Jumapili, 18 Machi 2018

WATENDAJI, NAIBU WASAJILI NA MAHAKIMU WATAKIWA KUSHIRIKIANA


Na Lydia Churi- Mahakama ya Tanzania
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali amewataka Watendaji, Naibu Wasajili na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi nchini kufanya kazi kwa kushirikiana ili kujenga imani ya wananchi kwa Mahakama na kuwapatia wananchi haki kwa wakati.

Akifunga Mkutano Maalum wa siku mbili wa Watendaji, Naibu Wasajili na Mahakimu wa Mahakama za Hakimu Mkazi jijini Arusha uliojadili namna ya kumaliza mashauri ya Mlundikano Mahakamani, Jaji Kiongozi amewaambia viongozi hao kuwa wanalo jukumu la kuhakikisha Mahakama ya Tanzania inatimiza azma yake ya kuboresha huduma zake kupitia Mpango Mkakati wake wa miaka mitano pamoja na Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama unaotekelezwa hivi sasa.
“Lazima tushirikiane kwa pamoja katika kutekeleza majukumu yetu ili Mahakama ya Tanzania isonge mbele, tufanye kazi kwa pamoja na kuacha tofauti zetu kwa kuwa kila mmoja ana umuhimu wake ndani ya Mahakama”, alisema Jaji Kiongozi.

Akizungumzia namna ya kupunguza mashauri ya muda mrefu kwenye Mahakama mbalimbali nchini, Jaji Wambali aliwaambia viongozi hao kuwa Mahakama inakusudia kuongeza idadi ya Majaji kwenye baadhi ya Kanda za Mahakama Kuu nchini zenye idadi kubwa ya mashauri ya mlundikano.
Jaji Kiongozi aliizitaja kanda za Mahakama Kuu zenye idadi kubwa ya mashauri ya mlundikano kuwa ni pamoja na kanda ya Bukoba, Dar es salaam na Njombe.

Wakati huo huo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bwn. Hussein Kattanga amewataka Viongozi hao kuhakikisha wanafanya kazi kwa bidii ili kuujenga Mhimili huo.
Aidha, Mtendaji Mkuu wa Mahakama aliwakumbusha viongozi hao dhamira ya  Mahakama kwenye maboresho ya utoaji haki kuwa ni pamoja na kuondokana na tabia ya makusudi ya uzuiaji wa haki ya msingi ya kukata rufaa kwa kuhakikisha  nakala za hukumu na mwenendo wa mashauri vinapatikana kwa wakati na bila vikwazo.

Alisema Mahakama imedhamiria kuongeza bajeti ya kanda, Mkoa na wilaya ili kutekeleza Mpango Mkakati wa Mahakama unaolenga kuongeza na kuboresha Watumishi, majengo, weledi maslahi, wadau, utawala bora na sheria na kupiga vita vitendo vinavyokiuka maadili na rushwa.
Kuhusu Mashauri, Bwn. Kattanga alisema Mahakama imedhamiria kusimamia utekelezaji wa umalizaji wa mashauri ya mlundikano katika Mahakama za Hakimu Mkazi, wilaya na Mahakama za Mwanzo hadi kufikia kutokuwa na mashauri ya aina hiyo kila mwaka wa Mahakama unapomalika Desemba ya kila mwaka.

Alisema Mahakama pia inayo dhamira ya kuimarisha Menejimenti ya mashauri tangu shauri linaposajiliwa mpaka linapomalizika pamoja na kusimamia na kusaidia kudhibiti mienendo isiyofaa ya Mawakili na Madalali wa Mahakama kama maofisa wa Mahakama.
Hivi sasa Mahakama ya Tanzania inatekeleza Mpango Mkakati wake wa miaka mitano (2015/16-2019/20) pamoja na Mradi wa Maboresho ya huduma za Mahakama ambapo kupitia Mpango Mkakati huo, Mahakama inasimamia matumizi bora ya rasilimali, upatikanaji wa haki kwa wakati na kurejesha imani ya wananchi kwa Mahakama.   

  Jaji kiongozi Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali akifunga Mkutano wa siku mbili wa Naibu Wasajli, Watendaji na Mahakimu wa Mahakama za Hakimu Mkazi uliofanyika jijini Arusha.
 Mtendaji  Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bwn. Hussein Kattanga akizungumza wakati wa Mkutano Naibu Wasajli, Watendaji na Mahakimu wa Mahakama za Hakimu Mkazi uliofanyika jijini Arusha. Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Ununuzi na Ugavi wa Mahakama ya Tanznaia, Bwn. David Kivembele. 
Naibu Wasajili, Watendaji na Mahakimu wa Mahakama za Hakimu Mkazi wakiimba wimbo wakati wa kufunga Mkutano wao jana jijini Arusha. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni