Jumanne, 22 Februari 2022

MTENDAJI MKUU MAHAKAMA ASISITIZA THAMANI YA FEDHA KATIKA UTEKELEZAJI MIRADI

Na Innocent Kansha – Mahakama.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka Wakandarasi kuhakikisha miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama katika maeneo mbalimbali nchini inatekelezwa kulingana na thamani ya fedha zinazotolewa.

Akizungumza kwenye kikao kazi na Wakandarasi hao leo tarehe 22 Februari, 2022 katika Ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni Jijini Dar es salaam, Prof. Ole Gabriel alisema Mahakama itaendelea kuwatizama kwa jicho la karibu katika utendaji wao na haitovumilia wakandarasi watakaofanya kazi kwa mazoea.

“Mahakama ya Tanzania inathamini sana kazi za wakandarasi wazawa, ni vema mkafanya kazi kwa weledi kwani miradi hii sio ya mwisho. Mahakama ya Tanzania ina miradi mingi inayoendelea na inayotarajiwa kutekelezwa, msitupe mbachao kwa msala upitao …fanyeni kazi zenu kwa ubora na kwa kasi ili miradi mingine ikitokea tuweze kuwapatia,”aliwasisitiza

Kadhalika, Mtendaji Mkuu aliwataka wakandarasi hao kujali utaalamu wa fani zao ili kazi zinazofanyika ziwe madhubuti na kuzingatia ubora kwa ufanisi unaokubalika, kwa vile kila kitabu kina zama zake kwani Mahakama ya sasa ni ya watu waadilifu.

Prof. Ole Gabriel aliwakumbusha wataalam hao kuwa hata Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya kilele cha siku ya Sheria mjini Dodoma alisisitiza miradi inayoendelea kujengwa kwa ubora unaozingatia fedha zinatolewa.

Aidha alimnukuu Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Khamis Juma ambaye naye amekuwa akisisitiza ujenzi wa majengo yote ya Mahakama kujengwa kwa kasi na kwa kuzingatia ubora unaotakiwa ili kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi.

Hivyo, Prof. Ole Gabriel aliwataka Wakandarasi wote kufanya kazi kwa karibu na wasaidizi wake ili kutatua kero zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, mathalani masuala ya malipo.

Aliishukuru Serikali kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundombinu ya Mahakama na kuwaahidi Wakandarasi hao kuwalipa fedha zao kwa wakati kwa wale watakaokamilisha taratibu kulingana na mikataba ya ujenzi.

Hata hivyo, Prof. Ole Gabriel aliwakumbusha kuwa wakandarasi watakaochezea fedha za umma zinazotumika kwenye utekelezaji wa miradi ya Mahakama hawataonewa haya. Alifafanuzi kuwa sio tu wakandarasi hao watavunjiwa mkataba bali pia watachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kushitakiwa kama watathibitika kujihusisha na vitendo hivyo.

“Msimamie miradi yenu kwa ukaribu na kwa kuzingatia thamani ya fedha za serikali kwani fedha hizo sio shamba la bibi”, alionya.

Mtendaji Mkuu akawashauri wakandarasi wote kuajiri wataalamu wenye sifa katika kutekeleza majukumu yao ya kimikataba, mfano kwenye maeneo ya masoko, waasibu, mainjinia na washauri wa miradi wenye uzoefu wa kutosha ili kuimarisha kampuni zao na kuondoa kasumba ya kutolipa watumishi kwa wakati, hivyo kuwajengea imani kwa wateja wao.

“Natamani wote twende pamoja na tushirikiane kwa hali zote, yaani Mahakama, Mkandarasi na Mkandarasi Mshauri ili tuwe kitu kimoja na kutatua changamoto zetu kwa pamoja ili kukamilisha miradi hii ndani ya wakati unao kubalika”, aliongeza.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama alitumia wasaa huo kuwakumbusha viongozi wa Mahakama wanaoratibu tenda za miradi ya Mahakama kuajili wakandarasi wenye uwezo wa kutekeleza miradi hiyo ili imalizike kwa wakati na kuangalia namna bora ya kuwatumia wazabuni wenye gharama za chini.

Prof Ole Gabriel alisema hadi hivi sasa Tanzania Bara ina Mahakama za Mwanzo 960, Mahakama za Wilaya 120 , Mahakama za Hakimu Mkazi 30, Mahakama Kuu 18 , Mahakama ya Rufani mmoja(1) na Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita katika mikoa mitano.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akizungumza leo tarehe 22 Februari, 2022 jijini Dar es salaam na Wakandarasi (hawapo katika picha) wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Wengine ni Mtendaji wa Mahakama ya Rufaa ya Tanzania Solanus Nyimbi(kulia) na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Leonard Magacha(kushoto).

Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Majengo wa Mahakama ya Tanzania Mhandisi Khamadu Kitunzi akitoa mada kuhusu hali ya maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya Mahakama katika maeneo mbalimbali wakati wa mkutano wa siku moja wa Wakandarasi na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) uliofanyika leo tarehe 22 Februari, 2022. 

Mhandisi kutoka Kampuni ya Ujenzi ya Moladi Tanzania Limited Noel Sylvester akichangia wakati wa mkutano wa Wakandarasi hao.

Meneja Mradi wa Kampuni ya Ujenzi ya Charles Limited John Bogomba akichangia wakati wa mkutano huo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akimuhoji Mkandarasi mshauri wa miradi ya Mahakama Bw. Boniface Charles (aliyesimama) kuhusu maendeleo ya miradi wakati wa kikao hicho na Wakandarasi wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama katika maeneo mbalimbali hapa nchini. 


(Picha na Innocent Kansha-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni