- Msajili Mahakama ya Rufani awataka kuzingatia maadili, viapo vyao
- Awakumbusha kazi ya uhakimu ni nyeti, haiwezi kufanywa na mtu yoyote
Na FAUSTINE KAPAMA na
HALIMA MNETE-MAHAKAMA, Dodoma
Mafunzo elekezi ya siku
tisa yaliyoandaliwa na Mahakama ya Tanzania, kwa kushirikiana na Chuo cha
Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], kwa Mahakimu Wakazi wapya 89 yamehitimishwa
leo tarehe 17 Octoba, 2025.
Msajili wa Mahakama ya
Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert amehitimisha mafunzo hayo yaliyokuwa
yanafanyika kwenye moja ya Kumbi za Mikutano zilizopo katika jengo la Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Akizungumza kwenye hafla
hiyo, Mhe. Herbert amewaeleza Mahakimu hao walioapishwa na Jaji Mkuu wa
Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, hivi karibuni kuwa anaamini mafunzo
hayo yaliyoanza kutolewa tarehe 7 Octoba, 2025 yamekuwa ya mafanikio makubwa
kwao.
‘Nimatumaini yangu kwamba
katika siku tisa za mafunzo mmeweza kupata uelewa mkubwa wa viwango vya kitaaluma
na kimaadili kwa nafasi mnayoenda kufanyia kazi. Napenda kuwakumbusha na
kuwasisitiza kuzingatia yale yote mliyofundishwa, iwe kwa upande wa weledi wa
kitaaluma au kwa upande wa unyoofu wa kimaadili,’ amesema.
Msajili wa Mahakama ya Rufani
amewaeleza washiriki hao kuwa pande hizo mbili zina umuhimu kwa Hakimu kwani
zinategemeana. Amesema kuwa Mahakama bora inajengwa na Maofisa wa Mahakama
wenye weledi wa kutosha na maadili ya kiwango cha juu.
Mhe. Herbert amesema kuwa
matendo ya kila mmoja wao yanaweza kuinua au kuharibu taswira ya Mahakama nzima
kwa jamii ambao ndiyo wanailenga katika kuihudumia. Amewasihi kuzingatia
mafunzo waliyopatiwa na kuishi kwa viapo vyao.
Amewakumbusha washiriki
wa mafunzo hayo kuwa kazi ya uhakimu ni nyeti, muhimu na ya kipekee na kwamba haipo
sawa na kazi nyingine yoyote. Huku akinukuu kutoka kwenye maandiko matakatifu,
Msajili wa Mahakama ya Rufani amewaeleza Mahakimu hao kuwa kazi ya uhakimu
inatoka kwa Mwenyezi Mungu.
‘Hivyo nyinyi Mahakimu mmekasimiwa
mamlaka haya na Mwenyezi Mungu ili mtende kazi yake ya kutoa uamuzi mkiwa hapa duniani,
huku mkijua uamuzi wenu utapimwa na Mwenyezi Mungu. Kazi hii ya uhakimu
muichukulie kwa uzito mkubwa, umakini na uadilifu wa hali ya juu,’ amesema.
Mhe. Herbert alimnukuu
pia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ambaye aliwahi kusema kwamba
kazi ya uhakimu au ujaji siyo kazi ambayo inaweza kufanywa na mtu yoyote, ni
kazi ambayo inahitaji umakini, uadilifu na kuwa na fikra tofauti na watu
wengine.
Ametumia fursa hiyo kutoa
shukrani kwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwa kutoa kibali cha kufanyika na
kwa yeye mwenyewe kufungua mafunzo hayo.
Kadhalika, Mhe. Herbert
ametoa shukrani kwa IJA, chini ya Uongozi wa Mkuu wa Chuo Jaji wa Mahakama ya
Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, kwa kuandaa na kuratibu mafunzo hayo kuanzia
yalipoanza hadi kufikia tamati.
Awali akizungumza katika
hafla hiyo, Mkurugenzi wa Mafunzo wa IJA, Mhe. Dkt. Patricia Kisinda amewashukuru
Mahakimu hao kwa kushiriki kikamilifu kwenye mafunzo hayo ya wiki mbili.
‘Sisi kama IJA kwa
kushirikiana na Mahakama ya Tanzania tunajisikia fahari kuwa mafunzo haya yameleta ufahamu na maarifa ya kutosha
kwa washiriki na imekuwa wakati mzuri kwao kukaa Dodoma na kufurahia mazingira
yake,’ alisema.
Mhe. Dkt. Kisinda aliwapongeza wawezeshaji wa mafunzo hayo ambapo jumla ya mada 27 ziliwasilishwa. Amewaeleza washiriki kuwa watakubaliana na yeye kwamba maarifa waliyopata ni matokeo ya ujuzi na uzoefu wa kina ambao wawezeshaji wameupata wakati wa utumishi wao mahakamani.
Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo hayo [juu na chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.
Sehemu nyingine ya tatu ya washiriki wa mafunzo hayo [juu na picha mbili chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri.