- Awaelekeza Mawakili 774 waliopokelewa na kukubaliwa kuhakikisha haki inatendeka kwa wananchi kwa kuzingatia Katiba, Sheria na maadili ya kitaaluma
- Awasisitiza kuwa mstari wa mbele kulinda haki, kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu
- Awataka kudumisha utawala wa sheria na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani
Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Jaji
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewaasa Mawakili wapya kuwiwa
kuona haki ikitendeka, huku wao wakiwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa wanatenda
haki kwa wananchi, kuzingatia uadilifu na wakijikita katika sehemu kuu mbili za
uadilifu ambazo ni kuzingatia Katiba na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania pamoja na Sheria zinazoongoza utumishi na maadili ya mawakili, sambamba
na mila na desturi za Tanzania, kudumisha
Utawala wa Sheria na kutokuwa chanzo cha uvunjifu wa amani.
Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye Sherehe za Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wapya 774 iliyofanyika katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.
“Sasa
mimi nichukue nafasi hii kuwaasa kwamba mtataka na kuendelea kuwa watu wenye
akili nzuri, kama Mawakili, moja mtapaswa kuwa ‘sensitive to justice’ muwiwe
kuona haki inatendeka na ninyi wenyewe
mtende haki, la pili mnapaswa kuwa waadilifu, uadilifu uko kwa maana mbili,
moja kuzingatia Katiba na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zikiwemo na
zile Sheria zinazoongoza utumishi wenu wa uwakili na ni sheria ya mawakili na sheria ya maadili
zinazotungwa na hiyo sheria lakini kuzingatia maadili na mila za Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania,” amesema Jaji Mkuu.
Aidha,
Mhe. Masaju amewataka Mawakili hao kuwa na uwezo wa kumudu kutekeleza majukumu
yao ya kazi ipasavyo, huku wakijiendeleza kielimu jambo ambalo litaongeza
utendaji wao na maarifa zaidi katika utendaji.
“Tatu mtapaswa kuwa watu mnaomudu majukumu yenu kwa jinsi ipasavyo,
viongozi hawa wamewaasa ni namna gani mnaweza kumudu majukumu yenu na
kujiendeleza kimasomo sio mnaridhika tu
na kukaa katika viwango mlivyonavyo, mtapaswa kusoma na hata yanayotokea nje ya
mipaka ya Taifa hili, mjue nini kinakufanya wewe kuwa Wakili.”
Akiendelea
kuzungumza kuhusu uwezo wa kumudu kutekeleza majukumu, Mhe. Masaju ameeleza
kuwa kitu kinachomtambulisha Mwanasheria ni uwezo wa kutafsiri sheria na kutoa
tafsiri hizo kwa watu wengine wanaofahamu na wale wasioifahamu Sheria, kwa Mahakama
au wateja.
“Kitu kingine unachokuja kukigundua katika nini kinachokufanya kuwa Mwanasheria ni uwezo wako wa kutafsiri sheria hizo lakini na kuzitoa hizi tafsiri ulizozitoa kwa watu wengine wasiojua sheria au wanaojua sheria, iwe ni mahakamani iwe ni kwa mteja wako, na ndio maana kuna somo linaitwa communication skills, na pale utaona kwamba hata alama ya kushagaa ina maana kubwa, muundo mbovu katika sentensi unaathiri maana iliyokusudiwa, kwa hiyo sio lazima usome ‘International Law’, ndio ujifunze mambo mengine yanayotokea duniani, suala la umahiri ni la muhimu sana,” amesema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amewataka pia Mawakili hao kuendelea kuzingatia fursa zinazotolewa na Serikali kwa
kujenga mahusiano mazuri ili kutetea maslahi ya taifa, pamoja na kushirikiana
katika majadiliano ya mikataba kwa kuzingatia utayari wa Serikali kupitia Ofisi
ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
“Kwa majukumu haya ambayo mnayo, na nimeona moyo wa utayari wa Serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuendelea kushirikiana na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na ikizingatiwa pia kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndio Mwanasheria namba moja, hivyo endeleeni kuzingatia fursa hizi mnazopewa na Serikali kujenga mahusiano mazuri na Serikali katika kutetea maslahi ya Taifa hili ikiwa ni pamoja na kwenye majadiliano ya mikataba, kama alivyokuwa anasema Rais Magufuli, sisi huku serikalini hatuwezi kujifanya tuna akili kuliko wote, kuna mashughuli ya mikataba tuna kazi nyingi za kufanya,” ameeleza Jaji Mkuu.
Aidha, Mhe. Masaju amewaeleza Mawakili hao kuwa, wanapaswa kufanya kazi bila kupuuza
maslahi ya wanyonge, kuwanyanyasa au kuchukua rushwa ili kupoteza haki zao
halikadhalika kutambua umuhimu wa uzalendo kwa taifa na kwamba mtu atakaye
mpuuza, kumnyanyasa au kuchukua rushwa ili kuipindisha haki ya mtu mnyonge basi
mtu huyo ataadhibiwa na Mungu.
“Mtu
atakayempuuza mnyonge na kumnyanyasa akachukua rushwa ili kuhatarisha haki na
maslahi ya mteja wake mnyonge huyo Mungu atamuadhibu, hawezi kufanikiwa, na Wakili miongoni mwenu ambaye hatambui
umuhimu wa uzalendo kwa Taifa hili ni kama hayupo, kwa sababu fursa yako
ya kufanya 'legal practice' ni katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sio
kwingineko, na fursa hizo ziko za kutosha, miongoni mwenu pia huwa wanateuliwa
Majaji na miongoni mwenu huwa wanateuliwa watu wengine kushika nyazfa
mbalimbali katika utumishi wa umma," amesema.
“Mungu
ni Mwanasheria na yeye ni wa utawala wa sheria na utawala wake unaongozwa na
Katiba, na Katiba ile ina Ibara mbili kumpenda Mungu na kumfanya kuwa wa kwanza
katika maisha yako yote, lakini na kumpenda jirani yako kama nafsi yako, lakini
hiyo katiba yenye Ibara mbili ina zile Amri kumi, kwa hiyo ukisoma kile kitabu
cha Kutoka sura ya 20 utapata zile Amri kumi, na Kutoka sura ya 21 mpaka 23 pale kuna zile sheria ndogo zinazotafsiri
zile amri nyingine.na ukizifuata hizo na kuziishi utafanikiwa katika maisha
yako, Mhe. Mwabukusi amesisitiza sana kuhusu hii ya kuwajali maskini na
wanyonge muwe na huruma hapo mtakuwa mnatekeleza ile amri kumpenda jirani yako
kama nafsi yako, katika ibara ya pili katika ile Katiba ya Mungu ambayo ni
upendo,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Katika
upande mwingine, Mhe. Masaju ametoa ushauri kwa Shule ya Sheria ya Tanzania kuanzisha
programu mbalimbali za vitendo ambazo zitatumika kuwapima Wanasheria kuliko zile
za nadharia, ili kutoa fursa kwa vijana wanaohitimu kutoa huduma ya kisheria
kwa jamii.
“Na kwa kuzingatia umuhimu wa ujuzi wa vitendo katika taaluma ya sheria, napenda kutoa ushauri kwa Shule ya Sheria ya Tanzania kuanzisha programu mbalimbali za mafunzo ya vitendo kwenye nadharia unakamata watu wengi lakini sio kwenye vitendo, sisi Serikalini tunachukua hatua tunataka kila mhitimu wa Shahada ya Sheria apate uwezo wa kusoma hicho chuo kusudi ije imsaidie na yeye ama kujiajiri au kuajiriwa,” ameeleza Mhe. Masaju.
Ameongeza kuwa, suala la wanafunzi wanaosoma katika Shule ya Sheria ya Tanzania kupata mikopo linafanyiwa kazi na Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria ili kutoa fursa kwa vijana kusoma Shule ya Sheria ya Tanzania.
“Nilivyokuwa
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali niliweka kwenye muswada kwamba Wanasheria
wanaoenda kusoma Diploma ya Sheria pale Shule ya Sheria ya Tanzania nao waweze kupata mkopo, hawa watu
watafanyaje, wao wanaenda kusoma Vyuo Vikuu kwa mikopo na ili waweze kufanya
kazi wanapaswa wawe wamesoma Shule ya
Sheria ya Tanzania, mikopo hawana sasa wataendaje kusoma, kwa hiyo
tumeshachukua hatua ndani ya Wizara ya Katiba na Sheria hili tatizo litapatiwa
utatuzi siku hizi za karibuni, Serikali lazima itoe mkopo kwa kila mwanafunzi
ili aweze kupata nafasi ya kusoma Shule ya Sheria ya Tanzania,” Mhe. Masaju
ameeleza.
Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju amewataka
Mawakili Wapya wa Kujitegemea kutawanyika katika maeneo mbalimbali nchini ili
kufikisha huduma zao za utetezi wa haki kwa wananchi wengi zaidi.
“Kwa sasa kama mnavyofahamu kwenye Mahakama za Mwanzo, makosa yote yanadhaminika maana yake ni kwamba kama milango ya dhamana itafunguka kuna uwezekano mkubwa sana Mahakama ya Mwanzo kuongezewa majukumu ambapo sasa ninyi mtakuwa mnaenda kufanya kazi huko kwa sababu soko lipo, hii habari ya kwenda kukaa Dar es Salaam, Dodoma na Miji mingine Mhe. Mwabukusi amewatajia maeneo mengine ambapo fursa zipo nyingi, kwahiyo niwaombe sana jiandaeni,” amesema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amesema mnamo tarehe 05 Aprili, 2025, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokuja kuzindua Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania aliridhia Sera ya Mahakama ya kuwa na Mahakama ya Mwanzo kila Kata maana yake zitajenga Mahakama za Mwanzo.
Jaji Mkuu amewaeleza Mawakili hao kutawanyika
kwani kwa sasa Mawakili wa Kujitegemea na Mawakili wa Serikali wanaruhusiwa
kwenda kwenye Mahakama za Mwanzo kama Hakimu ni Hakimu Mkazi yaani Hakimu
ambaye ana Shahada ya Sheria. Mhe. Masaju amesisitiza, “ninawahakikishia kuwa
nafasi ya kipaumbele cha kwanza katika msingi mkuu wa Dira ni Utawala Bora na
Haki na hivi vitu huwa vinaenda pamoja. Tunataka Wanasheria wanaohitimu wapate
soko wasiwe na sababu ya kuilalamikia Serikali.”
Mhe. Masaju amesema kuwa, hadi kufikia mwaka 2026 kuna Sheria ya Dhamana (The Bail Act) itatungwa ambayo inaweka taratibu za kina na sababu za kutoa dhamana au kuzinyima. Ameeleza kwamba, kabla mwaka 2026 haujaisha sheria hiyo itakuwa tayari na ikitokea ni hivyo na umewekwa utaratibu kwa makosa machache ambayo hayana dhamana itatakiwa kesi iwe imeanza kusikilizwa ndani ya kipindi cha miezi sita la sivyo watu watapata dhamana.
Kadhalika, Mhe. Masaju amekemea tabia ya baadhi
ya Mawakili kuwalazimisha wateja wao kufungua kesi zisizo na msingi sanjari na
tabia ya kuegesha mashauri mahakamani.
Aidha, Jaji Mkuu amewaasa Mawakili hao
kuzingatia Kanuni/vitendea kazi muhimu nane katika utumishi wao ambavyo ni
pamoja na Uadilifu (Integrity), Uwezo wa kutekeleza majukumu (Competency), Kuwiwa kuona haki inatendeka (Sensitivity to
justice), Uwajibikaji
(Accountability).
Vingine ni Ubunifu (Creativity), Uchukuaji
hatua kwa mapema (Proactivity), Uzalendo wa Kitaifa (National Patriotism) na
Uhalisia/ukweli usioegemea upande wowote (Objectivity).
Katika
kumalizia Mhe. Masaju amewatakia baraka Mawakili wapya na kuwaombea kwa
Mwenyezi Mungu awabariki katika shuhuli zao za kila siku za kutetea haki na
kuwa wakifanya hivyo watakuwa watu wenye mafanikio makubwa.
“Ombi
langu kwa Mwenyezi Mungu ni hili, kwamba Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki
katika maisha yenu katika utumishi wenu na shughuli zenu za kutetea haki, haki,
na mkifanya hivyo mtafanikiwa sana,” amesema.
Kwa mujibu wa Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, kukubaliwa na Kupokelewa kwa Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 kunafanya idadi ya Mawakili walioandikishwa nchini kufikia 14,220.
Kati ya Mawakili hao wapya 439 ni Wanaume na 335 ni Wanawake.
Sehemu ya Mawakili wapya wa Kujitegemea wakitoa heshima mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) mara baada ya Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wapya 774 kwenye Sherehe iliyofanyika leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi akitoa hotuba wakati wa Sherehe ya Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wa Kujitegemea 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.
Mawakili wa Kujitegemea wapya wakisaini Viapo vya maadili kwenye Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili Wapya wa Kujitegemea leo tarehe 05 Desemba, 2025 katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.






















































