Alhamisi, 5 Oktoba 2017

MAHAKAMA KANDA YA TABORA NA USHUGHULIKIAJI WA NIDHAMU YA WATUMISHI NA MALALAMIKO YA WANANCHI


Na Mary Gwera, Tabora
Mahakama-Kanda ya Tabora yaunda Kamati za ndani za Maadili kwa kila ngazi ya Mahakama katika Kanda hiyo kushughulikia maadili na nidhamu ya Watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo.

 Hayo yalisemwa na Mtendaji, Mahakama Kuu, Kanda ya Tabora, Bw. Sumera Manoti jana katika mahojiano maalum na Mwandishi wa habari hii ambapo alisema kuwa hii imetokana na maelekezo/maazimio yaliyotolewa katika kikao cha Wasajili/Watendaji kilichofanyika mkoani Dodoma Julai, 2016.

“Kamati hizi za nidhamu ambazo zipo katika kila ngazi ya Mahakama katika mkoa huu ziliundwa tangu mwaka jana na zimesaidia kurejesha maadili kwa Watumishi wa Kanda hii kwa kiwango kikubwa,” alisema Bw. Manoti.

Alisema kuwa Kamati hizi za Maadili ndani ya Mahakama, zinaundwa na baadhi ya Watumishi wa ndani ya Mahakama ambayo ni Mhe. Jaji Mfawidhi, Naibu Msajili, Mtendaji, na baadhi ya Wakuu wengine wa vitengo ambao hukaa katika vikao na kujadili na kuwahoji Watumishi ambao wameonaka kuonesha utovu wa nidhamu.

Bw. Manoti anasema kuwa endapo mtumishi atabainika kuwa amekiuka taratibu za kazi mfano kwa kutowahudumia wateja vizuri kwa kutoa lugha chafu na kadhalika, Mtumishi huyo huketishwa mbele ya Kamati na kujieleza na hatimaye kuwajibishwa aidha kwa kupewa onyo au vinginevyo.

Anaongeza kuwa Suala la Maadili na nidhamu nzuri ya kazi katika Ofisi yoyote hupelekea utoaji wa huduma bora na nzuri inayotolewa kwa wananchi/wanufaika wa huduma husika.

Kwa upande wake Afisa Malalamiko wa Mahakama Kuu-Tabora, Bi. Aisha Abdallah anasema kuwa idadi ya malalamiko imekuwa ikipungua mwaka hadi mwaka, anasema kuwa kwa mwaka huu jumla ya malalamiko 31 kutoka katika ngazi zote za Mahakama katika mkoa huo yalipokelewa.

“Kabla ya kuanzishwa kwa Dawati la Malalamiko katika Mahakama hii kulikuwa na malalamiko mengi na hakukuwa na mfumo unaoeleweka wa pokeaji na ushughulikiaji wa malalamiko hayo, lakini kwa sasa dawati hili limesaidia na malalamiko yote 31 tuliyoyapokea yamefanyiwa kazi yote,” alisema. Bi. Aisha.

Kutokana na malalamiko mbalimbali yaliyokuwa yakitolewa na wananchi wanaotafuta huduma ya haki nchini, Mahakama ya Tanzania kupitia Muundo wake  katika Sheria Namba. 4 ya Uendeshaji wa Mahakama ya mwaka 2011 (Judicial Administration Act.No.4,2011) ilianzisha Idara maalum ya Ukaguzi na Malalamiko lengo likiwa ni kushughulikia malalamiko hayo kwa mujibu wa Taratibu na  miongozo iliowekwa, na kwa maana hiyo kila Mahakama ina Dawati maalum la kushughulikia malalamiko yanayotolewa na wananchi.
 Mtendaji, Mahakama Kuu-Kanda ya Tabora, Bw. Sumera Manoti akifafanua jambo mahojiano maalum na Mwandishi.
Wananchi wakisubiri kupata huduma- Mahakama Kuu na ya Hakimu Mkazi-Tabora.
Utunzaji sahihi wa Kumbukumbu (Mahakama Kuu-Tabora): pichani ni muonekano wa Maboksi ambayo ndani yake yamepangwa majalada ya kesi zilizoisha, majalada hayo yamepangwa kulingana na mwaka, utunzaji sahihi wa majalada ya kesi na mengineyo hurahisisha upatikanaji wa kumbukumbu na hatimaye kurahisisha kazi ya utoaji haki nchini kufanyika kwa ufasaha kutokana na kwamba hutegemea ushaidi na nyaraka ili kesi iweze kusonga mbele na hatimaye kukamilika kwa wakati.
(Picha na Mary Gwera)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni