Jumatatu, 12 Mei 2025

VIONGOZI MAHAKAMA KUU NA WILAYA TABORA WAKAGUA MAHAKAMA ZA MWANZO UPUGE NA IMALAKASEKO

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Kanda hiyo, Bw. Emmanuel Munda pamoja na viongozi wa Mahakama ya Wilaya ya Uyui kwa pamoja wameambatana katika ziara ya kikazi iliyolenga kukagua miundombinu ya Mahakama za Mwanzo Upuge na Imalakaseko zilizopo katika Wilaya ya Uyui mkoani Tabora.

Ziara hiyo iliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita ililenga kufanya tathmini ya hali ya miundombinu ya majengo ya Mahakama hizo  ili kuangalia mazingira ya utoaji huduma za kimahakama katika maeneo hayo. 

Viongozi hao waliangazia masuala muhimu yanayohusu maandalizi ya kuanzisha huduma za kimahakama katika maeneo hayo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Mahakama ya Tanzania za kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi.

Wakiwa katika Kijiji cha Upuge, viongozi hao walikutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Kata na Serikali ya Kijiji, wakiongozwa na Diwani wa Kata hiyo, Mhe. Juma Luwanga ambaye alitoa shukrani zake kwa uongozi wa Mahakama kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kusogeza huduma za haki karibu na wananchi wa Kata hiyo.

“Tunaishukuru Mahakama kwa kutambua umuhimu wa wananchi kupata huduma karibu hivyo kuamua kuanza mipango ya kuanzisha Mahakama ya Mwanzo Upuge, hatua hii ni ya kupongezwa, sisi kama viongozi wa Serikali ya Mtaa na kwa niaba ya wananchi wa eneo hili tupo tayari kushirikiana katika utekelezaji wa jambo hili,” alisema Mhe. Luwanga.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo alieleza kuwa, Mahakama ya Tanzania inatekeleza Mpango Mkakati wake kwa kuhakikisha kuwa huduma za utoaji haki zinapatikana kwa urahisi, ufanisi na kwa wakati na kusisitiza juu ya umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama na wadau wa maendeleo katika jamii ili kufanikisha azma ya utoaji wa haki kwa wote na kwa wakati.

Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi katika eneo lililopendekezwa kwa ajili ya uanzishwaji wa Mahakama ya Mwanzo Upuge, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Bw. Emmanuel Munda, alieleza kwamba, taratibu za awali zinaendelea vizuri na mara tu maandalizi hayo yatakapokamilika, utekelezaji utaanza mara moja lengo likiwa ni kusogeza huduma za kimahakama kwa wananchi wa eneo hilo.

"Mara baada ya mipango hii kukamilika, Mahakama ya Mwanzo Upuge itaanza kazi mara moja ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kimahakama karibu na maeneo yao," alisema Bw. Munda.

Mahakama za Mwanzo Upuge na Imalakaseko zilianzishwa miaka mingi iliyopita kama sehemu ya kuimarisha utawala wa sheria katika maeneo hayo. Mahakama ya Mwanzo Upuge ilianzishwa mwaka 1953 kwa lengo la kutoa huduma za kisheria kwa wananchi wa kijiji hicho na maeneo jirani. Hata hivyo, kwa sasa mahakama hiyo haifanyi kazi katika eneo hilo  kwa zaidi ya miaka 30 kwa mujibu wa uongozi wa Kijiji cha Upuge.   

Shughuli za Mahakama ya Upuge kwa sasa zinafanyikia majengo ya Wilaya ya Uyui ambayo iko takriban kilometa 30 kutoka kijiji cha Upuge. Hali hiyo inawaathiri wananchi wa eneo hilo kwa kuwa wanakutana na changamoto za usafiri na upatikanaji wa huduma za kisheria kwa wakati muafaka.

Ziara hiyo imeonesha dhamira ya dhati ya Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha utoaji huduma kwa wananchi kama ilivyoainishwa kwenye Mpango Mkakati wake.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo akizungumza jambo hivi karibuni wakati wa kikao na wajumbe wa Kata na Serikali ya Upuge.

Diwani wa Kata ya Upuge, Mhe. Juma Luwanga akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kwa niaba ya wananchi wa Kata hiyo.
Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Tabora (walioketi) wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Kata na Kijiji cha Upuge  wakati wa kikao baina yao.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Bw. Emmanuel Munda akielekeza jambo wakati wa ukaguzi katika jengo linalotarajiwa kukarabatiwa kwa ajili ya kuanza kutoa huduma za Mahakama ya Mwanzo Kigwa.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


MAHAKIMU SAME WAKUTANA KUJINOA MABADILIKO MBALIMBALI YA SHERIA

Na JAMES KAPELE,  Mahakama-Moshi

Mahakimu Wakazi wote wa Mahakama ya Wilaya ya Same wamekutana katika Mahakama ya Wilaya ya Same kwa lengo la kupitia pamoja mabadiliko ya sheria mbalimbali ambazo zimefanyiwa marekebisho hivi karibuni ili kupata uelewa wa pamoja na kubadilishana uzoefu katika changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika kazi zao za kila siku za uendeshaji wa mashauri. 

Kikao hicho kilifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita tarehe 09 Mei, 2025 kikiwa kimeitishiwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Same, Mhe. Chrisanta Chitanda.

Awali akifungua kikao hicho ofisini kwake , Mhe. Chitanda aliwasihi  Mahakimu waliohudhuria kikao hicho kujenga utamaduni wa kuwa tayari wakati wote kuendana na mabadiliko ya kisheria pindi yanapotokea ili wafanye kazi yao ya kuzitafsiri sheria hizo kwa weledi wanapotekeleza majukumu yao ya kila siku.

“Kazi zetu ni za kusoma kila siku na kuhakikisha tunaendana na mabadiliko ya sheria kila wakati yanapotokea. Hii itatufanya tuifanye kazi yetu kwa weledi na kwa kujiamini zaidi, jengeni pia utamaduni wa kubadilishana uzoefu kila wakati hasa mnapokutana na changamoto miongoni mwenu. Hatua hii itawapa wepesi wa kutimiza majukumu yenu ya kila siku,” alisisitiza Mhe.Chitanda.

Pamoja na mambo mengine, kikao hicho kilipitia na kujadili mabadiliko ya Sheria mbalimbali ambazo ni Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura Na. 329, Sheria ya Mtoto Sura Na. 13 na nyingine zinazohusiana na uendeshaji wa mashauri.

 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Same, Mhe. Chrisanta Chitanda akisisitiza jambo wakati wa majadiliano ya kujadili mabadiliko ya sheria mbalimbali ambazo zimefanyiwa marekebisho hivi karibuni.

Katika picha ni sehemu ya Mahakimu Wakazi wa Mahakama Wilaya ya Same wakiendelea na majadiliano katika kikao hicho kilichofanyika tarehe 09 Mei, 2025.

 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Gonja, Mhe.Nassoro Nkumulwa (aliyesimama)  akichangia hoja wakati wa majadiliano hayo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




WATUMISHI KIGOMA WASISITIZWA KUDUMISHA UTAMADUNI WA KUFANYA MAZOEZI

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile kwa nyakati tofauti ameendelea kusitiza utamaduni wa watumishi kufanya mazoezi kwani yanasaidia kuimarisha afya za watumishi kuwa bora zaidi wakati wote na kuepuka magonjwa yasiyoambukizwa.

Rai hiyo ilitolewa hivi karibuni katika kikao kilichofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita,  na iliungwa mkono na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza ambaye alipendekeza utamaduni wa mazoezi  uzifikie Mahakama mbalimbali za Wilaya na Mwanzo zilizopo katika Kanda hiyo.  

Mhe. Rwizile ambaye ni muasisi wa mazoezi katika Kanda ya Kigoma, aliongeza kuwa  mazoezi hayo ambayo hufanyika siku Jumatano na Ijumaa licha ya kuimarisha afya za watumishi mazoezi hayo pia ni sehemu ya kuwaweka pamoja watumishi na kuongeza ushirikiano katika majukumu mbalimbali ya kuwahudumia wateja wa Mahakama.

“Niwaombe hata wale wasioweza kufika eneo la mazoezi kwa muda uliopangwa katika makao makuu yetu ya Kanda mjitahidi kutenga muda wenu mdogo majumbani kwenu kwa ajili ya mazoezi ya kuimarisha miili yenu,” alisisitiza Jaji Rwizile.

Kwa upande wake, Mlezi wa mazoezi wa Kanda hiyo, Mhe. Projestus Kahyoza alisema kuwa, mazoezi ni muhimu sana kama ilivyo chakula cha kila siku kwa mwanadamu, hivyo aliwataka watumishi kuona umuhimu wake ili kuiweka miili yao katika hali ya kukabiliana na changamoto za kiafya zinazoweza kujitokeza katika miaka ya uzee. 

Mhe. Kahyoza aliongeza kwa kubainisha kuwa, mazoezi ni tiba kubwa ya magonjwa mbalimbali na kuondoa magonjwa nyemelezi katika mwili wa binadamu.

Pamoja na mazoezi, Mhe. Kahyoza alisisitiza pia juu ya umuhimu kwa watumishi kuzingatia ulaji unaozingatia taratibu za kiafya ili kulinda afya za miili yao kwa ujumla. 

Jaji Mafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akifanya mazoezi hivi karibuni  katika eneo la juu la jengo la Mahakama hiyo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (wa kwanza kulia mstari wa nyuma) akishiriki mazoezi pamoja na watumishi wengine wa Kanda hiyo.

 Watumishi wa Mahakama Kuu Kigoma wakifanya mazoezi kuimarisha afya zao ili kuwa imara wakati wote wa kutoa huduma kwa wananchi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Mhe. Aristida Tarimo akijumuika na watumishi wa Mahakama Kuu Kigoma kufanya mazoezi eneo la juu la jengo la Mahakama hiyo.

Jaji Mafawidhi wa Mahakama Kuu Kigoma Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa kwanza kushoto mstari wa kwanza) akiwaongoza sehemu ya watumishi wengine wa Kanda hiyo kufanya mazoezi katika eneo la juu la jengo la Mahakama hiyo. 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




WANAFUNZI SHULE YA SEKONDARI MLOLE WATEMBELEA MAHAKAMA KUU KIGOMA

  • Wapata fursa ya kujifunza masuala mbalimbali ya kimahakama ikiwemo taratibu za usikilizwaji mashauri

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma imeendelea kuwa karibu na umma katika utoaji elimu ambapo hivi karibuni wanafunzi 23 wa kidato cha nne kutoka Shule ya Sekondari Mlole walipata fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ya kimahakama ikiwemo changamoto zinazoikabili Mahakama katika usikilizwaji wa mashauri na utoaji hukumu.

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola aliwaeleza wanafunzi hao juu ya jukumu kuu la Mhimili wa Mahakama ambapo alisema, “Mahakama ina kazi ya kuzikiliza kesi, na kutoa maamuzi juu ya masuala mbalimbali ya kisheria yanayofikishwa mbele yake.”

Pamoja na hayo, Mhe. Msola aliwaeleza wanafunzi hao kuwa, changamoto zinazoikabili Mahakama ni pamoja na uelewa mdogo wa sheria kwa wadau wa Mahakama, ushahidi hafifu unaoletwa mahakamani, ukosefu wa uwakilishi wa kisheria kwa wananchi wengi kutokana na kushindwa kumudu gharama za Mawakili wa Kujitegemea.

Aidha, aliwadokeza wanafunzi hao kwamba wao ni taifa la kesho hivyo wamefanya vema kufika mahakamani kufahamu sheria na taratibu mbalimbali ili wakawe wajumbe wazuri katika jamii ya wanafunzi na kupata utambuzi wa masuala mengi waliyojifunza.

Akijibu swali la mwanafunzi, Bw. Boid Noah aliyeuliza kuhusu wajibu wa Mahakama kwa wadaawa, Mhe. Msola alisema kuwa, Mahakama pamoja kazi kubwa ya kusikiliza mashauri na kutoa uamuzi inao pia wajibu wa kuwaongoza wadaawa katika usikilizwaji wa mashauri yao kwa mjibu wa sheria za uendeshaji wa mashauri husika ili kila upande upate haki ya kusikilizwa na baadaye maamuzi yanayozingatia misingi ya sheria kutolewa.

Kwa upande wake, Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo, Mhe. Victor Kagina aliwaasa wanafunzi hao kuendelea kusoma kwa bidii ili baadae baadhi yao au wote wawe wanasheria watakaozisaidia jamii zao katika masuala mbalimbali ya kisheria.

Pamoja na nasaha hizo kwa wanafunzi hao, Mhe. Kagina aliwashauri wawe mifano mizuri kwa jamii zao kwa kuishi kwa kufuata taratibu na sheria pamoja na kuwa na maadili kwa watu wanaowazunguka hususani walimu wao, wanafunzi wenzao, wazazi na walezi wao ili pia waje kuwa wazazi na viongozi wazuri hapo mbeleni. 

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole iliyopo mkoani Kigoma wakimsikiliza kwa makini Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Valerian Msola (hayupo katika picha) alipokuwa akiwafundisha wanafunzi hao waliotembelea Mahakakama hiyo hivi karibuni. 

Msaidizi wa Sheria Jaji wa Mahakama Kuu Kigoma Mhe. Valerian Msola akisisitiza  jambo kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole waliofika Mahakama Kuu Kigoma kwa lengo la kujifunza juu ya shughuli za Mahakama na changamoto zake. 

Msaidizi wa Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Valerian Msola akifafanua jambo wakati wa kutoa elimu kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole iliyopo Wilaya ya Kigoma Mjini waliofika Mahakama kuu kujifunza juu ya shughuli za Mahakama na changamoto zake. 

Picha ya pamoja ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole mara baada ya kumaliza kupata elimu juu ya shughuli za Mahakama.

 Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Victor Kagina (katikati), Msaidizi wa Sheria Jaji wa Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Valerian Msola (kushoto), na  Msaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma, Bi. Christina Mpungu (kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na   wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole (waliosimama).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)



JMAT MANYARA WAKUMBUSHANA JUU YA KANUNI ZA UANDISHI BORA WA HUKUMU

Na Christopher Msagati- Mahakama, Manyara

Wajumbe wa Chama cha Majaji na Mahakimu Nchini (JMAT) tawi la Manyara wamekumbushana juu ya taratibu na kanuni za uandishi bora wa Hukumu.

Akifungua mkutano huo, Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama hicho kwa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara katika mafunzo yaliyoambatana na Mkutano wa Chama hicho uliofanyika tarehe 9 Mai, 2025 katika Ukumbi wa Wazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.

Mhe. Kamuzora aliwasisitiza Majaji na Mahakimu kuzingatia miongozo mbalimbali inayotolewa katika kufanikisha kazi zao za kila siku kuanzia usikilizaji wa mashauri mpaka utoaji wa maamuzi.

“Hii miongozo na kanuni zinazotolewa, zimeandaliwa ili zituwezeshe kuzingatia taratibu zinazostahili ili kuwa na hukumu bora ambazo zitaleta tija kwa wadaawa wetu. Hivyo ni muhimu kuzingatia na kufuata kanuni hizi,” alisema Mhe. Kamuzora.

Naye, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza wakati wa kutoa Mada aliwaeleza wajumbe kuwa miongozo ya uandishi bora wa Hukumu husaidia katika kuleta uwazi ambao huonekana kwa wadaawa na uwazi huo husaidia kupunguza malalamiko au kutokuridhika katika maamuzi yanayotolewa.

“Kanuni hizi zikifuatwa vizuri, zitawasaidia nyinyi waheshimiwa Majaji na Mahakimu kuwa na uwazi miongoni mwa wadaawa wenu. Vile vile matumizi ya kanuni hizi huongeza usawa na kuwa na mfanano wa utaratibu katika uandishi wa hukumu zetu,” alisema Mhe. Kahyoza.

Akichangia mada katika mafunzo na Mkutano huo, Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Haydom Mhe. Zena Mgalula aliushukuru uongozi wa JMAT Tawi la Manyara kwa kuandaa Mkutano na Mafunzo hayo ambayo yatawapa weledi zaidi katika kuandika hukumu zenye kuzingatia kanuni na miongozo.

“kwa kweli tunashukuru uongozi wa JMAT kwa kuamua kuleta mafunzo haya Katikati ya mkutano huu kwani yatatufaa sana katika uboreshaji wa uandishi wa hukumu zetu,” alisema Mhe. Mgalula.

Katika upande mwingine wajumbe wa JMAT Tawi la Manyara walitumia mkutano huo kujadili masuala yao ambayo yatawasaidia katika kazi zao za kila siku lakini pia masuala mbalimbali ambayo yanapaswa kufanywa na JMAT katika jamii inayowazunguka.

Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha JMAT Mahakama Kuu Kanda ya Manyara akifungua mkutano huo ulioambatana na mafunzo kwa Maafisa Mahakama hao wa Kanda hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (katikati) akiwa pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara katika mkutano huo

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja Maafisa Mahakama walioshiriki mafunzo ya JMAT mkoani Manyara


Sehemu ya Maafisa Mahakama walioshiriki mafunzo ya JMAT mkoani Manyara wakifuatilia mawasilisho ya mafunzo hayo.







JAJI MKUU WA TANZANIA ASHIRIKI KUMUAGA CLEOPA DAVID MSUYA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ameungana na Viongozi wa kitaifa na Watanzania kwa ujumla kumuaga aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Mastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Marehemu Cleopa David Msuya.

Jaji Mkuu aliungana na Viongozi wengine, akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye maombolezo hayo yaliyofanyika kitaifa kwenye Viwanja vya Karimjee jijini Dar-es-Salaam.

Miongoni mwa Viongozi wengine wa kitaifa waliomuaga Marehemu Msuya ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Phillip Isdor Mpango, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.

Jaji Mkuu wa Tanzania anatarajia kuungana na Viongozi mbalimbali wa kitaifa kwenye maziko ya Marehemu Msuya yatakayofanyika kesho tarehe 13 Mei, 2025 Usangi, Wilaya ya Mwanga, Mkoa wa Kilimanjaro.

Mhe. Msuya alifariki tarehe 7 Mei, 2025 katika Hospitali ya Mzena Jijini Dar es Salaam alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa moyo.

Kufuatia kifo hicho, Rais Samia alitangaza siku saba za maombolezo hadi tarehe 13 Mei, 2025 na kuwapa pole ndugu, jamaa na Watanzania wote kwa msiba huo mzito kwa Taifa.

Msuya aliwahi kushika wadhifa wa Waziri Mkuu mara mbili. Mara ya kwanza ni kuanzia tarehe 7 Novemba, 1980 hadi tarehe 24 Februari, 1983. Mara ya pili ilikuwa ni tarehe 5 Desemba, 1994 hadi tarehe 28 Novemba, 1995, huku akishika pia wadhifa wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Baada ya kustaafu siasa aliendelea kushika nyadhifa kadhaa za uongozi katika Taasisi mbalimbali za Jamii.

Mhe. Cleopa David Msuya alizaliwa tarehe 4 Januari 1931 katika kijiji cha Chomvu, Usangi, wilayani Mwanga, mkoani Kilimanjaro. Alisoma katika Chuo Kikuu cha Makerere kuanzia mwaka 1952 hadi 1955. Baada ya hapo, alijihusisha na kazi za maendeleo ya jamii na huduma kwa Wananchi vijijini kuanzia mwaka 1956 hadi 1964.

Kuanzia mwaka 1964, Msuya alihudumu kama Katibu Mkuu katika Wizara mbalimbali: Wizara ya Maendeleo ya Jamii na Utamaduni (1964–1965), Wizara ya Ardhi, Makazi na Maendeleo ya Maji (1965–1967), Wizara ya Mambo ya Uchumi na Mipango (1967–1970) na Wizara ya Fedha (1970–1972).

Mnamo tarehe 18 Februari 1972, Mhe. Msuya aliteuliwa kuwa Waziri wa Fedha na alihudumu hadi alipohamishiwa kuwa Waziri wa Viwanda mnamo tarehe 3 Novemba 1975.

Baada ya kuhudumu kwa miaka mitano kama Waziri wa Viwanda, aliteuliwa kuwa Waziri Mkuu mnamo Novemba 1980, nafasi aliyoshikilia hadi Februari 1983. Baadaye, alirudi tena kuwa Waziri wa Fedha kutoka Februari 1983 hadi Novemba 1985.

Tarehe 6 Novemba 1985, Mhe. Msuya alipewa jukumu jipya akiwa Waziri wa Fedha, Mambo ya Uchumi na Mipango hadi Machi 1989, kisha alirudi kuwa Waziri wa Fedha tena kuanzia Machi 1989 hadi Desemba 1990, na baadaye kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara kutoka Machi 1990 hadi Desemba 1994.

Mwaka 1994, aliteuliwa tena kuwa Waziri Mkuu kwa mara ya pili, na pia kuhudumu kama Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hadi Novemba 1995.

Katika uchaguzi wa Bunge wa mwaka 1995, Mhe. Msuya alichaguliwa tena kuwa Mbunge na alihudumu hadi alipostaafu rasmi tarehe 29 Oktoba 2000.

Baada ya kustaafu, Msuya aliendelea kuwa mwanachama hai wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), na kufikia mwaka 2006 alikuwa bado ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM. Pia alikuwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Maendeleo la Kilimanjaro.

Mnamo Oktoba 23, 2019, akiwa na umri wa miaka 88, Mhe. Msuya aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Awamu ya Tano, Hayati John Pombe Magufuli kuwa Mkuu wa Chuo cha Ardhi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-wa pili kushoto-akiwa na Viongozi wengine wa kitaifa kwenye tukio la kumuaga aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Marehemu Cleopa David Msuya lililofanyika kwenye Viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam. Picha chini ni jeneza lililobeba mwili wa Mhe. Msuya.



Viongozi mbalimbali wa kitaifa wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassani wakiwa kwenye tukio hilo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-juu na chini-akisaini kwenye kitabu cha maombolezo.


Ijumaa, 9 Mei 2025

MAHAKAMA KUU TABORA YAANZA KUSIKILIZA SHAURI LA KIKATIBA KUHUSU UCHAGUZI MKUU

Na AMANI MTINANGI, Mahakama-Tabora

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora imeanza kusikiliza shauri la kikatiba lililofunguliwa na Bw. Alex Barunguza kupinga kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani kabla ya kufanyika kwa marekebisho ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Shauri hilo limeanza kusikilizwa jana tarehe 08 Mei, 2025 na jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora, Mhe. Dkt. Adam Juma Mambi na Majaji wengine katika jopo hilo ambao ni Mhe. Dkt. Zainabu Diwa Mango na Mhe. Dkt. Frank Mirindo.

Katika hatua ya awali, Mahakama imeanza kusikiliza mapingamizi yaliyowasilishwa kabla ya kuingia kwenye hoja za msingi za shauri hilo. Miongoni mwa hoja hizo ni ombi la shauri hilo kurushwa moja kwa moja na vyombo vya habari kwa lengo la kutoa fursa kwa umma kupata taarifa kwa wakati na kulinda dhana ya haki ya wazi (open justice).

Mapingamizi mengine yaliyoibuliwa ni pamoja na hoja ya kwamba Mahakama haina mamlaka ya kisheria ya kusikiliza shauri hilo, suala ambalo limeibua mjadala wa kisheria kati ya pande zinazohusika ambapo katika maamuzi madogo yamebainisha imeamuliwa kuwa Mahakama Kuu ndio iliyofanya maamuzi hivyo haiwezi kujiongoza  vingine katika maamuzi iyoyafanya.

Upande wa wajibu maombi umeongozwa na Wanasheria wa Serikali pamoja na Mawakili wa Serikali wakiwemo Bw. Mark Mulwambo, Bi. Jackline Kinyasi na Bw. Samwel Mahuma.

Mahakama imepanga kuendelea na usikilizwaji wa shauri hilo tarehe 19 Mei, 2025 ambapo itaendelea kusikiliza hoja za mapingamizi kabla ya kuingia katika kusikiliza hoja za msingi zilizowasilishwa na mlalamikaji, Bw. Barunguza. 


Jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Tabora liliposikiliziwa shauri la kikatiba lililofunguliwa na Bw. Alex Barunguza kupinga kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani jana tarehe 8 Mei, 2025.

Bw. Alex Barunguza akiwasilisha hoja zake mbele ya jopo la Majaji wanaosikiliza shauri lililowasilishwa mbele yao.


Mawakili wa Serikali waliowawakilisha wajibu maombi wakijadiliana jambo. Wa pili kulia ni 
Bw. Alex Barunguza Mtoa hoja ya kupinga kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani unaotarajiwa kufanyika Oktoba, 2025.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

MSAJILI MKUU ASHIRIKI MKUTANO WA KAMATI YA WIPO YA MAENDELEO NA MILIKI BUNIFU

  •   Aeleza mafanikio ya ushirikiano kwa kipindi cha miaka sita

Na INNOCENT KANSHA na MAGRETH KINABO - Mahakama

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya jana tarehe 8 Mei, 2025 ameungana na Nchi wanachama na Mabalozi takribani 193 kushiriki mkutano wa Kamati ya Maendeleo  ‘Miliki Binifu’ ya Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) alioshiriki kwa njia ya mkutano mtandao akiwa Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Akiuelezea ujumbe huo wa nchi wanachama wa shirika hilo wa Mabara yote Mhe. Nkya amesema Mahakama ya Tanzania imenufaika kwa kiwango kikubwa kutokana na kuwa sehemu ya shirika hilo la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) amebainisha kwamba, kupitia mashirikiano hayo,imewezesha kuwaongezea uelewa mkubwa wa masuala ya Miliki Bunifu kwa Maafisa Mahakama na kuongeza njia za kutatua migogoro inayotokana na kazi za miliki bunifu.

Aidha, Mhe. Nkya ametaja mafanikio mengine ni kutoa mafunzo kwa Maafisa Mahakama watapatao takribani 1,200 yaliyotokana programu ya Shirika hilo ya kubadilishana uzoefu.

“Takribani Maafisa Mahakama 404 walifanikiwa kushiriki mafunzo kwa njia ya masafa na kufuzu mafunzo ya sheria za haki bunifu na zaidi ya Maafisa 300 walishiriki makongomano ya Miliki Bunifu  kupitia Shirika hilo na kuwajenga uelewa mpana wa namna ya kuzitekeleza sheria zinazohusu  masuala ya Miliki Bunifu,” amesisitiza Msajili Mkuu.

Mafanikio mengine Mahakama ya Tanzania, iliyoyapata ni kwamba Majaji na Mahakimu   80  wakiwemo Majaji wa Mahakama ya Rufani, walipata walishiriki warsha za miliki bunifu kwa nyakati tofauti, ambapo Majaji hao hutoa maamuzi katika Mahakama ya ngazi ya mwisho ya utoaji wa haki nchini Tanzania.

Aidha, Mhe. Nkya amesema, kupitia ushiriki wa Tanzania Mahakama imeendelea kuwa mchangiaji mkubwa duniani katika utoaji wa maamuzi kuhusu miliki bunifu. Kuanzia mwaka 2019 jumla ya Majaji wapato 76 wamekuwa wakishiriki kwenye mkutano wa mwaka wa jukwaa la Majaji wa Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) ili kujiongezea uelewa na uzoefu kutoka kwa mamlaka zingine zinazotatua migogoro ya miliki bunifu.

Mbali na mafunzo ya mara kwa mara ya miliki bunifu, Mhe. Nkya amesema, ushirikiano umeisaidia Mahakama ya Tanzania kuandaa   miongozo ya kufundishia, mfano Mahakama imeandaa machapisho maalum ya kuendeshea mafunzo, kuandaa mkusanyiko wa vitabu vya maamuzi ya mashauri yahusuyo miliki bunifu, Vitabu Miongozo ambavyo vipo kwenye hatua ya mwisho ya maandalizi.

“Nyaraka hizo muhimu zitasaidia kutoa mwongozo na hadidu rejea kwa Maafisa Mahakama na zitachangia kukuza maendeleo ya taaluma na pia kusaidia ulinganifu wa tafsiri na kupunguza maamuzi yasiyoendani na kusaidia kujiamini kwa watoa maamuzi yanayohusu miliki bunifu,” ameongeza Msajili Mkuu.

Vilevile, Mahakama ya Tanzania mnamo mwaka 2022 ilisaini makubaliano na Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) ya kutoa na kusambaza maamuzi yatokanayo na mashauri ya miliki bunifu ili kuyachapisha kwenye kanzi data ya Shiriki ijulikanayo kama (WIPO Lex). Mpaka sasa ni maamuzi 41 ya mashauri ya miliki bunifu yamekwisha chapishwa ama kupandishwa kwenye mtandao huo wa Shirika na maamuzi mengine 39 yanafanyiwa mapitio kabla ya kuzichapisha.

Mhe. Nkya amesema, eneo lingine la ushirikianao ni kukuza matumizi na taratibu za usuluhishi, kupitia utaratibu huo wa WIPO na Mahakama imewezesha Majaji na Mahakimu wapatao 245 wameshafuzu mafunzo ya usuluhishi na upatanishi kwa njia masafa na Maafisa Mahakama wengine 159 wanendelea  kusoma kozi  maalum ya usuluhishi

“Mafanikio hayo ya usuluhishi na upatanishi yamewezesha Mahakama  kusuluhisha mashauri 26 ya miliki bunifu kwa. Aidha Majaji wa Kitanzania wanane,”  wameteuliwa kuwa wasuluhishi wa WIPO  ameongeza Msajili Mkuu.

Aidha, Mhe Nkya amesema kupitia program hizo mbalimbali za kuwajengea uwezo za shirika la WIPO zimewasidia Majaji na Mahakimu kuongeza uwezo na ujuzi wa kutosha wa kutoa haki kwa weledi na ufanisi katika eneo la mashauri ya miliki bunifu.

“Majaji na Mahakimu nchi nzima kwa sasa wanasikiliza mashauri ya miliki bunifu kwa uelewa, utaalum mkubwa na kwa kujiamini, hivyo kuchangia ufanisi na mashauri kuamriwa kwa wakati na kuondoa migongano katika kushughulikia migogoro ya miliki bunifu,” ameongeza Msajili Mkuu.

Vilevile, Mhe. Nkya amesema, ushirikiano huo umechangia kukuza ajenda ya maendeleo ya Taifa, kwani Mahakama yenye uwezo wa kutatua migogoro ya miliki bunifu kwa uthabiti na kwa kuzingatia sheria kunakuza ustawi na kuongeza imani kwa wananchi dhidi ya mfumo wa utoaji haki.

“Kwa kufanya hivyo inachangia uvumbuzi, kulinda ubunifu na kuhimiza uwekezaji wa ndani na wa nje ya nchi. Kuna nyakati miliki bunifu ilionekana kama masuala ya kiufundi na kutoyatilia mkazo, lakini kwa sasa yanatambulika kama nguzo ya kimkakati katika mageuzi ya kiuchumi nchini Tanzania,” amesema Mhe. Nkya. 

Kwa upande mwingine, kuhusu majadiliano ya nchi wanachama ilielezwa kuwa  kikao hicho kina malengo mbalimbali,  ikiwemo kujadiliana masuala ya maendeleo ya Nchi Wanachama, kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya Miliki Bunifu (IP), kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya nchi uanachama,  kuangalia maamuzi  yanayotolewa kuhusu suala hilo na kuendeleza program ya utoaji  elimu  kwa ajili ya kujengeana uwezo wa  kwenye  elimu na ujuzi juu Milki Bunifu

Katika mkutano huo, wa siku tano mambo mengine yaliyojadiliwa ni kuendana sambamba na mabadiliko ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kushughulikia mashauri yanayuhusu Miliki Bunifu kupitia uzoefu wa nchi  mfano; China, Ujerumani, India na nyinginezo. Pia kuangalia maamuzi ya Mahakama ya Juu nchini China (Supreme Court) na uzoefu wa Mahakama ya Juu ya Latvia.

Halikadhalika kutoa masaada kwa Majaji wanaoshughulikia mashauri ya IP, kutoa mwuongozo kwa Mabaraza ya Usuluhishi wa Migogoro ya Viwanda, Majaji wapya waeleweshe juu ya   masuala ya Milki Bunifu kutoka kwa wazoefu wa jambo hilo, kuangalia mikataba inayohusu Milki Bunifu  ikiwemo utoaji wa mafunzo kwa njia ya masafa.

Mambo mengine yaliyojadiliwa ni  kuangalia masuala ya Haki Miliki ya Bunifu  ya mtu, (Copy Rights), mizozo ya utumiaji  wa chapa za miliki ya mtu mwingine, mashauri yanayohusu mali za viwanda, utangazaji haramu wa matangazo ya kibiashara,  program (software), alama ya biashara na filamu(video), ikiwa ni hatua ya kuhakikisha utoaji wa haki za Milki Bunifu   unafanyika kwa viwango vinavyotakiwa.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya jana tarehe 8 Mei, 2025 ameungana na Nchi wanachama na Mabalozi takribani 193 kushiriki mkutano wa Kamati ya Maendeleo  ‘Miliki Binifu’ ya Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) kwa njia ya mkutano mtandao akiwa Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya(kushoto) jana tarehe 8 Mei, 2025 ameungana na Nchi wanachama na Mabalozi takribani 193 kushiriki mkutano wa Kamati ya Maendeleo  ‘Miliki Binifu’ ya Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) uliofanyika kwa njia ya mkutano mtandao akiwa Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.Kulia ni Mratibu  wa Shughuli za  WIPO Mahakama ya Tanzania.

Moja ya kazi zilizoandaliwa na Mratibu  wa Shughuli za  WIPO Mahakama ya Tanzania, Mhe.Upendo Ngitiri kwenye Mkutano huo.




  
Washiriki wengine wa Kamati hiyo.

Sehemu ya Mawasilisho mbalimbali kwenye mkutano huo


                    Sehemu ya Mawasilisho mbalimbali kwenye mkutano huo
     


(PICHA NA INNOCENT KANSHA- Mahakama)


Alhamisi, 8 Mei 2025

MAAGIZO MUHIMU MATANO YA JAJI MKUU KWA VIONGOZI WAPYA JMAT

  • Awataka kubaini maeneo yenye jiografia ngumu
  • JMAT watumie fursa uwekezaji kwenye teknolojia
  • Awataka kujiandaa na uchaguzi mkuu

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Viongozi wapya wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania-JMAT jana tarehe 7 Mei, 2025 walimtembelea Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na kufanya mazungumzo naye kwenye mambo mbalimbali yanayolenga kuimarisha utendaji kazi katika muktadha mzima wa utoaji haki kwa Wananchi.

Wakiongozwa na Rais wa JMAT, ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Elimo Massawe, Viongozi hao walifika katika ofisini ya Jaji Mkuu iliyopo kwenye Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma majira ya saa 3.00 asubuhi.

Viongozi wengine walioambatana na Mhe. Massawe, ni Katibu wa JMAT, Mhe. James Mniko, Katibu Msaidizi, Mhe. Teddy Mlimba, Mtunza Hazina, Mhe. Devotha Kasebele na Katibu Mwenezi wa Chama hicho, Mhe. Fratern Temba.

Akijibu baadhi ya maombi yaliyowasilishwa kwake na Viongozi hao, Jaji Mkuu aliahidi kufanyia kazi changamoto zinazowakabili Wanachama wa JMAT, ikiwemo kuziainisha vizuri na kuziwasilisha kwa wenzake ndani ya Mahakama ya Tanzania ili kuona njia bora ya kuzitatua kwa pamoja.

Aliwaelekeza Viongozi hao kubaini maeneo yenye jiografia ngumu ambayo Wanachama wa JMAT wanahudumu katika maeneo mbalimbali nchini na kuzungumza na uongozi namna ya kukabiliana na changamoto hiyo.

‘Hili eneo la mazingira magumu ya kazi lina changamoto, tuanze kubaini maeneo gani ambayo yenye jeografia ngumu. Vile vile tusome ile ripoti ya Repoa, nadhani wamejalibu kuelezea mazingira ambayo Watumishi wanakabiliana nayo,’ alisema.

Mhe. Prof. Juma aliitaka JMAT kutumia fursa ya teknolojia na jukwa la masomo ya masafa-e-learning platform ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto-IJA na kuomba kusanifu masomo mengine ambayo wanaweza kupata shahada kupitia njia hiyo, hasa kwenye maeneo mapya.

‘Tusisome sana maeneo ambayo hayaingiliani na teknolojia kwa sababu huko ndiko Dunia inakokwenda. Hili ni eneo ambalo lina potential kubwa sana,’ Jaji Mkuu alisema.

Mhe. Prof. Juma pia aliwataka Wanachama wa JMAT kushiriki kikamilifu katika Mpango Mkakati wa Tatu wa Miaka Mitano wa Mahakama ya Tanzania na kutoa mchango wao kwa kuzingatia kuwa wapo katika kila sehemu kama kupanga bajeti na uongozi.

‘Sijui mtafanyaje ili wanapopanga watilie maanani masuala ya JMAT. Mfano, sasa hivi tunazungumzia Mpango Mkakati wa Tatu wa Miaka Mitano wa Maboresho ya Mahakama. Nyinyi mnamchango wa aina gani katika mpango huo…

‘Mipango ndiyo inayozaa bajeti, mkisubiri mpango uliotayarishwa bila kuweka maslahi ya JMAT mtakuwa nje ya bajeti wakati wa utekelezaji. Sasa hivi nadhani wapo Arusha, bila shaka mna taarifa, masuala yenu yataingizwaje. Unaweza kukuta mambo mengi ambayo mmeyaibua yanaweza kuwa ni sehemu ya mpango,’ alisema.

Jaji Mkuu aliwahimiza pia kutengeneza hoja bila kutumia nguvu na mvutano zitakazosaidia uongozi kuzungumza na Mihimili mingine ili kutafuta namna ya kutatua changamoto zinazowakabili.

Kadhalika, Mhe. Prof. Juma aliitaka JMAT kujiandaa na Uchaguzi Mkuu kwa kuanza mafunzo kwa Mahakimu namna ya kushughulikia migogoro ya uchaguzi itakayoletwa mahakamani.

‘Jengeni hoja kwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ili awatengee maeneo ya kufanya mafunzo. Mkifanya hivyo nyinyi wenyewe kama maofisa wa Mahakama inakuwa na manufaa na uhuru zaidi,’ alisema.

Awali, akizungumza kwa niaba ya Viongozi wenzake, Rais wa JMAT alimpongeza Jaji Mkuu kwa kazi nzuri anazozifanya za kuwahudumia Watanzania na kwa ushirikiano ambao anawapa wakati wa kutekeleza majukumu yao.

Mhe. Massawe alimwomba Jaji Mkuu kuwasaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili Wanachama wa JMAT katika maeneo mbalimbali nchini.

Rais wa JMAT pia alimuomba Jaji Mkuu kuwa ili kuwezesha ufanisi, sheria zilizofanyiwa mapitio mwaka 2023 zipatikane kwenye maktaba ya Mahakama Mtandao ili Majaji na Mahakimu wapate urahisi wa rejea.

Kadhalika, aliomba maboresho ya bima ya afya ili waweze kupata huduma kwa upana zaidi kuliko ilivyo hivi sasa.

Ombi jingine lilihusu JMAT kuendelea kupewa fursa ya kuratibu mafunzo kwa Wanachama wake, kwani ni jukwaa zuri zaidi kwa Majaji na Mahakimu kuzungumza kitaaluma. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-juu na chini-akizungumza na Viongozi wapya wa Chama cha Majaji na Mahakimu walipomtembelea ofisini kwake jana tarehe 7 Mei, 2025 jijini Dodoma.


Rais wa JMAT, ambaye pia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Elimo Massawe, akizungumza na Jaji Mkuu baada ya uongozi mpya kumtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.

Viongozi wapya wa JMAT-juu na chini-wakichukua kumbukumbu mbalimbali walipokuwa wanazungumza na Jaji Mkuu-hayupo kwenye picha. Picha chini wa kwanza kulia ni Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi.


Kikao kinaendelea-juu-huku Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi-picha chini-akifuatilia kwa karibu kilichokuwa kinajiri.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-wa tatu kushoto-akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wapya wa JMAT. Picha chini akiongea na Viongozi hao baada ya kumaliza kikao hicho.