Na Faustine Kapama na Magreth Kinabo, Mahakama
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 10 Desemba, 2021 amewapokea
na kuwakubali Mawakili wapya 313, ambao wamekula kiapo cha uadilifu kwa mara ya
kwanza tangu kuanzishwa kwa tasnia hiyo hapa nchini.
Sherehe
za kuwapokea Mawakili hao zimefanyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es
Salaam na kuhudhuliwa na wageni na waalikwa mbalimbali, wakiwemo Majaji wa
Mahakama ya Rufani, Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mwanasheria Mkuu wa
Serikali, Mkurugenzi wa Mashtaka, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Wajumbe wa
Baraza la Elimu ya Sheria, Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) pamoja
na watendaji wengine wa Mahakama wa ngazi mbalimbali.
Mawakili
wapya na wageni mbalimbali walianza kuwasili katika viwanja hivyo majira ya
asubuhi na shamrashamra za sherehe hiyo zilizokuwa zikirushwa mubashara na Kituo
cha Televisheni cha Taifa-TBC 1, zilianza majira ya saa tatu asubuhi kwa Mhe.
Prof. Juma ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi kufika katika eneo hilo na
baadaye kuwakubali na kuwapokea Mawakili hao.
Baada
ya zoezi hilo, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Shamillah Sarwatt
aliwainua Mawakili hao wapya kwa ajili ya kula kiapo cha uadilifu, zoezi ambalo
limekuwa la kwanza tangu tasnia hiyo ianzishwe hapa Tanzania. Baadaye, Jaji
Mkuu wa Tanzania aliwakabidhi vyeti Mawakili hao kama ishara ya kuanzia sasa
wanakuwa Mawakili wa Kujitegemea na watakuwa na wajibu sio tu wa kuwawakilisha
wateja wao bali pia kuisaidia Mahakama ya Tanzania katika kufikia uamuzi wa
haki kwa wananchi.
Akizungumza
kwa ufupi kuhusu hatua hiyo, Mhe. Prof. Juma alibainisha kuwa hapo awali
Mawakili wapya walikuwa hawali kiapo cha uadilifu kama walivyo watumishi
wengine wa umma wanapoteuliwa kushika nyadhifa mbalimbali, jambo ambalo lilipelekea
uongozi mpya wa TLS kuja na pendekezo la kuwepo kwa utaratibu huo kwa Mawakili wote watakaokubaliwa na kupokelewa
kuwa Mawakili wa Kujitegemea, kuanza kula kiapo cha uandilifu, pendekezo ambalo
lilikubaliwa na Jaji Mkuu wa Tanzania.
“Nimefurahi
kuona kuwa mmekula kiapo cha uadilifu, na hili wazo lilitoka kwa Rais wenu wa Chama cha Mawakili Tanganyika aliponitembelea ambapo alionesha nia ya kupambana na
utovu wa maadili na akatuuliza kama kuna sehemu ambayo tunaweza kuwataka Mawakili
kula kiapo cha uadilifu. Ninyi ni Mawakili wa kwanza kabisa kula kiapo cha
uadilifu na tutapimana. Baada ya muda tutaangalia kama hicho kiapo kilikuwa ni
cha siku ya leo kuturidhisha mpate vyeti au mtakuwa waadilifu wa kudumu,”
alisema Jaji Mkuu.
Akizungumza
katika sherehe hizo, Rais wa TLS Prof. Edward Hosea amebainisha kuwa Chama
kinaendela na utekelezaji wa maono yake ya
kupambana na vitendo haramu na visivyo ya kimaadili vya utendaji wa kazi
za uwakili vilivyoshamiri mijini. Amesema kuwa vitendo hivyo vimesababisha
kushuka kwa hadhi ya taaluma hiyo adhimu, hivyo kusababisha kukosa kuaminiwa na
Serikali, wadau mbalimbali na jamii kwa ujumla.
Amevitaja
miongoni mwa vitendo hivyo kama uwepo wa Vishoka wa Uwakili, ambao ni baadhi ya
watu wanaofanya kazi za uwakili wakati sio mawakili. Kwa mujibu wa Prof. Hosea,
watu hao wamekuwa wakifanya kazi mbalimbali za kiuwakili kama kuandaa na kuthibitisha nyaraka, kushuhudia
viapo, kuwakilisha wateja mahakamani na kazi nyinginezo za uwakili.
“Wahalifu
wa vitendo hivi viovu ni watu wanaojifanya ni Mawakili lakini sio, pamoja na Mawakili
wanaofanya kazi zao kinyume na maadili ya uwakili kama kutoa huduma ya kisheria
bila kuwa na leseni halali, kufanya kazi za uwakili katika mazingira yasiyofaa
kama madukani, barabarani na vijiweni, kuruhusu
mihuri yao kutumiwa na mtu asiye Wakili na kutoza ada za uwakili chini ya
kiwango kilichowekwa kisheria,” amesema.
Amebainisha
pia kuwa Chama cha Wanasheria Tanganyika kimekua kikipokea malalamiko lukuki
kutoka wa wateja wakilalamika dhidi ya vitendo viovu visivyo vya kiuwakili
vifanywavyo na Mawakili kama kuwatekeleza wateja wao na kutohudhuria
mahakamani, matumizi mabaya ya fedha za wateja, kutokuwepo na mawasiliano
mazuri na kuvunjika kwa usiri kati ya Wakili na
mteja wake.
“Ni
wito wangu leo kwa Mawakili kuhudhuria mahakamani, kusimamia na kufanya kazi za
wateja wenu kwa uadilifu, ili
kuhakikisha haki za wateja zinapatikana kwa wakati na kwa utimilifu. Ni wito
wangu pia kwa Mawakili kufungua akaunti za wateja ili kuepuka kutumia
fedha bila idhini zao,” amesema.
Hivyo,
amesisitiza Mawakili wanapaswa kuwa na mawasiliano mazuri na wateja wao kwa
kuwapa mrejesho wa kesi au kazi zao, kupokea simu na kujibu ujumbe wa mteja, kutunza
siri zao na kwa kufanya hivyo wataweza kulinda taaluma hiyo adhimu na kurudisha
hadhi ya tasnia yao inayoonekana kushuka siku hadi siku.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa hotuba katika Mahafali ya 65 ya kuwapokea na kuwakubali mawakili wapya 313 yaliyofanyika leo tarehe 10 Desemba 2021, kwenye viwanja vya Karimjee Jijini Dar es salaam.
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt akiongoza kiapo cha Mawakili wapya (picha ya chini) mara baada ya kupokelewa na kukubaliwa kuwa Mawakili wa kujitegemea.
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika(TLS), Mhe. Prof. Edward Hosea akisisitiza jambo wakati wa sherehe hiyo.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma(kushoto) akikaribishwa na Kaimu Jaji Kiongozi Mhe. John Mugeta (katikati) leo kwenye viwanja vya Karimjee, Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuwapokea na kuwakubali mawakili wapya 313, (kulia) ni Msajili wa Mahakama ya Rufani (T) na Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Kevin Mhina.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma(kushoto) akiwaongoza Majaji wa Mahakama ya Rufani na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania kuingia katika viwanja vya Karimjee leo kwa ajili ya hafla ya kuwapokea na kuwakubali mawakili wapya, (Kulia) ni Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Kevin Mhina.
Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiingia katika viwanja hivyo.
Baadhi
ya wajumbe wa menejimenti ya Mahakama ya Tanzania wakifuatilia hafla hiyo.
(Picha
na Magreth Kinabo na Innocent Kansha-Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni