Alhamisi, 10 Machi 2022

UTOAJI HAKI KWA WAKATI CHACHU YA KUJENGA UCHUMI IMARA

 Na Lydia Churi- Mahakama, Morogoro

Kaimu Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika amesema utoaji haki kwa wakati ni muhimu katika kujenga uchumi imara na shindani utakaowezesha Tanzania kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ifikapo mwaka 2025.

Akizungumza kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama za Mkoa na Wilaya jana mjini Morogoro, Jaji Ndika alisema kuwa eneo la utoaji haki lina umuhimu mkubwa katika kujenga uchumi imara hivyo ni jukumu la Tume ya Utumishi wa Mahakama kujenga ufanisi wa shughuli za utoaji haki.

Kaimu Mwenyekiti huyo alisema huduma ya msingi ya utoaji haki inayotolewa na Mahakama ya Tanzania ni ya ustawi wa wananchi kwa lengo la kujenga utawala bora.

Alisema katika kujenga utawala bora, Mahakama ina wajibu wa kutatua migogoro inayotokea katika jamii. Akitolea mfano wa migogoro ya ardhi, Jaji Ndika alisema kama itakuwa mingi na isipotatuliwa inaweza kusababisha Mkoa kutotawalika kwa urahisi, hivyo huduma zinazotolewa na Mahakama zinalenga katika kujenga utawala bora.

“Ili kujenga utawala bora, kazi mojawapo ya Mahakama ni kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati”, alisisitiza Jaji Ndika ambaye pia ni Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Wakati huo huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta, ambaye amealikwa na Tume kutoa elimu amesema Watumishi wa Mahakama ya Tanzania wanao wajibu wa kufahamu haki na wajibu wao ili waweze kutambua matendo ambayo ni kinyume na maadili ya utendaji.

Alisema kwa kutambua matendo hayo, Watumishi hao watasaidia kuongeza tija katika kazi zao za kila siku, kuimarisha utendaji kazi wa Mahakama na kuongeza imani ya wananchi kwa Mhimili huo.

Jaji Mugeta alisema Watumishi wa Mahakama wana jukumu la kufahamu haki na wajibu wao kwa kuwa kuna changamoto kwa Watumishi hao ya kutofahamu ipasavyo haki na wajibu wao kwa taasisi.

Alisema wapo Watumishi ambao hawafahamu taarifa muhimu na sahihi zinazohusu kazi zao. “Changamoto hizi huweza kutatuliwa kwa kuwafahamisha na kuwashauri kusoma nyaraka mbalimbali ili kufahamu sheria za utumishi na masuala mbalimbali yanayohusu Mahakama,” alisema.

Tume ya Utumishi wa Mahakama inaendelea na ziara yake katika mkoa Tanga baada ya kukamilisha kwenye mikoa ya Pwani na Morogoro. Lengo la ziara ni kuitangaza Tume hiyo, kutoa elimu na kukutana na wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama za Mikoa na Wilaya pamoja na wadau wa Mahakama ili kuboresha huduma zinazotolewa na Mahakama ya Tanzania.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Temeke Mhe. Ilvin Mugeta akielezea Muundo na Majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama kwa wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama waliokutana na wajumbe wa Tume hiyo jana Machi 9, 2022 mkoani Morogoro.

Kaimu Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika akizungumza.

Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakiwa kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. Kutoka Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Morogoro Mhe. Paul Ngwembe akifuatiwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Temeke Mhe. Ilvin Mugeta, Jaji wa Mahakama Kuu kanda ya Morogoro Mhe. Said Kalunde na Jaji wa Kanda hiyo Mhe. Messeka Chaba. Kulia ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Sharmilla Sarwatt.

Kaimu Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika (katikati) akiwa kwenye Mkutano wa Tume. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Martine Shigela na kulia ni Katibu wa Tume hiyo ambaye ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni