Ijumaa, 28 Januari 2022

JAJI KIONGOZI AAGIZA WATUMISHI KUONGEZA KASI UTOAJI HAKI

Na Tiganya Vicent – Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani amewataka Watumishi wa Mahakama nchini kuongeza kasi katika kuwatumikia wananchi ili waweze kupata haki zao kwa wakati unaostahili.

Alisema ni vema uboreshwaji wa miundombinu ya Mahakama hapa nchini ikaendana na huduma bora zinazotolewa kwa wananchi.

Mhe. Siyani ametoa kauli hiyo leo tarehe 28 Januari, 2022 wakati wa kuzindua jengo linalojumuisha Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Bahi ambalo ujenzi wake umegharimu milioni 797.6 za Kitanzania.

Alisema uzinduzi wa Mahakama ya Wilaya ya Bahi na nyingine hapa nchini ni sehemu ya mpango wa maboresho ya miundombinu uliojikita katika kuboresha utoaji haki na kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

Mhe. Siyani aliishukuru Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya Mahakama.

Aidha, Jaji Kiongozi aliwaeleza watumishi wa Mahakama hiyo kuwa wamepata jengo nzuri ambalo ni kama vazi jipya kwao. Hata hivyo aliwataka kutambua kuwa wananchi wanatarajia uzuri wa jengo hilo uendane na ubora wa huduma zitakazotolewa.

“Jengo hili na mengine yaliyojengwa na yanayoendelea kujengwa kote nchini yanajengwa kwa kodi za wananchi. Kwa hiyo tambueni kuwa wananchi ndiyo wenye mamlaka na watawapima kwa ubora wa kazi zenu na kama nyinyi mnavyowahukumu wenye makosa mbele yenu,”alisema.

Kwa upande mwingine, Mhe. Siyani aliwakumbusha wananchi wanaotumia huduma za Mahakama kujua kuwa vipo vyombo maalum vilivyowekwa kisheria kwa ajili ya kuwasilisha malalamiko dhidi ya watumishi wa Mahakama na huduma wazitoazo.

Alitoa mfano kuwa malalamiko ya kimaadili dhidi ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo na Wilaya yanaweza kuwasilishwa kwenye kamati za maadili za Maafisa wa Mahakama ngazi ya Wilaya na Mkoa ambazo wenyeviti wake ni Wakuu wa Wilaya na Mikoa kote nchini.

“Watumieni viongozi hawa ambao mko karibu nao kuwasilisha kero za kimaadili. Kwa malalamiko dhidi ya huduma za Mahakama, kuna madawati maalumu ya malalamiko katika kila Mahakama ya Wilaya, Mkoa na Mahakama Kuu,”alisema.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu alisema kukamilika kwa jengo hilo litawezesha kutoa huduma kwa wakazi wapatao 271,000 kwa maoteo ya sensa ya mwaka 2019.

Naye Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof Elisante Ole Gabriel alisema uongozi wa Mahakama utaendelea kuhakikisha jengo hilo linatunzwa ili liweze kuwahudumia wananchi  kwa kadri ya malengo na fedha inayotolewa na Serikali.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma aliwataka wadau wa Mahakama kutoa ushirikiano ili kesi ziweze kupatiwa ufumbuzi kwa haraka na haki iweze kupatikana kwa mhusika kwa wakati.

Aliuomba Uongozi wa Wilaya ya Bahi kusaidia upatikanaji wa maeneo kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Bahi.

Awali, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma, Bi Maria Itala alisema jumla ya shilingi milioni 797.6 za Kitanzania zimetumika katika ujenzi wa mradi huo wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Bahi.

Alisema ujenzi wa Mahakama hiyo umelenga kusogeza huduma za kimahakama karibuni na wananchi ikiwa sehemu ya mpango mkakati wa uboreshaji wa miundombinu ya Mahakama nchini Tanzania.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (mwenye tai nyekundu) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa jengo linalojumuisha Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Bahi mkoani Dodoma katika hafla iliyofanyika leo tarehe 28 Januari, 2022.


Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kushoto) akifunua pazia kuashiria uzinduzi wa jengo linalojumuisha Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Bahi mkoani Dodoma. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Bi. Mwanahamis Mkunda.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akiongea na wananchi waliohudhuria uzinduzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Bahi mkoani Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdeme akitoa neno la utangulizi kumkaribisha mgeni rasmi.

Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Bi. Mwanahamis Mkunda akitoa salamu za Serikali katika hafla hiyo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Martin Chuma akieleza jambo katika hafla ya uzinduzi wa jengo linalojumuisha Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Bahi.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa nasaha kwa watumishi wa Mahakama ya Wilaya na Mwanzo Bahi katika hafla hiyo.


Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma, Bi. Maria Itala akiwasilisha taarifa ya ujenzi wa jengo hilo.

Sehemu ya maafisa wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria uzinduzi huo.


Sehemu ya watumishi wa Mahakama na wananchi waliohuduria uzinduzi wa jengo hilo.
Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania waliohuduria uzinduzi huo.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa Mahakama Dodoma waliohuduria uzinduzi huo.

                     (Picha na Innocent Kansha-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni