Ijumaa, 12 Machi 2021

MAHAKAMA YA TANZANIA NA WIPO ZASAINI MKATABA KUSHIRIKIANA KATIKA MASUALA YA MILIKI UBUNIFU

 Na Lydia Churi-Mahakama

Hivi karibuni Mahakama ya Tanzania pamoja na shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia  masuala ya Miliki Bunifu (World Intellectual Property Organisation-WIPO)  walisaini  mkataba wa makubaliano (Memorundum of Understanding) unaolenga kuendeleza ushirikiano katika kuimarisha huduma za kimahakama.

Mkataba huo ulisainiwa Machi 5, mwaka huu kati ya Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Chuma kwa upande wa Mahakama ya Tanzania pamoja na  Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Miliki Bunifu (WIPO)  Bw. Daren Tang.

Baadhi ya maeneo yaliyokubaliwa katika ushirikiano huo ni pamoja na kubadilishana uzoefu wa shughuli za Mahakama na kushirikiana kujengeana uwezo katika kazi za Mahakama kupitia mikutano na semina kwa Majaji na Mahakimu, uandaji wa majumuisho ya sheria na kesi zinazohusu miliki bunifu (Compendium of IP laws and digest of cases)

Maeneo mengine ya ushirikiano huo ni pamoja na kubadilisha taarifa zinazohusu maamuzi ya kimahakama, kushirikiana katika kufanya tafiti zinazohusu masuala ya miliki bunifu, kushirikiana katika kusisitiza matumizi ya njia ya usuluhishi katika utatuzi wa migogoro pamoja na maeneo mengine yatakayokubaliwa na pande zote mbili.

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania alisema kusainiwa kwa mkataba huo kunarasimisha ushirikiano uliokuwepo kati ya Mahakama ya Tanzania na shirika la WIPO.

Alisema mafunzo ya kuwajengea uwezo Majaji na Mahakimu yaliyofanyika nchini Tanzania mwaka 2019 yamesaidia kuwaongezea ujuzi watumishi hao wa Mahakama hivyo aliishukuru WIPO kushirikina na Mahakama ya Tanzania katika kuandaa mafunzo hayo muhimu katika shughuli za utoaji haki nchini.

Msajili Mkuu pia aliwashukuru Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na Mwakilishi wa Tanzania katika shirika hilo Mhe. Upendo Ngitiri ambaye ni Hakimu Mkazi- Kurugenzi ya Usimamizi  wa mashauri kwa jitihada zao zilizowezesha  Mahakama ya Tanzania na WIPO kusaini mkataba wa makubaliano hayo. 

Akizungumza wakati wa utiaji Saini wa Mkataba huo, Mkurugenzi Mkuu wa shirika la WIPO Bw. Daren Tang aliipongeza Tanzania na kueleza kuwa  utafiti  uliofanywa na  jarida la kimataifa linalopima nchi mbalimbali katika masuala ya uvumbuzi (Global Innovation  Index (GI)) katika utafiti wake ilieleza kuwa mwaka jana Tanzania ilishika  nafasi ya kwanza kati ya nchi 16 zenye kipato cha chini  (kwa wakati huo )  na nafasi ya nne (4) kati ya nchi 26 za kusini mwa jangwa la Sahara.

Bw. Tang alizitaja sababu za Tanzania kufanya vizuri kuwa ni uwepo wa miundonmbinu mizuri ya ubunifu, mazingira mazuri ya kimawasiliano kati ya Tanzania na mataifa mengine na ongezeko la viwanda.      

Hafla ya kusainiwa kwa mkataba huo ilifanyika kwa njia ya mtandao na kuhudhuriwa na viongozi wa Mahakama ya Tanzania akiwemo Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara Mhe. Stephen Magoiga ambaye alitoa ujumbe wa Mahakama kwa niaba ya Jaji Mkuu  pamoja na viongozi wengine wa juu wa Mahakama. Viongozi  wa WIPO  na Balozi wa Tanzania  nchini Geneva Mhe. Maimuna Tarishi aliyewakilisha Tanzania nchini humo pia walikuwepo kwenye half hiyo.

 Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Chuma (kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Miliki Bunifu (WIPO)  Bw. Daren Tang wakisaini  Mkataba wa Makubaliano (Memorundum of Understanding) kati ya Mahakama ya Tanzania na shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia  masuala ya Miliki Bunifu (World Intellectual Property Organisation-WIPO) unaolenga kuendeleza ushirikiano katika kuimarisha huduma za kimahakama.

 Hafla ya kusainiwa kwa Makubaliano hayo kama inavyoonekana katika picha. 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara Mhe. Stephen Magoiga  ambaye alitoa ujumbe wa Mahakama kwa niaba ya Jaji Mkuu akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Chuma akisaini Mkataba huo kwa upande wa Mahakama ya Tanzania.
Hafla ya kusainiwa kwa Makubaliano hayo kama inavyoonekana katika picha kwa upande wa Tanzania. Upande wa pili walisaini Mkataba huo nchini Geneva.


 











 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni