Alhamisi, 5 Aprili 2018

MAHAKAMA YA TANZANIA YAINGIA MAKUBALIANO NA SHIRIKA LA POSTA KWA AJILI YA KUSAMBAZA NAKALA ZA HUKUMU




Na Mary Gwera
MAHAKAMA ya Tanzania imeingia Mkataba na Shirika la Posta Tanzania kutoa huduma za usafirishaji wa nakala za hukumu, barua na nyaraka muhimu za Mahakama.

Mkataba huo ulisainiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta mapema Aprili 05 katika Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama Mahakama ya Rufani-Dar es Salaam.

Mkataba huu chini ya huduma mpya ya Posta mlangoni (The post at your doorstep) iliyoanzishwa na Shirika la Posta hivi karibuni, utalipa jukumu la kukusanya na kusafirisha/kusambaza nakala za hukumu na nyaraka mbalimbali za Mahakama na kuzifikisha kwa wahusika kulingana na anwani zao na mahali walipo (Anwani za makazi).

Akizungumza kabla ya utiani saini wa mkataba huo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Bw. Hussein Kattanga amesema kuwa hatua hii ni mwendelezo wa maboresho mbalimbali yanayoendelea kufanyika ili kuwafikia wananchi.

Aidha; Mtendaji Mkuu amelitaka Shirika hilo kutekeleza makubaliano hayo kwa ufanisi, ikiwa ni pamoja na kusambaza nakala za hukumu na nyaraka nyingine kwa wahusika na kwa wakati.

“Sitarajii kuona wananchi wanapanga foleni Mahakamani kutafuta hukumu zao na nyaraka nyingine, nina imani kuwa Posta mtafanya kazi ya kukusanya na kusambaza nyaraka hizo kwa wananchi ipasavyo,” alisema Mtendaji Mkuu.

Naye  Msajili Mkuu-Mahakama ya Tanzania, Mhe. Katarina Revocati ameeleza kufurahishwa kwake na hatua ya utiaji saini wa Mkataba huo kwani utasaidia kufikia ndoto ya Mahakama ya muda mrefu ya kuwafikia wananchi kwa karibu zaidi.

“Naomba kusema kuwa, nimefurahishwa sana na hatua hii , kwani ni ndoto ya Mahakama ya muda mrefu, vilevile hatua hii itarahisisha utekelezaji wa maagizo ya Mhe. Jaji Mkuu ya kutoa nakala za hukumu bure kwa zitawafikia wananchi popote watakapokuwa,” alisema Mhe. Revocati.

Kwa upande wake Posta Masta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Hassan Mwang’ombe alisema alimuhakikishia Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuwa watafanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa.

“Kusainiwa kwa Mkataba huu kutawezesha pia kuongeza kasi ya usambazaji wa barua za kawaida za Mahakama kuwafikia walengwa mapema zaidi kwani zitachukuliwa  Mahakamani na Maofisa wa Posta na kupelekwa moja kwa moja kwa wahusika/mhusika,” alisema Bw. Mwang’ombe.

Vilevile Mkuu huyo alitoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa Maofisa wa Posta hususani kwa kuandika anwani za makazi pamoja na postikodi.

Hafla hiyo fupi ilihudhuriwa na baadhi ya Maafisa Waandamizi kutoka Mahakama ya Tanzania pamoja na Shirika la Posta Tanzania.
 Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga (aliyeketi katikati) akiongea jambo katika hafla fupi ya utiani saini ya mkataba wa utoaji huduma ya usambazaji wa nyaraka mbalimbali za Mahakama huduma ambayo itatolewa na Shirika la Posta Tanzania.

 Msajili Mkuu- Mahakama ya Tanzania, Mhe. Katarina Revocati akiongea jambo katika hafla hiyo. (Waliosimama) wa kwanza kulia ni Mtendaji-Mahakama ya Rufani, Bw. Sollanus Nyimbi, wa pili kulia ni Msajili-Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ilvin Mugeta, wa tatu ni Mtendaji-Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha na Maofisa kutoka Shirika la Posta Tanzania.

 Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Hassan Mwang’ombe akiongea jambo kabla ya kutiliana saini Mkataba kati la Shirika la Posta na Mahakama ya Tanzania.

 Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga (katikati) akitia saini Mkataba huo, anayeshuhudia kulia ni Msajili Mkuu- Mahakama ya Tanzania, Mhe. Katarina Revocati aliyeketi kushoto ni Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Hassan Mwang’ombe, wanaoshuhudia (waliosimama) ni baadhi ya Viongozi/Maafisa kutoka Mahakama na Shirika la Posta.

 Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Hassan Mwang’ombe akitia saini Mkataba huo.

 Mwanasheria wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Peace Mpango akitia saini Mkataba huo aliyeketi kushoto ni Mwanasheria kutoka Shirika la Posta, waoshuhudia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama kulia pamoja na Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta.

 Wakikabidhiana Mikataba hiyo kwa nyuso za furaha mara baada ya kuhitimisha zoezi la utiaji saini. Kulia ni Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga na kushoto ni Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Hassan Mwang’ombe.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni