Ijumaa, 13 Agosti 2021

WADAU WA UTOAJI HAKI NCHINI WATAKIWA KUSHIRIKIANA

 Na Lydia Churi-Mahakama, Njombe

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ametoa wito kwa wadau wa Mahakama kushirikiana katika kutekeleza majukumu yao ya msingi ambayo yanagusa suala la upatikanaji wa haki kwa wananchi.

Akizungumza na wajumbe wa kamati za maadili za Maafisa wa Mahakama za wilaya na mkoa katika ziara ya Tume mjini Njombe, Jaji Mkuu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama amesema wadau hao hawana budi kushirikiana na Mahakama kwa kuwa changamoto zinazoukabili Mhimili huo ni za wadau wote.

“Kila mdau wa Mahakama anao mchango mkubwa kwenye mnyororo wa utoaji haki hivyo hatuna budi kushirikiana ili wananchi wapate haki kwa wakati”, alisema Jaji Mkuu.

Naye Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi amewataka Mahakimu wote nchini kuwa makini wakati wa kusajili mashauri na kahakikisha wanasajili yale yenye vigezo vya kupokelewa ili kupunguza mlundikano wa kesi mahakamani.

Aidha, Jaji Feleshi ametoa wito kwa vyombo vya upelelezi kuharakisha upelelezi wa mashauri na kuyafikisha mahakamani yale yenye mashiko. Aliongeza kuwa upelelezi unapochukua muda mrefu huweza kusababisha ushahidi wake kupungua nguvu.

Akizungumzia matarajio ya Mahakama kutoka kwa wadau ni kuona kuwa upelelezi wa mashauri unafanywa kwa kutumia ya njia za kisayansi ikiwemo matumizi ya kipimo cha Vinasaba yaani DNA ili kuharakisha upelelezi na kupata matokeo sahihi yatakayosaidia haki kutendeka.

Jaji Kiongozi pia ameishauri Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) kuchunguza malalamiko dhidi ya rushwa na kuyathibitisha ili yanapofikishwa mahakamani yamalizike kwa wakati. Aidha, Dkt. Feleshi pia ameitaka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali kuharakisha upelelezi wa kimaabara ili kesi zisikae mahakamani kwa muda mrefu.

Wakati huo huo. Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Njombe ambaye pia ni Mkuu wa wilaya ya Wanging’ombe, Bw. Lautery Kanoni ameiomba Mahakama ya Tanzania kuufikiria mkoa wa Njombe kuwa na Mahakama Kuu kutokana na mkoa huo kuwa na mashauri mengi ya mauaji.

Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wanaendelea na ziara katika mikoa ya Mbeya na Songwe kwa lengo la kuitangaza na kutoa elimu kwa wajumbe wa kamati za Maadili za Mikoa na Wilaya pamoja na wadau wa Mahakama.

Wajumbe wa Tume hiyo ni pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania (Mwenyekiti), Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji moja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, na wajumbe wengine wawili wanaoteuliwa na Rais.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akizungumza na wadau wa Mahakama katika Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wadau mjini Njombe.

Wadau wa Mahakama wakiwa katika Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama  mjini Njombe.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wakati Tume hiyo ilipokutana na wadau mjini Njombe.

Naibu Msajili na Mkurugenzi wa Usimamizi na Ukaguzi wa huduma za Mahakama na Maadili Mhe. Anna Magutu akizungumza katika Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wadau mjini Njombe.






 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni