Jumatano, 7 Julai 2021

MAWAKILI SASA KUAPA KIAPO CHA UADILIFU

 Na Lydia Churi- Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ameridhia ombi la Chama cha Mawakili Tanganyika (Tanganyika Law Society-TLS) la wanasheria wanaokubaliwa na kupokelewa kuwa mawakili kuongezewa kiapo cha uadilifu.

Ombi hilo lilitolewa kwa Jaji Mkuu wa Tanzania jana na Rais wa chama hicho Prof. Edward Hosea alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake kwa lengo la kujitambulisha na kuutambulisha uongozi mpya wa chama hicho.

“Kiapo cha uadilifu ni utaratibu unaotumika hata kwa viongozi wengine wanapoapishwa hivyo mimi sina pingamizi, kuna haja ya kukumbushana umuhimu wa maadili kwenye kazi za utoaji haki”, alisema Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu alisema Chama cha Mawakili Tanganyika ni wadau muhimu kwenye utekelezaji wa Mpango Mkakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania kwa kuwa mafanikio ya mhimili huo yanatokana na mchango mkubwa unaotolewa na chama hicho.

Kwa Upande wake, Rais wa TLS ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa matumizi ya Tehama pamoja na kutoa miongozo mbalimbali inayorahisisha upatikanaji wa haki nchini.

Alisema miongozo inayotolewa na Mahakama imesaidia kurahisisha upatikanaji wa haki huku akitolea mfano wa mwongozo kutoa adhabu (sentencing Manual) pamoja na ule wa masuala ya dhamana.

“Chama cha Mawakili Tanganyika kitaendeleza mahusiano mazuri yaliyopo kati yake na Mahakama ya Tanzania kwa lengo la kuboresha shughuli za utoaji haki nchini na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati”, alisema.

Kuhusu changamoto za chama hicho, Prof. Hosea alisema hivi sasa baadhi ya Taasisi zikiwemo za Serikali zimekuwa zikikataa viapo vya mawakili na kuelekeza matumizi ya viapo vinavyotoka mahakamani. Aidha, alimwomba Jaji Mkuu kukisaidia chama hicho ili viapo vya wananchama wake vikubalike kwa wote kama ambavyo sheria imeruhusu.

Rais wa chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Prof. Edward Hosea akizungumza wakati alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake kwa lengo la kujitambulisha na kuutambulisha uongozi mpya wa chama hicho. Aliyekaa katikati mbele ni Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akizungumza.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Chuma akizungumza wakati Rais wa TLS alipomtembelea Jaji Mkuu wa Tanzania ofisini kwake.   
 
 

 Viongozi wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS) wakiongozwa na Rais wa Chama hicho Prof. Edward Hosea (kushoto) wakisubiri kukutana na Jaji Mkuu wa Tanzania walipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es salaam. Katikati ni Makamu wa Rais wa chama hicho, Gloria Kalabamu. Wengine ni Mtendaji Mkuu Bw. Kaleb Gamaya (wa pili kushoto), Mwenyekiti wa Mawakili Vijana Bw. Dedis Bwana na Katibu Bi Mariam Othmani. 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni