Jumamosi, 1 Mei 2021

ZINGATIENI MIONGOZO YA UTOAJI ADHABU NA UTEKELEZAJI WA HUKUMU: JAJI KIHWELO

Na Rosena Suka- IJA, Lushoto

 

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ambaye pia ni na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo ametoa wito kwa Naibu Wasajili na Mahakimu kuzingatia miongozo ya utoaji adhabu na utekelezaji wa hukumu na amri za Mahakama.

Jaji Kihwelo ameyasema hayo alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili kuhusu utekelezaji wa hukumu na amri za Mahakama kwenye mashauri ya madai na utoaji adhabu kwenye mashauri mbalimbali ya jinai yaliyotolewa kwa Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi pamoja na Mahakama za wilaya wapatao 24.

“Mafunzo haya mliyoyapata yakawe na matokeo chanya hasa kwa vile wawezeshaji wa mafunzo wamebobea katika maeneo husika na wamewapa mbinu nyingi za utoaji wa adhabu na utekelezaji wa amri za mahakama na hukumu mbalimbali”, alisema Mhe. Kihwelo.

Jaji Kihwelo amewataka washiriki wa mafunzo hayo kuwapatia watumishi wengine wa Mahakama ambao hawakupata nafasi ya kushiriki mafunzo hayo kile walichokipata ili kusaidia kuimarisha utendaji kazi.

 Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Mtwara Mhe. Amir Msumi alisema kuwa mafunzo waliyopatiwa ni ziada ya faida ya kuimarisha uwezo kwao ikiwa ni pamoja na uwezo wa kufanya ukaguzi wa Mahakama za chini.

“Kama Mahakama zetu zitaimarika katika usahihi wa adhabu na ukazaji wa hukumu kwa kadri ya miongozo inavyoeleza, Imani ya wadau na Taasisi zingine itaongezeka na hivyo kujenga heshima kwa Mahakama ya Tanzania kwa upande mmoja na amani na ustawi wa nchi na wananchi kwa upande mwingine” alisema Mhe. Msumi.

 

Mafunzo hayo yaliandaliwa na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) chini ya ufadhili wa Mradi wa Kujenga Uwezo Endelevu wa Kupambana na Rushwa (Building Sustainable Anti-Corruption Action in Tanzania yaani BSAAT).

Hili ni kundi la pili kushiriki mafunzo ya aina hiyo ikiwa ni muendelezo wa mafunzo yanayotarajiwa kutolewa pia kwa Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wengine. Kundi la tatu la mafunzo hayo linatarajiwa kupatiwa mafunzo Mei 04 na 05, 2021 chuoni hapo.

Baadhi ya washiriki wa Mafunzo kuhusu Utekelezaji wa Hukumu na Amri za Mahakama kwenye mashauri ya madai na utoaji adhabu kwenye mashauri mbalimbali ya jinai wakiwa kwenye mafunzo hayo yaliyofanyika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto. Washiriki wa Mafunzo hayo ni Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za wilaya.
 
Baadhi ya Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za wilaya wakiwa kwenye Mafunzo hayo.
Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala wa Mahakama ya Tanzania Bw. Stephen Pancras akizungumza wakati wa mafunzo hayo.
Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akimkabidhi cheti moja ya wahitimu wa Mafunzo kuhusu Utekelezaji wa Hukumu na Amri za Mahakama kwenye mashauri ya madai na utoaji adhabu kwenye mashauri mbalimbali ya jinai.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni