Jumatano, 6 Oktoba 2021

NIMEONA BILIONI 9 KWENYE JENGO HILI; SAMIA

Na Mary Gwera, Mahakama

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameridhishwa na ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji haki nchini kutokana na ubora aliojionea katika uzinduzi alioufanya leo Oktoba 06, 2021 jijini Dodoma unaoakisi thamani halisi ya fedha iliyotumika.

Ujenzi wa Vituo hivyo sita (6) vilivyojengwa katika mikoa ya Dar es Salaam (Kinondoni na Temeke), Dodoma, Arusha, Mwanza na Morogoro umegharimu zaidi ya bilioni 51 za kitanzania ambapo jengo la Dodoma alilolizindua na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan limetumia zaidi ya bilioni 9.

“Ndugu zangu nimepata fursa ya kukagua jengo hili, jengo ni zuri na kusema ukweli linaendana na hadhi ya karne ya 21. Nimeliangalia wakati napata maelezo nikaambiwa bilioni 9 nikanyanyua uso na kuangalia zimeingia wapi, lakini nilivyoingia ndani nimeziona bilioni 9 zilivyotumika, kwa hiyo kwenye jengo hili thamani ya fedha kwa jengo iko sawasawa,” alisema Rais Samia.

Rais Samia alisifu mpangilio wa jengo kwa kuwa na huduma za watu wenye mahitaji maalum pamoja na vyumba vya kunyonyesha watoto, jambo ambapo amekiri kufurahishwa navyo.

“Ukilinganisha na Mahakama tulizonazo sasa kabla ya hizi, Mama anayenyonyesha hutakiwa kujifiche kwenye kichochoro ndio anyonyeshe mtoto wake na kusababisha usumbufu, kwahiyo yaliyomo kwenye jengo hili nikiri yamenifurahisha sana,” alieleza Rais Samia.

Aidha, Mhe. Rais amewashukuru Wadau wa Maendeleo hususani Benki ya Dunia (World Bank) kwa kufadhili mradi wa maboresho ya Mahakama, ikiwemo ujenzi wa Vituo hivyo kupitia fedha za mkopo.

Sherehe za uzinduzi wa vituo hivyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali, akiwemo Spika wa Bunge, Mhe, Job Ndugai, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Omar Makungu, Jaji Mkuu wa Tanzania mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Antony Mtaka na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Wananchi walianza kumiminika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kilichopo mtaa wa NCC, karibu na Benki Kuu, Dodoma majira ya saa moja na nusu na baadaye kupata burudani mbalimbali za ngoma kutoka kikundi cha Changamoto na nyimbo za kusisimua zilizoimbwa na Kwaya ya Mahakama ya Tanzania. Wimbo wa kuhamasisha chanjo kwa Watanzania ulionesha kukonga nyoyo za wananchi waliohudhuria sherehe hizo.

Mgeni rasmi katika sherehe za ufunguzi wa vituo hivyo aliwasili katika viwanja vya mahakama majira ya saa nne asubuhi na kupokelewa na mwenyeji wake Jaji Mkuu wa Tanzania pamoja na wageni wengine kutoka meza kuu na baadae alipata maelezo mafupi ya usanifu wa majengo hayo kabla ya kuzindua rasmi vituo hivyo kwa kufungua kitambaa na kukata utepe kwa kushirikiana na Mhe, Jaji Mkuu wa Tanzania.

Mhe. Rais aliingia ndani ya jengo ili kujionea uhalisia aliousikia huku akipata maelezo ya kina kutoka kwa Mtendaji Mkii wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Maboresho, Jaji Zahra Maruma.

Baada ya kukagua jengo hilo kwa ndani, Mhe. Rais alikaribishwa kwenye jukwaa kuu ambapo wimbo wa Taifa ulipigwa na kufuatiwa na wimbo wa Aftrika Mashariki. Baadaye, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbard Chuma, alitoa utambulisho wa viongozi waliohudhuria hafla hiyo, huku Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa maelezo ya mradi mzima unaohusiana na ujenzi wa vituo hivyo.

Ulifika wakati wa Waziri wa Katiba na Sheria ambaye alitoa neno juu ya ujenzi wa vituo hivyo na maendeleo ya Mahakama ya Tanzania tangu uhuru mwaka 1961 na baadaye Jaji Mkuu wa Tanzania alitoa salamu na kisha kumkaribisha Mhe, Rais kuzungumza na Watanzania kupitia hafla hiyo.

Muonekano wa mbele ya moja kati ya majengo sita, ambayo yamezinduliwa na Mhe. Rais Samia. Uzinduzi wa Kituo hicho umewakilisha vituo vingine ambavyo vimejengwa katika mikoa ya Arusha, Mwanza, Morogoro na Dar es Salaam yenye majengo mawili (Kanda ya Temeke na Kanda ya Kinondoni).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akitoa hotuba yake mara baada ya kulizindua rasmi jengo la Kituo Jumishi cha Utoaji Haki-Dodoma. Katika hotuba yake, Mhe. Jaji Mkuu ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa utekelezaji mzuri wa mradi wa maboresho ulioleta maboresho mbalimbali mojawapo ikiwa ni upatikana wa Majengo ya vituo hivi.
Waheshimiwa Majaji, Viongozi wa Mahakama pamoja na wageni waalikwa mbalimbali walioshiriki katika hafla ya uzinduzi wakimsikiliza Mhe. Rais alipokuwa akitoa hotuba yake katika hafla ya uzinduzi wa 'IJC' Dodoma.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni