Jumamosi, 15 Desemba 2018

MAWAKILI WAPYA 909 WAKUBALIWA NA KUAPISHWA NA JAJI MKUU WA TANZANIA

Na Lydia Churi-Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Mawakili nchini kuzingatia kanuni mpya za maadili na kutoa huduma bora za uwakili ili waendelee kuaminika na kuaminiwa na wananchi.
Akizungumza kwenye sherehe za kuwakubali na kuwaapisha Mawakili, leo jijini Dar es salaam, Jaji Mkuu amesema kanuni za maadili, nidhamu  na tabia njema za Mawakili tayari zimeshaanza kutumika mwaka huu. Lengo likiwa ni kuwasaidia Mawakili waendelee kuaminiwa na kuaminika, na kubaki ndani ya misingi ya maadili na huduma bora za uwakili.
Kwa mujibu wa Jaji Mkuu, kanuni hizo zinawataka Mawakili wote kuwa waadilifu wakweli, na wanaofanya kazi kwa kuheshimu misingi ya haki. Aliongeza kuwa endapo wakili yeyote atavunja kanuni atachukuliwa hatua za kinidhamu ikiwa ni pamoja na kusimamishwa kufanya kazi ya Uwakili.
Akifafanua kanuni hizo Jaji Mkuu amesema baadhi ya makosa yanayoweza kusababisha Wakili Wakili kuchukuliwa  hatua za kinidhamu ni pamoja na kushindwa kumpa mteja wake taarifa za masuala aliyoajiriwa kufanya, kushindwa kutoa taarifa kwa mteja wake pale anapohitaji, na kushindwa kutoa huduma kwa sababu ya ulevi au matumizi ya dawa za kulevya au pombe na kushindwa kuchukua hatua muhimu za kimahakama kwa niaba ya mteja wake na hatimaye shauri kuchelewa mahakamani.   
Alisema ingawa elimu ya mawakili kutoka shule za msingi, sekondari, vyuo na hata elimu ya sheria kwa vitendo imejengwa katika misingi na maudhui ya karne ya 20 lakini Mawakili hao hawana budi  kutoa huduma zinazokidhi ushindani na matarajio ya huduma za karne ya 21.
Akizungumzia umuhimu wa kazi ya Wakili, Jaji Mkuu amesema Wakili anahitaji  kuaminiwa na kuaminika ambapo maadili mema na uwezo ni nguzo kwa ushindani wa huduma za kiwakili hasa katika karne ya 21. Alisema huduma bora na ushindani stahiki kwa karne hii utawezekana tu endapo  Mawakili watajiendeleza kitaaluma na kutumia mifumo ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
Amesema kwa kuzingatia umuhimu wa sheria katika kila nchi, wakili ni kiongozi, mshauri, mtetezi na msimamizi wa kila jambo linaloratibiwa na kusimamiwa na sheria, hivyo amewataka watumie sheria kutatua na kumaliza migogoro, na kuweka mazingira ya ustawi wa maendeleo ya wananchi.
Naye Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Prof. Adeladius Kilangi amewataka Mawakili wanaofanya kazi na watakaoajiriwa serikalini kuzingatia sheria na taratibu za utumishi wa Umma kwa kutokutenda makosa ya jinai.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali pia amewataka Mawakili wanapotekeleza wajibu wao kuzingatia maslahi ya wateja wao badala ya kuweka mbele  maslahi binafsi. Kiongozi huyo pia amewataka Mawakili kujitafutia kipato chao kwa njia zilizo halali.
Jaji Mkuu wa Tanzania amewakubali na kuwaapisha wanasheria 909 kuwa Mawakili wapya wakiwemo Majaji, Naibu Wasajili, Mahakimu, Maprofesa wa sheria, Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Wananchi na Jeshi la Polisi, Wahadhiri, Mapadri, Mashehe pamoja na Balozi Mstaafu katika sherehe za 59 za Mawakili zilizofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Sheria jijini Dar es salaam. Sherehe hizo zilianza kufanyika rasmi mwaka 1986.
  Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa na Majaji wengine wakati wa sherehe ya kuwakubali na kuwaapisha Mawakili wapya 909 zilizofanyika jana kwenye viwanja vya shule ya Sheria jijini Dar es salaam. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Eliezar Feleshi.
  Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa sherehe  ya kuwakubali na kuwaapisha Mawakili wapya 909 zilizofanyika jana kwenye viwanja vya shule ya Sheria jijini Dar es salaam.

 Sehemu ya Mawakili 909 wakiwa sherehe hizo jana. 
 Sehemu ya Mawakili 909 wakiwa sherehe hizo jana. 
 Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza kwenye  sherehe ya kuwakubali na kuwaapisha Mawakili wapya 909 jana jijini
Dar es salaam.

 Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Prof. Adeladius Kilangi akizungumza kwenye  sherehe ya kuwakubali na kuwaapisha Mawakili wapya 909 jana jijini
Dar es salaam.
 Rais wa Tanganyika Law Society (TLS) Mhe. Fatma Karume akizungumza kwenye  sherehe hizo  jana jijini Dar es salaam.


 Sehemu ya Mawakili 909 wakiwa sherehe hizo jana. 
Sehemu ya Mawakili 909 wakiwa sherehe hizo jana. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni