Jumatano, 6 Desemba 2017

UJUMBE KUTOKA BENKI YA DUNIA WAISIFU MAHAKAMA KWA MABORESHO

Na Mary Gwera
Ujumbe kutoka Benki ya Dunia umeisifu Mahakama ya Tanzania kwa jitihada inazofanya katika utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama.

Hayo yalisemwa mapema Desemba 5, mara baada ya Ujumbe huo kupokea taarifa ya Utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama ya Tanzania iliyowasilishwa na Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mradi wa Maboresho ya Mahakama (JDU) Mhe. Zahra Maruma.

Akizungumza mbele ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania, Mtaalamu Mwandamizi wa Maboresho ya Utumishi wa Umma kutoka Benki ya Dunia, Bw. Waleed Malik alisema jitihada zilizofanywa na Mahakama katika kuboresha huduma za Mahakama ni kubwa hivyo kuna haja ya kutoa taarifa kwa jamii ili ifahamu masuala mbalimbali yenye tija yanayoendelea kufanyika.

“Natoa pongezi kwa timu nzima ya Mahakama kwa jitihada za maboresho, hivyo basi maboresho haya hayana budi kutangazwa ili watu waweze kujua mambo mazuri yanayoendelea ya kuboresha huduma ya utoaji haki,” alisema Bw. Malik.

Awali akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama ya Tanzania, Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mradi wa Maboresho ya Mahakama (JDU) Mhe. Zahra Maruma alitaja baadhi ya mafanikio ya Mradi ikiwa ni pamoja na uanzishwaji wa Madawati ya kushughulikia Malalamiko katika Mahakama zote nchini, usambazaji wa simu maalum kwa ajili ya kuwezesha wananchi kuwasilisha malalamiko ikiwa ni pamoja na rushwa, utovu wa nidhamu na kadhalika.

Mhe. Maruma aliongeza kuwa  kwa upande wa ushughulikiaji wa Malalamiko Mahakama imepiga hatua kwani kwa mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya malalamiko 2195 yaliyopokelewa 2068 yalishughulikiwa ipasavyo.

“Aidha kwa mwaka wa fedha 2017/2018 mpaka kufikia Septemba, jumla ya malalamiko 670 yamepokelewa na yaliyoshughulikiwa ni 797 ukijumlisha na yaliyokuwa yamesalia kwa mwaka 2016/2017,” alibainisha Mhe. Maruma.

Alisema jitihada mbalimbali zinaendelea kufanyika zote zikilenga katika kuhakikisha kuwa huduma bora ya upatikanaji wa haki kwa wananchi inafikiwa ambapo alisema pia kwa sasa wapo katika hatua za mwisho za ununuzi wa Magari maalum ‘mobile courts’ kwa ajili ya kusikilizia kesi.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga alisema kuwa katika utekelezaji wa Mradi huo unaofadhiliwa Benki ya Dunia, Watumishi wote wa Mahakama ya Tanzania wanachangia kwa namna moja ua nyingine kuhakikisha kuwa maboresho yanapatikana.

“Kwa hatua kidogo tuliyopiga si kazi ya Watawala pekee bali ni jitihada ya kila mmoja/Mtuumishi wa Mahakama, hivyo tunafanya kazi kama timu ambapo jitihada ya kila mmoja mmoja ni fanikio la kundi zima,” alisema Bw. Kattanga.

Ujumbe huo pia ulipata wasaa wa kutembelea Mradi wa Ujenzi wa Kituo cha Mafunzo cha Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kilichojengwa eneo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kawe pamoja na Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Kigamboni.

Ujumbe wa Benki ya Dunia upo nchini kwa takribani wiki mbili lengo likiwa ni kukagua utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama.
Baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania na Ujumbe kutoka Benki ya Dunia (WB) wakimsikiliza kwa makini, Mkuu wa Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mradi wa Maboresho ya Mahakama, Mhe. Zahra Maruma (hayupo pichani) wakati akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama ya Tanzania. .

Mkuu wa Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mradi wa Maboresho ya Mahakama, Mhe. Zahra Maruma akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama ya Tanzania.
Wajumbe wakifuatilia kwa makini.
Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga akichangia jambo katika kikao hicho.
Baadhi ya Wageni kutoka Benki ya Dunia (WB) wawili walioketi upande wa kulia pamoja baadhi Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama wakimsikiliza Mtendaji Mkuu, Mahakama (hayupo pichani) pindi alipokuwa akichangia juu ya Taarifa ya
Utekelezaji wa Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama pamoja na Mpango Mkakati wa miaka mitano (2015/16-2019/2010) wa Mahakama ya Tanzania.
Ujumbe kutoka Benki ya Dunia (WB) pamoja na baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti wakiwa ndani ya Jengo jipya la Kituo cha Mafunzo cha Chuo cha Uongozi wa Mahakama -Lushoto lililopo Kisutu jijini Dar es Salaam.
Muonekano wa jengo la Mafunzo-Kisutu.
 Wakiwasili kwa ajili ya ukaguzi wa Mahakama ya Mwanzo Kawe.
Picha ya pamoja katika ya Wageni kutoka Benki ya Dunia na Baadhi ya Wajumbe wa Menejiment ya Mahakama ya Tanzania wakiwa mbele ya jengo jipya  la Mahakama ya Wilaya Kigamboni mara baada ya ukaguzi.
(Picha  na Mary Gwera)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni