Jumatatu, 20 Desemba 2021

PROF. OLE GABRIEL AFANYA KIKAO KAZI KWA MKUTANO MTANDAO

Na Innocent Kansha – Mahakama.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewakumbusha Watendaji wote wa Mahakama nchini kutambua dhamana kubwa waliyonayo katika kujenga kwa weledi, uadilifu na kujiamini  na kusimamia shughuli za kiutendaji kwenye maeneo yao ya kazi na kuhakikisha Taasisi inabaki kuwa imara na mfano wa kuigwa.  

Akizungumza katika kikao kazi cha Watendaji wa Mahakama wa ngazi mbalimbali wapatao 44, pamoja na baadhi ya viongozi waandamizi kutoka Makao Makuu walioshiriki kwenye kikao hicho kilichoendeshwa kwa njia ya Mkutano Mtandao “Video Conference” leo tarehe 20 Desemba 2021 ofisini kwake Jijini Dar es Salaam, Prof. Ole Gabriel alisema kusimamia na kufuatilia kazi za Taasisi za kila siku ni jukumu lao la msingi kwa ngazi ya mikoa na wilaya, kwani ndiko waliko wateja wengi wanaohudumiwa na Mahakama.

“Tujitume kwa asilimia 100, tufanye kazi kwa uwazi, uwajibikaji na tuoneshe ufanisi mkubwa katika utendaji wetu. Tutoe uamuzi kwa wakati hasa kwenye mambo yote yaliyo ndani ya uwezo wetu na tuepuke utamaduni wa kulalamika,” alisema Mtendaji Mkuu huyo wa Mahakama ya Tanzania.

Prof. Ole Gabriel aliwasisitiza Watendaji kusimamia shughuli za Mahakama hasa upande wa miradi ya ujenzi iliyopo kwenye maeneo yao ya kiutawala ambapo aliwaasa kujua miradi inayotekelezwa kwenye maeneo yao, huku akibainisha kutokuridhishwa na kasi ndogo na usimamizi dhaifu wa miradi ya ujenzi na hivyo kuwataka kutambua kila jambo linalofanywa na kujua ni sehemu yao ya utendaji kazi.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo alisema kuwa Watendaji ni watu muhimu katika kusimamia uboreshaji mkubwa unaofanywa na Mahakama ya Tanzania, hivyo kuwataka kuchukua changamoto ndogo ndogo zilizopo katika maeneo yao, kuzigatia fursa na kuzitatua kwa ubunifu uliotukuka huku wakiongozwa na fikra chanya.

Kwa upande wa matumizi ya Ofisi Mtandao “e – Office Management System” Prof. Ole Gabriel amewataka Watendaji kujielekeza zaidi katika matumizi hayo ili kuondokana na matumizi ya ripoti na barua za watumishi kwa njia ya nakala ngumu, kwani Mahakama sasa hivi inaelekea kwenye mapinduzi ya kuepuka matumizi ya karatasi katika shughuli mbalimbali za kutendaji, hatua ambayo itasaidia usimamizi na ufuatiliaji wa haraka.

Akizungumzia suala la manunuzi, Mtendaji Mkuu huyo alisema kuwa Mahakama ya Tanzania inashughulikia mchakato wa kuanzisha bodi za manunuzi ili kugatua madaraka na taratibu za manunuzi ili zianze kufanyika kwenye ngazi za mikoa badala ya Makao Makuu na kusema kuwa hatua hiyo itapunguza ucheleweshaji wa taratibu hizo na kuongeza ufanisi katika kazi.

Aliongeza kuwa watendaji wanapaswa kuboresha taarifa kwenye mfumo wa ramani unaonesha maeneo mbalimbali ya kijiografia ya Mahakama “Judiciary Mapping”, ili kutoa mwanya wa kuonesha uboreshaji unaoendelea kufanyika ndani ya Mhimili huo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyenyosha kidole) akizungumza leo tarehe 20 Desemba, 2021 akiwa ofisini kwake jijini Dar es Salaam na  Watendaji wa Mahakama wa ngazi mbalimbali wakati wa kikao kazi kilichofanyika kwa njia ya Mkutano Mtandao. Waliokaa kushoto kwa Mtendaji Mkuu ni viongozi waandamizi wa Mahakama waliohudhuria kikao  hicho. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyekaa kushoto) pamoja na baadhi ya viongozi waandamizi kutoka Makao Makuu wakifuatilia mazungumzo katika kikao kazi hicho. 


Baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo walioshiriki katika mkutano huo.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni