Na Faustine Kapama, Mahakama
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 23 Novemba, 2021 amewaapisha
Mahakimu Wakazi wapya sita na kuwataka kutoa picha halisi ya ubora wa Mahakama
kwa kuishi viapo vyao katika kutekeleza kikamilifu jukumu la utoaji haki kwa
wananchi.
Akizungumza
katika hafla fupi ya uapisho huo iliyofanyika ofisini kwake Mahakama ya Rufani jijini
Dar es Salaam, Mhe. Prof. Juma aliwakumbusha Mahakimu hao kuwa wameapa kwa
kutumia Katiba na Kitabu Kitakatifu na kuahidi kwamba watalinda Katiba, kutetea
sheria na kutoa haki bila upendeleo wa aina yoyote.
“Hivyo
ahadi hii inatakiwa iwe sehemu ya maisha yenu mtakayoishi kama Mahakimu na
katika shughuli nyingine yoyote mtakayoifanya. Napenda kuwakumbusha kuwa
kiapo chenu kisiishie hapa. Ikiwezekana siku zote jitengenezeeni nakala iwaongoze
siku zote kwa sababu inatoa muhtasari wa kile ambacho kinategemewa kutoka kwenu,”
Jaji Mkuu aliwaasa Mahakimu hao.
Alibainisha
pia kuwa hapa Tanzania, asilimia 70 ya wanaotafuta haki wanaipata katika Mahakama
za Mwanzo, hivyo Mahakimu hao wanabeba mzigo mkubwa wa utoaji haki kwa sababu
wananchi wengi kituo chao cha kwanza cha kutafuta haki ni Mahakama za Mwanzo na
wengi huwa hawapati nafasi ya kuonana na Majaji.
“Kwa
hiyo, picha yao ya Mahakama ni Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo. Nawaomba mtoe picha
halisi ya ubora wa Mahakama. Sisi sote tutachafuka kama mkitoa picha ambayo sio
halisi ya Mahakama. Nyie ndiyo picha kwa mwananchi wa kawaida na sehemu yoyote
mtakayokwenda mtaishi pamoja na jamii,” alisema.
Jaji
Mkuu alikumbushia jambo jingine kuhusu ukubwa wa mamlaka waliyonayo Mahakimu kwa
kuangalia sheria ambazo huwa wanazitekeleza na kwamba amri yoyote wanayoweza
kutoa hugusa haki za wananchi, ikiwemo haki za binadamu za kila siku, haki za
mali au haki za uhuru wao binafsi, hivyo, aliwataka kutokuchelewesha maamuzi yao
yanayogusa haki hizo.
“Kwa
mfano, endapo utafuata sheria kwa umakini na ukatoa haki kwa umakini na
wahusika wakaridhika na kutokukata rufaa, ina maana shauri husika litaisha na
haki itapatikana ndani ya muda mfupi sana. Lakini kama utatoa uamuzi ambao sio
makini na ikapatikana rufaa, maana yake upatikanaji wa haki utachelewa. Kwa
hiyo ukiwa makini haki itapatikana kwa haraka zaidi na usipokuwa makini yule
mwananchi anayetafuta haki hiyo atasubiri mpaka Mahakama ya Rufani itakapotoa
uamuzi wake,” Mhe. Prof. Juma alisema.
Aidha,
Jaji Mkuu aliwataka Mahakimu hao kuendelea kujisomea na kufuatilia mabadiliko ya
sheria kadri yanavyotokea kwa sababu kila siku sheria inabadilika. Alitoa mfano
wa Bunge lijalo ambapo kutakuwa na mabadiliko ya sheria kadhaa na baadhi ya
mabadiliko hayo yatagusa utoaji haki mahakamani. “Tunatarajia mtafuatilia hayo
mabadiliko na yakipishwa na Bunge lazima muende na hayo mabadiliko,” aliwaambia
Mahakimu hao.
Naye
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani aliwasihi
Mahakimu hao wapya kuzingatia uadilifu, juhudi na kuzingatia sheria, miongozo,
taratibu na kanuni mbalimbali zinazotawala nchi yetu. “Bahati nzuri ninyi wote mmekuwa watumishi wa
Mahakama na mnafahamu yanayoendelea katika Mahakama ya Tazania hivi sasa. Hivyo
ni matumaini yetu mtaenda kufanya kazi inayotakiwa. Hivyo, nendeni mkafanye
kazi,” alisema.
Mahakimu
hao wapya walioapishwa leo ni Mhe. Raymond Kweka aliyekuwa Msaidizi wa
Kumbukumbu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. John Musiime ambaye
alikuwa Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama ya Wilaya ya Ilemela, Mhe. Clifford
Masinde, Msaidizi wa Kumbukumbu Mwandamizi Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Haudeface
Mpanju, Msaidizi wa Kumbukumbu katika Mahakama ya Wilaya ya Bagamoyo, Martha
Mabagala, aliyekuwa Msaidizi wa Ofisi Mahakama ya Mwanzo Kimara na Mhe. Protas
Honono, aliyekuwa Msaidizi wa Hesabu
Mahakama ya Wilaya Singida.
Viongozi
wengine wa Mahakama waliohudhuria hafla hiyo ya uapisho ni Mtendaji Mkuu wa
Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili wa Mahakama ya Rufani,
Mhe. Kelvin Mhina, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania anayeshughulikia
Mahakama za Mwanzo, Bw. Humphfrey Paya na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Bahati Chitepo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akitoa nasaha fupi kwa Mahakimu Wakazi wapya mara baada ya kuapishwa.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni