Alhamisi, 1 Julai 2021

JAJI MFAWIDHI MPYA WA MAHAKAMA KANDA YA KIGOMA AKABIDHIWA OFISI

Na Festo Sanga, Mahakama-Kigoma

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Kigoma ambaye kwa sasa ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Ilvin Mugeta amekabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi aliyehamia Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma Mhe. Jaji Lameck Mlacha huku akimhakikishia Mhe. Jaji Mlacha kuwa watumishi wa Kanda hiyo wana ari ya kufanya kazi.

Akifanya makabidhiano hayo Juni 30, 2021, Mhe. Jaji Mugeta alimfahamisha Jaji Mlacha kuwa Kanda hiyo iliyoanzishwa mwaka 2019 ilitumia muda wa kutosha   kuwajengea uwezo watumishi, kusimamia nidhamu na maadili na kuhakikisha kwamba kazi za wadau zinafanyika kwa kuzingatia taratibu za kimahakama na za kisheria zilizowekwa na kusema kuwa Kanda ni salama.

“Kanda ni salama, watumishi tuna ari ya kufanya kazi bila kutegeana na kwa moyo wote hivyo nakukabidhi watu ambao wako tayari kutekeleza majukumu yao kwa maelekezo ya kisheria,” alisema Jaji Mugeta.

Naye Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu, Kanda ya Kigoma, Mhe. Jaji Lameck Mlacha amewaomba ushirikiano watumishi katika utendaji kazi na kuwaasa kila mmoja kutimiza wajibu wake katika nafasi aliyonayo.

“Tuna wajibu wa kuendelea kujituma na kufanya kazi kwa kuzingatia weledi na kushirikiana. Nimefahamishwa juu ya Uhaba wa watumishi uliopo hivyo wale ambao wanafanya kazi zaidi tutaendelea kutambua na kuthamini jitihada zao ili kuwatia moyo”. Alisema Jaji Mlacha.

Mheshimiwa Jaji Mlacha amewataka watumishi kuendelea kuzingatia maelekezo mbalimbali yanayotolewa na wataalam wa Afya juu ya namna ya kukabiliana na ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu (COVID 19) ikiwa ni pamoja na kuvaa barakoa, kunawa kwa maji tiririka na sabuni na kujiepusha na mikusanyiko isiyo ya lazima.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Jaji Athumani Kirati wa Kanda hiyo, amemuahidi ushirikiano wa kutosha na kusema kuwa Uongozi na watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma wana imani kuwa atawavusha salama. Vilevile alimtakia Mhe. Jaji Mugeta majukumu mema katika kituo chake kipya.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi, Bi Rhoda Kijumbe ambaye ni katibu Mahsusi  alisema kuwa Mhe. Jaji Mugeta ameacha alama katika uongozi wake katika Kanda ya Kigoma hivyo atakumbukwa kwa mengi mazuri na alichukua nafasi hiyo kumkaribisha Mhe.  Jaji Mlacha katika Kanda ya kigoma.

Katika hafla hiyo Jaji Mugeta alimkabidhi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kigoma taarifa ya makabidhiano.

Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Jaji Lameck Mlacha akifafanua jambo  mbele ya watumishi wa Kanda hiyo (hawapo pichani) katika hafla ya makabidhiano yaliyofanyika Juni 30,2021.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Kigoma, Mhe. Jaji Ilvin Mugeta (aliyesimama) akitoa neno wakati wa hafla ya makabidhiano ya Ofisi na Jaji Mfawidhi mpya wa Kanda hiyo, Mhe. Jaji Lameck Mlacha (katikati). Kulia ni Mhe. Jaji Athumani Kirati.

 Watumishi wa Mahakama Kuu Kigoma wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo, Mhe. Jaji Mlacha.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni