Ijumaa, 4 Juni 2021

MRADI WA ‘IJC’ ARUSHA KUKAMILIKA JULAI MWAKA HUU; WAFIKIA ASILIMIA 83

 Na Mary Gwera, Mahakama

Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (Integrated Justice Centre) unaojengwa jijini Arusha unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Julai, 2021 huku ikielezwa kuwa kwa sasa umefikia asilimia 83 ya ujenzi wake.

Akizungumza na Waandishi wa Habari wa mkoani Arusha katika ziara maalum ya kutembelea mradi huo iliyofanyika mapema leo Juni 04, 2021, Mhandisi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Fabian Kwagilwa alisema kuwa kwa sasa Mkandarasi yupo katika hatua ya umaliziaji wa jengo ‘finishing stage’.

“Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Januari 2020, ambapo mpaka sasa umekamilika kwa asilimia 83, na mradi huu unagharimu fedha za kitanzania zenye thamani ya takribani shilingi bilioni 8.293,” alisema Mhandisi Kwagilwa.

Alisema kuwa mradi huu ni moja kati ya miradi sita (6) ya ujenzi inayoendelea kujengwa na Mahakama ya Tanzania katika mikoa ya Morogoro, Dodoma, Mwanza na Dar es Salaam ambapo yote inalenga kuwafikishia wananchi huduma ya upatikanaji wa haki kwa urahisi zaidi.

Aliongeza kuwa katika jengo hilo kutakuwa na ngazi zote za Mahakama kwa maana ya Mahakama ya Mwanzo, Mahakama ya Wilaya, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama Kuu.

Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Moses Mzuna amesema kuwa ujenzi wa jengo hilo na mengineyo ya Mahakama yawe ni chachu kwa Watumishi wa Mahakama kuendelea kuchapa kazi.

“Niseme kwamba, Mhe. Jaji Mkuu amesisitiza na mimi hili lazima niliseme kuwa Majengo haya ambayo Mahakama inajenga iwe ni chachu kwa sisi Watumishi kufanya kazi kwa ufanisi zaidi ili kuongeza Imani ya wananchi kwa Mahakama,” alieleza.

Aliongeza kuwa kupatikana kwa jengo hilo kutasaidia pia kupatikana kwa nafasi kuwa zaidi ambayo itawezesha kufanya kazi katika eneo kubwa zaidi tofauti na ilivyo sasa katika jengo la Mahakama Kuu kanda ya Arusha wanalotumia.

Mbali na hayo, Mhe. Jaji Mzuna alisema faida nyingine ya jengo hilo litawawezesha wananchi kupata huduma ya haki katika eneo moja kwa urahisi zaidi badala ya kusafiri umbali mrefu kutafuta haki zao.

“Wananchi wana kiu ya kufungua mashauri kwa sababu wanajua haki zao, hiki ni kitu kizuri badala ya kujichukulia sheria mkononi, na vilevile wana Imani na Mahakama hivyo itasaidia kushughulikia mashauri kwa muda mfupi na haraka zaidi,” alisema.

Mahakama ya Tanzania kwa sasa inaendelea kuboresha miundombinu yake kwa kukarabati majengo ya zamani na kujenga mengine mapya, hivi karibuni inatarajia kuanza ujenzi wa majengo 25 ya Mahakama za wilaya katika maeneo mbalimbali nchini yasiyokuwa na huduma ya Mahakama za wilaya.

Kupitia Mpango wa Miaka Mitano wa Maendeleo ya Miundombinu (Five Year Infrastructural Development Plan) 2016/2017-2020/2021 unaohusu ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama, maeneo ya kipaumbele yaliainishwa kwa kuzingatia vigezo vya idadi ya Watu, wingi wa mashauri, maeneo mapya ya utawala, umbali kwa wananchi kufuata huduma shughuli za kiuchumi, na mazingira ya kijiografia.

Mradi huu ya ujenzi wa kituo Jumuishi cha utoaji Arusha unatekelezwa na Mkandarasi ‘LIJUN DEVELOPMENT CONSTRUCTION CO. LTD’ chini ya usimamizi wa Mkandarasi Mshauri ‘HAB CONSULT LTD.’

Muonekano wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji haki kinachoendelea kujengwa mkoani Arusha. Jengo hili limefikia asimilia 83. Linatarajiwa kukamilika Julai, 2021.
Baadhi ya Waandishi wa Habari wa Mkoani Arusha waliofanya ziara la kujua maendeleo ya Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi kinachojengwa mkoani humo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Moses Mzuna akionyesha kufurahishwa na Mradi ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki, ambapo Arusha ni moja ya maeneo yaliyobahatika kupata mradi huo.
Mhandisi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Fabian Kwagilwa akiwaeleza Waandishi wa Habari maendeleo ya ujenzi wa Kituo hicho katika ziara ilyofanyika Juni 04, 2021.
Ukaguzi wa Mradi ukiendelea.




 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni