Jumanne, 31 Agosti 2021

MAHAKAMA YAKUBALI KUSIKILIZA HOJA ZA UTETEZI KATIKA SHAURI LA MBOWE KWA MAANDISHI

  Na Mwandishi wetu, Mahakama

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imekubali maombi ya Mawakili wa Serikali waliyoiomba Mahakama hiyo kusikiliza utetezi wa mapingamizi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na upande wa Serikali kwa njia ya maandishi.

Uamuzi huo umefikiwa leo Agosti 30 mbele ya Mahakama hiyo baada ya upande wa Mlalamikaji kushindwa kuwasilisha viapo vya ziada kama walivyotakiwa kuwasilisha viapo hivyo mahakamani hapo tangu tarehe agosti, 2021 na badala yake wameamua kuendelea na viapo vilivyowasilishwa awali.

Akizungumza mbele ya Mahakama hiyo, Wakili wa Serikali Mkuu, Bw. Hangi Chang’a ameiomba Mahakama kuridhia ombi hilo kwa madai kuwa baada ya upande wa mlalamikaji kushindwa kuwasilisha hoja zao za ziada, kama walivyotakiwa na Mahakama hiyo wao walitekeleza wajibu wao wa kisheria kwa kuwasilisha mapingamizi manne kwa lengo la kupinga hoja za upande wa mlalamikaji.

Mapingamizi yaliyowasilishwa leo yanalenga kuiomba Mahakama hiyo kuliondoa Shauri hilo Mahakamani kwa kuzingatia kuwa taratibu zilizotumika kufungua na kuwasilisha shauri hilo la kikatiba zilikiuka taratibu za kisheria.

Mlalamikaji katika shauri hilo analalamikia utaratibu uliotumika kumkamata na kumfikisha Mahakamani katika shauri analotuhumiwa kufadhili vitendo vya kigaidi kuwa ulikiuka na kuvunja haki zake za kikatiba.

Baada ya kusikiliza maelezo kutoka pande zote mbili Jaji anayesikiliza shauri hilo Mhe. John Mgetta ameutaka upande wa serikali kuwasilisha hoja zake kwa maandishi ifikapo tarehe 6 Septemba huku upande wa mlalamikaji ukitakiwa kujibu hoja hizo tarehe 09 Septemba na kama kutakuwa na hoja za kujibu kutoka upande wa serikali basi wawasilishe hoja hizo tarehe 13 Septemba mwaka 2021.

Mhe. Jaji. Mgetta ameahirisha Shauri hilo mpaka tarehe 23 septemba saa 8:00 mchana litakapotajwa tena Mahakamani hapo huku akueleza kuwa hakutakuwa na sababu  Mhe. Mbowe kuhudhuria Mahakamani hapo na badala yake atawakilishwa na wakili wake.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni