Ijumaa, 12 Machi 2021

TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA YA ARDHI AFARIKI DUNIA

Marehemu Kelvin Johnas Lungu enzi za uhai wake

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Mtumishi wake Bw. Kelvin Johnas Lungu (57) (pichani) aliyekuwa Mlinzi Mkuu wa Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi.

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Divisheni hiyo, Bi. Mary Shirima amesema kuwa marehemu alikutwa na umauti Machi 11, 2021 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.

Bi. Shirima ameeleza kuwa mwili wa marehemu Lungu unatarajiwa kuagwa kesho Machi 13, 2021 Muhimbili kuanzia saa 04:00 asubuhi.

Aidha amesema kuwa mara baada ya ratiba ya kuaga, mwili wa marehemu unatarajia kusafirishwa kesho hiyohiyo kuelekea Ruvuma-Songea Kijiji cha Hanga Ngadinda kwa ajili ya mazishi yanayotarajiwa kufanyika Machi 14, 2021.

Marehemu Lungu aliajiriwa na Mahakama tangu Agosti 11, 1999 akiwa Mlinzi cheo alichotumikia katika vituo kadhaa ikiwemo Mahakama Kuu-Masjala Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi-Kisutu na hatimaye Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi.

Mahakama ya Tanzania inaungana na ndugu, jamaa na marafiki kuomboleza msiba wa mpendwa wetu.

BWANA AMETOA, BWANA AMETWAA, JINA LAKE LIHIMIDIWE.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni