Jumamosi, 12 Machi 2022

JAJI MAGHIMBI AHIMIZA UADILIFU KWA WATUMISHI KUFANIKISHA MALENGO YA MPANGO MKAKATI

Na Innocent Kansha - Mahakama

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Salma Maghimbi amewakumbusha watumishi kutumia taaluma zao vizuri, kufanya kazi kwa Uadilifu bila upendeleo, kuongeza uwazi na mshikamano mahala pa kazi bila kuathiri maelekezo ya viongozi ili kusaidia kufanikisha malengo ya Mpango Mkakati wa awamu ya pili.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo ya Mpango Mkakati wa Mahakama wa awamu ya pili 2020/2021 hadi 2024/2025 na huduma kwa mteja kwa watumishi wote wa divisheni hiyo leo tarehe 12 Machi 2022, katika Ukumbi wa Mafunzo Kisutu jijini Dar es salaam, Mhe. Maghimbi amesema, anatambua kwamba katika safari ya uboreshaji wa huduma za Mahakama unasimamia nguzo tatu, (3) ambazo ni Utawala bora na usimamizi wa rasilimali watu, Utoaji haki sawa na kwa wakati na Ushirikishwaji wa wadau.

“Naelewa ilivyo ngumu kujenga jamii yenye uadilifu, kwani misingi ya uadilifu hujengwa kuanzia kwa wazazi wetu na walezi wetu, lakini kamwe hili haliwezi kutufanya tukaacha kukumbushana wajibu wetu kama wadau namba moja wa utoaji haki”, alisema Jaji Mfawidhi

Jaji Maghimbi ameongeza kuwa, kupitia mafunzo hayo yatawajengea uwezo watumishi kufahamu mikakati ya Taasisi, kuwaongezea watumishi uadilifu na pia kuwapa hamasa ya kutoaji huduma za kimahakama zinazoridhisha na hivyo kuimarisha ushirikiano wa watumishi katika kuboresha huduma.

Aidha, Jaji Mfawidhi aliwasisitiza washiriki kuwa mada zilizoandaliwa ni muafaka na zitasaidia kuwajengea uwezo watumishi wa kusimamia na kutekeleza nguzo ya pili ya Mpango Mkakati wa Mahakama ambao ndiyo jukumu la msingi lililowekwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kadhaa.

“Inanipa faraja kubwa kusema uboreshaji wa huduma  unaoendelea katika Taasisi yetu hauna budi kupongezwa na kuungwa mkono na kila mmoja wetu. Ni dhahiri kwamba kila mmoja analo la kusimulia kwa kuangalia tulipotoka na mahali tulipo sasa, ni wazi kwamba ilikuwa ni nadra sana kupata fursa kama hii ya kukutana kwa wingi wetu kama ilivyo sasa na kupata mafunzo”, alisema Jaji Maghimbi

Jaji Mfawidhi, alisema kuhusu Taarifa ya REPOA ni tafiti inayotoa tathmini iliyofanyika kwa Mahakama kupima huduma zinazotolewa ili kujua ni kwa kiasi gani zina kidhi viwango, hilo litasadia  kupima na kurekebisha pale ambapo hapakwenda sawa kama  taratibu za utoaji huduma zinavyopaswa.

“Maoni yaliyotolewa juu yetu isiwe sehemu ya kuwachukia wateja wetu bali iwe chachu ya mabadiliko, kibinadamu huwezi kutambua unapokosea isipokuwa kupitia watu wengine”.aliongeza Jaji Maghimbi

Kwa upande wa matarajio ya mafunzo hayo Mhe. Maghimbi alisema, ni imani kubwa baada ya mafunzo hayo watumishi watabadili mienendo yao binafsi na kushirikiana vizuri na wadau wote, kuwa waaminifu na wakweli katika utoji wa huduma. Kutotoa huduma kwa upendeleo na kuimarisha ushirikiano “team work”. Kuongeza uwajibikaji na uwazi kwa kulinda uhuru wa  Mahakama.

Jaji Maghimbi alihitimisha kwa kuwashukuru Shirika la Kazi Duniani (ILO) kwa mchango wake mkubwa wa kufanikisha mafunzo hayo “Nitakuwa mchoyo wa fadhila endapo sitatoa shukrani za dhati kwa wawezeshaji wa mafunzo haya  Shirika la Kazi duniani na wale wote ambao wameshiriki katika maandalizi ya mafunzo haya”,. 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Salma Maghimbi (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi wakiwa wamenyoosha mikono na kutaja neno TEHAMA ikiwa ni salamu ya Devisheni hiyo wakati wa mafunzo ya siku moja yaliyofanyika leo tarehe 12 Machi, 2022 katika Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama ya Haki Mkazi Kisutu Dar es salaam, wengine walioketi ni Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Augustine Rwizile (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Biswalo Mganga (wa pili kulia), Naibu Msajili, Mhe. Kinabo Minja (wa kwanza kushoto) na Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji na Tathimini Mahakama ya Tanzania Bw. Sebastian Lacha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Salma Maghimbi akitoa hotuba ya ufunguzi wa mafunzo ya Mpango Mkakati wa Mahakama wa awamu ya pili 2020/2021 hadi 2024/2025 na huduma kwa mteja kwa watumishi wote wa divisheni hiyo
 
Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Elizabeth Nyembele (wa kwanza kushoto) akiwa miongoni mwa washiliki akifuatilia mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Salma Maghimbi akimsikiliza mtoa mada wakati wa mafunzo hayo, wengine kwenye mstari wa mbele ni Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Augustine Rwizile (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Biswalo Mganga (wa tatu kutoka kushoto)

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mafunzo hayo.

Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Mahakama ya Tanzania Bw. Sebastian Lacha (aliyesimama mbele) akitoa mada ya Mpango Mkakati wa Mahakama wa awamu ya pili wa mwaka 2020/2021 hadi 2024/2025 wakati wa mafunzo hayo.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, waliohudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mafunzo hayo.

Naibu Msajili, Mhe. Kinabo Minja (aliyesimama mwenye koti jeusi) akitoa mada ya utafiti uliofanywa na Taasisi ya REPOA kwa Mahakama ya Tanzania kuhusu viwango vya huduma zitolewazo na Mahakama kwa mteja

Picha na Innocent Kansha - Mahakama

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni