Jumatatu, 17 Desemba 2018

BONANZA LA CHUO: MCHUANO MKALI IJA, JESHI LA POLISI LUSHOTO

Na Ibrahim Mdachi-IJA
Katika kusherehekea sikukuu ya Uhuru, Chuo Cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kimefanya Bonanza lililowashirikisha watumishi Chuo hicho pamoja na Taasisi mbalimbali kwa lengo la kuleta hamasa ya kufanya mazoezi ili kuimarisha afya ya mwili na akili.

Bonanza hilo lililoongozwa na Mkuu wa Idara ya Mafunzo ya Kimahakama na Sheria Bi. Mwanabaraka Mnyukwa lilianza asubuhi kwa mchaka mchaka (jogging) na kufuatiwa na mazoezi ya viungo ambapo kulikuwa na michuano mikali katika michezo mbalimbali iliyoungurimishwa katika viwanja vya Chuoni hapo.

Akifungua mashindano hayo, Mwanabaraka alisema kuwa mwaka huu mashindano yameboreshwa na kutoa fursa kwa taasisi nyingine kualikwa kushiriki ikiwemo Jeshi la Polisi Lushoto, Kampuni ya simu ya TTCL, Benki ya NMB, na Halmashauri ya mji Lushoto.
“Mwaka huu bonanza limeboreshwa zaidi ndio maana tumeamua kuwashirikisha watumishi wenzetu kutoka nje ya chuo, wanachuo na hata wanajumuiya inayotuzunguka” alisema Mwanabaraka.
 
Alisema Bonanza hili limetoa fursa adimu kwa Watumishi, Wanachuo na wanajumuiya wanaokizunguka Chuo kukutana na kushiriki kwa pamoja katika michezo.
Aidha, katika mashindano hayo, Washiriki kutoka polisi Lushoto walitoa ushindani mkali dhidi ya wenyeji wao IJA katika michezo mbalimbali iliyohudhurishwa viungani hapo ambapo katika michezo wa kuvuta Kamba wanaume, timu ya IJA iliibuka kidedea dhidi ya Polisi kwa seti 2 – 1, katika mchezo wa kukimbiza kuku IJA na Polisi walitoka suluhu kwa jinsia zote mbili kwa kila moja kujipatia kuku mmoja mmoja.

Katika mchezo wa riadha Bi. Catherine Macha wa IJA alinyakua nafasi ya kwanza na nafasi ya pili kuchukuliwa na Bi. Ansila Isidory wa Polisi Lushoto. Kwa wanaume Bw. Daniel Lussa wa IJA alishika nafasi ya pili nyuma ya Bw. John Gaudence wa Polisi.
 
Aliyetia fora katika Bonanza hilo ni Bw. Noel Njau wa IJA aliyewashangaza watazamaji kwa kumaliza sahani kubwa ya pilau huku akitafuna pilipili mbichi kwa muda wa dakika 2 huku Bw. George Barnoba akishika nafasi ya pili wote kutoka IJA.

Michezo mingine ilikuwa kama ifuatavyo; shindano la kukuna nazi ushindi ulinyakuliwa na Bi. Martha Bukuku wa IJA akifuatiwa na Bw. Masoud Juma wa Polisi Lushoto, shindano la kunywa lita 1.5 ya soda Bw. Masoud Juma wa Polisi Lushoto alinyakua ubingwa na mchezo wa mpira wa meza (pool table) Polisi Lushoto walinyakua ushindi kwa kushinda seti 2 – 1 ya IJA, mpira wa Pete (netball), mpira wa wavu (Volleyball), mpira wa kikapu (basketball) .
  Bonanza: Bw. Noel Njau wa IJA akiwa kwenye shindano la kula sahani kubwa ya chakula aina ya pilau pamoja na kutafuna pilipili mbichi kwa dakika 2. Bwn. Njau aliibuka mshindi kwenye mashindano hayo.

  Bonanza: Pichani Watumishi wakiendelea kukimbia huku wakiwa wamevaa magunia.


Bonanza: Timu ya Polisi Lushoto wakiwa wameibuka kidedea kwenye mchezo wa kufukuza kuku.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni