Jumatatu, 27 Septemba 2021

MAHAKAMA SPORTS WAANZA KUJIFUA

Na Innocent Kansha - Mahakama

Uongozi wa Shule ya Sheria kwa Vitendo umekiruhusu Chama cha Michezo cha Mahakama ya Tanzania, Mahakama Sports, kutumia viwanja vyake kwa ajili ya kufanyia mazoezi ya michezo mbalimbali ili kujiandaa na mashindano ya SHIMIWI yanayotarajiwa kufanyika mkoani Morogoro kuanzia Oktoba 20, 2021 hadi Novemba 2, 2021.

Hayo yalibainishwa leo Septemba 27, 2021 na Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Bw. Wilson Dede, alipokuwa akizungumzia juhudi zilizofanywa na uongozi wa Chama kwa kushirikiana na ofisi ya Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala ya Mahakama ya Tanzania katika kutatua changamoto ya ukosefu wa viwanja vya kufanyia mazoezi.

“Tunaushuru sana Uongozi wa Shule ya Sheria kwa Vitendo chini ya Kaimu Mkuu wa Shule hiyo, Mhe. Dkt Zakayo Lukumay, kwa kutoa kibali kutumia viwanja hivi kufanya mazoezi katika michezo mbalimbali. Inaonekana hata yeye anapenda sana michezo, maana kuna baadhi ya siku huwa tunashiriki naye katika mazoezi,” alisema.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, tayari “program” ya mazoezi inatekelezwa na watumishi wa Mahakama ambao wameanza kujitokeza kwa wingi kushiriki katika michezo mbalimbali, ikiwemo mpira wa miguu kwa wanaume, mpira wa pete, kuvuta kamba kwa wanaume na wanawake, riadha za mbio fupi kwa wanaume na wanawake pamoja na “draft.”

“Kwa hiyo nawaomba wanamichezo wenzangu kuhudhuria mazoezi kwa wingi ili kujiandaa vema kushiriki katika mashindano haya ya SHIMIWI,” alisema. Hata hivyo, Bw. Dede alisisitiza kuwa mazoezi ya michezo mbalimbali kwa watumishi wote wa Mahakama yataendelea mara baada ya mashindano hayo kumalizika.

Hivi karibuni, Uongozi wa Mahakama Sports ulikutana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Eliasante Ole Gabriel, ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam ambapo aliahidi kuwapa ushirikiano ili kuboresha ushiriki katika michezo inayoandaliwa na sekta mbalimbali hapa nchini.

Hata hivyo, Mtendanji Mkuu huyo aliwataka viongozi hao, kwa kupitia uongozi wa Mahakama ya Tanzania, kuona uwezekano wa kuomba kuwa na viwanja vya michezo katika jiji la Dodoma ili Mahakama Sports iwe na wigo mpana wa kushiriki michezo yote katika mashindano mbalimbali.


Baadhi ya wanamichezo wa Mahakama Sports wakimsikiliza Kocha Msaidizi wa Timu ya mpira wa miguu Said Albea wakati wakijiandaa kuanza mazoezi katika viwanja vya Shule ya Sheria kwa Vitendo mkoani Dar es Salaam.

Kocha Msaidizi wa Timu ya mpira wa miguu Said Albea akitoa maelekezo kwa wanamichezo  namna ya kupokea mpira.

Kocha Msaidizi wa Timu ya mpira wa miguu Said Albea akitoa maelekezo ya utekelezaji wa programu ya mazoezi  kwa mchezo huo.


Kocha Msaidizi wa Timu ya mpira wa miguu Said Albea akitoa maelekezo ya namna ya kufunga mpira kwa penati.

(Picha na Mahakama Sports.)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni