Ijumaa, 5 Desemba 2025

JAJI MKUU, MHE. GEORGE MASAJU AWAASA MAWAKILI WAPYA KUDUMISHA UADILIFU, UTAWALA WA SHERIA

  • Awaelekeza Mawakili 774 waliopokelewa na kukubaliwa kuhakikisha haki inatendeka kwa wananchi kwa kuzingatia Katiba, Sheria na maadili ya kitaaluma 
  • Awasisitiza kuwa mstari wa mbele kulinda haki, kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu
  • Awataka kudumisha utawala wa sheria na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani

Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewaasa Mawakili wapya kuwiwa kuona haki ikitendeka, huku wao wakiwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa wanatenda haki kwa wananchi, kuzingatia uadilifu na wakijikita katika sehemu kuu mbili za uadilifu ambazo ni kuzingatia Katiba na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Sheria zinazoongoza utumishi na maadili ya mawakili, sambamba na mila na desturi za Tanzania, kudumisha Utawala wa Sheria na kutokuwa chanzo cha uvunjifu wa amani.

Mhe. Masaju ametoa wito huo leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye Sherehe za Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wapya 774 iliyofanyika katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.

“Sasa mimi nichukue nafasi hii kuwaasa kwamba mtataka na kuendelea kuwa watu wenye akili nzuri, kama Mawakili, moja mtapaswa kuwa ‘sensitive to justice’ muwiwe kuona haki inatendeka  na ninyi wenyewe mtende haki, la pili mnapaswa kuwa waadilifu, uadilifu uko kwa maana mbili, moja kuzingatia Katiba na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zikiwemo na zile Sheria zinazoongoza utumishi wenu wa uwakili  na ni sheria ya mawakili na sheria ya maadili zinazotungwa na hiyo sheria lakini kuzingatia maadili na mila za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju amewataka Mawakili hao kuwa na uwezo wa kumudu kutekeleza majukumu yao ya kazi ipasavyo, huku wakijiendeleza kielimu jambo ambalo litaongeza utendaji wao na maarifa zaidi katika utendaji.  “Tatu mtapaswa kuwa watu mnaomudu majukumu yenu kwa jinsi ipasavyo, viongozi hawa wamewaasa ni namna gani mnaweza kumudu majukumu yenu na kujiendeleza kimasomo sio mnaridhika tu na kukaa katika viwango mlivyonavyo, mtapaswa kusoma na hata yanayotokea nje ya mipaka ya Taifa hili, mjue nini kinakufanya wewe kuwa Wakili.”

Akiendelea kuzungumza kuhusu uwezo wa kumudu kutekeleza majukumu, Mhe. Masaju ameeleza kuwa kitu kinachomtambulisha Mwanasheria ni uwezo wa kutafsiri sheria na kutoa tafsiri hizo kwa watu wengine wanaofahamu na wale wasioifahamu Sheria, kwa Mahakama au wateja.

“Kitu kingine unachokuja kukigundua katika nini kinachokufanya kuwa Mwanasheria ni uwezo wako wa kutafsiri sheria hizo lakini na kuzitoa hizi tafsiri ulizozitoa kwa watu wengine wasiojua sheria au wanaojua sheria, iwe ni mahakamani iwe ni kwa mteja wako, na ndio maana kuna somo linaitwa communication skills, na pale utaona kwamba hata alama ya kushagaa ina maana kubwa, muundo mbovu katika sentensi unaathiri maana iliyokusudiwa, kwa hiyo sio lazima usome ‘International Law’, ndio ujifunze mambo mengine yanayotokea duniani, suala la umahiri ni la muhimu sana,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amewataka pia Mawakili hao kuendelea kuzingatia fursa zinazotolewa na Serikali kwa kujenga mahusiano mazuri ili kutetea maslahi ya taifa, pamoja na kushirikiana katika majadiliano ya mikataba kwa kuzingatia utayari wa Serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

“Kwa majukumu haya ambayo mnayo, na nimeona moyo wa utayari wa Serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuendelea kushirikiana na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na ikizingatiwa pia kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndio Mwanasheria namba moja, hivyo endeleeni kuzingatia fursa hizi mnazopewa na Serikali kujenga mahusiano mazuri na Serikali katika kutetea maslahi ya  Taifa hili ikiwa  ni pamoja na kwenye majadiliano ya mikataba, kama alivyokuwa anasema Rais Magufuli, sisi huku serikalini hatuwezi kujifanya tuna akili kuliko wote, kuna mashughuli ya mikataba tuna kazi nyingi za kufanya,” ameeleza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju amewaeleza Mawakili hao kuwa, wanapaswa kufanya kazi bila kupuuza maslahi ya wanyonge, kuwanyanyasa au kuchukua rushwa ili kupoteza haki zao halikadhalika kutambua umuhimu wa uzalendo kwa taifa na kwamba mtu atakaye mpuuza, kumnyanyasa au kuchukua rushwa ili kuipindisha haki ya mtu mnyonge basi mtu huyo ataadhibiwa na Mungu.

“Mtu atakayempuuza mnyonge na kumnyanyasa akachukua rushwa ili kuhatarisha haki na maslahi ya mteja wake mnyonge huyo Mungu atamuadhibu, hawezi kufanikiwa, na Wakili miongoni mwenu ambaye hatambui  umuhimu wa uzalendo kwa Taifa hili ni kama hayupo, kwa sababu fursa yako ya kufanya 'legal practice' ni katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sio kwingineko, na fursa hizo ziko za kutosha, miongoni mwenu pia huwa wanateuliwa Majaji na miongoni mwenu huwa wanateuliwa watu wengine kushika nyazfa mbalimbali katika utumishi wa umma," amesema.

“Mungu ni Mwanasheria na yeye ni wa utawala wa sheria na utawala wake unaongozwa na Katiba, na Katiba ile ina Ibara mbili kumpenda Mungu na kumfanya kuwa wa kwanza katika maisha yako yote, lakini na kumpenda jirani yako kama nafsi yako, lakini hiyo katiba yenye Ibara mbili ina zile Amri kumi, kwa hiyo ukisoma kile kitabu cha Kutoka sura ya 20 utapata zile Amri kumi, na Kutoka sura ya 21 mpaka  23 pale kuna zile sheria ndogo zinazotafsiri zile amri nyingine.na ukizifuata hizo na kuziishi utafanikiwa katika maisha yako, Mhe. Mwabukusi amesisitiza sana kuhusu hii ya kuwajali maskini na wanyonge muwe na huruma hapo mtakuwa mnatekeleza ile amri kumpenda jirani yako kama nafsi yako, katika ibara ya pili katika ile Katiba ya Mungu ambayo ni upendo,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Katika upande mwingine, Mhe. Masaju ametoa ushauri kwa Shule ya Sheria ya Tanzania kuanzisha programu mbalimbali za vitendo ambazo zitatumika kuwapima Wanasheria kuliko zile za nadharia, ili kutoa fursa kwa vijana wanaohitimu kutoa huduma ya kisheria kwa jamii.

“Na kwa kuzingatia umuhimu wa ujuzi wa vitendo katika taaluma ya sheria, napenda kutoa ushauri kwa Shule ya Sheria ya Tanzania kuanzisha programu mbalimbali za mafunzo ya vitendo kwenye nadharia unakamata watu wengi lakini sio kwenye vitendo, sisi Serikalini tunachukua hatua tunataka kila mhitimu wa Shahada ya Sheria apate uwezo wa kusoma hicho chuo kusudi ije imsaidie na yeye ama kujiajiri au kuajiriwa,” ameeleza Mhe. Masaju. 

Ameongeza kuwa, suala la wanafunzi wanaosoma katika Shule ya Sheria ya Tanzania kupata mikopo linafanyiwa kazi na Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria ili kutoa fursa kwa vijana kusoma Shule ya Sheria ya Tanzania. 

“Nilivyokuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali niliweka kwenye muswada kwamba Wanasheria wanaoenda kusoma Diploma ya Sheria pale Shule ya Sheria ya Tanzania  nao waweze kupata mkopo, hawa watu watafanyaje, wao wanaenda kusoma Vyuo Vikuu kwa mikopo na ili waweze kufanya kazi wanapaswa wawe  wamesoma Shule ya Sheria ya Tanzania, mikopo hawana sasa wataendaje kusoma, kwa hiyo tumeshachukua hatua ndani ya Wizara ya Katiba na Sheria hili tatizo litapatiwa utatuzi siku hizi za karibuni, Serikali lazima itoe mkopo kwa kila mwanafunzi ili aweze kupata nafasi ya kusoma Shule ya Sheria ya Tanzania,” Mhe. Masaju ameeleza.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju amewataka Mawakili Wapya wa Kujitegemea kutawanyika katika maeneo mbalimbali nchini ili kufikisha huduma zao za utetezi wa haki kwa wananchi wengi zaidi.

“Kwa sasa kama mnavyofahamu kwenye Mahakama za Mwanzo, makosa yote yanadhaminika maana yake ni kwamba kama milango ya dhamana itafunguka kuna uwezekano mkubwa sana Mahakama ya Mwanzo kuongezewa majukumu ambapo sasa ninyi mtakuwa mnaenda kufanya kazi huko kwa sababu soko lipo, hii habari ya kwenda kukaa Dar es Salaam, Dodoma na Miji mingine Mhe. Mwabukusi amewatajia maeneo mengine ambapo fursa zipo nyingi, kwahiyo niwaombe sana jiandaeni,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema mnamo tarehe 05 Aprili, 2025, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokuja kuzindua Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania aliridhia Sera ya Mahakama ya kuwa na Mahakama ya Mwanzo kila Kata maana yake zitajenga Mahakama za Mwanzo. 

Jaji Mkuu amewaeleza Mawakili hao kutawanyika kwani kwa sasa Mawakili wa Kujitegemea na Mawakili wa Serikali wanaruhusiwa kwenda kwenye Mahakama za Mwanzo kama Hakimu ni Hakimu Mkazi yaani Hakimu ambaye ana Shahada ya Sheria. Mhe. Masaju amesisitiza, “ninawahakikishia kuwa nafasi ya kipaumbele cha kwanza katika msingi mkuu wa Dira ni Utawala Bora na Haki na hivi vitu huwa vinaenda pamoja. Tunataka Wanasheria wanaohitimu wapate soko wasiwe na sababu ya kuilalamikia Serikali.”

Mhe. Masaju amesema kuwa, hadi kufikia mwaka 2026 kuna Sheria ya Dhamana (The Bail Act) itatungwa ambayo inaweka taratibu za kina na sababu za kutoa dhamana au kuzinyima. Ameeleza kwamba, kabla mwaka 2026 haujaisha sheria hiyo itakuwa tayari na ikitokea ni hivyo na umewekwa utaratibu kwa makosa machache ambayo hayana dhamana itatakiwa kesi iwe imeanza kusikilizwa ndani ya kipindi cha miezi sita la sivyo watu watapata dhamana.

Kadhalika, Mhe. Masaju amekemea tabia ya baadhi ya Mawakili kuwalazimisha wateja wao kufungua kesi zisizo na msingi sanjari na tabia ya kuegesha mashauri mahakamani.

Aidha, Jaji Mkuu amewaasa Mawakili hao kuzingatia Kanuni/vitendea kazi muhimu nane katika utumishi wao ambavyo ni pamoja na Uadilifu (Integrity), Uwezo wa kutekeleza majukumu (Competency)Kuwiwa kuona haki inatendeka (Sensitivity to justice)Uwajibikaji (Accountability).

Vingine ni Ubunifu (Creativity), Uchukuaji hatua kwa mapema (Proactivity), Uzalendo wa Kitaifa (National Patriotism) na Uhalisia/ukweli usioegemea upande wowote (Objectivity).

Katika kumalizia Mhe. Masaju amewatakia baraka Mawakili wapya na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu awabariki katika shuhuli zao za kila siku za kutetea haki na kuwa wakifanya hivyo watakuwa watu wenye mafanikio makubwa.

“Ombi langu kwa Mwenyezi Mungu ni hili, kwamba Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki katika maisha yenu katika utumishi wenu na shughuli zenu za kutetea haki, haki, na mkifanya hivyo mtafanikiwa sana,” amesema.

Kwa mujibu wa Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa, kukubaliwa na Kupokelewa kwa Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 kunafanya idadi ya Mawakili walioandikishwa nchini kufikia 14,220.

Kati ya Mawakili hao wapya  439 ni Wanaume na 335 ni Wanawake.

Sehemu ya Mawakili wapya wa Kujitegemea wakitoa heshima mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) mara baada ya Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wapya 774 kwenye Sherehe iliyofanyika leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.



Picha za makundi mbalimbali ya Mawakili wapya wa Kujitegemea wakiwa katika sherehe za Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Mawakili wapya wa Kujitegemea mara baada ya 
Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wapya wa Kujitegemea 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno akitoa hotuba wakati wa Sherehe ya Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wa Kujitegemea 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.


Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi akitoa hotuba wakati wa Sherehe ya Kuwapokea na Kuwakubali Mawakili wa Kujitegemea 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.

Sehemu ya Viongozi walioshiriki kwenye Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili Wapya wa Kujitegemea leo tarehe 05 Desemba, 2025 katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma. 


Mawakili wa Kujitegemea wapya wakisaini Viapo vya maadili 
kwenye Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili Wapya wa Kujitegemea leo tarehe 05 Desemba, 2025 katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma. 

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja kwenye 
Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili Wapya wa Kujitegemea leo tarehe 05 Desemba, 2025 katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma. 

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika sherehe hizo.



Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na makundi kadhaa ya Mawakili wapya wa Kujitegemea mara baada ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili Wapya wa Kujitegemea 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 katika ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma. 

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

 

 

MAKUMBUSHO YA MAHAKAMA TANZANIA YANUKIA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Watumishi 12 wa Mahakama ya Tanzania, wakiongozwa na Mkurugenzi kutoka Idara ya Usimamizi wa Kumbukumbu, Bw. Malimo Manyambura, walifanya ziara maalum kwenye Makumbusho ya Taifa jijini Dar es Salaam kwa lengo ka kujifunza mambo mbalimbali, ikiwemo mbinu bora za uanzishaji, usimamizi na uendeshaji wa makumbusho.

Ziara hiyo ya siku mbili ambayo ilifanyika kuanzia tarehe 2 Desemba, 2025 imewawezesha watumishi hao wa Mahakama kupata uelewa wa namna ya kuanzisha makumbusho, jinsi ya kukusanya taarifa na uendeshaji kwa ujumla.

Wakiwa katika Makubusho hayo ya Taifa, ujumbe huo wa Mahakama ulipokea mada mbalimbali zilizowasilishwa na wataalam waliobobea kwenye masuala ya uhifandhi, walioongozwa na Mkurugenzi wa Makumbusho na Malikale, Bi. Adelaide Sallema.

Mada zilizowasilishwa wakati wa ziara hizo zilihusu makumbusho ni kitu gani, majukumu na kazi zake kwa ujumla na muundo wa uongozi wa makumbusho.

Watumishi wa Mahakama pia walipishwa kwenye mada inayohusu Sheria, Sera na Miongozo ya uanzishwaji na usimamizi wa makumbusho; Dhana ya uhuifadhi katika makumbusho na Kanuni na taratibu za utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka kama rasilimali muhimu katika Taasisi.

Mada nyingine zilihusu usimamizi na uendeshaji wa makumbusho na ushiriki wa umma na katika makumbusho. Miongoni mwa wataalam wengine waliowasilisha mada wakati wa ziara hiyo walikuwa Mkuu wa Idara ya Utafiti, Uteuzi wa Maonesho na Uhifadhi Wilbard Lema na Ofisa Utalii Antonia Mkama.

Baada ya kupata mada hizo, watumishi wa Mahakama walipitishwa kwenye maeneo mbalimbali katika Makumbusho ya Taifa kujionea hazina ya makumbusho yaliyopo tangu uhuru, yakiwemo magari ya kifahari yaliyokuwa yanatumiwa na Baba wa Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Awamu ya Kwanza, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Watumishi wa Mahakama pia walitembelea Kijiji cha Makumbusho kilichopo Kijitonyama na kujionea makazi ya asili ya Watanzania wa makabila kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Mahakama ya Tanzania imepitia vipindi mbalimbali vya kihistoria tangu kuanzishwa kwake. Historia hii inajumuisha mabadiliko ya kimfumo, uongozi, changamoto zilizojitokeza na mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha utoaji wa haki na utawala wa sheria. Hifadhi ya historia hii ni muhimu kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo na ni nyenzo muhimu ya elimu, kumbukumbu na utambulisho wa kitaifa.

Kwa msingi huo, Mahakama ya Tanzania inampango wa kuanzisha Makumbusho ya Mahakama ya Tanzania itakayohifadhi na kuonyesha vifaa na taarifa za kihistoria (Objects and Documentary Materials) ikiwa ni pamoja na nyaraka, vielelezo, picha na vifaa vilivyotumika katika nyakati mbalimbali za kihistoria kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo na kuimarisha uelewa wa umma kuhusu mchango wa Mahakama katika maendeleo ya taifa na utawala wa sheria.

Watumishi wa Mahakama waliofanya ziara hiyo walitoka katika Idara na Vitengo mbalimbali, ikiwemo Idara ya Usimamizi wa Kumbukumbu (DRM), Idara ya Usimamizi wa Mashauri (DCM), Idara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia (DICT), Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu (DARHM), Idara ya Usimamizi na Uendelezaji wa Milki (DEDM) na Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano (HIECU).


Watumishi 12 wa Mahakama ya Tanzania wakiwa na wenyeji wao wakati wa ziara kwenye Makumbusho ya Taifa jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi kutoka Idara ya Usimamizi wa Kumbukumbu, Bw. Malimo Manyambura [kushoto] akipokea zawadi kutoka Mkurugenzi wa Makumbusho na Malikale, Bi. Adelaide Sallema wakati wa ziara hiyo.

Mkurugenzi kutoka Idara ya Usimamizi wa Kumbukumbu, Bw. Malimo Manyambura akizungumza wakati wa ziara hiyo. Picha mbili chini ni Mkurugenzi wa Makumbusho na Malikale, Bi. Adelaide Sallema.
 


Watumishi wa Mahakama ya Tanzania [juu na chini] wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa ziara hiyo.



Ofisa Utalii Antonia Mkama akifafanua jambo.

Ofisa Utalii Lisa Shirima akitoa maelezo kwa watumishi wa Mahakama wakati wa ziara hiyo. Picha chini akitoa maelezo kuhusu magari ya kifahari yaliyotumiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.


Muhifadhi Elimu Mwandamizi kutoka Kijiji cha Makumbusho, Bi. Wilhelmina Joseph akitoa maelezo kwa watumishi wa Mahakama walipotembelea kijiji hicho.

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania wakifanya 'demo' ya kusikiliza shauri kwenye Mahakama ya Wakinga baada ya mtuhumiwa [aliyekaa katikati] kukamatwa ugoni. Watumishi hao walikuwa kwenye Kijiji cha Makumbusho.




UWAKILI NI WITO WA HAKI: MWABUKUSI

  • Serikali yasisitiza ushirikiano kuwezesha upatikanaji wa haki kwa wananchi

Na HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno wamewahimiza Mawakili wapya 774 kuutumikia wito wao kwa uadilifu, uzalendo na ushirikiano katika kuboresha mfumo wa utoaji haki nchini.

Akizungumza leo tarehe 05 Desemba, 2025, kwenye Sherehe za Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili hao wapya, Wakili Mwabukusi amesema kuwa kazi ya uwakili siyo ajira ya kawaida bali ni wito wa kuhudumia haki na jamii kwa mujibu wa Katiba na misingi ya utawala bora.

Akizungumza katika Sherehe hito, Rais wa TLS amesema kuwa kuwakilisha wateja ni kuhudumia haki, kulinda misingi ya katiba na kuendeleza utawala wa sheria unaozingatia usawa na haki za binadamu.

“Wakili ni mtu ambaye kiwango chake cha uzalendo kwa Taifa, ujasiri katika kusimamia na kulinda Katiba na sheria, pamoja na utawala bora na haki za binadamu, kinapaswa kuwa cha juu kuliko kitu kingine chochote,” amesema Wakili Mwabukusi.

Ameongeza kuwa, Mawakili ni nguzo muhimu katika jamii na wanapaswa kuishi kwa maadili, uadilifu na ukweli, huku akisisitiza kuwa uaminifu kwa wateja, mahakama na jamii ni mtaji mkubwa unaojengwa kwa muda mrefu lakini unaweza kupotea kwa kosa moja.

Wakili Mwabukusi pia amewakumbusha mawakili wapya umuhimu wa elimu endelevu, kujitolea kwa ajili ya wanyonge, kuheshimu mahakama na kushirikiana kwa karibu na mihimili ya dola kwa maslahi ya taifa. Aidha amesisitiza kuwa Chama cha Wanasheria Tanganyika si mpinzani wa Serikali bali ni mshirika katika kusimamia utawala wa sheria, haki za binadamu na utawala bora.

Kwa upande wake, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali amewapongeza mawakili wote waliokubaliwa pamoja na Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo (Law School of Tanzania) kwa kazi kubwa ya kuwaandaa wanataaluma hao.

Amesema mafanikio ya Mawakili wapya ni matokeo ya jitihada za muda mrefu za walimu, wazazi, walezi, Serikali na wadau mbalimbali waliochangia katika safari yao ya kitaaluma.

Bw. Maneno ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya Sheria, akieleza kuwa ongezeko la mawakili nchini litaongeza kasi ya upatikanaji wa haki kwa wananchi na kusaidia kupunguza changamoto za kisheria.

Ameeleza kuwa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itaendelea kushirikiana bega kwa bega na mawakili pamoja na wadau wa haki jinai na madai katika kuboresha mfumo wa utoaji haki nchini.

“Mawakili ni kiungo muhimu kati ya wananchi na mahakama. Mna nafasi kubwa sana ya kuhakikisha haki inapatikana kwa ufanisi na kwa kuzingatia sheria, usawa na haki za binadamu,” amesema.

Kauli za Viongozi hao zimekuja wakati ambapo Taifa linaendelea kushuhudia ongezeko la idadi ya mawakili, hali inayotajwa kuwa chachu ya kuimarisha utawala wa sheria, amani na maendeleo ya jamii kwa ujumla.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno akizungumza wakati wa Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi akitoa hotuba yake wakati wa Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.






Baadhi ya makundi ya Mawakili wa Kujitegemea wapya wakifuatilia hotuba zilizokuwa zikitolewa wakati wa Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)