Jumatatu, 20 Septemba 2021

MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA AKUTANA NA UJUMBE WA TAWJA

Na Magreth Kinabo na Innocent Kansha-Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel, leo amekutana na viongozi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) ambapo amewashauri kubuni miradi itakayowawezesha kupata fedha za kujiendesha.

Viongozi hao wakiongozwa na Mwenyekiti wa TAWJA, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Joaquine De-Mello, walifika katika ofisi ya Mtendaji Mkuu Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujitambulisha na kuwasilisha baadhi ya changamoto zinazowakabili, ikiwemo Chama hicho kukabiliwa na uhaba wa fedha za kuendesha shughuli mbalimbali.

‘’Fikirieni miradi ambayo itawasadia kupata fedha za kuweza kuendesha shughuli mnazozifanya ili chama kisije kushindwa kujiendesha. Miradi hiyo ikifanikiwa itawasaidia kupata fedha na kuondokana na utegemezi wa wafadhili mbalimbali’’, Prof. Ole Gabriel alisema.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo alikishauri Chama hicho kuangalia vyanzo vinavyopelekea vitendo vya kikatili na unyanyasaji wa kijinsia wanavyofanyiwa wanawake na watoto ili kubaini mapungufu yaliyopo, hatua itakayowawezesha kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi kujiepusha na vitendo hivyo.

Prof Ole Gabriel pia alikishauri chama hicho kinapofanya shughuli zake kuwashirikisha viongozi wa dini na wabunge, hasa wa jinsia ya kike, ambao ni miongoni mwa wadau muhimu katika kupunguza vitendo hivyo.

Kwa upande wake, Mhe. Jaji De-Mello, kwa niaba ya TAWJA, alipendekeza suala la jinsia katika Tume ya Utumishi wa Mahakama kuangaliwa upya ili kuongeza uwakilishi wa wanawake miongoni mwa wajumbe wa tume hiyo. Akijibu pendekezo hilo, Prof. Ole Gabriel alikumbushia kuwa swala hilo ni la kikatiba ambalo linapaswa kutazamwa kwa jicho la kipekee.

Hata hivyo, Mtendaji Mkuu huyo, ambaye ni Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama alisema kuwa watatafuta namna bora itakayojadiliwa na wadau ili kuongeza uwakilishi wa kijinsia ambao hautaathiri sheria iliyounda tume hiyo.

TAWJA ni chama cha Kitaaluma, ambacho hutoa elimu katika maeneno mbalimbali juu ya ukatili wa kijinsia, unyanyasaji wa watoto na mambo yanayohusu haki za binadamu, hususani katika mashule na vyuo na pia hushiriki katika matukio ya kitaifa kama vile Wiki ya Sheria, Wiki ya Utumishi wa Umma na kwenye Maonesho ya Biashara ya Kimataifa, “SabaSaba.”

Mhe. Jaji De-Mello, ambaye aliambatana na viongozi wengine wa TAWJA alimwelezea pia Mtendaji Mkuu huyo majukumu mengine ambayo Chama kinafanya kama kuandaa machapisho mbalimbali ambayo hulenga kuelimisha Umma haki za mtoto, haki za mwanamke na haki za binadamu kwa ujumla.



Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel akipokea machapisho yanayoandaliwa na kuchapishwa na Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake (TAWJA) walipomtembelea ofisini kwake kwa ajili ya kujitambulisha, leo Septemba 20, 2021. Kulia ni Mwenyekiti wa TAWJA na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Joaquine De-Mello.

 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel, akifafanua jambo wakati akiongea na Viongozi wa TAWJA.


Mwenyekiti wa TAWJA na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Joaquine De-Mello akimuelezea Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel, baadhi ya shughuli zinazofanywa na Chama hicho.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel (katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa TAWJA, wa kwanza kulia kutoka kwa Mtendaji Mkuu ni Mwenyekiti wa TAWJA, Jaji Joaquine De - Mello, akifuatiwa na Jaji Dkt. Zainabu Mango na Jaji Nyigulila Mwaseba, wa kwanza kushoto kutoka kwa Mtendaji Mkuu ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt, akifautiwa na Hakimu Mkazi Mahakama ya Jiji, Mhe. Anipha Mwingira na Afisa Mradi Bi. Asha Komba.

Picha na Innocent Kansha - Mahakama. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni