Alhamisi, 3 Februari 2022

WAKAZI 30,000 MOROGORO WANUFAIKA NA WIKI YA SHERIA

 Na Evelina Odemba - Morogoro

Wakazi Zaidi ya 30,000 mkoani Morogoro wamenufaika na Maadhimisho ya Wiki ya Sheria kwa kupatiwa elimu mbalimbali juu ya haki za watoto na mambo mbalimbali ya kisheria.

Hayo yalielezwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe, alipokuwa akizungumza katika kilele cha maazimisho ya Siku ya Sheria tarehe 2 Februari, 2022 yaliyofanyika katika viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki mkoani hapa.

Mhe. Ngwembe alisema kuwa maelfu hayo ya wananchi waliojitokeza kwenye vituo vilivyoandaliwa kwa ajili ya kutolea elimu katika kipindi chote cha maadhimisho ya Wiki ya Sheria ili kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu sheria, Mahakama na wadau wake.

Alivitaja vitaja vituo hivyo kuwa ni stendi ya mabasi ya Msamvu, Soko la Kingalu, Soko la Chamwino, viwanja vya shule ya Msingi, kiwanja cha Ndege pamoja na viwanja vya Mahakama Kuu- Kituo Jumuishi cha utoaji Haki (IJC -Morogoro).

Mhe. Ngwembe alieleza kuwa Mahakama kwa kushirikiana na wadau wake waliwafikia wananchi kupitia vyombo vya habari 11 ikiwemo Televisheni tatu vilivyoko mkoani hapa, elimu kwa shule saba za msingi na pia  Magereza mawili ya Mkoa wa Morogoro, chuo cha ualimu Kigurunyembe pamoja na chuo Kikuu cha Mzumbe.

Jaji Mfawidhi huyo amesema kuwa maboresho ya Mahakama kwa sasa yanasaidia kufanikisha shughuli za kimahakama kwa wakati sahihi na tayari teknolojia imeanza kutumika kwenye usikilizaji wa mashauri na kusajili mashauri kwa njia ya mtandao.

Akitoa salamu kwa niaba ya Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Mwenyekiti Msaidizi wa Chama cha Wanasheria Morogoro, Bi Mariam Kapama alisema kuwa maboresho makubwa yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania ni ya mfano, hivyo wanasheria wanaomba Mahakama inapojenga majengo yake izingatie pia kuweka ofisi za mawakili wa kujitegemea, jambo litakalorahisisha utoaji haki kwa wakati.

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali Mfawidhi wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Xavier Masalu kutoka ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali alisema kuwa Mahakama imesaidia kupambana na rushwa kwa kuweka mfumo wa kusajili mashauri kwa njia ya mtandao, jambo ambalo limeleta uwazi na linaokoa gharama na muda.

Ametoa rai kuwa maboresho hayo pia yafanyike kwa wadau wa Mahakama ili nao waweze kwenda na kasi ya utendaji wa Mahakama.

Naye mgeni maalumu, Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Mhe. Albert Msando alitoa pongezi kwa Mahakama kwa kuweza kutoa elimu ya sheria kwa wananchi.

Ameagiza Wakurugenzi kutenga maeneo kwa ajili ya kuweka miundombinu ya Mahakama na ofisi zote zinazohusika na utoaji haki , huku akizitaka ofisi hizo zenye uhitaji wa maeneo kuandika barua kwa Mkurugenzi wa Manispaa ili waweze kupatiwa maeneo ya kujenga ofisi hizo.

Wiki ya sheria nchini ilizinduliwa mnamo tarehe 23 Januari 2022 jijini Dodoma ambapo kwa Kanda ya Morogoro uzinduzi huo pia ulifanyika katika viwanja vya Jamuhuri, ukifuatiwa na uzinduzi wa vituo vya kutolea elimu ya sheria tarehe 24 Januari 2022 ambapo ndani ya muda huo shughuli mbalimbali za utoaji elimu ya kisheria kwa wananchi ulifanyika.

Kilele cha Siku ya Sheria kinaashiria kuanza rasmi kwa shuguli za Mahakama nchini. Ikumbukwe kuwa Mahakama itatembea na kauli mbiu isemayo “zama za mapinduzi ya nne ya viwanda: safari ya maboresho kuelekea Mahakama Mtandao.”

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akifutilia jambo wakati wa maadhimisho ya kilele cha Siku ya Sheria tarehe 2 Febriari, 2022.
Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando, ambaye alikuwa Mgeni Maalum akitoa salamu katika maadhimisho hayo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akikagua gwaride lililoandaliwa na Jeshi la Polisi kuashiria kuanza kwa mwaka mpya wa shughuli za kimahakama 2022.
Wadau mbalimbali waliohudhuria maadhimisho hayo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akipokea salamu za heshima kutoka kwa kiongozi wa gwaride.
Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe( katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Morogoro (juu na chini). Wengine waliokaa kutoka kushoto kwa Mhe. Ngwembe ni Majaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Messe Chaba na Mhe. Said Kalunde ambao wanafuatiwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa Foutunatus Muslim. Kulia kwa Mhe. Ngwembe ni Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Xavier Masalu na Mwenyekiti Msaidizi wa Chama cha Wanasheria Morogoro, Bi Mariam Kapama (kushoto).

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe( katikati aliyekaa) ikiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa (juu) na watumishi wa Mahakama (chini). Wengine waliokaa kutoka kushoto kwa Mhe. Ngwembe ni Majaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Messe Chaba na Mhe. Said Kalunde ambao wanafuatiwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa Foutunatus Muslim. Kulia kwa Mhe. Ngwembe ni Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Mhe. Albert Msando, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Xavier Masalu na Mwenyekiti Msaidizi wa Chama cha Wanasheria Morogoro, Bi Mariam Kapama (kushoto).


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni