Jumatatu, 17 Desemba 2018

WATUMISHI WAKUMBUSHWA KUZINGATIA MAADILI KAZINI

Na Emmanuel Oguda- Shinyanga

Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga wamekumbushwa kufanya kazi kwa kuzingatia maadili pamoja na kuipenda kazi yao kwa muda wote.
Hayo yamesemwa mwishoni mwa wiki na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka za Mahakama ya Tanzania Bw. Thomas Manyambula alipofika Shinganya na kufanya kikao cha pamoja na Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama Mkoa wa Shinyanga.

Akizungumza na Watumishi hao wa Mahakama, Bw. Manyambula aliwasisitiza Watumishi hao kuwa makini na matumizi ya Mitandao ya Kijamii hususani katika suala la usambazaji wa Nyaraka za kiofisi, utunzaji wa siri za Mahakama, kuhifadhi kwa usahihi kumbukumbu zote za Mahakama pamoja na kuthamini kazi wanazozifanya.
Akizungumza wakati wa kikao hicho,  Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga Mhe. Sekela Mwaiseje alimshukuru  Mkurugenzi huyo wa nyaraka kwa kuwakumbusha watumishi kutekeleza wajibu wao hasa katika uhifadhi wa nyaraka za Mahakama pamoja na kupenda na kuithamini kazi za kuhudumia wananchi.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga Bw. Ernest Masanja aliwaasa watumishi wa Mahakama kuzingatia yale yote waliyoelekezwa na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Nyaraka na Kumbukumbu za Mahakama ili kuleta ufanisi na tija katika suala zima la utoaji haki kwa Wakati.
 Mkurugenzi wa Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka za Mahakama ya Tanzania Bw. Thomas Manyambula akizungumza na Watunza Kumbukumbu wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Shinyanga (hawapo Pichani).
Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Shinyanga (Watunza Kumbukumbu) wakimsikiliza Mkurugenzi wa Usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka za Mahakama ya Tanzania Bw. Thomas Manyambula
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Shinyanga Bw. Ernest Masanja akizungumza na Watumishi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni