Jumapili, 27 Septemba 2020

MWILI WA JAJI MMILLA KUZIKWA KESHO DAR ES SALAAM

Mwili wa aliyekuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Bethuel Mpakani Kasefu Mmilla unatarajiwa kuzikwa kesho Jumatatu Septemba 28, 2020 kwenye mji wake, Goba Michungwani jijini Dar es salaam.

Kwa mujibu wa ratiba ya mazishi iliyotolewa na Mahakama ya Tanzania, mwili wa marehemu Jaji Mmilla utaagwa katika viwanja vya Karimjee ambapo shughuli za kuaga zitaanza kuanzia saa 3:00 mpaka saa 5:30 Asubuhi.

Aidha mwili wa Marehemu utapelekwa katika kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (K.K.K.T) usharika wa Mwenge na kufanyiwa Ibada itakayoanza saa 7:00 na kumalizika saa 9:00 mchana.

Mwili wa marehemu Jaji Mmilla utapumzishwa katika nyumba yake ya milele kwenye mji wake uliopo Goba Michungwani jijini Dar es salaam kuanzia saa 10:00 jioni.

Jaji Mmilla alifariki dunia usiku wa Septemba 25, 2020 katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Awali marehemu alilazwa katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo jijini Dar es salaam Septemba 23, 2020 alipokuwa akipatiwa matibabu na baadaye kuhamishiwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) alipofariki dunia.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni