miliki bunifu Tanzania.

 

Kwa upande wake, Mkurugenzi huyo alishukuru kwa kazi kubwa iliyofanywa na Mahakama ya Tanzania na ushirikinao mkubwa uliopo. Aliongeza kuwa, wamekuwa wakitolea Mahakama ya Tanzania mfano kila mwaka katika Jukwaa la Majaji kwa kuwa imefanya kazi kubwa na wao wanapenda Nchi zingine   wafanye vizuri kama Tanzania inavyofanya.

 

Katika kikao hicho, pande zote mbili zilijadili mipango ya mwakani, ikiwemo kufanya mafunzo ya ana kwa ana, kukamilisha awamu ya pili ya   miongozo ya kufundishia (IP Training Materials), uhuishwaji wa maamuzi ya Mahakama ya Tanzania katika WIPO Lex na kukamilisha maandalizi ya “IP Bench book.” 

 

Akiwa WIPO Academy, Msajili Mkuu alipokea taarifa fupi ya ushiriki wa Mahakama ya Tanzania kwenye masomo ya masafa marefu ya miliki bunifu maaalum kwa Majaji (General Distance Learning Course on IP for Judges) ambayo Majaji na Mahakimu walianza kusoma tangu mwaka 2021. 

 

Katika taarifa hiyo,  Msajili Mkuu alijulishwa kuwa Tanzania inafanya vizuri na  mpaka mwaka huu wa 2024 jumla ya Majaji na  Mahakimu 402 wameshanufaika na kozi hiyo. Mhe. Nkya aliwashukuru WIPO Academy kwa mafanikio hayo makubwa na kuwahidi kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kushirikiana nao kwa karibu.

 

Kufuatia majadiliano yaliyofanyika, mbali na Mahakama ya Tanzania kunufaika na kozi maalum ya Majaji inayotolewa kwa njia ya masafa marefu, WIPO Academy kwa kushirikiana na Mahakama itakamilisha maandalizi ya kozi mahsusi kwa Majaji na Mahakimu wa Tanzania (Customized IP course for Tanzanian Judges) pamoja na kutafsiri   kwa lugha ya Kiswahili miongozo ya kufundishia kozi hiyo.

 

Mbali na kukutana na “WIPO Judicial Institute” na “WIPO Academy”, Msajili Mkuu alipata pia fursa ya kufanya mazungumzo na Mkuu wa Idara ya Usuluhishi, Bi. Heike Wollgast. Katika kikao hicho, Mhe. Nkya alishukuru Kituo cha Usuluhishi cha WIPO kwa kushirikiaana na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi katika kuboresha usuluhishi wa migogoro kupitia utoaji wa mafunzo juu ya usuluhishi na huduma za usuluhishi kwa njia ya mtandao. Msajili Mkuu aliwashukuru pia kwa kuwateua Majaji nane wa Tanzania kuwa Wasuluhishi wa WIPO.

 

Baada ya kufanyika kwa vikao hiyo kati ya Msajili Mkuu, Afisa Kiungo baina ya Mahakama ya Tanzania na WIPO na Viongozi hao wa Divisheni za WIPO, ujumbe kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ulishiriki kwenye Jukwaa la Majaji la WIPO. Jukwa hilo lilifanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 09 Oktoba, 2024 na lilihudhuriwa na Majaji zaidi ya 350 kutoka Nchi mbalimbali duniani. 

 

Viongozi kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walioshiriki jukwaa hilo katika Makao Makuu ya WIPO nchini Uswisi ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani.   

 

Washiriki wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.  Aisha Ally Sinda, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, Mrajisi wa Mahkama Zanzibar, Mhe. Valentine Katema, Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Jaji Kiongozi, Mhe. Aidan Mwilapwa na Naibu Msajili wa Mahakama ya Tanzanian na Afisa Kiungo  baina ya  Mahakama ya Tanzania na WIPO, Mhe. Upendo Ngitiri. 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (kushoto akiwa na Mkuu wa Idara ya Usuluhishi, Kituo cha Usuluhishi na Upatanishi cha WIPO, Bi. Heike Wollgast. 


Kutoka kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, Naibu Msajili na Afisa Kiungo baina ya Mahakama na WIPO, Mhe. Upendo Ngitiri, Mwanasheria wa WIPO Judicial Institute, Bi. Ines Fernandez, Mkuu wa Idara ya Usuluhishi, Kituo cha Usuluhishi na Upatanishi cha WIPO, Bi. Heike Wollgast na Mkurugenzi wa WIPO Judicial Institute, Bi. Min Eu Joo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kushoto) akiwa na Maafisa Waandamizi kutoka WIPO Academy.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (kushoto) na Afisa Kiungo baina ya Mahakama na WIPO, Mhe. Upendo Ngitiri. 

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

MAHAKIMU, MAWAKILI TABORA WAPIGWA MSASA MATUMIZI YA TEHAMA, AKILI MNEMBA

Na AMANI MTINANGI, Mahakama - Tabora

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora kwa kushirikiana na Chama cha Wanasheria wa Kujitegemea Mkoa wa Tabora imeandaa mafunzo kuhusu Sheria ya Mtandao na Akili Mnemba kwa Mawakili wa Kujitegemea na baadhi ya Mahakimu wa Kanda hiyo.

Akizungumza hivi karibuni wakati wa Mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Tabora, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi alisema kuwa, katika maisha ya sasa shughuli nyingi kibinadamu zimeunganishwa na mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) sambamba na Akili Mnemba.

“Ninatambua kuwa siku hizi maisha ya sasa shughuli nyingi kibinadamu zimeunganishwa na mifumo ya TEHAMA na Akili Mnemba hivyo ni jukumu letu kama wanasheria kujua njia sahihi za kushughulika na mashauri na masuala yanahusisha akili mnemba na uwasilishaji wa vidhibiti vya kielekroniki mahakamani,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Jaji Mfawidhi huyo alisisitiza kuwa, ni muhimu na ni jukumu la Wanasheria kufahamu njia sahihi za kushughulikia mashauri na masuala yanayohusisha akili mnemba pamoja na uwasilishaji wa vidhibiti vya kielekroniki pale vinapohitajika mahakamani.

Wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Wakili Kelvin Kayaga kutoka Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Tabora, alisema Chama hicho kimeandaa mafunzo jumuishi kwa ajili ya Mawakili na Mahakimu wa Kanda ya Tabora kwa lengo la kuongeza ujuzi na maarifa ya Mawakili katika eneo la ushahidi wa kimtandao na akili mnemba.

“Tunafurahi kuandaa mafunzo jumuishi ambapo washiriki wake ni Mawakili wa Kujitegemea na Mahakimu wa Kanda ya Tabora, tukilenga kuongeza ujuzi na maarifa ya Mawakili katika eneo la ushahidi wa kimtandao na akili mnemba,” alisema Wakili Kayaga.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya Sheria ya Mtandao na Akili Mnemba yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora Mhe. Jaji Dkt. Mambi akiwasilisha mada kwa washiriki.
 
Washiriki wa Mafunzo wakifuatilia kwa makini somo linalofundishwa.


Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria wa Kujitegemea Tabora, Wakili Kelvin Kayaga akitoa neno la ufunguzi wa mafunzo ya Mawakili na Mahakimu.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora Mhe. Jaji Dkt. Mambi akiwasilisha mada kwa washiriki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Mambi akiwasilisha mada kwa washiriki wa mafunzo (hawapo katika picha).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)








JAJI MKUU ZANZIBAR, JAJI KIONGOZI MAHAKAMA KUU WASHIRIKI JUKWAA LA KIMATAIFA WIPO

Na Upendo Ngitiri-Mahakama ya Tanzania, Uswisi, Geneva 

 

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdallah na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani hivi karibuni walishiriki kwenye Jukwaa la Majaji nchini Uswisi - Geneva kujadili mambo mbalimbali, ikiwemo Miliki Bunifu (Intellectual Property) na Akili Mnemba (Artificial Intelligence).

 

Jukwa hilo lilifanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Miliki Bunifu “World Intellectual Property Organization” (WIPO) kwa siku mbili kuanzia tarehe 09 Oktoba, 2024. Mbali na kushiriki katika Jukwaa hilo, Viongozi hao walifanya pia mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa WIPO, Bw. Daren Tang na Mkurugenzi Mkuu Msaidizi wa WIPO, Dr. Aleman Marco.

 

Wajumbe wengine kutoka Tanzania walioshiriki Jukwaa hilo ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Aisha Ally Sinda, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, Mrajisi wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Valentine Katema Naibu Msajili na Katibu wa Jaji Kiongozi, Mhe. Aidan Mwilapwa na Naibu Msajili na Mratibu wa Masuala ya Miliki Bunifu wa Mahakama ya Tanzania, Upendo Ngitiri.  

 

Jukwaa hilo lilihudhuria na Majaji  zaidi ya 350 kutoka Nchi mbalimbali duniani na dhumuni lake lililenga kubadilishana uzoefu  wa namna bora ya kushughulikia mashauri yanayohusu miliki bunifu.

 

Ushiriki wa Mahakama katika jukwaa hilo ni sehemu ya utekelezaji wa hati ya makubaliano baina ya Mahakama ya Tanzania na WIPO iliyosainiwa mwaka 2021 na utekelazaji wa ahadi wa ushirikishwaji wa Zanzibar katika shughuli mbalimbali zinazofanywa na WIPO kwa kushirikina na Mahakama ya Tanzania. 

 

Itakumbukwa mwezi Novemba, 2023 alipofanya ziara ya kikazi WIPO, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania aliaomba katika hotuba yake Mahakama ya Zanzibar ishirikishwe kwenye shughuli mbalimbali za WIPO kwa lengo la kuboresha utoaji haki katika eneo la miliki bunifu. 

 

Katika kutekeleza ahadi hiyo, Jaji Mkuu wa Zanzibar na Mrajisi wa Mahkama Zanzibar walipata fursa ya kushiriki jukwaa hilo na kukutana pia na viongozi wa juu wa WIPO. 

 

Wakati wa Jukwaa hilo, Majaji walipata fursa ya kujadili mada mbalimbali   ikiwemo; Akili Mnemba (Artificial Intelligence); Hati Miliki; Alama za Biashara, (Trademarks), Hataza (Patent), Maboresho mahakamani, na nyingine nyingi.  


Majaji kutoka Nchi mbalimbali walitoa  pia uzoefu za Nchi zao, ikiwemo uwepo  wa Mahakama maalum ya kutatua migogoro  ya Miliki Bunifu, kutumika kwa Majaji waliobobea katika Miliki Bunifu kwenye usikilizaji wa mashauri yanayohusu miliki bunifu, uwepo wa “Technical Judges” ambao  kazi yao kubwa ni kushauri Majaji katika eneo linalohitaji  ushauri wa kitaalamu, uwepo wa kanuni  maalum  zinazotoa muongozo  na kuharakisha usikilizaji wa mashauri ya miliki bunifu.

 

Aidha, wakati wa kufanya wasilisho katika jukwaa la Majaji, Mkurugenzi wa WIPO Judicial Institute, Bi. Min Eun Joo alieleza kuwa WIPO inafanya kazi mbalimbali na Mahakama kwa dhumuni la kuziwezesha kutatua migogoro ya miliki bunifu  kwa ufanisi zaidi.

 

Mkurugenzi huyo alieleza pia kuwa WIPO imesaini Hati ya Makubaliano na Mahakama mbalimbali ikiwemo Paraquagy, Ukraine, China, Tanzania, Korea, Thailand, Misri, Albania na  Morroco.

 

 Bi. Min alitolea mfano wa Mahakama ya Tanzania na kueleza kuwa inafanya vizuri na imefanya mambo mengi kwa kushirikiana na WIPO na wangependa kufanya hivyo katika Nchi mbalimbali wanachama. Aliwaeleza Majaji walioshiriki jukwaa hilo shughuli mbalimbali zilizofanywa na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na WIPO tangu mwaka 2018.

 

Mkurugenzi huyo alileza kuwa, mwaka 2019 WIPO kwa kushirikiana na  Mahakama ya Tanzania walifanya  mafunzo  ya ana  kwa ana  kwa Mahakimu jijini Dar es Salaam  na  kuanzia mwaka 2021  hadi 2024,  Majaji na Mahakimu walipata ufadhili wa kusoma  kozi maalum  ya Majaji, kozi ambayo mpaka sasa imeshawanufaisha  Majaji na Mahakimu 402 na itaendelea kutolewa kila mwaka.

 

 Aliongeza kuwa, mwaka 2021 Mahakama kwa kushirikina na WIPO waliandaa pia miongozo maalum kwa Majaji na Mahakimu ya kufundishia mada zinazohusu Miliki Bunifu na mwaka 2022 maamuzi ya Mahakama ya Tanzania na muhtasari wa maamuzi hayo yalianza kuchapishwa kwenye WIPO Lex Judgment Database, zoezi ambalo ni endelevu.

 

Alieleza vilevile kuwa, mwezi Februari, 2023 kongamano la miliki bunifu   lilifanyika kwa njia ya mtandao na Mwezi Novemba, 2023 ujumbe kutoka Mahakama ya Tanzania ulioongozwa na Jaji Kiongozi ulifanya ziara WIPO na mwezi Juni, 2024 kongamano kubwa la kimahakama kuhusu miliki bunifu   lilifanyika  Jijini Dar es Salaam. 

 

Bi.  Min aligusia pia kuwa hivi sasa WIPO kwa kushirikina na Mahakama ya Tanzania inaandaa “IP benchbook” na inatarajiwa kukamilika mwaka 2025.


Mbali na kushiriki jukwaa hilo wakiwa Geneva, Jaji Mkuu wa Zanzibar na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na wajumbe waliombatana nao, walipata fursa ya kukutana na Mkurugenzi Mkuu wa WIPO, Bw.  Daren Tang ambaye alieleza furaha yake juu ya ushirikiano baina ya Mahakama ya Tanzania na WIPO na kupongeza kazi kubwa iliyofanywa na  Mahakama ya Tanzania  kwa kushirikiana na WIPO katika eneo la miliki bunifu. 

 

Daren Tang alieleza kuwa tangu Mahakama ya Tanzania iliposaini hati ya makubalino na WIPO   milango ya Mahakama za Nchi zingine kusaini hati ya makubaliano na WIPO ilifunguka 

 

Naye Mkurugenzi Mkuu Msaidizi wa WIPO, Dkt. Aleman Marco, alipokutana na ujumbe huo katika kikao maalum kilichoandaliwa kwa dhumuni la kuwasilisha salaam za Jaji Mkuu wa Tanzania na kuwatambulisha rasmi Jaji Mkuu wa Zanzibar na wajumbe wengine waliongozana na viongozi hao, aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kushiriki katika jukwaa hilo na kwa  kazi mbalimbali zilizofanywa  na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikina na WIPO.   

 

Dkt. Aleman alieleza pia kuwa, tangu Mahakama iliposaini Hati ya Makubalino     zimefanyika shughuli mbalimbali kwa kushirikiana na WIPO lakini bado wanapenda kusikia kutoka Mahakama ya Tanzania ni mambo gani mengine  wanapenda  kufanyiwa na WIPO.

 

Kwa upande wake, Jaji Kiongozi baada ya kumtambulisha Jaji Mkuu wa Zanzibar na wajumbe alioambatana nao, alifikisha salamu na shukrani kutoka kwa Jaji Mkuu wa Tanzania.  Jaji Kiongozi   aliwashukuru WIPO kwa mchango mkubwa kwa Mahakama na majadiliano yenye tija yaliyofanyika baina ya Msajili Mkuu, Afisa Kiungo baina ya Mahakama na WIPO na Divisheni mbalimbali za WIPO siku ya tarehe 08 Oktoba, 2024.  

 

Baada ya Mkutano huo kukamilika, Viongozi hao walitembelea Ubalozi wa Tanzania Geneva siku ya tarehe 11 Oktoba, 2024 ambapo walifanya mazungumzo na Balozi na Mwakilishi wa Kudumu katika Ofisi za Umoja wa Mataifa Geneva, Uswiswi, Mhe.  Dkt. Abdallah Possi.  Aidha, viongozi hao walimshukuru Balozi kwa ushirikiano mkubwa aliouonesha kwa kipindi chote walipokuwa Geneva na kwa ukarimu wake. 

 

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (wa kwanza kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Shirikika la Miliki Bunifu, "WIPO” Bw. Daren Tang (katikati) na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Mohamed Siyani.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirikika la Miliki Bunifu, “WIPO” Bw. Daren Tang (wa nne kutoka kushoto),wa nne  kulia ni Jaji Kiongozi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, wa tatu kutoka kulia ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, wa kwanza kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Aisha Sinda, wa pili kutoka kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, wa kwanza kushoto ni Mrajisi wa Mahkama Zanzibar, Mhe. Valentine Katema na wa pili kutoka kushoto ni Naibu Msajili na Mratibu wa Masuala ya Miliki Bunifu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Upendo Ngitiri.

Washiriki kutoka nchi mbalimbali duniani waliohudhuria Jukwaa la Miliki Bunifu la Majaji. 


 Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kutoka kulia) akibadhi zawadi kwa Mkurugenzi Mkuu Msaidizi wa WIPO, Dkt. Aleman Marco.



Mkurugenzi Mkuu wa Shirikika la Miliki Bunifu, “WIPO” Bw. Daren Tang (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili na Mratibu wa Masuala ya Miliki Bunifu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Upendo Ngitiri.


Picha ya pamoja ikiwajumuisha Balozi Dkt. Abdalla Possi (wa nne kutoka kulia), wa nne kutoka kushoto ni Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, wa tatu kutoka kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, wa   tatu kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Aisha Sinda, wa pili kutoka kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, wa pili kutoka kushoto ni Mrajisi wa Mahkama Zanzibar, Mhe.Valentine Katema, wa kwanza kutoka kushoto ni Naibu Msajili, Mhe. Aidan Mwilapwa na   wa kwanza kulia ni Naibu Msajili na Mratibu wa Masuala ya Miliki Bunifu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Upendo Ngitiri.


(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 


 

Jumanne, 15 Oktoba 2024

MAHAKAMA KUU SONGEA YATOA MAFUNZO KWA MAHAKIMU KUELEKEA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA

Na NOEL SYLIVESTER – Mahakama, Songea

Kufuatia uchaguzi wa Serikari za Mitaa mwezi Novemba 2024, Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, imetoa mafunzo ya uchaguzi kwa Mahakimu katika Kanda hiyo ili kuwajengea uelewa wa masuala mbalimbali, ikiwemo sheria zinazotumika kwenye zoezi hilo.

Mafunzo hayo yalifanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Huntlcub Ruhuwiko mjini Songea na kufunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songea Mhe. James Karayemaha.

Akizungumza kwenye ufunguzi huo, Jaji Karayemaha alisema mafunzo hayo yameandaliwa kama sehemu ya utekelezaji wa sera ya mafunzo ya mwaka 2019 ambayo yatawajengea uwezo Mahakimu kufahamu sheria mbalimbali zinazohusiana na uchaguzi wa Viongozi wa Serikali za Mitaa kwa mwaka 2024. 

“Mafunzo haya yatawasaidia washiriki kujua sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza uchaguzi, yatasaidia kujua namna bora ya kupokea, kusikiliza na kuamua migogoro ya aina yoyote itakayoletwa mbele yao,” alisema.

Jaji Mfawidhi alieleza kuwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni muhimu katika suala zima la kidemokrasia nchini ambapo Mahakimu wote wa Tanzania ni sehemu ya mchakato wa kufanikisha uchaguzi huo kama Makamishina wa Viapo.

Alisema kuwa Mahakimu kuwa ndiyo watakaowaapisha Wasimamizi wa Uchaguzi na Viongozi watakaochaguliwa kabla ya kuanza kufanya shughuli zao kwa mujibu wa sheria.

Kwa upande wake, Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea, Mhe. Japhet Manyama amemshukuru na kumpongeza Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe kwa kuendesha mafunzo hayo. 

“Mafunzo haya yanatolewa kwa Mahakimu kwa lengo la kuwaandaa kwa ajili ya  kusikiliza na kuamua mashauri yatakayotokea wakati wa  uchaguzi wa Serikali za Mitaa,” alisema.


Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Emmanuel Kawishe akitoa mafunzo.

Sehemu ya Mahakimu wakifatilia mafunzo. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songea Mhe. James Karayemaha (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Emmanuel Kawishe (wa kwanza kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea, Mhe. Japhet Manyama.

Picha ya pamoja kwa waliohudhuria mafunzo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)