Alhamisi, 3 Juni 2021

UWAZI, UWAJIBIKAJI NA UADILIFU IWE MSINGI WA KAZI YAKO – JAJI CHANDE.

Na Innocent Kansha – Mahakama Lushoto.

Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman amewataka Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania kuongeza uwazi, uwajibikaji, kujenga utamaduni wa kufikika na kutoa maamuzi kwa wakati na kwa kushirikiana na wadau.

Akizungumza na Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania alipowatembelea wakati wa mafunzo elekezi katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto mnamo Juni 3, 2021 Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman aliwapongeza kwa kuteuliwa na Kuwakumbusha Majaji kuwa mwananchi wa kawaida anatamanani kuona shauri lake linamalizika mapema ili ajue hatima yake

 “Ili Mahakama ifikie lengo hilo ni lazima tuwe na Majaji, Mahakimu na Watumishi wa kada mbalimbali wenye weledi, wanaoaminika na wenye sifa za uwajibikaji na uadilifu”, aliongeza Mhe. Othman

Aidha, Kila Jaji alieteuliwa ana kipawa na karama zake mkatumie huo uwezo wenu mliobarikiwa nao kuisaidia Mahakama ya Tanzania kuleta mabadiliko ya kweli, kila mmoja wenu kama Kiongozi atumie maarifa yake kuisaidia Taasisi na kumsaidia Jaji Kiongozi na Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu Msataafu Mhe. Othman pia aliwakumbusha Majaji matumizi ya lugha sahihi wakati wa kukosoa ama kusahihisha hukumu za mahakama za chini, tambueni kuwa hukumu au maamuzi unayoyatoa ni kumbukumbu ya kudumu, hivyo lugha inatakiwa kuwa yenye ufasaha wa hali ya juu.

Majaji mnatakiwa kupambana na rushwa kwa nguvu zote ndani ya Taasisi. Muangalie suala la maadili kwa jicho la tatu, lazimisheni maadili miongoni mwenu ili yaonekane yanatendeke itajenga taswira chanya kwa watumishi wengine.

Jaji Chande aliwashauri watumishi wa Mahakama kuendelea kujiendeleza kielimu kwa kusoma fani mbalimbali ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa kila siku wa Taasisi, hii itasaidia kuendana na kasi kubwa ya maboresho yanayoendelea mahakamani.

Mathalani, Maboresho makubwa na ufanisi unaoonekana umetokana na kuanzishwa Tume huru ya Utumishi wa Mahakama na pia kutenganisha kada mbili za taaluma ya watendaji na wasajili, kwa maana ya Watendaji kushughulika na masuala ya utawala na fedha na Wasajili kushughulika masuala ya utaratibu wa mashauri mahakamani. Mfumo huu wa uendeshaji shughuli za kimahakama Tanzania iliiga mfumo huo kutoka Tume ya utumishi wa Mahakama ya Jamhuri ya Ireland, aliongeza Jaji Othman.

Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman akizungumza na Majaji wapya walio kwenye mafunzo elekezi (hawapo pichani) mara baada ya kuwatembelea mnamo Juni 3, 2021


Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama Kuu ya Zanzibar wakimsikilia Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman alipowatembelea darasani.


Baadhi ya Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama Kuu ya Zanzibar wakimsikilia Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman alipofanya mazunzungumzo nao.

Picha na Innocent Kansha - Mahakama.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni